HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

IV

Willy na wenzake walikuwa wanaingia kwenye barabara kuu iendayo Themi Hill. walipishana na F.K. ambaye alikuwa akiendesha gari la Hamisi na kuelekea mjini. Si F.K. wala Nyaso ambaye alimtambua mwenzake kwani wote walikuwa wanaendesha magari ambayo hayakuwa yao.  Lakini Willy aligeuka na kuliangalia gari hilo ambalo lilikuwa linakwenda kasi na kupotea gizani.

Hilo ni kama gari la mzee Hamisi", Willy alisema baada ya kugutuka.

"Itakuwaje akuite halafu atoke", Bon aliuliza kwa mshangao.

"Hapo sasa", Willy aliitikia.

"Kama una hakika ni lenyewe, basi hilo siyo jambo la kawaida", Rocky alisema.

"Huenda ameona nimechelewa hivyo akaamua anifuate", Willy alijibu.

"Lakini hatujachelewa hata kidogo", Rocky alijibu.

Wakati huo walikuwa wamekaribia sehemu ya Kijenge ambako Hamisi alikuwa anakaa.

"Nyaso! Simama hapo pembeni", Willy alisema, Nyaso alijisikia raha kwani alijua yeye alikuwa msichana peke yake aliyepata fursa ya kuwaendesha wapelelezi mashuhuri wa Afrika, hasa wakiwa katika harakati za mapambano. Alisimamisha gari pembeni mwa barabara na Willy akatelemka.

"Haya nendeni lakini jihadharini sana. Huko mwendako panaweza kuwa moto. Nawatakia kila la kheri", Willy alisema.

"Ahsante", Bon na Rocky walijibu kwa pamoja.

Nyaso aliendesha kuelekea Themi Hill baada ya kumwacha Willy. Willy naye taratibu aliambaa kwa kufuata ua wa sehemu hii kuelekea nyumbani kwa Hamisi. Nyumbani kwa marehemu mzee Hamisi Stumke alikuwa amepanga watu wake tayari.

"Mtu huyu akiingia sharti auawe pale pale. Hakuna kusubiri. Yeyote atakayekuwa kwenye sehemu nzuri ya kumuua lazima afanye hivyo mara moja. Kama tulivyokwisha ambiwa, mtu huyu ni hatari sana. Kila mtu awe macho", Stumke aliwaonya wenzake.

Stumke alitokomea gizani. Aliambaa kwenye ua huku akielekeza macho na mawazo yake kwenye lango la nyumba. Majasusi wengine wawili walikuwa wamejibanza kwenye ua. Mmoja wao mwingine alikaa langoni kwani yeye ndiye ambaye angemfungulia Willy. Kila wakati waliposikia muungurumo wa gari, walijiweka tayari lakini hakuna gari lililojitokeza pale nyumbani. Gari la Nyaso liliposimama Stumke kutokana na uzoefu wa kazi yake, alihisi huenda mtu wao angeweza kuteremshwa njiani na kuingia pale kwa kutembea. Hivyo aliwashauri watu wake wawe macho kama mtu huyo angeingia kwa miguu.

Kengere ya ilani ilizidi kulia kichwani mwa Willy baada ya kila hatua aliyopiga kuelekea kwenye nyumba ya Hamisi. Ilikuwa kawaida yake kwamba kila hali hiyo ilipotokea, Willy alichukua tahadhari ya hali ya juu. Wakati huo huo Willy alimua kupita mlango wa nyuma badala ya mbele ya nyumba ile. Alizunguka ua wa nyumba huku akinyatia kama nyani. Aliruka ua huo wa michongoma na kutua ndani kwa kishindo kidogo.

Jasusi aliyekuwa upande wa kulia aligutuka kidogo halafu akaamua kuja kuangalia kuna nini. Alikuja kwa mwendo wa kunyatia kiasi kwamba hakutoa sauti yoyote. Lakini kwa kuwa masikio ya Willy yalikuwa na uzoefu kama wa mnyama awindwaye porini, aliweza kusikia mtu anajongea. Willy aliinuka mara moja na kujibanza kwenye pembe ya kulia ya nyumba. Aliangalia kwa chati na kuona yule kaburu anasogea huku bastola ikiwa mkononi. Macho ya Willy kama ya wale majasusi yalishazoea giza. Hivyo aliweza kuona vizuri.

Willy alikuwa na bastola mkononi, mara akaamua kuirejesha mahali pake, akajitayarisha kumkabiri jasusi yule kwa mikono. Pale pale akijuwa kuwa kuitwa kwake kulikiwa ni mtego na kwa hiyo ilibidi awe tayari kwa mapambano.  Yule jasusi alisogea karibu kabisa na pale Willy alipokuwa amejibanza. Willy alimwacha afike kabisa kwenye usawa alipokuwa amesimama. Ndipo alipomrukia na kumkaba koo kiasi kwamba yule jasusi hakuwa na muda wa kuweza hata kukohoa. Willy alivunja shingo ya yule jasusi ambaye alikata roho bila kutoa sauti. Taratibu Willy aliilaza chini maiti yake.

Jasusi mwingine alipoona mwenzake anakawia kurudi, alitoa ishara kwa yule aliyekuwa kwenye lango. Alikuwa anamjulisha kuwa anaelekea nyuma ya nyumba. Wakati huo damu ya Willy ilikuwa tayari imechemka kwa hali ya vita. Mara alimwona jasusi mwingine anakuja mbio. Willy alimsubiri huku akimwemwesa kwani alikuwa anakwenda hovyo bila tahadhari yoyote. Lakini alipokaribia mahari Willy alipokuwa, yule jasusi alisimama kana kwamba alikuwa amegutushwa na jambo fulani. Willy alijua kuwa kama angesubiri, bila shaka angeonekana. Kama risasi, Willy alifyatuka na kumrukia yule jasusi pale alipokuwa amesimama. Alimkata mkono wa karate na kumpasua kichwa. Wote walianguka chini.

Walianguka kwa kishindo ambacho kilimshitua Stumke na yule jasusi aliyekuwa kwenye lango. Wakiwa kama watu waliotiwa ufunguo walikimbia kuelekea mahali alipokuwa, mmoja akipitia kushoto na mwingine akipita kulia. Hapo hapo Willy aligundua kuwa jasusi yule alikuwa kafa, hivyo aliinuka haraka. Aliruka kama nyani na kukamata sehemu ya juu ya ukuta. Alijipinda na kupanda juu ya paa akajibanza. Mara tu baada ya kupanda juu ya paa ya nyumba, Stumke na mwenzake walifika sehemu ambayo Willy alikuwa amesimama muda kitambo. Walikuta wenzao wawili wamekufa. Waliingiwa na woga sana.

"Grande, mtafute haraka tumuue, unasikia", Stumke alimwamrisha mtu wake wasiwasi mwingi.

"Willy, uko wapi? njoo tuonane uso kwa uso kama kweli wewe ni mwanaume", Grande alisema kwa sauti. Willy ambaye alikuwa amelala juu ya paa alijisikia raha alipoona majasusi yale yanapaparika kwa woga. Mara aliinuka na kwa spidi kubwa Willy alijirusha katikati yao. Lakini wakati akiwa bado yuko hewani aliipiga teke bastola ambayo Grande alikuwa nayo mkononi. Silaha hiyo ilianguka upande wa pili wa ua. Stumke ambaye alikuwa ameangalia upande mwingine aligeuka na kufyatua risasi. Wakati ule ule Willy alijiviringisha chini na risasi zile zikampata Grande.

"Stumke, umeniua! Aibu", Grande alilalamika halafu akakata roho pale pale. Willy aliamka na kumwahi Stumke. Aliipiga teke bastola yake ambayo iliruka na kutua juu ya paa ya nyumba. Mara mapambano makali yakaanza.

Stumke alimpiga Willy teke la tumbo ambalo lilimpata barabara na kumwangusha chini. Kabla hajaweza kusimama, Stumke alimwongeza teke jingine la ubavuni. Halafu aliamua kumrukia ili ammalize kabisa. Kumbe Stumke alikuwa amefanya makosa. Wakati huo huo Willy alijiviringisha kidogo na Stumke akamkosa. Willy alijipinda na kusimama. Alikuwa amejisikia damu yake imeanza kwenda mbio kutokana na kupigo. Hasira zilikuwa zimempanda. Angeweza kummaliza Stume pale pale, lakini Willy alimpa nafasi naye ainuke. Jambo hilo lilimshangaza sana Stumke.

"Simama kaburu mshenzi, wee! Ulichokuja kutafuta leo utakipata. Kama mlifikiri mkutano hautafanyika mlijidanganya. Wakati ukiwa jehanamu mkutano utakuwa unaendelea", Willy alisema kwa hasira.

Stumke alikuwa bingwa wa karate katika jeshi la KULFUT. Hivyo alimsikitikia Willy kwani alifikiri angeweza kumamliza mara moja. Aliamini kwamba hakukuwepo mtu yeyote kutoka katika nchi za Afrika ambaye angediriki kupigana naye. Stumke alikuwa mwoga kila mapambano yalipokuwa sura ya kutumia silaha kama vile bastola. Lakini kama mtu alipambana naye kwa kutumi mbinu za karate, basi Stumke alimhesabu mtu huyo kuwa ni marehemu.

"Utajijutia leo", Stumke alisema. Mara alimrukia Willy na kutoa mapigo matatu ya karate ambayo hata Willy hakutarajia kamwe. Stumke alishangaa kwani Willy aliyazuia yote. Ni mara chache ambazo Stumke alikuwa ametumia mapigo ya namna hiyo wakati wa mapambano. Na kila alipoyatumia ni watu wachache ambao waliweza kuyazuia. Jambo ambalo alikuwa hajui Willy alikuwa Ninja.

Stumke alibadili mbinu na kutumia zile za hali ya juu kabisa. alitoa pigo la kwanza ambalo Willy alilikwepa. Alitoa pigo na pili na Willy alilizuia. Alipotoa pigo la tatu Willy alimkamata mkono ghafla. Aliukata kwa kiganja chake nao ukavunjika. Hata hivyo Stumke alijirusha na kumpiga Willy teka farasi ambalo lilimwangusha chini. Wakati huo huo Stumke aliguna kutokana na maumivu ya mkono wake uliovunjika. Alimtupita teke la mauti Willy lakini alikuta patupu! Willy alikuwa amejipinda kama swala na kuushika mguu wa Stumke akiwa bado hewani. Aliupinda na kufyatua mfupa wa goti.

Willy alimsukumiza Stumke kwenye ukuta ambapo aligonga kichwa chake na kuona nyota. Fahamu zilimpotea. Willy alimfuata kasi na kumkata karate iliyoacha mkono wake wa pili bila kuwa na kazi. Alimtingisha huku akisubiri fahamu zimrudie. Stumke alipopata fahamu, alijuwa kuwa ameshindwa. Hivyo kama lile jasusi Paul lilivyokuwa limefanya, Stumke alitoa ulimi wake nje na kuukata haraka kwa meno. Kwa haraka, Willy alimtia ngumi moja Stumke halafu akamwacha akate roho kwa kutokwa na damu.

"Ama kweli majasusi hawa ni watu wa ajabu. Kujiua kwa kujikata ulimi ni jambo geni kabisa", Willy alijisemea huku akielekea ndani ya nyumba. Mle ndani alikuta maiti ya mzee Hamisi. Hapo hapo akagudua kuwa mzee hamisi alikuwa amelazimishwa kumwita ili aje auawa kama yeye. Vile vile Willy aligundua kuwa kama majasusi hawa waliweza kuutumia uhusiano wake na Hamisi, basi tayari walikuwa na habari nyingi juu yao. Willy alijipongeza, bahati yake nzuri kwani mtego waliokuwa wamemwekea ilikuwa bahati kuukwepa.

Mara wazo likamjia. Alifikiri jinsi F.K. alivyokuwa anaaminiwa hapo Arusha kuwa mtu mwaminifu kwa Serikali na Chama. Kama kweli anahusika, bila shaka ndiye anayetayarisha mpango mzima. Mzee Hamisi asingeweza kumhisi kitu F.K. Ndio sababu waliweza kumwingia kwa urahisi. Mzee Hamisi alikuwa anajulikana kama mtu matata. Isingekuwa rahisi kwake kuuawa 'kike' hivyo. Willy aliamua kurudi alipokuwa amelala Stumke. Alimkuta bado hajakata roho kabisa. Alimpapasa ili kuona kama angepata kielelezo chochote. Hakukuta kitu bali funguo za gari. Alizichukua na kuelekea sehemu ya mbele ya nyumba.

Alikuta gari aina ya Benz. Alichukua kalamu yake ambayo ilikuwa na tochi vile vile, na kumulika kwenye karatasi ya bima iliyokuwa imebandikwa katika kioo cha mbele cha gari. Bima hiyo ilikuwa imechukuliwa kwa jina la Feroz Kassam. Kwa kutumia funguo zile zile, Willy alifungua mlango wa gari na kuingia ndani. Aliwasha gari lile na kuondoka. Wakati akiendesha Willy alijikuta akisema.

"We gari, nipeleke nyumbani kwenu, na leo hii bwana yako atanitambua!".

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU