MIGUU YA
NYOKA
III
Col.
Gatabazi alikuwa kati ya watu wa kwanza kufika kwa Luteni Silas Biniga, maana alikuwa akiishi nyumba ya nne tu kutoka pale. Alipofika hakuamini macho na akili yake ilishindwa kukubali. Watu wote hawa waliouawa walikuwa watu makini katika kundi lake, watu ambao alijua ndio wangemsaidia kuchukua madaraka muda
utakapofika. Hili jambo lilimshitua sana. Watu wote hawa walikuwa askari
shupavu, jasiri na waliojuwa kazi yao vizuri.
Yeyote yule aliyefanya kitendo hicho
hakuwa mtu wa kawaida na kama ni kikundi, hakikuwa kikundi cha kawaida. Hawa
watu watatu walikuwa na uwezo wa kuangamiza kikosi kizima cha jeshi la maadui
lakini leo wameuawa kirahisi na wote kwa pamoja! Suala hili lilimshitua sana
Col. Gatabazi, akaingiwa na woga na wasiwasi.
Gari la
jeshi lenye king'ola, lilikuwa tayari limefika pale likiwa na askari wa doria
wa sehemu zile, askari hao walifika mara baada ya kusikia milio ya risasi.
"Vipi
hamjaona au kukutana na mtu au watu wowote waliofanya kitendo hiki?", Col.
Gatabazi aliwauliza wale askari wa doria kwa ghadhabu.
"Hapana
afande, kote hapa ni shwari", mmoja wapo alijibu.
"Haiwezekani
kuwa shwari wakati maafisa wanaotegemewa kama hawa wameuawa hovyohovyo
hivi", Col. Gatabazi alieleza tena kwa ukali.
"Huenda
wameuana wao wenyewe afande", askari wa pili wa doria alijibu.
Col.
Gatabazi alimwangalia kwa jicho baya mpaka yule askari akarudi hatua moja
nyuma.
"Chukueni
hizi maiti pelekeni hospitali na poteeni hapa mara moja", Col. Gatabazi
aliamrisha mara moja.
Col.
Gatabazi alirudi nyumbani kwake ili apige simu Ufaransa. Alipofungua mlango wa
mbele aliukuta uko wazi. Alishituka, akatoa bastola yake tayari kukabiliana na
lolote ambalo lingetokea mbele yake. Alifungua mlango kwa ghafla huku bastola
yake ikiwa tayari tayari.
"Vipi!
mbona wasiwasi?", Bibiane alimuuliza huku akiweka mguu mmoja juu ya
mwingine pale sebuleni alipokuwa ameketi.
"Hujui
kumetokea mauaji mabaya sana usiku huu na vijana wetu watatu wameuawa?",
Col. Gatabazi alihoji huku akirejesha bastola yake kwenye mkoba wake na macho
yake yakiangalia mapaja ya Bibiane ambayo yalikuwa yameachwa wazi kwa kitendo
chake cha kuweka miguu juu ya mwingine na kufanya nguo yake iliyokuwa fupi na
ya kubana kuyaacha wazi.
Bibiane
Habyarimana alikuwa mtoto wa Kinyarwanda ambaye baba yake alikuwa Mhutu na Mama
yake chotara wa Kitutsi na Kifarasa. Alikuwa msichana aliyeumbika kwa sura na
mrembo katika warembo. Alikuwa na urefu wa futi tano na inchi nane, hivyo,
alikuwa mwanamke na urefu wa kutosha. Alikuwa na nywele ndefu za singa, macho
makubwa ya blue, mashavu ya kumimina, pua ya kuchonga, midomo ya tasi, meno
meupe yaliyopangika na kuacha mwanya kwenye safu ya juu. Hakika, alikuwa
kapendelewa na muumbaji. Mwili wake mzima ulikuwa na muundo wa nyigu, juu
mwembamba chini kajaa, akimalizia na miguu minene ivutiayo macho.
Ilimchukua
Col. Gatabazi muda mrefu kupata la kusema maana kila alipoonana na msichana
huyu alijikuta ulimi wake unakuwa mzito, anashindwa hata kusema. Mara nyingi
alipatwa na kigugumizi kwani moyo ulimwenda mbio.
"Aliyewaua
mimi nimemwona", Bibiane alieleza bila wasiwasi utafikiri alikuwa
anazungumza kitu cha kawaida tu.
"Unasemaje?",
Col. Gatabazi alimuuliza kwa mshangao.
"Aliyewaua
nimemuona mimi. Nilikuwepo alipofika pale kwa Luteni Biniga", Bibiane
alijibu tena kwa utulivu, kisha akasema, "Hamna hata kinywaji humu
ndani". Kila wakati Col. Gatabazi alishangazwa na tabia ya huyu binti.
"Kinywaji
kipo, huenda kweli tunakihitaji maana sasa wewe unazidi kunichanganya",
Col. Gatabazi alisema na kuelekea kwenye kabati la vinywaji akatoa chupa ya
whisky na gini, akaleta barafu na glasi mbili.
"Utakunywa
nini?".
"Whisky
niwekee barafu tu usiiharifu na maji".
"Sawa
mama, ehee unamaje eti ulikuwepo kwa Luteni Biniga?", Col. Gatabazi
aliuliza kwa shauku ya kutaka kujua.
Bibiane
alimweleza kwa kirefu yaliyotokea pale kwa Luteni Biniga na kumalizia,
"Watakati natoka ndani walikuwa wakimwuliza maswali pale nje, awaeleze
yeye ni nani. Sikuwa na wasiwasi maana nilijuwa yule kaisha. Mbele ya wale
wanaume hakuna ambaye angefanya kitu. Niliposikia risasi zinalia ile ya kwanza
nilijuwa kauawa, lakini niliposikia milio ya risasi inazidi nikawa na wasiwasi
nikarudi haraka kuchungulia na nikaona uliyoyaona, lakini mimi nilikuwa na
bahati ya kumwona akiruka ukuta upande ule mwingine, akapotelea gizani. Yule ni
mwanaume wa shoka na hapa kazi ipo, sina shaka yule ni Willy Gamba kama Jean
alivyomwelezea. Hivyo, umeshindwa mtihani wako wa kwanza huyu mtu hakufa ndani
ya ile ndege mliyoitungua. Fanya utafiti, utakuta amekuja na ndege nyingine,
kakuzidi maarifa, tayari alishajuwa ni Luteni Silas Biniga aliyeamrisha ile
ndege kupigwa. Mtu huyu ni hatari, mbona ni hatari sana! Kazi kwako Gatabazi.
Kama unataka Uras kwanza inakubidi huyu mtu ummalize. Hizi habari
zitamsikitisha sana Jean, wewe unajua.
"Usipommaliza
haraka basi ujuwe wewe umekwisha kwani atakuumbua na RPF watakumaliza na
utakuwa umewaangamiza Wahutu", Bibiane alimalizia na tabasamu la mauti.
Woga
ulimwingia Col. Gatabazi maana naye alihisi kuwa huenda yule alikuwa Willy Gamba.
Rwanda hakukuwa na mtu mwenye uwezo kama huo. Jean alimweleza kwa kirefu uwezo
wa huyo Willy Gamba na sasa aliudhihilisha. Vilevile, alijuwa Jean
angekasirishwa sana kuona huyu mtu amejipenyeza mpaka kuleta maafa makubwa
hivi.
Mtu wa kuweza kumsaidia kumweleza Jean mpaka amwelewe na kumsaidia katika
mapambano na mtu huyu alikuwa ni Bibiane. Ingawa alikuwa akimtamani sana
Bibiane, lakini alikuwa mwangalifu sana asimguse maana alijuwa siku moja
angeweza kumtumia.
Bibiane
alikuwa karibu sana na Jean alikuwa mpenzi wake lakini vilevile Bibiane alikuwa
mhitimu wa fani ya upelelezi na usalama na akiwa amesomeshwa kwa msaada wa
Jean. Jean alikuwa akifanya mambo yake kwa ufasaha. Alihitaji kuwa na mtu
Afrika Mashariki na Kati ambaye angeangalia mambo yake bila kuhisiwa. Pamoja na
kuwa alikuwa ametumbukia katika lindi la mapenzi na Bibiane, lakini kwa upande
mkubwa alimtumia Bibiane kufanikisha mambo yake yaliyokuwa yakimletea maslahi.
Sababu hizi ndizo zilizomfanya Jean amugharamie Bibiane mafunzo ya hali ya juu
ya upeleelezi na kweli msichana huyu alifuzu vizuri na alikuwa mjuzi. Idara ya
upelelezi na usalama ya Ufaransa inayoshughulikia usalama wa nje (DGSE)
ilimuongezea ujuzi msichana huyu na mara nyingi walimtumia katika kazi zake.
Ni huyu
msichana, kwa kutumwa na DGSE, alikisambaratisha kikundi cha wanajeshi
waliotaka kuipindua serikali ya Hassan Gouled wa Djibouti na kufanya wakamatwe,
kwani siri zao zote alitoa wa serikali kupitia DGSE mpaka leo haikujulikana
jinsi alivyoweza kupata ushahidi huo ambao hata kikundi hicho cha wanajeshi
kilibaki kimepigwa na butwaa. Msaada huo wa Bibiane kwa DGSE ulimwongezea Jean
uhusiano wa karibu.
Hivyo hata Bibiane alitumia idara hiyo kwa kumsaidia katika
mambo yake. Ni Bibiane aliyekuwa kiungo kikubwa kati ya Jean na familia ya
Rais. Ingawaje na yeye aliitwa Bibiane Habyarimana hakuwa na uko na Rais kwani
familia za Kinyarwanda hutumia jina lake na siyo jina la ukoo kama jamii
zingine.
vilevile,
msichana huyu ndiye aliyekuwa kiungo kikubwa na wakubwa wengine wa serikali katika
Afrika. Kutokana na umbile na sura yake ya kuvutia, ambayo kila siku
ilimuonesha kuwa msichana mdogo asiyezidi umri wa miaka kumi na minane, hakuna
aliyeweza kumuhisi kama mmoja ya watu hatari waliokuwa kiungo cha uhaini na
ugaidi kati ya wakuu wa serikali, wafanyabiashara na magaidi wa Ulaya.
Inasemekana wakati wa mkutano wa amani uliofanyika mjini Arusha, Tanzania,
Bibiane alikuwapo kama mkalimani.
Baada ya
mkutano huo, rais alimpa nafasi aondoke nae kwenye ndege yake, kwani alikuja
kama mkalimani wake lakini Bibiane alikataa na kuondoka na Jean kwa barabara
kupitia Nairobi, nchini Kenya. Inasemekana alijua nini kingetokea, kwani yeye
aliingia kwa ndege ya jeshi la Ufaransa akitokea Nairobi, mara tu baada ya
marais kuuawa tarehe 6 aprili Bibiane alisaidia kumchukua mke wa rais na
familia yake ya watu kumi na watano na kuwapeleka Ufaransa.
Pia.
Inasemekana. Kwa kusaidiana na Jean aliwawezesha Protais Naimana na Feldinand
Zigilanyilazo kuwapatia visa ya kusafiria na kuwawezesha kwenda Ulaya. Hivyo.
yote hii inaweza kukuonyesha jinsi gani msichana huyu mwenye umri wa miaka
ishirini na saba tu alivyoweza kufanya mambo makubwa. Alikuwa msichana hatari
sana.
Lazima
tumweleze Jean hali halisi", Col. Gatabazo alimweleza Bibiane.
"Piga
simu!".
"Sawa.
Lakini uzungumze nae kwanza".
"Sawa!",
Bibiane alijibu. Alimwangalia Col. Gatabazi. Akaona kuwa ameingiwa na woga.
Bibiane aliwaponda sana wanaume walioonekana waoga. Kwa mara ya kwanza
alimponda Col. Gatabazi, aliwapenda sana watu jasiri mwanaume yeyote shupavu
aliifanya damu yake ichemke na kuchochea tamaa zake za mwili. Lakini mwanaume
mwoga hata awe mzuri na sifa aina gani alimtia baridi. Mara hii alihisi baridi
na kumchukia Col. Gatabazo mawazo yake yalitembea na kumfikiria Jean. Ile
kumfikiria tu alihisi damu yake ikichemka. Kwake Jean ndiye alikuwa mfano wa
mwanaume ampendaye, jasiri, shupavu anayepata kile anachokitaka hata iwe kwa
gharama gani, hata ikibidi kuhatarisha maisha yake.
Ndivyo Jean
alivyokuwa. Bibiane alimpenda Jean kikwelikweli. Ingawa Jean alikuwa mzungu,
lakini alikuwa mzungu wa aina yake. Alijuwa kupenda na alijuwa jinsi ya
kumfurahisha mwanamke mpaka kumaliza haja zake za kimwili. Lakini zaidi ya yote
alimpenda kwa ujasiri na ushupavu wake katika mambo yake. Iwe biashara, iwe siasa yeye alikuwa ndie
bingwa wa mchezo.
Alifikiria jinsi watu wenye vyeo vikubwa, wakuu wa nchi,
matajiri walivyo yeyuka kama barafu mbele ya Jean kila alipopambana nao. Kila
siku ndiye aliyetokea kuwa mshindi. Hata rais alipojaribu kumgeuka na kukabiliana
na mambo kinyume na matakwa yake, Jean aliibuka mshindi na rais akapoteza
maisha. Hata hali ya sasa ya Rwanda, kuwepo RPF, ilikuwa kata ya mbinu zake. Na
Bibiane aliamini kabisa kuwa hii ilikuwa ni mipango yake ili baadae aiondoe
serikali ya RPF na kumuweka mtu wake Col. Gatabazi. Mwanzo Bibiane alirudi kwa
Col. Gatabazi.
Alimfikiria na kisha akatambua mtu kama yeye ndiye angewafaa
yeye na Jean, mtu mwoga, mtu anaependa fedha, mtu ambaye anafanya kile ambacho
angeambiwa. Kiongozi kama viongozi wengine wa Afrika, mtu anayejifikiria yeye
na wala sio nchi au watu wake, mtu mbinafsi, kama walivyo watawala wengi wa
kiafrika, Col. Gatabazi alifaa sana kutawala Rwanda.
"Njoo
Jean yupo kwenye simu," Col. Gatabazi alimshtua Bibiane kutoka kwenye
lindi la mawazo.
"Oh
asante sana"" alijibu.
"Mpenzi
hujambo?" Bibiane alimsalimia Jean.
"Sijambo,
pole na matatizo huko," Jean alijibu.
"Col.
amekueleza?"
"Amesema
wewe ndiye utanipa safi!"
"Una
maana sikupagi safi?"
"Wacha
masihara huu si wakati wake. Hebu nieleze imekuwaje?"
"Huwenda
na mimi ningekuwepo ningekuwa nimekufa," Bibiane alijibu.
"Sawa
tu hiyo ingekuwa kifo kazini," Jean alijibu kwa sauti kavu.
Mara Bibiane
akasikia damu yake inasisimka kwani alitaka mwanamume kama huyu asiye na
huruma. Huyu ndiye aliyekuwa mwanamume wa kiwango chake.
"Yaani
ningekufa asingejali."
"Bila
shaka nigejali, lakini kama ungekufa katika mstari wa kazi ni vizuri zaidi kuliko
kufa kibudu," Jean alijibu na kuendelea, "Hebu nipe imekuwaje".
Bibiane
alichukuwa muda kumwelezea jinsi mambo yalivyotokea.
"Yaani
huyu Willy Gamba umemuona kwa macho yako?.
"Ndiyo
kwanza sikumtilia maanani sana, nilishtuka kuwa ni yeye baada ya kazi aliyokuwa
ameifanya. Mwanzoni nilifikiri ni ka-Inyezi kalikopata fununu ambako vijana
walikuwa tayari kushughulika," Bibiane alijibu
"Lazma
umsaidie Col. Gatabazi kummaliza huyu mtu, Na mimi nitafanya mipango ya
kukupeni msaada wa watu wenye ujuzi wa juu wawasaidie kumuondoa huyu funza
anayetaka kula nyama yetu," Jean alijibu.
"Ukisema
wewe sisi tutatekeleza, tunaomba hua msaada wako haraka maana hata siye tuna
wasiwasi ," Bibiane alijibu.
"Usiwe
na wasiwasi, unajua watu kama huyo Willy Gamba ndio nawataka mimi,"
"Najua
Jean, wewe tena! Bwana nakuwaza, nataka nije huko unikumbatie, najua huwezi
kuja huku sasa!. Bibiane alijibu kwa sauti ya mahaba.
"Baada
ya kazi hiyo ya Willy Gamba tuonane Nairobi hata mimi nakutamuni sana,"
Jean alijibu.
"Haya kazi
kwanza."
"Halafu
kama kazi," Jean alimalizia na kumuomba Col. Gatabazi tena.
"Kwaheri
mpenzi!"
"Kwaheri
Bibiane. Col. Gatabazi atakupa mipango yote," Jean alimalizia.
Jean
alipozungumza na Col. Gatabazi alimweleza mipango yake ya kummaliza Willy
ambayo ilikuwa ikiendelea kichwani mwake.
"Nafikiri
mawazo yako ni sahihi tutafanya hivyo. Asubuhi nitawasiliana na wewe,"
Col. Gatabazi alijibu.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment