UCHU



TAFUTA UKWELI

Ilikuwa yapata saa saba unusu. Musoke na Willy walipofika nyumbani kwa Temu. Walimkuta Temu akitembeatembea mbele ya nyumba yake katika bustani huku ameweka mikono yake nyuma. Kwa vile nyumba ilikuwa juu kwenye kilima, na wao walimwona kabla hajawaona mpaka walipopiga honi ya gari ili kufunguliwa lango la mbele. Alipoona ni gari la kukodi la Musoke, mara moja alikimbia na kulifungua lile lango hata askari wake anayelinda nyumba yake hakuwahi mbio za mzee huyu. Hii yote ilionyesha shauku aliyokuwa nayo Temu juu ya suala hili la Rwanda.

"Shikamoo", Willy alimshalimia.

"Marahaba, karibu".

Temu alipeana nao mikono na wote na kuwakaribisha kule uani kwenye bustani ya nyumba.

"Wengine?", Musoke aliuliza.

"Saa nane watafika".

"Vizuri".

Walipokuwa wameketi kule uawani kwenye kivuli kizuri cha miti, Musoke alitumia nafasi hiyo kuwafahamisha.

"Bwana Temu, huyu ni kijana wetu, anaitwa Willy Gamba, sasa hivi anafanyakazi za kujitegemea, lakini alikuwa kwenye idara ya upelelezi ya Tanzania kabla hajaamua kuacha kazi ili ajitegemee. Yeye ameombwa na marafiki zetu wengine aje atusaidie kwenye hili tatizo letu", Musoke alieleza huku Temu akionekana kushikwa na butwaa.

"Na bwana Gamba, huyu ni mzee Temu na ndiye Mkuu wa PAM upande wa Tanzania.

Willy aliinuka na kumpa Temu mkono.

"Mimi siamini macho na masikio yangu", Temu aliendelea kuonyesha kama mtu aliyeshituka sana. "Hivi kweli Willy Gamba yupo! na ni wewe! Hivi ni kweli baba yangu, ni kweli. Mimi siku zote husikia habari za Willy Gamba na huamini kuwa ni hadithi tu, maana mambo ambayo ameyafanya wakati wa ukombozi wa nchi zilizo kusini mwa Afrika tulifikiri ni propaganda tu ya kamati ya ukombozi ya OAU. Kumbe mtu mwenyewe upo na ni kweli. Eehe, ama kweli kuishi kwingi kuona mengi. Basi bwana Musoke, kazi yetu itafanikiwa", Temu alieleza.

"Huyu kijana wetu Mwenyezi Mungu amemjaalia uwezo mkubwa sana katika kazi hii ya upelelezi. Hakuna mtu unayeweza kumlinganisha naye hapa Afrika, sijui huko Ulaya, lakini hata majasusi wa huko Ulaya ndiye aliyekuwa akiyakomesha wakati wote huo. Kwa kweli hata mimi niliposikia amekubali na ni yeye anayekuja basi roho yangu ilitulia, najuwa tutafanikiwa. Hivi kwanini wamekukubalia kustaafu mapema hivi?", Musoke alimuuliza Willy lakini kabla ya kujibu, mhudumu wa pale nyumbani alifika na kutaka kujuwa watakunywa nini.

"Bwana Gamba unataka kunywa nini?, kunywa kitu kidogo, maana huko ndani wanatengeneza chochote cha mchana, sisi wachaga ndizi ndicho chakula chetu, sijui wewe utapendelea?", Temu aliuliza.

"Kinywaji naomba klabu soda, na nitafurahia sana macharari", Willy alijibu huku Temu akicheka na kufurahi kusikia macharari.

"Kumbe unayajuwa eeh basi baba yangu tutakula hayo maana wanaandaa. Na wewe mzee Musoke?".

"Mimi nitakunywa ki-wiski kidogo, unajuwa sisi wazee lazima ushituwe damu kidogo upate joto".

"Sawa kabisa, nenda kalete haraka", Temu alimwagiza mhudumu wake. 

"Ehe Willy, kwanini umeruhusiwa kustaafu mapema hivi?, au kwa sababu ya Afrika Kusini kupata uhuru?", Musoke aliuliza tena.

"Hapana, mimi niliomba kustaafu ili niweze kuoa na kuanza maisha ya kifamilia maana kazi hii haifai kama umeoa na una familia. Sasa hivi nimeoa na mke wangu ni mjamzito. Na hata kazi hii nimekubali tu, kwanza kwa sababu na mimi nimeumwa sana na hali hii ya mauaji ya Rwanda na pili kwa sababu Chifu alisema nisipokwenda mimi atakwenda yeye. Na unajuwa bwana Musoke, mimi nisingependa hata kidogo kuruhusu kitu kama hicho".

"Ni kweli kazi hii inahitaji kuweka mawazo yako pamoja, usiwe na fikira zingine, lakini ndivyo hivyo, taifa bado linakuhitaji mara kwa mara kama hivi, ingawaje si sana kama ulivyokuwa jikoni", Musoke alikubaliana na Willy. Mara wakaona wenzao wengine wanaingia na wote wakasimama kuwasalimia.

Temu alichukuwa nafasi ya kuwafahamishe wenzake kwa Willy Gamba. "Hawa ni wana PAM kutoka sehemu mbalimbali za Afrika. Na wamekuja kwa ajili ya kikao hiki cha kutathimini jinsi mambo yalivyokuwa huko Rwanda. Huyu ni bwana Kimani kutoka Kenya, huyo ni Abakusi toka Nigeria, huyu ni Makwega toka Zambia na huyu kijana mwenzio ni Malisa kutoka hapa hapa Tanzania". Kisha akageuka na kumgusa Willy. "Na huyu ndiye mgeni tuliyemtarajia kwa ajili ya kazi yetu. Bwana Willy Gamba.

Kimani na Malisa waliwahi kusikia habari zake nao walishikwa na mshangao kama wa Temu. Musoko alitumia nafasi hiyo kunong'ona na Abakusi na Makwega kuwaeleza Willy Gamba hasa alikuwa mtu wa sifa za namna gani. Bila hata kusema mengi, alipoeleza kazi zake mbili alizofanya na kuutingisha ulimwengu kwa kuwazuia majasusi wa Afrika Kusini tayari wote wakamtambua na kupigwa na butwaa vilevile.

"Wakati mwingine binadamu akili inashindwa kuamini kitu. Mimi nilisikia jinsi mpelelezi wa Afrika alivyoyaangamiza majasusi kule Kinsasa, Zaire, na nikaamini kuwa zilikuwa hadithi tu. Sasa namuona hapa mtu mwenyewe, akili inashindwa kuamini. Inashangaza", Abakusi alisema.

"Kama Willy Gamba ndiye huyu kijana, basi mambo yetu yameiva", Makwega naye alinena na kutokwa na wasiwasi aliokuwa nao usiku.

Bila kupoteza muda mkutano uliendelea huku wakipata huduma za vinywaji na chakula.

"Nafikiri wasiwasi wetu wote sasa umepungua baada ya kumpata kijana huyu?", Musoke alisema kama vile akitoa maoni ya mkutano.

Wote walitingisha vichwa kama ishara ya kukubali.

Kwa vile kijana huyu yuko hapa, tumpe maelezo tunataka atufanyie nini. Nafikiri mimi niendelee na kama mtu ataona nimepwelea mahala naomba asisite kuongezea, sawa".

"Sawa", wote walimjibu mzee Musoke.

"Bwana Willy, wewe mwenyewe naami unazo habari nyingi kuhusu matukio ya Rwanda. Ila sisi, kama wana PAM tungetaka tupate undani zaidi wa mambo yalivyotokea huko Rwanda mpaka yakafikia yalipofikia na watu zaidi ya milioni moja katika nchi ya watu milioni tano kuteketezwa kwa siku kadhaa tu. Kitu hiki kinatisha na kama hakiwezi kuangaliwa kwa undani na kuthibitiwa inaweza kutokea tena si Rwanda tu bali hata mahali pengine Afrika. Sijui unanielewa?", Musoke alimuuliza Willy.

"Nakuelewa, ila nataka nijie ni nini hasa mnataka mimi nifanye maana kule sasa kuna serikali ya RPF, kuna mashirika ya kimataifa, kuna mashirika yanayotetea haki za binadamu, mnafikiri mimi nitafanya nini zaidi ya watu hawa na wenye uwezo na mapesa mengi nyuma yao, maana na wao wanachunguza kwa kina maovu yaliyotendeka Rwanda", Willy alisema akitaka ufafanuzi zaidi.

"Sawa bwana Gamba, kitu tunachotaka sisi ni uchunguzi wetu wenyewe. Hawa watu wengine wote wanaweza kuwa na nia zao tofauti. Serikali ya RPF ni mhusika kwa kiasi fulani. hatuwezi kupata ukweli asilimia mia toka kwao. Mashirika ya kimataifa yenyewe yanaweza kuwa na ajenda tofauti, tena wanaweza kutoa ripoti kutokana na ajenda yao. Wanaotetea haki za binadamu nao wana mtazamo wao kwa maana ya kuonyesha kuwa kulikuwa na ukiukwaji wa haki za binadamu Rwanda. Sisi tunataka uende zaidi ya pale, ujue kama haki za binadamu zilikiukwa, na kwa nini zilikiukwa, lazima kuna sababu. Mauajiyaliyotokea nini kiini chake, maana yanaonekana yalikuwa yamepangwa toka mapema. Na vilevile kwanini Afrika na dunia kwa ujumla, ikiwa kimya pamoja na nchi jirani kama Uganda, Tanzania, Zaire na Burundi hazikufanya chochote kuzuia mauaji haya. Tukishajuwa chanzo na sababu zilizofanya mpaka binadamu akafikia kuwa mbaya kuliko mnyama, nafikiri tutakuwa tumejifunza; na hili fundisho litatusaidia kuweka mkakati wa kuzuia kitu kama hicho kitakapotokea. Vilevile tujue namna ya kukidhibiti kabla hakijaleta maafa makubwa kama haya", Musoke alijibu.

"Oke, nimeelewa nini mnataka, nitajitahidi niweze kuchimbua mambo uliyoyataja hapo ili nipate vyanzo vyake", Willy alijibu.

"Lakini haitakuwa kazi lahisi, lazima uwe macho maana ukweli wa mambo haya unaweza kuwa na athari nyingi kwa watu mbalimbali ndani ya Rwanda na pengineko duniani. Kwa hiyo ikijulikana kuwa kuna mtu anatafuta ukweli na ikaonekana kuwa ataupata, basi ujuwe masiha yako yanaweza kuwa hatarini maana mpaka sasa tunaamini kuna watu wanajaribu kufukia ukweli usijulikane. Na hawa watu watakuwa watu hatari. Tafadhali, hadhari ni lazima", Abakusi alimwasa Willy.

"Nitalitazama hilo", Willy alijibu na kuendelea, "Na malipo yangu yatalipwaje, maana sasa ni mfanyabiashara na si mfanyakazi wa serikali tena. Kazi hii nimeichukua binafsi".

"Malipo utalipwa na PAM. Kwa ajili ya kazi hii PAM iliwaomba michango wafanyabiashara wa kiafrika ambao wanaunga mkono msimamo wa PAM na wametoa michango mizuri sana na tukitoka hapa tutapitia hotelini kwangu nikupatie malipo yako. Sijui utahitaji kiasi gani?", Musoke aliuliza.

"Mimi vilevile, kama nilivyosema, naunga mkono madhumuni ya PAM, kwani ni mpaka pale Mwafrika atakapojitambua kuwa lazima azungumze na Waafrika wenzake kupambana na ukoloni mambo leo ndipo atakapokuwa amejikomboa kutoka katika umasikini, ujinga na maradh. Kwa jinsi hiyo na mimi nikiwa mshabiki wa PAM nitaomba nilipwe gharama zangu tu nitakazotumia, lakini utaalamu wangu nautoa bure".

Makofi na kupeana mikono ya shukrani vilisikika.

"Sijui hii kazi unafikiri itachukuwa muda gani?", Kimani aliuliza.

"Mimi nitawafanyia kazi, nipeni muda", Willy alijibu.

"Wiki mbili?", Makwega aliuliza pia.

"Nitajitahidi".

"Basi tuonane hapa baada ya wiki mbili", Musoke aliagiza.

"Sawa".

"Lakini Willy Gamba atakuwa anawasiliana na mimi Kampala kwa kila hatua atakayofikia. Kama ikionekana kazi inakuwa bado baada ya hizo wiki mbili, nitawajulisha", Musoke alieleza.

"Sawa".

"Haya, asanteni sana wazee, tutaonana Mwenyezi Mungu akitujaalia baada ya wiki mbili. Sasa hivi ngoja niende na mzee Musoke akanikamilishie masuala ya mapesa", Willy aliaga huku akiwachekesha.

"Nilitaka kusahau. Tumekupatia nafasi ya kulala Impala, ukienda tu pale mapokezi watakupa funguo, tumelipia kila kitu, kazi kwako. Sijui kama utahitaji usafiri kesho kukupeleka uwanja wa ndege?", Temu alieleza na kuuliza.

"Hapana, nitajitegemea kwenda uwanja wa ndege".

Musoke alipoangalia saa ilikuwa saa kumi na nusu. Willy alipewa mkono wa heri na wajumbe wa PAM huku kila mmoja akimwombea mafanikio na usalama. Willy aliupokea mkono huo wa heri huku naye kimoyomoyo akiomba sala zao ziwe pamoja naye, kwani hawa walikuwa watu wenye roho za ubinadamu, ambao walikuwa wakitumia muda wao kujaribu kuwasaidia wengine bila malipo ya aina yoyote. Kweli Mungu awabariki.

Musoke na Willy aliondoka, wakaelekea Maunt Meru.

"Kesho umesema ndege saa ngapi?", Musoke alimwuliza Willy.

"Saa tatu asubuhi".

"Nije nikupeleke?".

"Hapana, nina marafiki wengi hapa watanipeleka".

"Na leo jioni tunaweza kula pamoja?", Musoke alimkaribisha chakula cha usiku.

"Hapana, nitakwenda kwa dada yangu jioni, alifiwa na mjukuu wake na nilikuwa sijapata nafasi ya kumsalimia na hii ndio nafasi pekee niliyopata".

"Umeua ndege wawili kwa jiwe moja".

"Bila shaka", Willy alijibu huku akijuwa kabisa kuwa angeondoka jioni ile. Willy kama kawaida yake, aliendelea kuonyesha kama angelala Arusha. Hii inaonyesha jinsi ambavyo Willy hamwamini mtu yeyote mara akishakuwa kazini.

"Huwezi kujuwa, kikulacho ki nguoni mwako, uzoefu wa siku nyingi umenifundisha", Willy alijisemea moyoni.

Walipofika Hoteli ya Mount Meru, walikwenda chumbani kwa Musoke na kuanza kuelezana tena. Kwa vile Musoke naye alikuwa na uzoefu wa siku nyingi na kazi ya upelelezi alijuwa Willy angetaka nini.

"Bwana Gamba, unajuwa kazi hii inaweza ikawa ngumu na ya hatari kuliko hata jinsi tunavyotegemea. Hivyo, jitayarishe kwa yote, nadhani unanielewa?", Musoke alimwuliza.

"Nakuelewa sana, kazi hii naichukulia uzito uleule wa kawaida, sintaipuuza hata chembe. Kwa kawaida uzoefu umenionyesha kuwa kwa kawaida kazi rahisi ndio hugeuka kuwa ngumu sana".

"Vizuri, mimi ninao wenyeji kule Rwanda, ambao nafikiri wanaweza kukusaidia kupata fununu za awali", Musoke alisema na kufungua mkoba wake na kutoa kitabu chake cha anuani. "Yuko rafiki yangu ambaye kwa miaka amekuwa akiipinga siasa ya chama cha MRND. Yeye ni mwanajeshi. Alikuwa kamanda katika jeshi la kumlinda Rais, lakini kwa vile hakukubaliana na sera yao, aliacha na kuanza kwa siri kueneza habari kwa vyombo vinavyotetea haki za binadamu jinsi serikali ya Rwanda ilivyokuwa inavunja haki za binadamu nchini humo. Wakati Rais alipouawa Aprili 6, 1994, yeye alikuwa Nairobi kuonana na Katibu wa Chama cha kutetea Haki za Binadamu ulimwenguni. Hata hivyo, huku nyuma mke wake na watoto wake sita na wapwa wake wawili, wote waliuawa tarehe 7, Aprili. Hii ina maana angekuwepo Kigali na yey vilevile leo angekuwa marehemu. Anakaa Kimihurura nyumba namba 168. Simu yake kwa bahati ni moja ya chache zinazofanyakazi sasa hivi na ni namba 50486. Yeye ni Mhutu.

"Umeishazungumza naye?", Willy aliuliza.

"Nitazubumza naye, tuna uelewano mzuri, na yeye anajuwa mengi kwa watu wachache waliokuwa wanaipinga serikali waliobaki. Na ujuwe huyu mtu alikuwa karibu sana na serikali ya Rwanda, na huenda karibu sana na Rais mpaka kufikia kuwa kamanda wa jeshi lake. Hivyo, anajuwa serikali ilivyoondolewa madarakani na RPF vizuri sana, na ndio sababu vilevile kumtafuta ili kumuua ili kuua ukweli wa mambo".

"Vizuri, nikifika Rwanda nitamtafuta kama nitamhitaji".

"Tumekupangia kwenye hoteli iitwayo Des Mille Collines. Hoteli hii ni maarufu maana wakati wa mauaji watu wengi, hasa wa mataifa ya nje, walijificha hapa na hivyo hata wanyarwanda waliokuwa wanatafuta ili kuuawa kati ya walionusurika ni wale waliobahatika kufika hoteli hapo. Hivyo, nayo itakupa fursa nzuri kupata fununu mbalimbali.

Vilevile ningependa umwone Padre mmoja ambaye tunafahamiana na yeye alinusurika kimiujiza baada ya mapadri, maburuda , watawa na watu wote waliokuwa kwenye kituo hicho cha dini kiitwacho Centre Christus, kuuawa na Wahutu wenye siasa kali. Padri huyu anaitwa Jean Marie Karangwa. Utapata mengi toka kwake vilevile".

"Bado yuko kwenye kituo hicho?", Willy aliuliza.

"Ndio yupo, na anajaribu kukianzisha upya. Na wa mwisho ambaye ningependa umwone ikiwa unahitaji msaada, maana huwezi kujuwa, unaweza kuwa kwenye hatari ambayo inahitaji msaada wa kiserikali, hasa kijeshi. Huyu ni rafiki yangu saana, tumekaa naye jirani mjini Kampala na ni mmoja wa makamanda wa RPF, mtu shupavu kama wewe na msomi kama wewe na kijana wa rika lako. Naamini mkionana mtashibana tu. ana roho safi sana. Anaitwa Col Thomas Rwivanga, namba yake ya simu 60314".

"Asante, nikihitaji msaada wake nitamtafuta", Willy alijibu.

"Utaondoka lini na kwa njia gani?", Musoke aliuliza.

"Mimi kesho kutwa nitakutafuta Kampala nikiwa Kigali kukujulisha nimefika".

Musoke hakuuliza zaidi maana alielewa maana yake. Kisha akatoa bahasha kubwa iliyokuwa na pesa za dola za Kimarekani. Idadi yake haikuzungumzwa, lakini bila shaka ilikuwa maelfu ya madola.

Baada ya kumpa mzigo huo walisimama na kuagana.

"Haya, nakutakia safari njema na kazi njema. Nakuombea heri", Musoke alimshika mkono akionyesha uchungu kidogo.

"Asante sana, tuombe Mungu", Willy alijibu na kuondoka.

Willy alipoachana na Musoke alikodi teksi pale nje ya Mount Meru Hotel na kuelekea Impala. Alipofika Impala alijitambulisha. "Naamini nina nafasi ya chumba hapa, naitwa Willy Gamba.

Msichana wa mapokezi aliangalia kwenye orodha yake ya majina kisha akaliona jina la Willy Gamba.

"Ndio baba, chumba 212", alijibu huku akitoa funguo na kumkabidhi.

"Una mizigo?".

"Hapana, huu mkoba wangu una kila kitu".

"Kila kitu?".

"Kila kitu nakuambia, utashangaa nikiufungua, mrembo zaidi yako atatokea".

Yule msichana akacheka na Willy akapandisha ngazi.  Alikifungua chumba na kukuta kidogo lakini kizuri sana. Aliangalia saa yake akaona ilikuwa saa kumi na mbili kasoro robo.

Alikwenda kitandani akatoa blanketi,  akaliweka pembeni na kufunua shuka na kutengeneza kama kwamba kulikuwa na mtu aliyelala pale.  Kisha, akauweka ufunguo kwenye kufuli la mlango kwa ndani, akachukua mkoba wake.  Akafungua mlango na kuurudisha bila kuufunga na funguo kwa vile aliziacha ndani makusudi na kutelemka chini.  Alipoangalia pale mapokezi na kuona wapokeaji wapo shughulini,  alichepuka na kutoka nje. Akelekea kwenye maegesho ya teksi na kukodi teksi kuelekea uwanja wa ndege wa Arusha.

Ilikuwa yapata saa kumi na mbili na robo alipofika uwanja wa ndege na kukuta ndege imeshatua tayari. Rubani wa ndege alimfuata na kumpokea mkoba wake.

"Habari za jioni?", Rubani alimshalimia.

"Za jioni nzuri asante".

"Huna mzigo zaidi?".

Sina,  ni huo huo".

Rubani aliufungua mlango wa ndege hii ya Tanzanair,  aina ya Cessina Mark 4, na kumkaribisha abiria wake huyu mmoja, ambaye walikaa pamoja kwenye viti vya mbele, na kisha akawasha injini  za ndege, na kuruka.

ITAENDEA 0784296253 

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU