HOFU

MAMBO BADO

III

Wakati F.K na George wanamkabiri na kumtesa Willy katika kile chumba cha mateso, Bon na Mike walikuwa wamefika kwenye seng'enge ya jumba la F.K. tayari kwa mapambano makali.

"Tusipite kwa chini maana wanayo televisheni watatuona. Tupite njia ya kawaida ila tujuwe kuwa wanatusubiri", Bon alisema.

"Sawa", Mike alijibu.

"Pande zote mbili, kushoto na kulia zinayo madirisha makubwa. Jambo la kufanya ni kujitahidi kuingia na sisi tuonane huko ndani", Bon alimweleza Mike. Wote waliangaliana ili kupeana moyo.

"Jihadhari sana", Mike alimweleza Bon.

"Na wewe vile vile", Bon alijibu huku akimkumbuka marehemu Rocky aliyekuwa amemuaga kwa namna ile.

"Jambo la kwanza ni kuangalia kama Willy angali hai. Nina wasi wasi juu ya maisha yake", Bon alimnong'oneza Mike huku wakiachana. Mike alimuonyesha ishara ya kumwelewa Bon. Wakiwa wamejificha kwenye vivuli wanaume hao wawili walilisogelea jumba la F.K. kwa tahadhari na hamasa kubwa.

Mike aliambaa ambaa katika upande wake; mara alisimama kimya na kwa tahadhari alijaribu kusikia kila aina ya jambo ambalo lingetokea. P.G alikuwa upande wa kaskazini wa jumba lile. Mara alimwona Hecke aliyekuwa achunge upande wa kushoto wakati yeye P.G akichunga upande wa kulia.Wakati P.G alipokuwa anaambaa na ukuta wa kulia huku bastola mkononi. Mike naye alishafika kwenye ukuta ule ule akiangalia akiangalia namna ya kufungua dirisha bila kuwashitua watu waliokuwa ndani.

Mara P.G. alisikia jasho jembamba likimtoka. Pale pale alijuwa kuwa alikuwa katika hali ya hatari kwani hali hiyo humtokea mara tu hatari inapobisha hodi. Mike ambaye alikuwa amevaa nguo nyeusi alisogea mbali kidogo kutoka alipokuwa kwani naye alihisi kitu kinatembea karibu na ukuta ule. Alibana chini ya mti huku macho yake yamezoea giza. Mara alikia kitu kama mti kinakatika! Alipoangalia umbali wa mita mbili kutoka chini ya mti alipokuwa amesimama aliona kitu kinatingishika. Alipoangalia vizuri aliona mtu anasogea. Mike alisimama kama mti mkavu. P.G. naye alikuwa ananusa nusa huku na kule kama mbwa wa polisi huku bastola yake tayari kufyatuliwa wakati wowote.

Alipotembea na kufika sehemu ya mita moja kutoka mahali Mike alipokuwa amesimama, naye alisimama. Wakati huo huo Mike aliruka kama risasi. Alimkumba P.G. na wote wawili wakaanguka chini. Bastola ya P.G. ilianguka kando na kuzitema risasi zake. mlio wake haukusikika ndani ya jumba kwa sababu bastola ile ilikuwa na kiwambo cha kuzuia sauti. Walipoinuka, Mike alimtambua P.G. mara moja.

"Ni bahati iliyoje kwangu P.G.? Nilidhani umenikimbia huko Nairobi. Sasa mimi na wewe", Mike alisema na kumshangaza P.G. ambaye hakutarajia kukutana na Mike Arusha.

"Umejileta wewe mwenyewe kwenye kifo chako Mike Maina. Baada ya kukumaliza wewe nitarudi Nairobi. Kisha nitajibadilisha na kuhakikisha vile vikaragosi vyako kwenye ofisi yenu ambao walitaka kuharibu kazi yangu nawafagilia mbali. Kwa kutumia uwezo wangu wa kipesa, nitahakikisha Masoga anakuwa mkuu wa idara yenu..." P.G. alisema. Kisha alikatisha sentesi ili amchukue Mike kwa ghafla ili amtie 'mapigo ya kifo', kama yeye alivyokuwa anayaita. Lakini P.G. alipotupa mapigo yake hayo Mike aliyazua yote kwa ufundi wa hali ya juu.

"Nilimwahidi Mwaura kwamba nitalipa kisasi chake kwa mikono yangu mwenyewe. Sasa P.G. umekufa", Mike alisema na pale pale aliona sura ya maiti ya Mwaura ilivyokuwa imepigwa risasi. Mori ulimpanda. Alijisikia akipata nguvu zisizo kifani. Mike alimtia pigo la kifuani P.G. ambalo karibu lingemdondosha. Lakini alijitahidi na kurudishia mapigo makali sana. Mike aliteleza mpaka chini. P.G alivuta upanga wake ili ammalize Mike. Upanga ulikuwa umefichwa kiunoni. Huku akiamsha upanga, tayari kumkata Mike P.G. alisema.

"Burian Mike!", wakati huo huo Mike alijiviringisha na upanga ukamkosa, P.G. alijirusha na kujitayarisha tena kumkata Mike. Alimkosa mara ya pili na mara ya tatu. Mike aliruka na kuumpiga teke mkono ule wenye upanga ambao ulianguka chini. Mkono wa P.G. ulikuwa umevunjika. Maumivu yalikuwa makali na Mike alichukua nafasi hiyo. Mike alimtia P.G. kipigo cha mbavu ambazo zilivunjika. P.G. aliamua kujikakamua lakini akawa amezidiwa mbinu.

"P.G. Afrika itashinda na Afrika Kusini itaondokana na udhalimu wa ubaguzi wa rangi na kuwa huru chini ya wazalendo walio wengi. Ukiwa huko ahera utaona kuwa unyama wenu haufui dafu kwa wapigania haki. Hata Mwenyezi Mungu yuko kwenye upande wa wanyonge", Mike alimwambia P.G. ambaye alikuwa anatokwa damu puani na masikioni. Alijua alikuwa amekaribia mwisho wake lakini aliamua kama ni kufa ilibidi afe kiume. Alikusanya nguvu zake zilizobakia na kumrukia Mike. Lakini Mike alikuwa tayari. Hivyo alimpisha P.G. ambaye alijigonga kwenye ukuta na kuanguka chini. Mike alichukua ule upanga wa P.G. na kuutumia kumkata kichwa.

"Malipo ya dhambi ni mauti", Mike alisema huku akiwa ameinua upanga na kuangalia maiti ya P.G. Akiwa bado amepandwa na mori alivunja dirisha kwa kutumia upanga akiwa tayari kwa mapambano makali.

"Leo ni leo. Liwalo na liwe. Sisi na washenzi makaburu ", Mike alisema huku akipanda dirisha ili ajitose ndani.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU