UCHU

GISENYI

VII

Mpinda alipofika kwenye nyumba aliyokuwa amefikia, aliteremka haraka kutoka ndani ya gari na kuingia ndani ya nyumba hii, akawagongea wenzake waliokuwa ndani ya vyumba, akiwataka kwenye mkutano pale sebuleni.

Alifikiria na kuona kwamba Mwenyezi Mungu alikuwa ameyajibu maombi yake. Hii ilikuwa nafasi aliyoisubiri kwa muda mrefu sana. Na yeye vilevile kama wenzake wa Rwanda aliona nafasi hii ilikuwa inazifaa pande zote tatu zilizokuwa zinahusika kwenye harakati hizi za mapambano. Kati ya wote waliokuwa katika sakata hilo, alijiona ndiye mwenye fursa ya kufaidika zaidi ingawaje Serikali ya Rwanda ndio ingefaidika zaidi kwa kuhakikisha kuwa haina mgogoro au wasiwasi wa kushambuliwa na Wahutu wenye msimamo mkali chini ya wanamgambo wa Intarahamwe na Banyamulenge ambao nao wangefaidika kwa kutobuguziwa tena na Serikali ya Zaire, na wangeendelea na maisha yao raha mstarehe.

Makamanda hawa walipokusanyika pale sebuleni Mpinda aliwaeleza kila kitu jinsi mambo yalivyokuwa wamejipa.

"Tunachotakiwa kufanya ni kukishawishi na kukikahakikishia kikao cha Serikali ya Rwanda na viongozi wa Banyamulenge kuwa tutakapoanzisha vita hii ni kweli uwezo wa kushinda tunao?. Pande zote zimekubali kuwa sababu tunayo na nia tunayo, swala hapa ni uwezo, wakiridhika kuwa uwezo upo, basi mambo tayari", Mpanda aliwaeleza wenzake.

"Mkuu, wala tusipoteze muda wa kufikiri, sisi tumekuwa hapa tukijaribu kuwashawishi siku zote, tusingekuwa na uhakika na uwezo wetu kivita tusingekuja kuomba watuunge mkono, uwezo tunao. Nenda kawaeleze kwa uhakika kama watatoa msaada kidogo tu, basi nchi yetu tumeikomboa kutoka kwenye mikono ya utawala wa Kidikteta na kifashisti", Col. Mkengeri, mmoja wa makamanda wa wapinzani wa serikali ya Zaire alijibu. Wenzake wote walitingisha vichwa kukubali maneno yake.

"Azimio, tunakwenda wote kushiriki kikao hicho", Mpinda alijibu.


ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU