HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

V

"Jumba lenyewe ni lile pale", Nyaso aliwaonyesha mara walipofika kwa F.K.

"Seng'enge yote ile mnayoiona imezunguka eneo la jumba hilo", waliangalia eneo hilo kwa makini kwani kila sehemu ilikuwa inawaka taa.

"Hili ni jumba hasa", Rocky alisema.

"Wacha kulishangaa kwa nje. Ndani yake ni zaidi. Siku moja mimi nililala humo. Mara nilisikia mlio wa vitu fulani kutoka chini. Nilipomwuliza nini ilikuwa, F.K alijibu huku akiwa mwenye nusu usingizi.

"Hao ni watu wanafanyakazi huko chini, wewe lala usiwe na wasiwasi. Mambo haya hayakufai! Siku hiyo ndiyo nilijuwa jumba hilo lilikuwa na vyumba chini ya ardhi. Siku nyingine F.K alifurahi sana halafu akanieleza kwamba, kama lingetokea jambo la dharura, jumba lile lina njia mbili za kutokea nje kupitia chini kwa chini. Aliongeza kusema kwamba njia moja ilitokea Magharibi na nyingine ilitokea Kusini mashariki mwa jumba hilo. Alinieleza pia kwamba kwa nje mtu yeyote angefikiri labda sehemu ya nje ni mahali palipofunikwa tu. Aidha mfuniko wa njia ulionekana kama ule wa machafu", Nyaso alieleza huku akiendesha pole pole.

"Mimi naona usimame hapa. Sasa hivi ni saa nne kamili. Sijui utaegesha wapi halafu utasubiri, tusingependa waone gari lako", Bon alimwambia Nyaso.

"Itawachukua muda gani?", Nyaso aliuliza.

"Tupe nusu saa. Ukikuta hatujarudi, ujuwe mambo yameharibika. Hivyo utakwenda Hotelini na kumweleza Willy", Bon alijibu.

"Una maana gani?", Nyaso aliuliza.

"Usiniulize maswali, fanya kama nilivyokwambia kwani hiyo itakuwa rahisi kwako", Bon alijibu kwa sauti kali kidogo.

"Haya bwana, mimi nakwenda kwa rafiki yangu hapo juu kwenye nyumba za wasabato. Saa nne na nusu juu ya alama nitakuwa hapa", Nyaso alijibu.

"Sawa, tutakuwa tumejibanza kwenye mti ule pale", Bon alieleza na halafu wakatelemka. Nyaso aliondoka huku roho ikimdunda.

Kufuatana na maelezo ya Nyaso, jumba hili linazo njia mbili za kuingilia kwa chini. Moja iko magharibi na nyingine iko kusini mashariki, wewe utaingilia magharibi na mimi nitapita kusini mashariki. Kama hatukuonana ndani basi tukutane mahali petu kabla ya saa nne na nusu", Bon alimweleza Rocky.

Wote walitazamana kwa hisia zao zilizowajulisha kwamba walikuwa wanaingia mahali pa hatari. Huku wakiwa wamejidhatiti, walipeana mikono na kuingia kazini. Rocky alikuwa wa kwanza kuona mfuniko ulioziba mlango wa njia. Aliuinua taratibu na kuona ngazi za kutelemkia chini. Aliuweka kando mfuniko ule ili wakati wa kutoka nje usije ukampa tabu. Baada ya kufanya hivyo, alichukua tochi yake yenye saizi ya kalamu akamulika na kutelemka ngazi jambo ambalo Rocky hakufahamu ni kwamba wakati mfuniko ule ulipofunguliwa ulikuwa unapeleka miale ya ilani, ambayo ambayo ilionekana kwenye televisheni iliyokuwa chumbani, kwa ajili ya usalama.

Dave alikuwa ndani ya chumba cha kumi akiangalia helikopta ya namna yake ambayo ilikuwa chumbani tayari kwa ajili ya kuwachukua majasusi baada ya kufanya maovu yao. Mara alisikia jasusi mmoja kwa jina la Terre akimwita. Terre na wenzake wawili walikuwa wamejinyoosha kwa mapumziko. Aligutushwa na makelele kutoka kwenye televisheni pamoja na picha ya mtu aliyeonekana akiingia kwenye njia ya siri upande wa magharibi. Dave alipofika na kuona picha hiyo, aligundua mara moja kwamba yule alikuwa Rocky kutoka Zimbabwe. Dave aliweza kumtambua Rocky kwa sababu alikuwa ameonyeshwa picha za wapelelezi mashuhuri wa Afrika, majina yao na nchi walizotoka.

"Haya sasa, kazi imebaki kwenu. Huyu amejileta mwenyewe badala ya sisi kumtafuta. Terre na Gary nendeni kwenye mlango ule. Akifungua tu nataka mmalize mara moja. Sisi tunamwona lakini yeye hatuoni. Hivyo kazi yenu itakuwa rahisi. Hakuna haja yangu mimi kuhangaika. Nitakuwa nawaangalia kwenye televisheni. Sitaki mtumie bastola bali mikono yenu. Hapo ndipo watu hawa watatambua sisi ni nani", Dave aliamrisha huku furaha imemjaa. Dave na Howe walikaa tayari kushuhudia mapambano ambayo yangefuatia.

"Huyu ni chakula chetu", Terre alijibu huku akiondoka pamoja na Garry. Walikuwa wamepandwa na mori kwani walitaka kuonyesha uhodari wao, pia kuwa mtu wa kwanza kumuua mpelelezi mashuhuri wa Afrika. Bila kujua kuwa alikuwa anaonekana kwenye televisheni, Rocky aliendelea taratibu kwa tahadhari kubwa sana. Alipomaliza ngazi za kwanza, aliufikia mlango. Upande wa pili wa mlango, Terre na Garry alikuwa wakisubiri tayari.

Ili wamsaidie kuingia kwenye mtego, walikuwa wamefungua mlango na kuuacha umerudishiwa tu. Rocky alipojaribu kufungua mlango alikuta umerudishiwa. Kutokana na uzoefu wake wa kazi wa muda mrefu. Rocky alifungua mlango ghafla na kwa nguvu. Terre na Garry walitarajia Rocky angefungua taratibu na kuendelea kutembea. Badala yake alijirusha chini kwenye njia. Alifanya kitu ambacho hakikutarajia mpaka wakashindwa kufanya yale waliyokuwa wamepanga. Alijiviringisha chini na kujipinda huku akichukua bastola yake. Alifyatua risasi mfululizo ambazo zilimpata Terre na Garry. Wote wawili walikufa pale pale.

Dave na Howe ambao walikuwa wanafuatilia mapambano kwenye televisheni, walishangazwa na kitendo hicho cha Rocky chenye kuonyesha ujuzi wa hali ya juu.

Howe, twende tukamkabiri kwani naona mtu huyu ni hatari sana. Chukua bastola na mimi nipatie moja", Dave alimwagiza Howe.

"Wewi ni Ninja, huyu atakuwa nini kwako?", Howe alimpambisha Howe moto.

"Unasema kweli, kama hujaniona basi leo utaniona", Dave alijigamba huku wanaelekea kwenye mlango katika njia ambayo Rocky alikuwa akitokea.

"Dave, nafikiri tusisogee kwenye mlango kwani mtu huyu anaweza kutufanya kama Terre na Garry. Heri tumsubiri hapa. Kwa kuwa chumba hiki ni kipana kiasi cha kutosha, hata kama akijirusha bila shaka ataimba tu", Howe alisema huku akijitayarisha na kumwangalia Rocky kwenye televisheni kwa mara ya mwisho. Rocky aliendelea kunyata na kuusogelea mlango wa chumba kile cha mapumziko.

Mlango wa sita wa maarifa ulimjulisha Rocky kwamba chumba alichokuwa akisogelea kilikuwa cha hatari zaidi. Hivyo alichukua tahadhari zaidi. Alikuwa tayari amepandwa na mori wa kupigana. Kwa hiyo alijiona kuwa alikuwa na uwezo wa kupabana katika hali yoyote ile. Dave ambaye alikuwa amesimama pembeni karibu na mlango ule, alitarajia Rocky angejirusha chini baada ya kufungua. Badala yake Rocky aliruka hewani na kuufungua mlango kwa kuupiga teke akitumia miguu yake miwili. Wakati bado akiwa hewani, Rocky alijipinda na kutua njiani nyuma yake. Howe aliyekuwa anasubiri Rocky kwa hamu alifyatua risasi tatu ambazo zote zilikosa Rocky. Kitendo cha sasa cha Rocky kilikuwa hakikutarajiwa pia.

Dave alimtolea ishara Howe ili amfuate Rocky. Howe alijiviringisha chini kwenye njia huku akifyatua risasi ambayo ilimpata Rocky kwenye mkono wa kushoto karibu na bega. Wakati huo huo Rocky aliachia risasi ambayo ilimpata Howe kwenye paji la uso. Alikata roho pale pale. Akiwa anasikia maumivu makali. Rocky alikimbia mpaka nyuma ya mlango kulikokuwa na maiti ya Terre na Garry. Alirudisha mlango huo. Alichana shati lake mwenyewe na kujifunga mkono ili kuzuia damu isitoke kwa wingi. Dave alijuwa Rocky alikuwa ameumia hivyo alimfuata na kufungua mlango ule. Rocky alikuwa ameweka bastola yake chini. Dave aliruka na kumkumba Rocky na wote wakajiviringika chini.

"Rocky! Unakufa sasa", Dave alisema kwa sauti ya juu. Rocky alikuwa anasikia maumivu makali lakini hali halisi ilimfanya asahau maumivu hayo. Aliinuka haraka akiwa tayari kukabiliana na jasusi hilo. Hapo mapambano makali yalianza. Dave alimshambulia Rocky kwa mapigo safi yapatayo saba lakini yote yalizuiwa. Hapo ndipo Dave alipogundua kuwa alikuwa anapambana na mtu mwenye ujuzi zaidi ya vile alivyotarajia. Hivyo aliamua kutumia mafunzo ya U-Ninja. Vile vile Rocky aligundua kuwa Dave alikuwa na ujuzi wa hali ya juu. Hivyo ilimbidi atumie mbinu kali kuweza kumshinda adui.

Dave alitupa ngumi lakini Rocky aliikwepa nayo ikagonga ukuta na kulitoa tofari moja lililoangukia upande wa pili. Wakati huo huo Rocky alichukua nafasi hiyo kumtia mapigo makali Dave ambayo yalimfanya aanguke chini. Hapo aliamua kuchukua bastola yake kwani aliamini kuwa mtu huyu hakuwa saizi yake. Hivyo alijirusha lakini kabla hajawahi kuichukua bastola yake iliyokuwa chini, Dave naye aliruka na kumwahi Rocky hewani alipompiga teke la kichwa. Rocky alipoteza fahamu na kuanguka chini kwa kishindo.

Bon alikuwa amenyatia toka chumba hadi chumba wakati alipofika kwenye chumba cha televisheni alimwona Dave anampiga Rocky teke la kichwa. Bon aligundua kwamba Rocky alipigwa teke la ki-Ninja ambalo asingeweza kulistahamili.

Bon alikimbia haraka kuelekea kwenye njia ambayo aliamini ndiko walikuwa wakipigania huku hasira na chuki zimemjaa. Rocky alikuwa anapigana kishujaa. Bon alipofungua mlango na kuingia kwenye chumba walichokuwa wanapigania, kumbe alikuwa amechelewa. Dave alikuwa amemrukia Rocky na kumpiga teke la moyoni ambalo lilimuua pale pale Rocky.

"Kufa mbwa mweusi, we!" Dave alitukana. Mara aliona mlango unafunguliwa ghafla na Bon akiingia ndani.

"Mbwa we, umemuua Rocky, nawe utaambatana naye mpaka peponi", Bon alisema kwa uchungu huku machozi yakimtoka. Bon alikuwa na bastola mkononi. Angeweza kumpiga risasi Dave. Lakini badala yake aliitupa kando. Dave alishangazwa na kitendo cha Bon. Vile vile alimwonea huruma kwani aliamini hakuna mtu mweusi ambaye angepambana naye kwani yeye alikuwa ni Ninja.

"Pole sana mbwa mweusi! Na wewe umejileta kwenye kaburi lenu", Dave alijibu kwa dharau. Bila kuchelewa Bon alimrukia Dave na kumpiga vipigo, moja baada ya kingine mpaka akaanguka chini. Lakini alijiviringisha na kuinuka haraka tayari kumkabiri Bon. Bon hakumpa nafasi kwani kabla hajasimama sawa sawa Dave alipewa vipigo kadhaa ambavyo vilimtatanisha. Pale pale alijuwa kwamba alikuwa anapambana na Ninja kama yeye mwenyewe, Bon aliruka na kumtia Dave teke la ubavuni na kumzidishia hasira.

Bon alimwahi Dave na kumpiga teke moja la shingoni na jingine la kichwani kwa wakati ule ule, ambayo yalimfanya Dave achanganyikiwe. Bon alipima hali ya Dave na kuona mbaya. Hivyo alichukua nafasi hiyo na kumtia pigo takatifu la kifuani ambalo lilikibomoa na kufanya damu ifumke na kutapakaa kila mahali. Kabla dave hajaanguka chini, Bon alimwonyesha kiganja na kama kusema. 'pigo linalofuata ni kisasi cha Rocky! Alimzibua tumbo na kuyatoa matumbo ya Dave nje'.

"Kufa Kaburu mshenzi, we!" Bon alisema kwa hasira. Dave alianguka chini akiwa maiti. Bon aliangalia saa yake. Ilikuwa saa tano kasoro dakika tano.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU