KAZI IMEANZA
Baada ya
kuzungumza na Phillipe JKS alimpigia simu ofisa mmoja wa usalama aliyekuwa
anashughulikia maswala ya uchukuzi wa abiria. JKS ndiye aliyemsaidia sana ofisa
huyu kupanda hadi kufikia ofisa usalama mwandamizi.
"Mulamba",
JKS aliita baada ya simu kupokelewa.
"Ndiyo,
nani mwenzangu?".
"Pole
kwa kukuamsha, naona ulikuwa bado umelala, huyu ni JKS".
Mulamba mara
moja usingizi ulimtoka na kuinuka kabisa kitandani na kuketi kwenye ncha ya
kitanda.
"Ndiyo
mzee, hapana nilikuwa nimeamka ila bado nilikuwa najinyooshanyoosha tu kwani
jana nilichelewa kulala", alimjibu kwa woga. Ile sauti ya woga
ilimfurahisha JKS maana alipenda na kufurahia kutetemekewa.
"Hamna
neno, sasa sikiliza, hii ni amri toka juu kuliko hata mimi. Si unamjuwa Willy
Gamba?".
"Ndiyo
mzee, nani asiyemjua katika fani yetu hii", Mulamba alijibu.
"Amepewa
kazi toka ngazi za juu, na jana alienda Arusha na ndege za Shirika la Ndege
Tanzania. Kwa vile sasa hayuko tena kwenye ajira ya serikali, hii kazi amepewa
nje ya mipango ya kiserikali maana ni kazi nyeti na serikali haitaki itambulike
kuwa inahusika. Ila alitakiwa ajulikane yuko wapi kila wakati, lakini toka jana
jioni hajulikani aliko. Sasa imeamriwa tutumie ofisi yako tujuwe yuko wapi na
ripoti hiyo isiende kwa mtu yeyote ila mimi", JKS alimaliza.
"Hilo
nitalifanya sasa hivi mzee, ila nataka kujua alikuwa anatarajia kwenda wapi
baada ya kutoka Arusha?", Mulamba aliuliza.
"Baada
ya kutoka Arusha alitakiwa kurudi hapa Dar es Salaam, halafu anende Kigali.
Kuna ndege ya asubuhi sana ya ATC toka Kilimanjaro ambayo itaondoka saa moja,
kama yumo nipe habari, kama hayumo tafiti ujuwe anakuja Dar es Salaam na
usafiri gani, nipate habari haraka. Angalia usafiri wote mabasi, malori na
kadhalika.
"Usiwe
na wasiwasi mzee, nitakujulisha baada ya saa chache, tutampata tu. Tukimpata
tumfanyeje?".
"Usifanye
chochote, wewe eleza tu yuko wapi".
"Haya,
asante".
"Kwa
heri", JKS alikata simu.
Baada ya
kukata simu ya Mulamba, JKS alipiga simu Paris kwa Jean na kumweleza mambo yaliyotokea
Arusha na hadhari aliyokuwa amechukuwa tayari. Jean, akiwa bado na usingizi
kwani Paris ilikuwa yapata saa kumi na nusu za asubuhi, tulikuwa tunapishana
saa mbili.
"Nataka
utakaponipigia tena simu unieleze kuwa tayari keshauawa, vinginevyo usinipigie
simu mpaka utakapofanikiwa kazi hiyo. Natuma pesa leo asubuhi kupitia kwa yule
rafiki yangu mwenye kampuni ya kitalii ya Concord Tours zikusaidie kukamilisha
kazi. Vilevile nitawapigia simu na marafiki zangu wengine huko Afrika Mashariki
wakupe msaada wowote utakaohitaji", Jean alimalizia na kukata simu bila
bila kumsubiri JKS ajibu.
Kwa mara ya
kwanza katika maisha yake JKS alisikia woga. Alizijua nguvu za Jean na akajuwa
itabidi atimize hii kazi, vinginevyo mambo yangeweza kumgeukia. Alifikiria jinsi
Jean alivyokuwa amemwahidi kumsaidia kuunyakuwa urais wa Tanzania na alikuwa
anaujuwa uwezo wa Jean kuifanikisha azma yake hiyo. Na dhamira ya JKS kuwa Rais
ilizidi vitu vingine vyote, lakini leo huyu Willy Gamba angeweza kumfanya akose
nafasi hii. Asubuhi hii alisikia jasho la baridi likimtiririka mgongoni na
kujisemea kwa sauti. "Kwa kila hali lazima aondoke".
Bila kujua
amesema kwa sauti kubwa mke wake aliyekuwa amelala bado alishtuka na kuuliza.
"Unasemaje?".
"Hapana,
sijasema kitu", JKS alijibu.
Mke wake
alimjua sana. Hivyo, akanyamaza lakini alijuwa mzee alikuwa anasumbuliwa na
kitu fulani.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment