GISENYI
IV
Ilikuwa saa
kumi na moja na nusu jioni, Jeana na wenzake walipowasili kwenye uwanja wa
ndege wa Kimataifa wa Goma. Baada ya kuwasiliwa, walipokelewa na Col. Gatabazi aliyesindikizwa na askari wake. Jean aliwasili akiwa pamoja na kiongozi wa Akazu, Bwana Anatoile Kabuga,
Bwana John Ngeze, ambaye ni Mjumbe wa Baraza la Akazu, Jenerali Kasongo,
ambaye ni mshauri wa Rais wa Zaire, Meja Karongo, Mkuu wa kikosi cha jeshi linalomlinda
Rais wa Zaire, Bwa, George Karikutis, ambaye ni dalali wa mamluki aliyefanya mipango
yote ya kuwawezesha Jean na wenzake wa Akazu kupata askari wa kukodi.
Baada ya
kuwasili uwanja wa ndege walipelekwa moja kwa moja hadi Ikulu, ambako Rais
alitoa kibali Jean na wenzake wafikie kwenye jumba hilo. Ikulu hii ilikuwa ya
kifahari sana. Ili uweze kuelewa kwa kifupi, vyoo, bafu na vyumba vya kulala
alivyokuwa akitumia Rais vilijengwa kwa vito vya dhahabu tupu. Sasa naamini
utakuwa umeelewa maana yake. Karibu na Ikulu hii kulikuwa na Jumba jingine
kubwa ambalo Majemedari wa jeshi wa ngazi za juu walikuwa wakifikia. Ndani ya
jumba hilo ambalo pia lilikuwa la kifahari sana, ndimo alipofikia Col. Gatabazi
na wenzake. Kisha, wakaenda kukaa kwenye sebule ya kifahari ajabu. Wasichana
warembo sana wapatao kumi hivi walijitokeza kwa ajili ya kutoa huduma, wakiwa
wamevaa kaputula fupi, matiti nje, yaani asilimia tisini walikuwa uchi.
"Hivi
ndivyo mzee anavyoishi hapa duniani Jean, hapa panaweza kuwa peponi ukitaka.
Mzee ameyafanya maisha yake hapa duniani kuwa sehemu ya peponi. Hivyo, na wewe
onja pepo kidogo ukiwa hapa", Jenerali Kasongo alimweleza Jean, ambaye
wakati huo alikuwa akitikisa kichwa, maana pamoja na utajiri wake mkubwa usio
kifani alikuwa hajawahi kukalia viti na meza za kahawa vilivyotengenezwa kwa
dhahabu tupu, ukiacha sehemu za kukaa ambazo zilivishwa kwa ngozi ambazo hata
yeye hakuwahi kuziona kabisa duniani.
Huku wale
wasichana wakiendelea kuwahudumia, kila mmoja alikuwa amejichagulia mrembo wa
kumhudumia, wakileta vinywaji vya kila aina vilivyokuwa ndani ya jumba hilo.
Baada ya muda mazungumza yalianza.
"Ehe,
hebu Nkubana tueleze ilikuwaje hata huyu Willy Gamba akachafua mipango yetu
namna hii, maana inaniuma sana kufikia hatua ya Bibiane kuwa mikononi na
mshenzi huyu. Hebu tueleze", Jean aliuliza kwa hasira.
Huku
akitetemeka Nkubana alieleza jinsi mambo yalivyokuwa huku wote wakimsikiliza
kwa makini sana, kisha akamalizia kwa kusema, "Tulichukua tahadhali ya
kila aina, lakini nafikiri huyu Willy Gamba alikuwa na bahati kuliko sisi.
Katika biashara kama hii yetu, wakati mwingine ni bahati tu inaweza kukusaidia",
Nkubana alijitetea.
"Unafikiri
huyu mtu ana mipango gani sasa?", Jenerali Kasongo aliuliza.
"Sijui,
lakini naamini Bibiane anaweza kumleta huku. Hizi ni hisia zangu, maana Bibiane
atakuwa na uchungu wa kutaka kulipiza kisasi na siri zetu zote anazijua. Hivyo,
atataka amtumie Willy Gamba baada ya kuona umahiri wake, alipize kisasi",
Nkubana alijibu.
"Mbona
hiyo itakuwa raha, maana nitaua ndege wawili kwa jiwe moja, Col. Bazimaziki na
Meja Massamba, moja ya kazi zenu ni kuweka kikosi imara chenye wapiganaji
jasiri cha kuweza kuwakamata hawa watu wawili, nataka Nkubana akiongoze kikosi
hicho, Nkubana, ukiweza kuwakamata usiwaue hao ni halali yangu. Nataka
niwafanyie kitu ambacho wakiwa ahera wasinisahau milele", Jean aliamru.
"Sawa
bosi", Nkubana alijibu hku Col. Bazimaziki na Meja Massamba wakiitikia kwa
vichwa vyao.
"Ratiba
ikoje?", Jean alimuuliza Col. Gatabazi.
"Nafikiri
kwanza twendeni wote tukaangalie hali ya vikosi vyetu ilivyo, hasa hapa
Kibumba, maana mtapata mwanga baada ya kuona jinsi tulivyojiandaa tayari kwa
vita. Tumetuma habari kwa vikosi vyetu vingine vilivyoko karibu na Bukavu,
navyo vijiweke tayari. Ile simu moja kati ya simu nne za Satellite ulizoleta
tuliwapelekea na sasa tunawasiliana vizuri sana kati ya hapa na sehemu zingine zote
ambako kuna vikosi vyetu, lakini kwa kuwa nguvu yetu kubwa iko hapa nafikiri
twende mara moja Kibumba mkajionee wenyewe, kwani ni kilomita thelathini tu
kutoka hapa Goma. Halafu tukirudi tutakula chakula hapa na baadaye kidogo
tutaanza mkutano wetu. Mimi naamini kuwa mkishaona kama nilivyoona mimi mkutano
wa leo utaruhusu tuanze uvamizi leoleo", Col. Gatabazi alimalizia.
Wote
walikubaliana naye. Kabla hawajaondoka alichukua simu ya Satellite akapiga simu
Tanzania. Nia yake ilikuwa kumpata JKS ili ampatie habari za wakati ule kuhusu
nyendo za Willy Gamba kama alikuwa amezipata kutoka kwenye vyanzo vyake vya
habari. Kwa mshangao alipata habari kutoka kwa mke wa JKS kuwa alikuwa ameumwa
ghafla na kuondoka jioni ile Tanzania kuelekea Uingereza kwa ajili ya matibabu.
Na mama huyo alieleza kuwa mumewe aliondoka kwa ndege ya shirika la ndege la
Uingereza. Mara moja Jean alihisi kuna tatizo. huku akitingisha kichwa huku
wengine wakimwangalia kwa kustaajabu, Jean aliwaambia wenzake wote wamsubiri
nje.
Walipotoka
nje Jean alipiga simu zingine tatu zilizomchukua dakika kama kumi hivi na baada
ya kuzipiga aliagua kicheko kwa sauti mpaka askari aliyekuwa karibu akashangaa
akifikiri kuwa huyu mzungu alianza kupata uchizi kwa kucheka peke yake hivi.
Jean alipoangalia saa yake ilikuwa yapata saa moja na nusu jioni, hivyo
aliungana na wenzake wakaondoka kuelekea Kibumba.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment