BIBIANE
II
Willy Gamba
alimkuta Col. Rwivanga anakula chakula. Alipomuona Willy alionekana kufurahia
"Nimekusubiri sana mpaka nikaamua bora niendelee na chakula maana ni zaidi
ya saa nne sasa na unajuwa mimi nakula mara moja tu kwa siku, njaa ilikuwa inauma
sana", Col. Rwivanga alijitetea.
"Usijali
Kamanda", Willy alijibu huku akielekea jikoni kuchukua sahani na kisha
akaketi kwenye meza pamoja na Col. Rwivanga na kupakuwa chakula.
"Hiki
chote kilikuwa chako peke yako", Willy alimkejeli Col. Rwivanga.
"Hapana,
nilijuwa tu utanikuta nakula", Col. Rwivanga alijibu huku akicheka. Willy
alichota kijiko cha kwanza na kukitia mdomoni, chakula kilikuwa wali na
mchemsho wa nyama.
"Lo,
mpishi ni wewe?".
"Kwani
vipi?".
"Kitamu
sana chakula hiki", Willy alijibu.
"Wapi,
na wewe una njaa vilevile, upishi wangu mimi ni mchemsho tu".
"Hapana
si njaa ila wali umepikwa vizuri na nyama ya mchemsho, napenda sana mimi",
Willy alieleza.
"Ehe
vipi huko, umewakuta?".
"Bwana
nimewakuta wale mapadri na nimewekwa shule hasa, na sasa hivi naijua historia
ya utawala wa nchi vizuri sana kuanzia kabla ya ukoloni".
"Wacha
bwana".
"Nakuambia
wale mapadri wanaijua nchi hii kuliko viganja vya mikono yao", Willy
alimweleza Col. Rwivanga, kisha akamgusia kwa muhtsari mambo muhimu
aliyoelezwa.
"Kumbe
hili swala la Akazu hata hawa wazee wanalifahamu sana?", Col. Rwivanga
aliuliza baada ya maelezo ya Willy.
"Sana,
na wamesema bila hawa watu kukamatwa hakuwezi kuwa na amani katika nchi
hii".
"Hilo
ni kweli kabisa na sisi tunalijua na ninafikiri ndio walio nyuma ya hili swala
la kutaka kukuua maana hawa watu wana mahusiano dunia nzima na pesa nyingi.
Hivyo, tunajua wanajipanga kuja kutuhujumu, hilo tunajua. Ila hatujui kwa sasa
hivi wanafanya shughuli zao kutoka wapi. Nia yetu imekuwa ni kuimarisha
serikali yetu, halafu ndipo tuangalie habari yao", Col. Rwivanga alieleza.
"Ni
sawa, lakini mimi nafikiri jambo hili mgelishughulikia sasa hivi wakati bado
nao wamechanganyikiwa, lakini mkisubiri watakusanya nguvu halafu itakuwa shida
tena", Willy alishauri.
"Kutokana
na matokeo ya siku hizi mbili nasi tumeshituka sana, maana inaonekana hawa watu
bado wana watu ndani ya serikali yetu na wameanza kutuhujumu. Kama unavyosema,
nasi tumeamua kulishughulikia mara moja swala hili na tutakuwa na mkutano na
makamanda wote wa jeshi pamoja na baraza la mawaziri kesho saa moja na nusu
asubuhi", Col. Rwivanga alieleza.
"Hivyo
itakuwa vizuri. Ingawaje mimi kazi iliyonileta haikuwa ya mapambano, lakini kwa
sababu wao ndio wamenianza na mimi naomba ruksa yako unilinde mbele ya wakubwa
wako, kwani nataka nami kwa kiasi fulani nijuwe habari ya watu hawa na vipi
wameamua kutaka kuniangamiza. La maana hasa nataka nijuwe nani hasa anahusika
na kutaka kuniua mimi. Hilo Col. Rwivanga ningependa sana unipe hiyo nafasi
nifanye kazi yangu", Willy alijieleza.
"Ni
sawa lakini tungeomba na sisi utufahamishe kila hatua unachofanya ili tuweze
kukusaidia itakapobidi kwani ukweli ni kuwa kazi hii ni yetu na wala si
yako", Col. Rwivanga alijibu.
"Asante
Col. Rwivanga. Vipi yule msichana wa jana usiku, Bibiane umepata habari
zake?".
"Ahaa,
ndio nilikuwa nakusubiri nikueleze. Hivi usingewahi ungenikuta nimeshaenda
kumfuata. Huyu msichana inasemekana ni mkalimani, anajuwa lugha kama nane hivi
na amekuwa akifanya kazi serikalini kama mkalimani hivyo, alikuwa akisafiri na
Rais au mawaziri ama maafisa wakubwa wa serikali wanaposafiri nje ya nchi na
vilevile ndiye aliyekuwa mkalimani wa serikali kama wageni wasiojuwa kifaransa
wakija nchini hapa. Inasemekana wakati wa mauaji yeye hakuwepo. Alikuwa
Nairobi, lakini ni kati ya watu wa kwanza kabisa kurudi na amekaa katika nyumba
yake aliyokuwa akiishi toka zamani mtaa uleule wa Silas Biniga, lakini nyumba
ya nne mbele kwenye kona watu wamekuwa hawana wasiwasi nae kwani inasemekana ana
asili ya Kitutsi ingawa ni chotara na uzuri wake watu wengi wameuchukulia tu
kuwa huenda ni chakula ya wazee. Kwa hivyo hakuna ambaye amediliki kumgusa.
Hivyo nataka nikajuwe habari zake", Col. Rwivanga alieleza.
"Hapana,
usiende wewe, maana wewe ni afisa wa ngazi za juu na unajulikana hapa la pili
wewe ni mwanajeshi. Kazi hii ni ya mpelelezi kama mimi. Tatu, nina kisasi naye.
Naomba uniachie, usiku huu lazima nitapambana naye kama bado yuko hapa mjini na
nitakujulisha habari zake baadae".
"Sawa
Willy, kazi kwako, mzee naye alinieleza ndio zako hizo ikibidi msichana au
mrembo".
"Zamani
siyo sasa, sasa nimestaafu maana nimeoa lakini kwa msichana kama yule ambaye
hatishiki na mtu kuuawa, nataka mimi mwenyewe nijuwe habari zake. Habari
ulizonazo ni kwamba bado yuko mjini?".
"Jioni
hii ameonekana akiendesha gari lake aina ya MB 190E. Na hilo ni gari lake hata
kabla ya mauaji na kabla sisi hatujaingia hapa. La ajabu si sisi wala si
Intarahamwe aliyegusa gari lake, ni jambo la kushangaza na limefanya nitaka
kujuwa huyu binti vipi mambo yake".
"Basi
niachie maMBO yake utayapata. Si bure huyU binti ni mtu hatari, na hatari
sana".
ITAENDELA
0784296253
Comments
Post a Comment