UCHU



GISENYI

II

Ilipofika saa nne asubuhi JKS alikuwa tayari ameshapata kibali kutoka kwa Rais ili aweze kwenda Uingereza kwa matibabu. Daktari alikuwa ameiandikia serikali barua kufanya haraka na kila njia JKS aondoke siku ileile kwani alihisi kuendelea kusubiri kungeweza kumletea shinikizo la damu lenye nguvu kubwa ambalo huenda wao wasingeweza kumsaidia kabisa.

Ni barua hii ya Daktari iliyomfanya Rais akubali kutoa kibali harakaharaka na kuamru kuwa ifikapo jioni ile JKS awe ameondoka kwenda Uingereza kwa matibabu. Hadi saa saba mchana Wizara ya Afya ilikuwa imefanya mipango yote na ikawa wamempatia usafiri kuondoka na ndege ya shirika la ndege la Uingereza usiku ule.

JKS alikataa kusindikizwa na maofisa wa serikali kwa kisingizio kuwa atapokelewa na watoto wake walioko mjini London, Uingereza ambao alisema watamwangalia kwa karibu zaidi wakati wa matibabu yake. Bila watu kujua, alifanya mipango yake mwenyewe ili usiku uleule aweze kuunganisha ndege kwenda hadi Geneva, Uswisi, kitu ambacho alifanikiwa. "Hakika Willy Gamba hataniweza, nikirudi na mapesa yote yale, hakika naamini ataiona dunia na ardhi ya Tanzania chungu", JKS alijisemea mwenyewe huku mapigo ya moyo yakimwenda mbio.
.............................................................................................................................
III
Wakati Willy na Bibiane wanaondoka Kigali kuelekea Goma, saa kumi na mbili asubuhi. Col. Gatabazi na Nkubana walikuwa wanapokelewa na Col. Marcel Bazimaziki na kikundi cha wanajeshi wa jeshi la Zaire kikiongozwa na Meja Massamba kwenye mpaka wa nchi hizo za Rwanda na Zaire.

"Pole sana na safari, ulipokaribia kufika Gisenye natumaini umepita ile njia yetu na nadhani hukupata shida", Col. Bazimaziki aliwasalimia kuwapa wageni wake mkono huku kila kikundi cha askari kikijiweka sawa kutoa heshima kwa gwaride rasmi lililoandaliwa kwa ajili ya Col. Gatabazi ambaye kama walivyokuwa wameelekezwa kuwa baada ya muda si mrefu ndiye atakuwa kiongozi wa Rwanda.

"Safari ilikuwa safi kabisa na hizi Benz ni gari imara sana ha hata kile kinjia tulichopita hatukupata taabu sana. Asante kwa kutuma mtu wa kutuongoza, maana tungeweza kubabaika kufika hapa", Col. Gatabazi alijibu.

"Jean tulizungumza kwenye simu yetu aliyoleta hivi karibuni ya Satellite. Sasa mawasiliano ni mazuri sana kati yake na sisi. Hata kabla ya kuja kukupokea tulizungumza nae, alikuwa akielekea uwanja wa ndege, nae tayari amepanda ndege na imeondoka Paris tangu saa kumi na mbili.

"Anatumia ndege yake ile ya Falcon, atakuwa hapa saa kumi na mbili jioni, maana atapitia Kinshasa kuonana na viongozi wa serikali kule, mkutano utafanyika uwanja wa ndege ili waweke msimamo, halafu watakuja na Jenerali Kasongo ili kuangalia hali pamoja na wewe mwenyewe ukiwepo ili mkiridhika na hali kazi ianze", Col. Bizimaziki alieleza na kisha Col. Gatabazi akaelekea kwenye gwaride ili apokee heshima zake kutoka kwa kikundi cha wanajeshi wa Zaire.

Baada ya kupokea heshima na kukagua gwaride. Col. Gatabazi na wenyeji wake waliamua kuondoka kuelekea Kibumba kwanza na kisha jioni ndio waelekee Goma kwenda kuonana na Jean na maofisa wengine wa juu.

"Acheni hilo gari hapa mpakani, hakuna matatizo askari wa jeshi la Zaire wapo wataliangalia maana kule kwenye makambi lazima kwenda na magari ya jeshi la Zaire ndio idara na taasisi za Kimataifa zinazoshughurikia wakimbizi haziwezi kushituka", Col. Bizimaziki alieleza.

"Sawa, vipi minong'ono kwamba watu wetu wanajitayarisha kuishambulia tena Rwanda huku wakitumia kinga ya wakimbizi?", Col. Gatabazi aliuliza.

"Usijali kabisa kuhusu hilo, serikali ya Zaire itakanusha vikali huku sisi tumetia pamba masikioni. Na kama ujuavyo kiongozi wa baraza la Akazu, Anatoile Kabuga. Alitusihi tusisikilize propagada za vyombo hivi isipokuwa tujiimarishe kijeshi tayari kwa kuikomboa nchi yetu kutoka kwa wavamizi wa Kitutsi. Kwanza nilitaka kusahau, vilevile Bwana Kabuga anakuja pamoja na Jean ili maamuzi yaweze kufanyika, ameeleza kuwa mjumbe mwingine wa Akazu ambaye anaweza kufika ni John Ngeze ambaye sasa yuko Afrika Kusini, lakini ameambiwa apande ndege ya shirika la ndege la Afrika Kusini inayoingia mjini Kinshasa saa sita na kama akiwahi atawasubiri pale uwanjani na wao wakiwahi watamsubiri|.

"Lo, kumbe tutakuwa na mkutano mkubwa", Col. Gatabazi alinena.

"Wakati umefika kwa wewe Col. Gatabazi kuchukua nchi kutoka mikononi mwa wavamizi wa Kitutsi. Siri zote za adui yetu unazijua, nguvu ya RPF yote unaijua, ya kijeshi na kisiasa. Sasa nini kitazuia?, wao hawajui nguvu yetu wanafikiri tunacheza. Utaenda sasa hivi kujionea mwenyewe salaha za kisasa, magari, vifaru. Tuna silaha ambazo zina uwezo wa kupiga masafa marefu hadi kilomita mia mbili, na kuna mafunzo makali yanayoendelea kutoka kwa askari wale tuliowakodi kutoka Afrika Kusini na wana kazi kubwa na vijana wetu wana ari kubwa maana wanajua tusiposhika nchi tena maisha yao yako hatarini. Ni kweli kama ulivyosikia wakimbizi tumewazuia kurudi ili siku tutakapoamua kuanza kazi ndiyo siku ambayo wakimbizi wote wanaume tutaandamana nao. Wakirudi wakati huu uhalali wa kuivamia tena Rwanda hatutakuwa nao. Hii vurugu ya wakimbizi kwanza inaficha mambo yote tunayoyafanya, pili itatupa uhalali na nguvu za kuvamia. Rafiki zetu wote watasema. "mlitaka wafanye nini, yaani mamilioni ya watu yabaki kuwa wakimbizi nje ya nchi yao", Col. Bazimaziki alieleza, kisha wakaelekea kwenye kambi.

Walipofika huko kambini walitumia muda mrefu kuangalia aina mbalimbali za silaha za kisasa kabisa, mafunzo makali ya kijeshi, ari ya vijana wa Kihutu, hasa wale Intarahamwe waliotaka siku hiyohiyo kwenda kuvamia Inyenzi na kurejesha madaraka yao. Kutokana na aina ya silaha walizonazo na mafunzo waliyokuwa wakipata na moto waliokuwa nao wa kutaka kupigana na adui. Col. Gatabazi aliamini kabisa kuwa wakisaidiwa na Wahutu waliokuwa ndani ya Rwanda ushindi ulikuwa wao asilimia mia. Col. Gatabazi alipandwa na mori akatamani kama vita vingeanza saa ile. Kisha, wakaondoka kuelekea Goma.

ITAENDELEA 0784296253 
 

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU