NJAMA

SURA YA NANE

USIKU WA HEKAHEKA

Tulipofika Kilimanjaro Hoteli ilikuwa yapata saa tatu kamili. Tulipokuwa njiani kuelekea Kilimanjaro nilimweleza Eddy mambo yote niliyokuwa nimepata toka kwa Zabibu, mambo ambayo hata yeye alisema yalionyesha ufumbuzi wa jambo hili kwa mtu mwenye kufikiri. Tuliingia hotelini tukapanda lifti iliyotushusha orofa ya pili. Tulipotoka ndani ya lifti mara ile hali ya tahadhari ilituingia. Mimi nilitoa bastola yangu nikaiweka tayari na Eddy akafanya vile vile.

Tulipofika mlango wa chumba namba 206 tulikuta umefungwa, niligonga nikiwa nimesimama upande kabisa. Niligonga mlango mara mbili haraka haraka, halafu nikatulia kidogo kisha nikagonga tena, kwani hivi ndivyo Veronika alikuwa amenielekeza namna ya kujitambulisha lakini sikusikia kitu. Nilimonyesha ishara Eddy abane ukutani wakati mimi nafungua.

Nilifungua mlango ghafla. Tishio nililolikuta sijawahi kulipata tena, kwani Veronika alikuwa amelala kwenye sofa na kisu chenye mpini mwekundu kikiwa kimemwingia juu kidogo ya titi la kushoto. Kidogo ningezimia lakini nilijikaza nikakimbia pale kwenye sofa huku nikikanyaga maiti za watu wengine hapo chumbani.

Veronika alikuwa bado ameshikilia mkono wa simu mikononi mwake. Nilipomfikia nilimkuta bado yuko hai. Wakati huo Eddy nae alikuwa ameingia akanipa glasi ya whiski.

"Bosi jikaze, mnyweshe hii whiski mimi naita gari la hospitali"'

Nilimnywesha Veronika kisha nikamtingisha akafunua macho akapata fahamu kidogo.

"Vero, Willy hapa, niambie nani amefanya hivi".

"Walikuja.... watatu... nikapam...bana ...nikawaua nikakupigia simu.... ku...ku...kumbe walikuwepo... wengine ...wawili ... mmoja ... akamwita ... Shu... Shu...Shuta muue.... mimi kugeuka ... akanichoma... ki... kisu... nikawahi ...kumpiga yule mwingine ...kwa... akafa... Shuta... akakimbia ...nika...

Hakuweza kusema tena. Nikamwongeza whiski na kumtingisha.

"Oh Vero, nimeita gari la wagonjwa na mganga anakuja sasa hivi utapona tu.

"Si...siwezi...nitakufa...nimekufa...ame...moyo...Willy na...nakufa...na...ku...penda ...hakuna  tena... mwanamume... niliye... mpenda...kama wewe. Ni...nimefurahi...kukuona ...ma...mara... ya...mwisho...nikifa ...kwa ajili ya Afrika... siogopi...kufa...kwani nimekufa ...kwa sa...sabab...bu...nzuri. Ende...le..za ...ma...pa...mba...no... Willy ...Mungu...a...ku...sai...die...uni...ku...pi...zie...kisasi Afrika. Ni...busu...na... ku...

Nilijua Veronika hawezi kuchukua dakika moja zaidi, niliweka midomo yangu kwenye midomo yake na kulamba damu yake ambayo sasa ilikuwa inatoka mdomoni.Alitabasamu na macho yake yakang'ara kiasi ambacho sikuwahi kuyaona yanang'ara vile halafu akayapepesa akafariki. Alikufa huku akitabasamu.

Sikuwahi kulia na kupata uchungu kama wakati wa kifo cha Veronika. Nilijilaumu. Kama ningekwenda nae kwa Zabibu asingekufa.

Eddy alinikuta nabubujika machozi kama mama anayemlilia mtoto wake wa pekee.

"Bosi jikaze", Eddy alinishauri.

"Washenzi hawa, nduli hawa, watanitambua. Kwanini Mungu anaruhusu mtu kama Veronika kufa mikononi mwangu?. Eee Mungu nisaidie nilipize kisasi kwa ajili ya mwanamapinduzi huyu wa Afrika nzima", niliomba kwa sauti huku machozi yananitoka. Vero alikuwa amekufa kishujaa. Alikuwa amewaua maadui wanne pale pale chumbani.

Niling'oa kile kisu nikasafisha damu yake kwenye nguo zake.

"Kisu hiki hiki kitawauwa kama walivyomwua Veronika", nilisema.

"Bosi ninataka toka sasa tuwe pamoja".

"Hapana sasa hivi, fanya mpango wa kuondoa maiti hizi humu ndani. Na umwarifu Chifu, polisi wala wakuu wa hoteli wasiingilie. Na halafu kampashe Sherriff habari hizi za huzuni. Muushughulikie mwili wa Veronika uweze kupelekwa kwao. Mwambie Sherriff ashughulike na habari hiyo tu mambo mengine aniachie. Mwambie Chifu mambo yote yalivyo mpaka sasa mimi namfuata Shuta lazima alipe. Fanya hayo kwanza halafu nitakapokuhitaji nitakujulisha".

Niliondoka na kumwacha Eddy mle ndani ya chumba nikakimbia kwenye lifti iliyonitelemsha chini. Nilipita pale mapokezi huku nikikimbia kiasi cha watu wote kunishangaa.

Niliingia ndani ya gari Eddy alilokuwa amekodi na kuliacha Kilimanjaro Hoteli nikaondoka kwenda kumtafuta Shuta.








ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU