HOFU

MAMBO

II

Willy alipopata fahamu kidogo akajikuta ndani ya chumba kikubwa. Alikuwa amefungwa kwenye mti mfano wa msalaba uliokuwa katikati ya chumba. Ingawa Willy alikuwa amepata fahamu huku akiumwa sana na kichwa, hakuonyesha kama amepata fahamu. Alifanya hivyo 'kununu muda' Alishangaa kukuta majasusi walikuwa bado hawajamuua. Hapo hapo aligundua kuwa walikuwa na sababu ya kumweka hai. Kwa kutumia sababu hiyo aliweza kununua muda zaidi. Alijikuta amefungwa barabara kiasi kwamba asingeweza hata kujitingisha.

Mara alisikia mlango unafunguliwa na taa kali zaidi zinawashwa na kuelekeza mwanga wake kwake. Pale pale Willy alitambua kuwa chumba kile kilikuwa chumba cha mateso. Alikuwa amevuliwa nguo zake zote na kubaki na chupi tu.

"Hecke, bila shaka umempiga sana mtu huyu, nusura umwue. Unajuwa mtu huyu tunamhitaji sana angalau kwa muda wa dakika tano zaidi akiwa hai", F.K alisema. Willy aliyasikia maneno hayo.

"Mtu huyu ni hatari sana F.K. Hecke alichofanya ni sawa sawa", mtu mmoja alisema na Willy akamsikia.

"Sharti turudishe fahamu yake maana yule mwenzake anaweza kuwa anajongea kwa wakati huu", F.K. alisema.

"P.G yuko nje tayari kumfungia kazi. Hecke na wewe nenda nje ukamsaidie P.G. kama ikibidi. Akidiliki kupitia njia ile ya chini kama alivyofanya mwanzo, huo ndio utakuwa mwisho wake, kwani nimemtegeshea bomu moja safi", George alijigamba.

"Hebu kwanza Hecke, nenda ukawashe ile swichi ya umeme ili umshitue mbwa huyu kwani amezirai muda mrefu", F.K. alimwamrisha Hecke. Willy akajiweka tayari huku akili yake ikifanya kazi haraka haraka. Hecke alikwenda akawasha swichi. Umeme ulimshitua Willy naye akajifanya kaupata fahamu tayari ili asiumizwe zaidi. Alipofungua macho alimwona F.K. amesimama mbele yake pamoja na George. Kule pembeni alimwona Hecke.

"Karibu kwetu Willy Gamba. Ni jambo lisilofurahisha kukukaribisha hapa nyumbani kwangu katika hali hii. Lakini umeyataka mwenyewe na kama ujuavyo msiba wa kujitakia hauna kilio. Haya, huyu hapa ni mwenzetu na kiongozi wetu Geoge ambaye anaongoza kikundi cha 'KULFUT' kilichotumwa kuja kuifundisha adabu Tanzania", F.K alisema akiwa anamtazama Willy. Baadaye alimgekia George.

"George, huyu ndiye Willy Gamba kama umewahi kumsikia. Ni bahati yake mbaya kwamba amekutana na wewe", F.K. alisema.

"Hata mimi nimefurahi kumwona, nimesikia habari zake nyingi. Nasikitika kumwona katika hali hii, hata anapokuwa amefikia mwisho wa maisha yake haya yote yametokana na nchi ya Tanzania kujiweka kimbelembele na kujiingiza kwenye mambo yasiyowahusu", George alijigamba.

Aliposikia hayo Willy alianza kuzungumza ilimradi aweze kusukuma wakati.

"F.K... ni lazima umweleze kaburu huyu swala la ukombozi Kusini mwa Afrika ni swala la Afrika huru nzima. Hivyo kwa watu kufa ili vizazi vilivyobaki viweze kuwa huru ni jambo takatifu. Kwa hiyo mimi sina wasiwasi na kufa".

"Hecke, hebu nenda huko nje ukamsaidie P.G. kumumaliza huyo mbwa mweusi mwingine kwani naona hawa wana vichwa vigumu kama vya paka", George alimrisha.

"Kitu kimoja ambacho unapaswa kuweka maanani Willy ni kwamba, mtu mweusi hawezi kujitawala. Sana sana atapata uhuru wa bendera lakini uchumi wenu utatawaliwa na mtu mweupe daima. Chukua mfano wa Tanzania ni nani anayefaidi matunda ya uhuru hapa kama siyo mzungu na mhindi?, Mhindi akiendesha Benz ni halali yake; thubutu mtu mweusi aendeshe Benz kama hakutiwa msukosuko. Sasa, kisa gani hata kupoteza maisha yenu kwa kupigania uhuru wa bendera ambao huna faida? kweli mtu mweusi hawezi...", F.K. alisema na kukatizwa.

"F.K. unazungumza maneno ya kitoto. Nchi huru za Afrika zinapigana dhidi ya ubaguzi kwa sababu hazitaki ubaguzi. Nyinyi wahindi mnaonekana kama watanzania machoni mwa watanzania. Mawazo yako katika kuhusu uhitilafiana kimapato ni jambo lililopo Ulimwenguni kote. Amini usiamini, kama usaliti wako utagunduliwa, hata kama mimi nitakuwa nimekufa, wahindi wenzako watakuwa wa kwanza kutamani kukurarua. Siyo wahindi wote wenye mawazo finyu kama yako", Willy alimwambia F.K.

"F.K. unamchelewesha huyu mtu. Hebu muulize atupe habari zetu halafu... Usiku unakwenda haraka sana", George alimwambia F.K.

"Kusema kweli Willy nilipenda kifo chako kije haraka. Hata hivyo huo ni uamzi wako. Kama utajibu swali langu, utakufa haraka bila kupata mateso. La hasha, utakufa pole pole na kwa uchungu mkubwa. Chumba hiki kina kila aina ya vifaa vya kutesea. Sina haja ya kukueleza kwani wewe mwenyewe ni mwenyekiti katika shughuli hii. Sasa jibu swali langu: Viongozi wa wapigania uhuru wamefichwa wapi?", F.K. aliuliza. Mara Willy aligundua kwamba mpango wa kuwaficha viongozi wa wapigania uhuru ulikuwa wa busara sana.

"Sijui. Kawatafute wewe mwenyewe. Kwani sisi tulipogundua hawa makaburu ulipowaficha ulituambia?", willy alijibu kwa kiburi. Jibu hilo liliwafanya wahamaki. George alimrukia Willy na kumtia makonde ya haraka haraka mpaka Willy akapoteza fahamu kwa muda.

"Sisi hatutaki mchezo. Tumekuja Tanzania kuwatia hofu na kiwewe. Jibu lako litatusaidia kuua viongozi peke yake kuliko kufagilia mbali umati wa watu na mji mzima wa Arusha. Kipigo tutakachotoa kitasikika mpaka huko ahera. Nyumba hii imejaa silaha za kisasa za kuweza kuuteketeza mji mzima. Sasa sema ama hakika utaumia", F.K. alisema kwa hasira. Willy alifahamu fika kwamba hakuna mtu ambaye angethubutu kumuua, kwani alijuwa wao walitaka kufahamu viongozi wa wapigania uhuru wako wapi. Hilo ndilo jambo muhimu lililokuwa limewaleta.

"Sijui walipo, fanya unavyotaka", Willy alijibu.

"Umeyataka mwenyewe", F.K. alijibu huku akitoa kitu mfano wa saa kutoka kwenye mfuko wa shati na kukiwasha. Mara Willy alijisikia moto unamchoma kutoka kwenye ncha ya kidole mpaka utosini. Alijaribu kuvumilia. Lakini uchungu ulizidi na Willy akaanza kupoteza fahamu. Bila ya kujifahamu Willy alitoa sauti kali.

"Aaaaaa! Nitakuelezeaaa!".

ITAENDELEA

Comments

Post a Comment

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU