NGUVU YA
RUSHWA
V
Baada ya
Col. Gatabazi kuvaa nguo vizuri, walichukua silaha mbalimbali na fedha zilizokuwa pale ndani. Wote walivaa mavazi ya kijeshi na kutumia gari ndogo aina ya MB 230E,
ambalo awali Nkubana alikuwa amepewa na Col. Gatabazi kwa ajili ya Operesheni
ya usiku. Gari hii ni mojawapo ya magari yaliyokuwa yameachwa na viongozi wa
serikali iliopita, baada ya kukimbia mji wa Kigali, wakati RPF inaingia madarakani.
Nkubana
alikaa kwenye usukukani kwa ajili ya kuendesha gari, Col. Gatabazi akakaa upande wa kulia, maana gari hili lilikuwa na usukani upande wa kushoto.
"Aha,
kumbe gari limejaa mafuta kwenye tenki".
"Ndio,
nilijaza kwa sababu kama hizihizi kama dharura itatokea", Col. Gatabazi
alijibu.
"Tuchukue
njia gani?", Nkubana aliuliza.
"Najua
sasa hivi wataanza kututafuta. Hivyo, twende na barabara kubwa iendayo
Ruhengeri. Kwa vile bado mawasiliano ni shida kati ya vikosi, tunaweza kupata
bahati tukafika Gisenyi kabla habari zetu hazijaenea. Kwa vile vikosi vya RPF
vinanifahamu na kuniheshimu njiani hatutaulizwa wala kupata tatizo lolote,
watajua kuwa niko kazini. Kwa hiyo tutumie barabara kubwa mpaka Ruhengeri, halafu
moja kwa moja mpaka Gisenyi, halafu tutavuka mpaka na kuingia Goma. Upande ule
Jean ameshafanya mipango, hatutakuwa na shida. Nimemweleza amweleze Mkuu wetu
wa Majeshi Col. Marcel Bazimaziki atukute mpakani"Col. Gatabazi alieleza.
"Sasa
hivi ni saa sita na robo, itatuchukua masaa kama manne kwa gari hii, kwa hiyo
saa kumi na moja alfajiri tutakuwa Goma?", Nkubana aliuliza huku akitia
gea na kuondoa gari kwa kasi kuelekea Goma.
NGUVU YA
RUSHWA
VI
Baada ya
Jean kumweleza JKS mambo yote yaliyokea Kigali, palepale JKS usingizi ulimtoka. Aliona
na kuamini kuwa huo ndio ulikuwa mwisho wake. Ndoto zake za kuwa Rais wa
Tanzania zilianza kuyeyuka mfano wa seluji. Hakujua afanye nini. Aliamini kuwa
Willy Gamba akipata habari zake kuwa yuko kwenye mtandao wa kuisaliti Afrika
haitamchukua zaidi ya siku mbili kabla mambo yake hayajabainika na kuanikwa
hadharani.
JKS alimjua
vizuri Willy Gamba alivyokuwa makini na hodari katika kufanya kazi zake.
Alifikiri asubiri Willy arudi kwanza nchini ndio amkabiri yeye mwenyewe au aieleze
serikali ya Tanzania kilichokuwa kinafanyika Rwanda. Aliona kashifa kubwa
inakuja mbele yake. Ingawaje Rais wa sasa wa Tanzania alikuwa rafiki yake
mkubwa, lakini ingekuwa vigumu sana kuizuia kashifa hii, maana vyombo vya
habari vingemmaliza kabisa. Kisha, akakumbuka kuwa alikuwa na mapesa mengi
ambayo Jean alimwekea kwenye akaunti zake katika mabenki ya huko Uswisi na
Cyprus.
Baada ya
kutafakari kwa muda mrefu huku jasho jembamba likimtoka. JKS akaamini kuwa
mapesa hayo yangeweza kuzuia kashifa hii kwa kuwanunua wamiliki wote wa vyombo
vya habari Tanzania kama Radio, magazeti na taasisi zingine kama polisi,
usalama wa Taifa na idara zingine nyeti za serikali ambazo zingeonekana
kumletea madhara kwenye safari yake ya kuelekea Ikulu.
"Watanzania
karibu wote wana njaa, nitawanunua kwa mapesa tu. Hapo ndipo Willy atajuwa
jeuri na nguvu ya pesa. Hakuna mtu atakayemsikiliza tena Willy Gamba, mimi
nitaendelea na mambo yangu bila hofu. Uchu wangu wa kuwa Rais wa Tanzania
utafanikiwa", JKS alijisemea mwenyewe huku akiwa amelala mfano wa mtu
aliyeko katika usingizi mnono akiota ndoto.
Hivyo, baada
ya kutafakari hili na lile kwa mapana na marefu, JKS aliamua kuwa atamfuata
Rais ili amuombe ruhusa na kusafiri kwenda Ulaya kwa ajili ya kuangaliwa afya
yake kwa madaktari wake walioko Uingereza, na angemwambia daktari mkuu wa
Hospitali ya Muhimbili atoe ushauri wa haraka. Akiwa amejiwekea malengo kuwa
akifika Ulaya akusanye mapesa yake halafu ndipo ajue kitu cha kumfanyia Willy
Gamba aliyemwona mchawi wa safari yake ya kuelekea Ikulu ya Tanzania.
JKS aliamini
kuwa akiwa na mapesa mkononi, ataweza kufanya chochote atakavyo. Akapiga moyo
konde, akamkumbuka tena Willy Gamba moyo wake ukapata maumivu makali, akahisi
mtu huyu ni mchawi. Hata hivyo akaapa kuwa hatarudi nyuma.
ITAENDELEA
0784296253
tuko pamoja
ReplyDelete