KAZI IMEANZA
II
Willy alitua
kwenye uwanja wa ndege wa Mwanza mnamo saa mbili na nusu za asubuhi. Asubuhi
kabla hajaondoka nyumbani alimpigia simu rafiki yake mmoja ambaye alikuwa na
wadhifa wa juu ndani ya Chama cha Msalaba Mwekundu na kumwomba msaada kati ya
ndege zao zilizokuwa Mwanza moja impeleke Kigali. Willy aliwahi kukisaidia sana
Chama hiki, na huyu rafiki yake aliona bahati sana kupata fursa kama hii ili
nae alipe angalau fadhila kidogo za Willy kwa yote aliyowahi kuwatendea.
"Bila
shaka Willy, sasa hivi nitapiga simu Mwanza na hiyo saa mbili na nusu
unayotegemea kufika Mwanza utakuta ndege ndogo ya injini mbili aina ya Cessina
yenye namba MMT 3 ikikusubiri. Sisi tunaruhusiwa bila matatizo kutua Kigali
kutokana na hali ilivyo Wilayani Ngara. Hivyo, huna haja ya kuhangaika kupata
kibali cha kutua, hicho sisi tunacho na utakuta maofisa wetu pale Mwanza
wameshawasiliana na Kigali", yule rafiki yake Willy alieleza.
"Nitafurahi
sana, na kama vilevile mtawaeleza kuwa mimi ni afisa wenu", Willy
aliongezea.
"Bila
shaka", rafiki yake alijibu huku akicheka maana alijua Willy haendi Kigali
bure.
Kwa hiyo,
Willy alipotelemka ndani ya ndege ya kukodi ya Tanzanair alikuta ndege ya Chama
cha Msalana Mwekundu iko tayari.
"Ina
maana mimi sasa nitarudia hapa?", rubani wa Tanzanair alimuulizia
alipomwona anashuka na mfuko wake.
"Ngoja
kidogo", Willy alimjibu.
Willy
alikwenda mpaka kwenye ile ndege na kumkuta rubani na ofisa mmoja wa Msalaba
Mwekundu wakimsubiri Willy.
"Karibu
mzee", wote wawili walitamka kwa pamoja Willy akawapa mikono kuwasalimia.
"Asanteni
sana", alijibu.
"Sisi
tuko tayari, ila tu tunaomba uende na ndugu yetu mmoja ambaye anaenda huko
vilevile kikazi", yule afisa alimwambia willy.
Willy
alimwangalia yule jamaa, na kumwona ni wa makamu yake na wa umbo lake.
"Sawa,
lakini ningeomba aje na ile ndege ndogo ambayo nimekuja nayo ili rubani awe na
mtu wa kuzungumza nae, maana hiyo nayo inakuja Kigali, ila kwa sababu lazima
ijaze mafuta na kukaguliwa kidogo ndio sababu imebidi mimi nikifika tu hapa
nipate ndege nyingine kwa vile nina miadi maalumu ya kiserikali pale uwanja wa
Kigali na mtu ambaye ataondoka saa moja kuanzia sasa", Willy alieleza.
"Basi,
vizuri sana. Je, ndege yako ina vibali vyote vya kutua?", yule ofisa
aliuliza maana alijua jinsi hali ilivyokuwa uwanjani pale Kigali.
"Hamna
taabu, kila kitu kipo", Willy alijibu, kisha akaenda kwa rubani wa ndege
yake.
"Sasa
ukishajaza mafuta utakuja na yule bwana pale, naye anakuja Kigali.
Ukishamshusha tu basi wewe urudi", Willy alimweleza.
Yule rubani
alishangaa kwanini wasitumie ndege moja badala ya ndege mbili. Lakini kwa vile
haikuwa shughuli yake na kwa vile alikuwa ameagizwa kwenda mpaka Kigali aliamua
kubaki ameshangaa lakini atekeleze wajibu wake.
"Sawa
mzee", yule rubani alimjibu huku sauti ikionyesha mshangao. Willy alitoa
dola mia za kimarekani, akampa.
Tabasamu
safi likaonekana usoni mwa rubani.
"Asante
sana mzee", alijibu tena na kupeana mikono ya kuagana. Willy alikwenda
kwenye ndege, na rubani wa Chama cha Msalaba Mwekundu akaiondoa ndege kuelekea
Kigali ikiwa yapata saa tatu kasoro robo. saa za asubuhi.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment