UCHU



GISENYI

VI

Baada ya kupata habari hizi walikubaliana kuitisha mkutano wa dharura mnamo saa sita na nusu mchana. Rais alipiga simu tena kwa Jenerali Bunyenyezi na kumwambia afike ofisini kwake haraka akiwa pamoja na kiongozi wa upinzani wa Zaire, aliyekuwa akiunganisha vyama vyote vya upinzani na ambaye askari wake waliwahi kupigana vita bega kwa bega na majeshi ya RPF, wakati wa mapambano dhidi ya Serikali ya Rwanda ili wapate uzoefu kutoka kwao. Bwana Mpinda ambaye nae alikuwa mjini Kigali kwa mazungumzo.

Haikuchukua zaidi ya saa moja wote walifika ofisini kwa Rais.

"Bwana Mpinda karibu sana. Nimekuita pamoja na Kamanda hapa ili tuzungumze kama uliyonieleza juzi, maana naona hali imegeuka, sasa inakupendelea wewe", Rais alicheka kidogo na wote wakatabasamu.

"Asante sana Mheshimiwa Rais, nashukuru Mungu, kama umegeuza uamuzi wako na uko tayari kutuunga mkono sisi", Mpinda alijibu.

"Kama nilivyosema naona hali inakupendelea, kuna mambo ambayo yametokea na kuashiria tulifikirie kwa makini ombi lako. Askari wako wote bado wako kwenye ardhi ya Rwanda?", Rais aliuliza.

"Hapana Mheshimiwa, wengine wengi bado wapo lakini baadhi yao  wamevuka wapo mpakani, wakisaidia kufundisha jeshi la Wabanyamulenge", Mpinda alimwambia Rais.

"Kamanda Bunyenyezi, nataka basi ufanye mpango na kiongozi wa Banyamulenge nae awepo kwenye mkutano wa saa sita na nusu", Rais aliagiza.

"Na hilo tumelifikiria, na Col. Rwivanga ameshatuma Helikopita kwenda kumchukua", Kamanda Bunyenyezi alijibu.

"Oh, vizuri sana. Sasa bwana Mpinda unakaribishwa kwenye kikao saa sita na nusu, na naomba ujieleze vizuri, na kama ukiweza kuwashawishi mawaziri na makamanda wangu, basi utakuwa umefanikiwa. Hii ni nafasi nzuri sana kwako kwani na sisi sasa tunalazimika kutumia mpango wako ili nasi tukidhi lengo letu. Hivyo, kazi kwako kukishawishi kikao kama kweli una mipango thabiti ya kuweza kufanya kazi", Rais alimalizia.

"Mheshimiwa Rais, naenda kukaa na makamanda wangu, na kwa vile viongozi wa Banyamulenge nao watakuwepo na wako upande wenu na wetu, basi naamini nitaweza kukiridhisha kikao kuwa tuko tayari kufanya kweli", Mpinda alijibu.

"Haya Bwana Mpinda kwa heri. Kamanda Bunyenyezi, wewe ngoja kidogo".

Walimtoa nje Bwana Mpinda na wakamrudisha kwenye nyumba ya wageni ya Serikali alikokuwa amefikia na makamanda wake. Rais na makamanda wake walipobaki nyuma, walitafakari swala zima kwa undani. Wakaangalia jinsi ambavyo wangeweza kufaidika kwa kuwatumia wapinzani wa Serikali ya Zaire ili waweze kutimiza lengo lao kuwaondoa Intarahamwe na Wahutu wote wenye siasa kali pale mpakani kwao ili wasije wakaivamia Rwanda, huku bila kulaumiwa na Jumuia ya Kimataifa kuwa wamevamia nchi nyingine na kuwaua wakimbizi.

"Nafikiri hii ndio nafasi yetu ya pekee kumaliza tatizo hili. Kwa hiyo, inabidi tulieleze kwenye mkutano vizuri", Kamanda Bunyenyezi alieleza.

"Je, hawa wapinzani na waasi wa Banyamulenge wakishindwa, itakuwaje? si siri itavuja?", Rais aliuliza.

"Hilo litakuwa jambo jingine, sisi tutakuwa tumetimiza lengo letu na tutakuwa tumewaondoa na kuwamaliza kabisa hawa Intarahamwe karibu na mipaka yetu. Tutakuwa tumewatokomeza mstuni huko Zaire. Shida na wasiwasi kwetu vitakuwa vimemalizika kabisa. Kazi yako itabaki kujenga nchi na si kupigana tena", Kamanda Bunyenyezi alijibu.

"Kweli, sasa tumepata kisingizio; Mungu yuko pamoja nasi, maana chochote tungefanya serikali ya Zaire na Jumuia ya Kimataifa visingetupa nafasi. Basi nenda kajitayarishe, Mkutano utakuwa mgumu sana, maana najua mawaziri wengi itakuwa vigumu kukubali", Rais alijibu.

"Asante Mheshimiwa Rais, nafikiri watatuelewa kwa sababu hii ni kwa faida ya Taifa la Wanyarwanda ambalo limeteseka sana, lazima wananchi wapate muda wa kupumua na si vita kila siku", Kamanda Bunyenyezi alijibu na kueondoka kwenda kujitayarisha.                       

ITAENDELEA 0784296253                    

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU