NGUVU YA RUSHWA
III
Simu
ilipoita Jean alikuwa amelala. JKS alikuwa amemweleza kuwa vijana walikuwa wamefika
salama na kazi ya kumsaka na kumuua Willy Gamba ilikuwa ifanyike usiku ule. Alikuwa amefikiria jinsi Bibiane
angeshangaa sana baada ya kuelezwa kuwa Jean ndiye aliyetoa amri ya yeye
kumuua. Jean alikuwa mtu aliyefurahia uovu, alikuwa mtu katili afadhali ya
mnyama. Alifurahi kusikia mtu akipata maumivu, na hapo ndipo roho yake
ilipopata faraja. Pamoja na miaka yoye sita aliyokaa na Bibiane, utafikiri
walikuwa mtu na mke wake, yaani mume na mke, bado alipomweleza Col. Gatabazi
kuwa lazima Bibiane auawe moyoni mwake hakusikia masikitiko. Kilichomfurahisha
na kumridhisha ilikuwa ni pesa na nguvu ya pesa, na si mapenzi. Jean aliabudu
pesa kwani aliamini kuwa pesa ndizo zilizompatia uwezo alionao duniani.
Kwa kutumia
pesa, Jean aliweza kuwakamata wakuu wa nchi nyingi duniani, hasa katika Afrika
na Asia, lakini vilevile viongozi wa ngazi za juu katika serikali za nchi za
Ulaya. Alipata kila alichokitaka kwa kutumia pesa. Hivyo, simu ilipolia alijua
analetewa habari njema za kuuawa kwa Bibiane na Willy Gamba maana alikuwa
amesema alikuwa amesema wakishauawa aelezwe. Kila alipopewa taarifa ya kuuawa
kwa mtu alipata faraja ndani ya moyo wake, Ndio sababu maelfu ya Watutsi
walipouawa alisikia raha isiyo kifani. Hakika mtu huyu alikuwa mgonjwa, tena
mgonjwa sana!.
"Jean",
aliitikia kwenye simu.
"Col.
Gatabazi hapa".
"Sema
Col. Gatabazi".
"Kazi
imeharibika".
"Nini?".
"Kazi
imeharibika. Vijana wote wameuawa. Bibiane yuko hai na ameokolewa na Willy
Gamba. mimi na Nkubana tunaondoka kwenda Kibunda, hatuna muda maana wakati
wowote wataanza kutusaka, afadhari tuyaandae majeshi yetu tayari kwa
vita", Col. Gatabazi alimwambia Jean.
"Ilikuwaje",
Jean aliuliza kwa sauti ya kukata tamaa. Col. Gatabazi alimweleza kwa ufupi
kama Nkubazi alivyomweleza.
"Basi
tuonane kesho Goma, saa tisa mchana nitakuwa huko, natarajiwa kuja na ndege
yangu, lakini nitampitia rafiki yetu Kinshasa", Jean alieleza na kukata
simu kabla hata Col. Gatabazi hajajibu kitu.
Jean
alipokata simu ya Col. Gatabazi, alitumia muda huo kupiga simu Zambia, Zaire,
Afrika Kusini, Angola, Kenya na kumalizia Tanzania.
"Umenipata
JKS?", Jean alimuuliza JKS baada ya kumweleza yote yaliyotokea na
maelekezo mengine huku JKS akipatwa na shinikizo la damu.
"Nimekupata",
JKS alijibu kwa sauti ya kutetemeka.
........................................................................................................................
NGUVU YA
RUSHWA
IV
Bibiane
alipomaliza kuoga alimkuta Willy amemtengea kikombe.
"Kahawa
au chai?"
"Kahawa."
Willy
alimmiminia kahawa na alipotaka kumwekea sukari Bibiane alikataa.
"Bila
sukari," alisema.
Kwa mara ya
kwanza vilevile Bibiane alimuangalia Willy vizuri na kumuona mwanaume mzuri
sana, na alipofikiria namna alivyowasambaratisha akina Xavier na kundi lao,
mwili wake mara moja ulisisimuka. Halafu, palepale akamfikiria Jean na jinsi
alivyompenda na kumfanyia kila kitu lakini akaamua kumuua. Hasira ilimpanda
sana, na akaapa kiroho kuwa kwa vile yupo hai atalipiza kisasi.
"Unafikiri
nini?" Willy alimwuliza Bibiane.
"Ahera."
"Umeshapona
sasa?".
"Xavier
alisema mimi na wewe tutaonana ahera baada ya masaa machache, akili yangu
inafikiri huenda tupo ahera." wote walicheka.
"Uko
tayari kuzungumza lolote," Willy alimuuliza Bibiane huku sauti yake ikiwa
imebadilika ghafla na kuwa sauti yenye uzito fulani.
"Niko
tayari, nimekuambia kila unachotaka," Bibiane alijibu kwa sauti ya mahaba.
"Wewe
ni nani?" Willy alimwuliza.
"Mimi
naitwa Bibiane Habyarimana, ni Mnyarwanda, na wewe?".
Willy
alishtuka namna alivyo mjibu na kuzidi kuimarisha hisia zake kuwa huyu msichana
vilevile alikuwa si mtu wa hivihivi ila alikuwa mtaalamu katika nyanja kama
yake. Mara ya kwanza alipohisi, ilikuwa jinsi alivyojirusha nyuma ya kochi pale
nyumbani kwake baada ya yeye kuwapiga risasi wale watu wawili, na alivyochupa
dirishani kumfuata Xavier. Kwanza alifikiri alikuwa na mafunzo ya kijeshi tu,
lakini kutokana na jinsi ya majibizano yao aligundua alikuwa na utaalamu zaidi.
"Willy
Gamba, Mtanzania," alijibu na wote wakaangaliana kama wanapimana saizi.
"Ningependa nijue historia yako nzima, na usinifiche kitu, mpaka kufikia
uhusiano wako na hawa wauaji na hasa huyu aliyekuhukumu kifo bwana Jean",
Willy alimwambia Bibiane.
"Nimeshatoa
kauli yangu kuwa nitakueleza kila kitu unachotaka niseme. Hivyo, usiwe na
wasiwasi nitakueleza, ila itabidi uwe na subira maana ni hadithi ndefu",
Bibiane alijibu.
Bibiane
alimweleza Willy kwa kirefu maisha yake ya utoto, maisha ya shule, juu ya baba
yake na mama yake na akaendelea, "Mwaka nilipoanza kazi baada ya kuhitimu
digirii ya kwanza ya lugha katika Chuo Kikuu cha Kigali, wazazi wangu wote
wawili walikufa kwa ajali. Nilikuwa nimeanza kazi Wizara ya Mambo ya Nje kama
mkalimani.
"Inasemekana
kuwa wazazi wangu hawakufa kwa ajali ya kawaida ila waliuawa na vikaragosi vya
Watutsi ambao walifikiri kuwa baba yangu alikuwa ndugu yake na Rais. Hivyo
waliwaua wazazi wangu ili kumkomoa Rais. Kitendo hicho kiliniuma sana
nikawachukia sana Watutsi", Bibiane alieleza.
"Pole
sana", Willy alisema kwa sauti ya huruma.
"Kwa
kunisikitikia kutokana na yaliyowakuta wazazi wangu, serikali ikanihamishia
ofisi ya Rais, huko ndiko nilipokutana na Jean Yves Francois, yeye ni Mfaransa
anaishi Paris lakini alikuwa rafiki kipenzi na Rais. Tulionana naye nyumbani
kwa Rais ambako alikaribishwa na tulianza urafiki siku hiyohiyo", Bibiane
alieleza Willy huku akimwangalia kwa jicho la kuiba.
"Huyu
Jean Yves Francois ndiye aliyekufundisha ujasusi?", Willy alimuuliza.
"Umejuaje?".
"Nimehisi".
"Jean
ni mfanyabiashara na alikuwa akifanya biashara na kundi la marafiki wa Rais
pamoja na familia ya Rais, wakati mimi nafahamiana naye serikali ilikuwa
imeanza kuwa na matatizo kwani Watutsi waliokuwa humu ndani na nje, nchini
kwenu na Uganda walikuwa wakipigana ili waiangushe serikali. Jean ndiye
aliyekuwa akimsaidia Rais kwa kumjenga kijeshi, kiusalama na kiutawala. Huyu
Jean ana utajiri usio kifani, kwani ndiye anayezifadhili serikali na wakuu
wengi wa nchi za Afrika. Kwa vile mimi pia nilikuwa kwenye himaya yake
alinipeleka kwenye mafunzo ya kiusalama sehemu mbalimbali duniani".
"Na
ukahitimu vizuri", Willy alidakia.
"Vizuri
sana".
"Ehee,
endelea".
"Si ni
wewe unanikatisha".
"Huu
utajiri aliupataje?", Willy aliuliza.
"Sijui
mwenyewe ameupataje, ila anashughulika na mambo ya silaha. Hapa alikuwa analeta
silaha, halafu anachukua chai yote na kahawa inayolimwa katika nchi. Hili suala
ni moja ya malalamiko mengi ya wananchi maana Jean ndiye aliyekuwa akipanga bei
anayotaka, na hakukuwa na mtu wa kusema kitu, maana alikuwa akifanya biashara
na Rais na kundi lake, lililokuwa likiitwa Akazu. Kusema kweli Jean na hilo
kundi la Akazu ndio waliokuwa wanatawala na si baraza la mawaziri au
Bunge", Bibiane aliendelea huku sasa Willy akimsikiliza kwa makini zaidi.
"Huoni
kuwa hiyo haikuwa sawa?", Willy aliuliza.
"Mimi
ningefanya nini, nilibaki kufanya kila nilichoagizwa kama ilivyokuwa kwa
wengine wengi maana sasa hii ndio ilikuwa namna ya maisha. Ama uko na Akazu,
vinginevyo hupati kitu cha aina yoyote, iwe mali, elimu au kazi ya aina yoyote
Rwanda".
"Kwa
hiyo rushwa ndio ilitawala utawala uliopita?", Willy aliuliza.
"Inategemea
unavyotafasiri rushwa", Bibiane alijibu huku akiwa kama haelewi anasema
nini.
"Rushwa
ni pale vyombo vya serikali vinaposhindwa kufanya kazi zake, kwa sababu hiyo
kushindwa kutoa haki kwa wananchi wake, na kuwafanya wananchi wengi wapoteze
imani, utu, uhuru na maadili kwa serikali yao kwani wote sasa huishi kama
wanyama ambapo mwenye nguvu na pesa ndiye anayepata anachohitaji", Bibiane
alisema.
"Hivyo
ndivyo, maana nchi inakosa maendeleo kwani mapato yote ya nchi badala ya
kuendeleza watu wote huingia kwenye mifuko ya watu wachache. Na kama ulivyosema
uhalali wa serikali kama chombo cha watu unakwisha, badala yale wale
wanaofaidika ndio wanakuwa na nguvu zaidi ya serikali yenyewe", Willy
alitafasiri rushwa.
"Kwa
tafasiri hiyo nakubali kuwa rushwa ndiyo imetawala. Na sasa Watutsi na Wahutu
walipoanza kudai demokrasia isingewezekana maana Jean na Akazu hawakutaka
kusikia kitu kama hicho kwa vile kingeweza kuingila maslahi yao. Na ndio sababu
Watutsi walipokazana na kusikia eti wako tayari hata kupigana na Akazu, kwa
kufadhiliwa na Jean, walianza kulifundisha jeshi la wahutu lililoitwa
Intarahamwe ili liweze kuwadhibiti Watutsi wa ndani na nje ya Rwanda".
"Kwa
hiyo huyu bwanako Jean ndiye alikuwa Rais hapa?".
"Si
hapa tu, mimi najuwa nchi nyingi ambako amewakamata wakuu wa nchi na viongozi
wa ngazi za juu serikalini na anawajaza mapesa kila wakati".
"Huoni kuwa
yeye ndiye ananufaika zaidi, maana anajaza mapesa watu wachache lakini yeye
anachukuwa mali za wananchi wengi", Willy alijaribu kumwelimisha Bibiane.
"Najuwa,
maana hata huko kwenu Tanzania pia amewakamata wakubwa, ndio sababu nchi yenu
imekuwa ikisita juu ya suala hili la Rwanda".
Willy
alisitushwa na taarifa hii lakini hakutaka kujionyesha maana kweli msimamo wa
serikali ya Tanzania ulikuwa unalegalega kabla na hata baada ya mauaji.
"Ina
maana maamzi yoyote ilikuwa lazima Jean akubaliane nao?".
"Ndiyo,
na mapesa yalitembea sana kuhusu swala hili na viongozi wengi wamenufaika.
Unafikiri kama swala hili lingefanyiwa maamuzi mapema mauaji yangetokea!",
Bibiane alimwambia Willy kwa njia ya kushangaza.
"Kwa
hiyo huyu Jean ndiye aliamru mauaji haya?".
"Baada
ya Rais kuonekana kwamba angekubali mkataba wa Arusha. Jean na Akazu
walikasirika sana maana hawakutaka, kama nilivyosema mwanzo, kugawana madaraka
na mtu mwingine. Hii ingegusa maslahi yao. Kwa hiyo, kwanza ndio waliamru Rais
auawe na pili tayari walikuwa wamewatayarisha na kuwahamasisha Wahutu
kuwamaliza Watutsi wote asibaki mtu ili wajihakikishie uwezo wa kutawala
milele. Mpango ulikuwa kwamba hata kama jeshi la RPF la Watutsi lingeshinda
jeshi lao lazima baada ya kuchukuwa nchi wangeshindwa kutawala maana
wangemtawala nani huku Watutsi wote wakiwa wameshauawa, waliobaki ni Wahutu
watupu ambao hawawaungi mkono. Hivyo, ingewachukuwa siku chache kuuangusha na
kuutokomeza kabisa utawala wa RPF. Hii ingebaki nchi ya Wahutu chini ya utawala
wa Jean na Akazu.
Bibiane
alipofika hapa ndipo Willy alipoanza kuelewa kwa undani mambo yalivyokuwa.
Kumbe mauaji yote haya yalitokana na watu wachache kutaka kulinda maslahi yao
ya kunyonya mali ya wananchi, na kutumia hiyo mali kuweza kuwachochea wananchi
kuuana!.
Kwa mara ya
kwanza Willy aliona jinsi ambavyo nchi zote za Afrika zilivyo hatarini kutokana
na rushwa. Kwa vile viongozi wa nchi hizi kuabudu rushwa, hivyo Willy akaamini
kuwa tukio kama la Rwanda kumbe linaweza kutokea mahali pengine katika Afrika!.
"Baada
ya RPF kushinda na mipango ya Jean kushindwa, wana mikakati gani sasa?",
Willy alihoji.
"Kama
nilivyosema hawajashindwa. Wewe ndiye umeingilia ndani ya mipango yao, kuna
mpango kabambe wa kuisambaratisha serikali ya RPF kutokea jimbo la Kivu, Zaire.
Akazu wamekuwa wakiliimarisha jeshi lao katika makambi ya wakimbizi kule Goma
na Bukavu, Zaire, huku Jean akiwatumia rafiki zake kutoka Afrika Kusini hasa
waliowahi kuwa katika idara ya ujasusi ya makaburu, alikokuwa akinunua silaha
na kuzipitishia Angola ya UNITA, Zaire na Zambia kwa kutumia viongozi wa ngazi
za juu za serikali za nchi hizo ambao wako kwenye orodha ya malipo kutoka kwa
Jean. Kwa hiyo mambo bdo sana Willy, vita ndio sasa karibu vitaanza".
"yaani
dunia inafikiri kuwa kambi zilizoko Zaire ni za wakimbizi kumbe ni kambi za
jeshi".
"Ni
kambi za jeshi na serikali ya Zaire inajua na ndio inayosaidia hata mafunzo.
Hata katika kambi zilizoko kwenu Tanzania kuna wanajeshi wa jeshi la zamani na
Intarahamwe, na kuna watu wazito katika serikali yenu ambao wanalipwa na huyu
Jean ili kuwasaidia hawa watu, kwa hiyo hili si dogo. Kama ulivyosema pesa ni
kitu kibaya sana, watu hawaoni tena madhara ya mauaji yaliyotokea bali wanaona
pesa tu".
"Swala
la rushwa ni swala linalohujumu haki za binadamu, yapaswa lichukuliwe hatua
kimataifa katika uzito huo wa haki za binadamu", Willy alijibu kwa hasira.
Bibiane
alikaa kimya bila kujibu kitu.
"Wewe
ulikuwa uwasaidie vipi Jean na Akazu katika kutekeleza huu mpango wao wa
kuivamia tena Rwanda", Willy aliuliza.
"Usije
ukanipeleka kwenye mahakama ya mauaji ya Arusha maana mauaji yale sikuyajuwa
pia sikushiriki, nilikuwa Nairobi nikitokea kwenye mkutano Arusha. Ila juu ya
hili la sasa Jean amekuwa akinituma kupashana habari kati ya kambi za wakimbizi
ambazo ni kambi za jeshi lao huko Zaire, yeye na Akazu. Vilevile kuna wanajeshi
na viongozi wa RPF ambao tayari wamenunuliwa na wako upande wa Akazu, mmoja wao
ndiye anayetarajiwa kuchukua madaraka mara tu jeshi la Akazu litakapotwaa
madaraka tena".
Willy
hakuamini masikio yake kuwa tayari hata ndani ya RPF kuna wasaliti.
Mara moja
Willy alielewa jinsi alivyotaka kuuawa na akagudua kuwa kweli kama anavyosema
Bibiane kuna kiongozi wa juu na karibu sana katika serikali ya Tanzania amabye
anamtumikia Jean na kundi la Akazu.
"Utasaidia
kunipa majina ya watu wote unaowajuwa kuwa wanahusika, maana hiyo ndio njia
pekee tunaweza kulikosha jina lako", Willy alimuasa Bibiane.
"Swala
la Jean kunisaliti mimi, na kunihukumu kifo, bila kujali yote niliyomtendea kwa
hali na mali ikiwa pamoja na kumpa mwili wangu auchezee atakavyo, na jinsi
nilivyojitoa kumstarehesha. Willy mimi niko upande wako, kama uko tayari
kupambana nao nihesabu na mimi. Jean akishaambiwa kuwa umenichukua ninavyomjua
atataka apambane na wewe yeye mwenyewe, ikifika hapo niachie mimi. Majina na
mipango yao yote ni juu yako na uongozi wa RPF mjuwe la kufanya kwani jeshi la
Akazu, likisaidiwa na viongozi wa nchi kadhaa ambao ni marafiki na Jean
watakuwa tayari kuingilia kati. Ni lazima liwahiwe mapema kabla halijajiimarisha
sawasawa", Bibiane alieleza.
"Nafikiri
swala la vita si letu, ni la serikali ya Rwanda na RPF, mimi nipe hayo majina
na kutokea hapo ndipo nitajua kama kazi yangu imeisha au ndio kwanza
inaanza", Willy alieleza taratibu.
Bila kuwa
ameandika mahali popote, Bibiane alitoa kichwani jina hadi jina akianza na
kundi la Akazu mpaka viongozi wa nchi mbalimbali wanaolipwa na Jean huku Willy
akiyaandika chini kwa mshangao mkubwa, kwani watu waliokuwa wanatarajiwa wengi
wao ni viongozi wanaoheshimika Afrika na kote duniani. Alishangaa zaidi Bibiane
alipotaja jina la yule waliyekuwa wakimwita JKS wa Tanzania.
"JKS,
hii imenishangaza sana, maana huyu ndiye anayetegemewa kugombea urais wa
Tanzania katika uchaguzi mkuu unaokuja," Willy alimweleza Bibiane.
"Najua
kabisa, na tayari Jean ameshamtengea mamilioni ya dola za Kimarekani zitakazo
msaidia katika kampeni hiyo ya uchaguzi kuusaka urais. Nia ya Jean ni kuwa na
marais vibaraka kote Afrika ili yeye na wenzake huko Ulaya, waweze kufanya vile
wanavyotaka katika nchi hizi. Jean anaongoza kundi la wafanyabiashara wakubwa
wanaomiliki makampuni makubwa ya kimataifa. Na nia yao ni kuhakikisha kuwa
Afrika inakuwa soko lao tu, na hata siku moja Afrika isisimame kiuchumi.
Ingawaje nchi zao zinapigia kelele rushwa, lakini nchi hizohizo ndizo
zinazoyasaidia makampuni makubwa kwa madogo kutoa rushwa kwa nchi
zinazoendelea, maana makampuni hayo yakitoa hongo, hongo hii huchukuliwa kama
gharama na kutolewa kwenye kodi ya mapato. Hii yote inaonyesha unafiki wa nchi
za magharibi, na kila wakati Jean alikuwa akinieleza kuwa kelele zote hizi
kuhusu rushwa, demokrasia na soko huria ni kelele za kinafiki tu, lakini huku
nyuma katika vikao vya viongozi wa nchi za magharibi ni kuchochea rushwa.
Wanajuwa kuwa rushwa ikiisha Afrika basi demokrasia na soko huria vitashamiri
na hivyo uchumi wa nchi hizo utakua haraka sana, kitu ambacho hawataki kitokee.
Jean anasema, rushwa ndiyo sera inayotumiwa kuendeleza umaskini katika nchi za
Afrika ili nchi zilizo endelea ziendelee kuitawala Afrika kiuchumi. Kwa hiyo,
iwapo JKS ataitawala Tanzania rushwa itazidi mara dufu, na kutokana na fedha
alizotengewa na Jean lazima atashinda, kwani kila walipoweka mtu wao hajawahi
kushindwa uchaguzi", Bibiane alieleza.
Sasa Willy
alikuwa na picha kamili namna JKS alivyokuwa anahusika na swala zima la Rwanda.
na sababu za Tanzania kutokuwa na msimamo dhabiti juu ya swala hili na kuweza
kuyumbisha mikutano kule Arusha kiasi cha kutofikia maamzi kwa muda mrefu maana
swala hili la Rwanda kwa muda mrefu lilikuwa chini ya Tanzania kwa muda mrefu
na JKS alikuwa mmojawapo wa viongozi walioonyesha kuchoshwa na mauaji ya
Rwanda. Na alifanya hivyo kwa shinikizo la Jean aliyekuwa akimlipa pesa nyingi
na uchu wake wa kutaka madaraka kwa njia ya ruswa ili aweze kuyatumia kwa faida
yake na kujinifaisha yeye na rafiki zake. Na ni hii rushwa iliyowanyima
Wanyarwanda haki yao mpaka kufikia hatua ya kuuawa vibaya namna ile kweli ni
aibu! Aibu sana kwa Afrika nzima.
"Vizazi
vijavyo vitakapoyasoma na kuyaelewa matukio haya, hakika hawataamini, watajuwa
sisi wote tulikuwa wendawazimu kabisa, kwani ni sisi wote ndio tulioachia hali
hii ikafikia hapo ilipo, kwa kuwapa walarushwa madaraka kwa gharama ndogo ya
kuuza kura zetu na wao kutumia madaraka tuliyowapa kwa malipo ya fedha kidogo,
lazima wayatumie kutuangamiza", Willy alisema kwa uchungu huku akikuna
kichwa chake.
Mara moja
Willy alimkumbuka Malisa wa Arusha, aliyekuwa mshauri wa JKS katika masuala ya
uhusiano wa Kimataifa kabla hajarudi Chuo Kikuu. Hivyo basi, alijuwa Malisa
ndiye aliyemweleza JKS kuhusu msimamo na mipango ya PAM na kuteuliwa kwa Willy
kufuatilia jambo hili. Willy aliamini kuwa JKS ndiye aliyetoa taarifa za safari
ya Rwanda kwa Jean na kundi lake na ndi sababu ndege aliyopanda ikapigwa kabla
ya kutua uwanja wa ndege wa Kigali.
"Kwa
hiyo JKS ndiye aliyotoa habari zangu zote kwa Jean?", Willy aliuliza kwa
shauku.
"Ndio,
na ndio sababu Col. Gatabazi aliamru ndege hiyo ipigwe kabla ya kutua uwanja wa
ndege, lakini kwa bahati na umahiri wako ukawaponyoka", Bibiane alijibu
huku akimwemwesa. Mara mlango wa mbele ukafunguliwa na Col. Gatabazi akaingia
ndani.
Willy
alipoangalia saa yake ilikuwa yapata saa tisa usiku. Wote walisimama, na Willy
akawatambulisha.
"Pole
Kanali, leo tumepata mgeni na anaitwa Bibiane, na Bibiane huyu ndiye mwenyeji
wetu. Col. Rwivanga, kiongozi katika serikali mpya ya RPF".
"Nashukuru
kumfahamu", Col. Rwivanga alijibu.
"Nami
nimefurahi kukuona leo, nimekuwa nikisikia sifa zako nyingi kwa muda mrefu,
toka kwa Col. Gatabazi kuwa wewe ni mpiganaji hodari, hongera", Bibiane
alijibu kwa tabasamu akimwangalia Col. Rwivanga.
"Asante
kwa sifa hizo zilizotoka katika kinywa cha msichana mrembo kama wewe",
Col. Rwivanga alijibu akaendelea, "Ehe, imekuwaje Willy, hebu nipe habari
kamili, maana kazi tumeiona kwa Bibiane, sasa halafu ikawaje hivi", Col.
Rwivanga alionekana kuwa wasiwasi na Bibiane.
"Mimi
naomba nikalale ili mzungumze vizuri, nionyeshe chumba cha kulala",
Bibiane aliomba.
Willy na
Col. Rwivanga aliangaliana na Willy ndiye alikuwa wa kwanza kujibu, "Kwa
vile nyumba hii ina vyumba viwili tu vya kulala, basi kalale chumbani kwangu,
maana tayari hata kuoga umeoga huko. Mimi nitalala hapa sebuleni kwenye kochi
hamna taabu".
"Asante",
Bibiane aliwaaga na kuelekea chumbani huku wote wakimwangalia. Kisha
wakatazamana na kutabasamu.
"Ehe,
hebu nipe mambo".
Willy
alichukua muda mrefu kumweleza mambo yalivyotokea na mambo mengine yote
aliyoelezwa na Bibiane. Col. Rwivanga akasimama na kumshika mkono Willy kwa
hatua aliyofikia haraka na kwa umakini mkubwa.
ITAENDELEA
0784296253
kazi nzuri sana hii ila nakuomba kaka usikae siku nyingi bila kuiweka
ReplyDelete