MIGUU YA
NYOKA
Willy
alipowasili kwa Col. Thomas Rwivanga, alimkuta anamsubiri. willy alikuwa
amemweleza kuwa angekuwa anaendesha gari la Msalaba Mwekundu na angekuja peke
yake bila Vicent. Col. Rwivanga alikuwa
amemweleza njia ya kupita mpaka huko nyumbani kwake, Kimihurura.
Col.
Rwivanga aliposikia mwungurumo wa gari alitoka nje na kwenda kumpokea Willy.
"Habari
yako?", Col. Rwivanga alimsalimia Willy huku akimpa mkono.
"Safi,
na wewe?", Willy alimjibu.
"Safi
kabisa, nafurahi sana kuonana na wewe, Mzee Musoke amenieleza habari zako, nami
nilikuwa na shauku kubwa ya kukutana nawe. Karibu ndani", Col. Rwivanga
alimkaribisha Willy.
"Asante
sana, nimekaribia", Willy alijibu huku akiingia ndani na kuketi.
"Nikupe
kinywaji gani?|".
"Klabu
soda inatosha", Willy alijibu.
Col.
Rwivanga alileta Klabu soda mbili na kuzifungua, wakaanza kunywa.
"Ehee,
habari ya maisha?", Col. Rwivanga aliuliza.
"Safi,
naamini Mzee Musoke amekueleza kwanini niko hapa".
"Ndio
amenieleza".
"Imebidi
nikuone mapema maana kuna jambo lililotokea ambalo linaonyesha kuwa katika
uongozi wenu kuna mtu aliyejuwa kuwa mimi nimo ndeani ya ile ndege
iliyotunguliwa leo asubuhi, akiwa na nia ya kuniua, bahati nzuri sikuwemo ila
nilitakiwa kuwemo kwenye ndege hiyo. Na ninafikiri yeyote yule aliyeagiza hiyo
ndege itunguliwe anaamini kuwa mimi sasa ni marehemu", Willy alimweleza
Col. Rwivanga ambaye wakati huo alikuwa akimwangalia kwa mshangao mkubwa.
"Hivi
swala unaloijia hapa ni nyeti kiasi hicho, mpaka wanataka kukuua! Mimi Mzee Musoke
aliponieleza, sikutegemea kama kunaweza kuwa na hatari yoyote, maana wewe
unakuja kutathimini tu hali ya mambo yalivyotokea mpaka kufikia watu wengi
namna ile kuuawa. Lakini sasa inaonekana kuja kwako kumetia watu wasiwasi na
wameamua kukumaliza kabisa hata hujaanza huo uchunguzi. Ndugu Gamba hii
inaonekana kuna jambo kubwa ambalo hata sisi hatulifahamu. Hii ni hatari na ni
hatari kubwa", Col. Rwivanga alijibu.
"Je,
unaweza kujuwa ni nani au ni vipi ile ndege ilitunguliwa?, Huenda tukaanzia
hapo ndipo tutajuwa hasa ni nani anahusika na kwa sababu gani?", willy
aliuliza.
"Taarifa
niliyopata kuhusu tukio hilo kwenye kikao cha makamanda wa jeshi, ambayo
imetolewa na Col. Gatabazi, ambaye ndiye mkuu wa utawala jeshini, inasema ndege
hiyo ilipoitwa kwenye rada ijitambulishe haikufanya hivyo. Kwa hiyo Luteni
Silasi Biniga, ambaye ndiye anaongoza wanajeshi wanaolinda uwanja alimtaarifu
Meja Juvenal Mukama, Mkuu wa Kikosi cha Mizinga kinacholinda mji huu, ambaye
alitoa amri kuwa kama inakaribia kutua na bado haitoi taarifa yoyote
itunguliwe. Na ndivyo ilivyofanyika. Baada ya kujuwa kuwa ilikuwa ndege ya
kukodi ya kampuni ya kukodisha ndege ya Kitanzania, habari zilipelekwa Dar es
Salaam, na habari tulizopata toka Wizara ya mambo ya Nje ya Tanzania ni kwamba
ndege hiyo ilikuwa imekodiwa na mtu mmoja kwa jina la Juma Omari
aliyejitambulisha kama mwandishi wa habari na masuala yote ya kupata vibali vya
kutua alifanya mwenyewe. Hivyo, serikali ya Tanzania inaunga mkono kutunguliwa
kwa ndege hiyo ambayo imeingia anga ya watu bila kibali wala kujitambulisha na
huku rubani na kampuni hiyo ikijuwa hali ya hatari iliyomo nchini Rwanda.
Taarifa hiyo tumeipata jioni hii na serikali ya Tanzania imezidi kusema
itaichukulia hatua kampuni hiyo ya ndege kwani inaweza kuwa inatumiwa na maadui
wa Rwanda na kuweza kuleta uhusiano mbaya kati ya nchi zetu rafiki", Col.
Rwivanga alieleza na ukawa ni wakati wa Willy kushangazwa na maelezo hayo.
"Rafiki
yangu, hapa kuna jambo kubwa maana sababu ya kutunguliwa ndege hii ni moja tu,
ambayo ni kutaka kuniua mimi. Lakini sasa maelezo ya makamanda wenu. Col.
Gatabazi na maelezo kutoka Dar es Salaam, yamenichanganya kabisa na nahisi kuna
kitu kikubwa tusichokijua", Willy alijibu.
"Sasa
tufanye nini?", Col. Rwivanga alimwuliza.
"Kwanza,
nataka aliyetaka kuniua aendelee kufikiri kwamba ameniua. Pili, huenda huyu Lt.
Silasi Biniga anaweza akawa na habari zinazoweza kutusaidia kufumbua hiki
kitendawili hivyo anafaa kuonwa na kuulizwa", Willy alijibu.
"Basi
niache huyu mimi nitamwuliza", Col. Rwivanga alijibu.
"Hapana,
niachie mimi, swala hili linaweza kuwa vilevile linaugusa uongozi wenu. Mimi
nikiwa mtu baki naweza kupata ukweli bila kuleta kasheshe sasa hivi. Ni lazima
tujitahidi tujue undani wa jambo hili maana ni zito. Naomba tu unieleze huyu
Luteni Biniga anakaa wapi nami nitaenda kumwona", Willy alijibu.
"Inaweza
kuwa hatari kwako, unajuwa hawa watu ni wanajeshi safi", Col. Rwivanga
alimwasa Willy.
"Usijali,
hatari ndio jina la kazi yangu", Willy alijibu.
Wote
wakacheka, maana Musoke alikwishampa Col. Rwivanga maelezo kamilifu kuhusu
Willy na uwezo wake.
"Sawa,
huyu Luteni Biniga anakaa barabara ya tatu tu kutoka hapa kwangu, sehemu hiihii
ya Kamihurura". Kisha akamweleza mtaa na nyumba ilipo.
"Sasa
hivi naanza kushangaa, wakati wanajeshi wa cheo chake wengi bado wako kambini
na wengine wako huko Ndera ambako ndiko kuna nyumba za maofisa wa ngazi ya
chini yeye anakaa sehemu ambayo wanakaa maofisa wa ngazi za juu. Sijui huenda
ikawa tu bahati yake", Col. Rwivanga alisema kama vile anajisemea
mwenyewe.
"Nafikiri
nikionana naye nitajua. Naona niende kama saa tatu hivi. Nitaacha gari hapa na
kwenda kwa miguu", Willy alisema.
"Uamzi
wako. Kwa vile bado kuna muda mpaka saa tatu ngoja nitengeneze chakula
kidogo", Col. Rwivanga alieleza.
"Na mimi
nitakusaidia kupika, kupika ni moja ya starehe zangu", Willy alieleza huku
wakiinuka kuelekea jikoni.
ITAENDELEA 0784296253
Comments
Post a Comment