HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

VI

Ilikuwa yapata saa tano hivi wakati Willy alipokuwa anaegesha gari la F.K karibu na ofisi za mjini za mauzo ya General Tyre. Alikwenda haraka kwenye hoteli yake. Alibisha hodi kwenye chumba chake Mike akamfungulia.

"Vipi mwenzetu, mbona umenuna", Mike alimwuliza Willy.

"Hatari, akina Bon hawajarudi?", Willy aliuliza.

"Bado, mimi nina wasiwasi mkubwa", Mike alisema, "Je, umeonana na mzee Hamisi?".

"Mzee Hamisi ameuawa. Sasa hivi mtu wetu ni F.K. Hivi ninavyokueleza, nimeshaua makaburu wanne", Willy alisema na kisha alianza kumsimulia Mike yote yaliyotokea.

"Hivyo Mike, hapa mjini kuna kundi kubwa la makaburu wenye ujuzi mkubwa wa kupigana", Willy alimalizia.

"Kama ni hivyo, mimi napendekeza tulivamie jumba hilo kwani bila shaka majasusi wako humo. Nashauri kwamba kama ikibidi, tuombe msaada wa polisi ama jeshi", Mike alisema.

"Hapana Mike, kazi ya kupambana na majasusi haistahili kuhusisha polisi ama jeshi, kwani wao wanaweza kutumia mbinu za kijeshi tu na kusababisha maafa makubwa. Inatubidi sisi wenyewe tufunge vibwebwe na".... kabla hajamaliza sentensi, alisikia mtu anabisha hodi kwa kugonga mlango. Bastola za wanaume hawa zikawa tayari mikononi. Kwa tahadhari kubwa. Willy alifungua mlango huku bastola yake mkononi.

"Ni mimi....", Nyaso alisema kwa hofu alijikuta amekabiliana na mtutu wa bastola.

"Pole, usiwe na wasi wasi", Willy alisema huku akimvuta Nyaso ndani na kuurudisha mlango.

"Wenzako wako wapi?", Mike alimwuliza Nyaso huku akitweta.

"Waliniambia niwapitie saa nne na nusu. Nilipokwenda kwenye sehemu tuliyoagana, sikuwakuta. Hapo mwanzo walikuwa wamenieleza kwamba kama nisingewakuta basi ilibidi nije moja kwa moja huku ili niwaambie nyinyi", Nyaso alijibu huku machozi yakimlenga. Willy aliangalia saa yake na kuona kwamba ilikuwa saa tano na dakika kumi za usiku.

"Nyinyi subirini hapa. Mimi nitakwenda kuchunguza nini kimetokea, maana tukiondoka wote tunaweza kupishana nao, hivyo tutakuwa tumewachanganya. Nipeni mpaka saa sita na nusu, kama hamkuniona basi mjuwe mambo yameiva hivyo njooni", Willy aliwaambia.

"Hapana Willy, tuondoke wote. Nyaso atabaki hapa ili kama akina Bon wakirudi atawaambia watufuate", Mike alisisitiza.

"Hapana Mike, Willy halielewi sawa sawa lile jumba. Sharti nifuatane naye ili nimwelekeze", Nyaso alisema.

"Sawa Mike, utabaki hapa nami nitafuatana na Nyaso. Akisha nionyesha atarudi hapa. Kama ikifika saa sita na wewe hujaniona, basi nifuate", Willy alitamka.

"La hasha, mimi nitabaki huko na wewe....", Nyaso alisema na huku Willy akimkatisha.

"Nyamaza! Wewe unajuwa watu wale pamoja na bwana yako ni wauaji. Je, unataka kufa ama nini", Willy alisema kwa ukali.

"Hebu usiniambia kuwa bwana yangu ni muuaji! Kuna tofauti gani kati yake na wewe. Nyote wauaji tu. Kwani mimi nilifahamu kuwa yeye ni muuaji?", Nyaso alijibu kwa hasira. Willy alishikwa na hasira nusura ya kumnasa kibao Nyaso. Lakini Mike aliingilia kati.

"Basi basi, acheni hayo. Tunapoteza muda wetu. Wewe Nyaso usipende kugombana na wanaume. Utaumia. Mpeleke Willy kama alivyokwambia.

Nyaso alimtazama Willy kwa macho ya upendo. Alimkimbilia na kujilaza kifuani kwake huku akisema kwa sauti nyororo.

"Samahani Willy, sikuwa na maana hiyo. Nakupenda, tafadhali jihadhari", Willy alimvuta na wote wakatoka nje.

"Nawatakia kila la heri", Mike alisema.

"Ahsante!", Willy na Nyaso walijibu kwa pamoja wakati wakitoka nje.

ITAENDELEA

Comments

  1. Asante kaka......naifuatilia sana hii riwaya....naomba uendelee nayo kaka

    ReplyDelete

Post a Comment

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU