HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

VII

Mnamo muda wa saa tano na robo za usiku F.K, PG, George na vijana wao walikuwa wanarudi Themi Hill nyumbani kwa F.K. Hii ilikuwa baada ya kutega mabomu kwenye ukumbi wa mikutano wa AICC.

"Kesho Afrika itagwaya", P.G alisema.

"Kesho, watu hawa watatambua nguvu zetu. Tanzania imezidi kuzihamasisha nchi zilizo mstari wa mbele lakini baada ya kesho serikali itawafukuza wapigania uhuru wote kutoka nchini. Hiyo inatokana na kwamba baada ya pigo la kesho, tutatoa tangazo kuwa kama wataendelea kuwasitiri wapigania uhuru, tutaingia Ikulu na kutia kipigo", George alijigamba huku F.K akiegesha gari mbele ya nyumba yake. Walipotelemka walishangaa kuona kwamba gari la F.K lilikuwa bado halijawasili.

"Lo, hii ina maana kuwa Stumke na wenzake bado wanamsubiri Willy?", George aliuliza.

"Sidhani..." P.G alisema kwa sauti yenye kuonyesha wasiwasi kwamba kuna jambo ambalo halikwenda sawa. Waliingia ndani kwa kupitia mlango wa mbele. Walikwenda moja kwa moja mpaka kwenye chumba cha mapumziko walipokuwa wamemwacha Dave na wenzake. Walifungua mlango na kuingia ndani. Walipoangalia kwenye televisheni waliona maiti zimelala njiani.

"Mungu wangu", wote walisema kwa pamoja huku wakikimbilia yalipokuwa maiti.

"Mambo makubwa haya", F.K aligwaya.

"Sasa kazi imeanza", George alisema huku akiangalia maiti ya Dave na yale ya Rocky.

"Nakubali kwamba hawa watu siyo wa kawaida, njooni hapa niwaeleze", George aliwaita F.K na PG. waliokuwa wakiangalia maiti kwa mshangao. "Kazi hii ni ya Ninja", George alimaliza kusema na kwa mara ya kwanza alijisikia hofu.

"Dave, nitalipiza kisasi kwa ajili yako rafiki yangu", George alisema huku akichukuwa shuka na kuifunika maiti ya Dave. Mara wote walirudi chumbani na kukaa ili kupanga nini wafanye kwani mambo yalikuwa yamebadilika.

"Jamani, mmeona wenyewe jinsi mambo yalivyobadilika. Mimi nahisi Stumke na wenzake wameshauawa. Hata hivyo ni lazima tushinde vita hivi. Hatuwezi kushtushwa na haya yaliyotokea. Kulingana na habari tulizonazo ni kwamba Willy na Bon bado wangali hai. Kuanzia sasa ni wao wawili dhidi yetu watatu na vijana wetu wawili. Ninayo hakika watatufuata hapa kwani wameshajuwa siri yetu. Ni heri tuwasubiri hapa ili tuweze kuwamaliza watu hawa kwanza, tulijiamini kupita kiasi na kuwadharau wao. Lakini askari hawezi kufanya kosa lile lile mara mbili...", George alieleza.

"Maneno yako ni mazuri. Lakini mimi napendekeza tuwafuate kwa kuwa wanajuwa mahali tulipo. Kuna uwezekano wakatafuta msaada wa polisi na hata jeshi ili kutuvamia. Huo utakuwa mwisho wa kazi yetu ambayo bado haijamalizika na ushindi bado. Hatuwezi kuruhusu hali hiyo itokee kwani lazima kazi yetu ikamilike", P.G alishauri.

"Hapana P.G, tukifanya hivyo ujuwe tumekwisha. Kwanza tunajuwa watu hawa wako New Arusha Hoteli. Lakini baada ya mambo yaliyotokea ni vigumu kubashiri wao wako wapi. Hatimaye tutaanza kutafutana tusikutane hadi kesho asubuhi. Hiyo ina maana kazi yetu itakuwa haikumalizika usiku huu kama ilivyopangwa. Pili lazima tufahamu kwamba watu hawa ni wapelelezi wa muda mrefu. Wanaelewa sheria ya mchezo huu. Hivyo, amini usiamini, hawawezi kutumia polisi wala jeshi. Watatuwinda wao wenyewe. Muda siyo mrefu watakuja hapa maana mchezo umebadilika. Hivi sasa, sisi ndio wawindwa. Wao wanazo habari kamili kuhusu sisi kama sisi tulivyo na habari juu yao. Lililopo ni kujiweka tayari kupambana nao", George alisisitiza.

"Mimi nakubaliana na maneno yako George. Kama nilivyokueleza hapo mwanzoni, imetokea ghafla tu. Viongozi wa vyama vya ukombozi hawalali kwenye hoteli walizopangiwa. Tena hata polisi hawajui lolote kuhusu viongozi hao. Habari kuhusu viongozi hawa zimekuwa nyeti. Ni wapelelezi hawa tu ambao wanajuwa viongozi hawa wamepelekwa wapi. Nasi tutawaulia mbali washenzi hawa, wasije wakaharibu kazi yangu, ambayo imetokana na mpango wa muda mrefu wa kuleta hofu katika nchi hii. Lazima ushindi ni wetu", F.K aliwatia mori wenzake. Baada ya hapo George alianza kuwaeleza mpangilio wa kujiweka tayari wakati wakisubiri wapelelezi maarufu wa Afrika wakiongozwa na Willy Gamba.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU