HOFU


KABLA YA USIKU WA MANANE

VIII

Wakati George alipokuwa anawaelekeza wenzake. Willy alikuwa anaagana na Nyaso karibu na nyumba hii.

"Willy, tafadhali jihadhari sana. Nakupenda sana Willy. Tafadhali...", Nyaso alisema kwa sauti ya unyonge.

"Tulia mtoto, usinililie mimi kwani nakwenda kazini. Lakini nitachukua tahadhari na tutaonana baadaye", Willy alisema huku akimvuta Nyaso na kumbandika busu moto moto. Kisha Nyaso alianza kumpa maelezo kuhusu jumba la F.K.

"... Upande wa kushoto kuna madirisha mawili makubwa", Nyaso alimaliza kueleza.

"Unasema Bon na Rocky walipita kwenye njia za siri ulizowaeleza?", Willy aliuliza.

"Bila shaka maana baada ya kuwaelekeza, wote walitoa ishara ya kukubali kwa kutumia vichwa vyao", Nyaso alijibu.

"Oke, mpenzi! Kwa heri", Willy alisema huku akimvuta Nyaso na kumbusu tena.

"Willy tafadhali... tafadhali...", Nyaso alibembeleza huku machozi yakimlenga.

"Usinitilie uchuro, mtoto we!", Willy alisema huku akiyeyuka na kutokomea gizani.

Roho ya Nyaso ilikuwa nzito sana lakini aliwasha gari na kurudi hotelini.

Willy alipanda na kuruka seng'enge akaingia uani. Kwa kuwa taa zilikuwa zinawaka kuzunguka eneo hilo, ilimbidi aende huku ameinama. Kwa kujificha kwenye vivuli vya miti mingi mizuri iliyopandwa kuzunguka nyumba hiyo. Willy hakuonekana na mtu. Alifika kwenye ukuta wa kushoto wa jumba hilo. Alijibanza na kisha kutambaa ili aweze kuona upande wa mbele wa nyumba. Alipofika tu kwenye kona ya jumba hilo, aliliona gari la mzee Hamisi limeegeshwa mbele karibu na mlango. Mara Willy alihisi mambo mawili. Kwanza, Majasusi wa makaburu walikuwa ndani wakimsubiri. Pili, kwamba Bon na Rocky walikuwa wameuawa na ndio sababu walikuwa hawakurudi. Aligundua kwamba alikuwa katika hatari kubwa. Hivyo ilibidi achukue tahadhari zaidi.

Akiwa sasa amelala chini Willy alisikia kishindo. Aligeuka na kuangalia upande huo lakini hakuona kitu. Aliamua kusubiri. Alijua fika kwamba katika mchezo huo, subira ni jambo muhimu. Kumbe aligundua kuwa kile kishindo kilikuwa cha mmoja wa askari wawili waliobakia kwani alimwona anatokea kwenye mti. Alikuwa amepangiwa kukaa juu ya mti huo na kutoa ishara kama angekitilia kitu chochote mashaka. Ajabu ni kwamba askari huyo alikuwa hakumwona Willy wakati alipoingia. Hivyo alikuwa ameamua kutelemka na kupanda mti mwingine. Kutokana na woga baada ya kuona wenzake walivyokufa askari huyo alikuwa anatembelea kwa uangalifu mkubwa. Willy alimwona askari yule karibu naye huku akinyata.

Alimsuburi mpaka walipokuwa sambamba ndipo Willy alipomrukia kwa spidi ya umeme na kumbana mdomo. Alimkata mkono wa shingo na kumuua pale pale. Kisha alimburuza taratibu na kumlaza alipokuwa yeye. Willy aliamua kuingia ndani ya nyumba kwa kupitia dirisha la kushoto. Baada ya kuangaza huku na kule na kuona kwamba kila kitu kilikuwa shwari, alijongea mpaka kwenye dirisha mojawapo na kulikagua. Alikuta limefungwa. Willy alichukua kisu chake maalumu chenye ncha ya almasi na kukata kipande cha kioo kutoka kwenye dirisha. Alipitisha mkono wake kwenye tundu na kufungua dirisha. Kisha alikwea dirishani na kutumbukia ndani ya chumba kilichokuwa giza. Baada ya kusimama tu alisikia sauti inasema.

"Shenzi kabisa". Halafu alisikia kitu kinamgonga kichwani. Willy alidondoka chini na kupoteza fahamu pale pale.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU