BIBIANE
IV
Wakati Willy
anafika nyumbani kwa Bibiane. Col. Gatabazi alikuwa akifunguliwa lango la mbele
nyumba hiyo akatoka na kuondoka akihofia matatizo aliyokumbana nayo kwa Luteni
Biniga. Willy alichukuwa hadhari kubwa sana maana alichukuwa vifaa vya kazi si
mchezo. Kwa vile nyumba ya Bibiane ilikuwa kwenye kona ya barabara mbili, Willy
alibana kwenye kona moja na kuchungulia mbele ya nyumba na kuona lango
likifunguliwa. Alimuona mtu mmoja akitoka na kukatisha barabara na kuelekea
kwenye uchochoro na kutokomea. Willy alirudi nyuma kidogo na kuhisi kuwa sehemu
ile ndiyo ilikuwa nyuma ya nyumba hii. Kwa hadhari sana alikwea ukuta
uliozungishiwa vyuma vilivyochongoka juu. Kwa vile Col. Rwivanga alimweleza
kuhusu hilo. Willy alikuwa amejitayarisha vizuri kabisa kwa lolote. Alikwea na
kuchungulia ndani, baada ya kuangaza vizuri macho yake aliweza kuona kivuli cha
mtu amebana kwenye ukuta wa nyumba hii karibu na upande wa pale alipokuwa yeye.
Mtu huyu alikuwa amebeba bunduki kubwa. Hivyo, Willy alihisi ni mlinzi wa pale nyumbani.
Baada ya
muda kidogo, Willy alimuona mtu mwingine anakuja akitokea upande wa mbele kuja
upande huu ambao huyu mwingine alikuwa amebana. Willy alijining'iniza juu ya
ukuta kwa nje ili asionekane huku macho yake yakiwa usawa wa ukuta. Yule mtu
alikuja moja kwa moja mpaka usawa wa yule mwingine alipokuwa amesimama.
"Unataka
sigara?", yule aliyekuja eneo hilo alimuuliza mwenzake.
"Sitaki,
hao jamaa ndani si wamalize mambo yao haraka ili waondoke na sisi twende zetu,
maana hapa tunapoteza muda na huku kazi yenyewe bado", yule wa pili ajibu.
"Mbona
kama una wasiwasi, vipi unaogopa?".
"Kwanini
nisiogope, mimi si binadamu bwana?".
"Acha
woga wewe, wajuwa Kaisari alisema watu waoga mara nyingi hufa kabla ya tarehe
ya vifo vyao kufika, komaa mtoto wa kiume", mwenzake alisema kwa
kujiamini.
"Bwana,
hebu nenda kalinde sehemu yako na umwambie huyo Nkubana aharakishe kutoka
sehemu hii".
Baada ya
kuelezwa, yule mtu aliyekuja sehemu hii kutoka mbele aliondoka kimyakimya
kurudi kule alikotoka huku mwenzake akimsindikiza. Willy akatumia nafasi hiyo.
Kama tumbili aliukwea ule ukuta haraka sana. Kufumba na kufumbua akaruka juu ya
vile vyuma na kujitosa ndani bila hata kusababisha kishindo na kujibanza kwenye
ukuta. Kwa vile Willy alikuwa amevaa nguo nyeusi pale alipokuwa amejibanza
ilibidi umsogelee karibu sana ndipo uweze kumtambua maana upande huu wa nyumba
hapakuwa na mwanga. Mara akamsikia yule mlinzi akirudi upande wake, kutokana na
mazungumzo aliyokuwa ameyasikia alihisi hawa nao bila shaka walikuwa kundi lilelile
kama alilopambana nalo kwa Luteni Biniga. Bila shaka walikuwa wamekuja kwa
malipo kwa huyu mwanamke. Willy alijitayarisha na kujibanza kwenye ukuta
utafikiri buibui. Yule mtu alikuja akinyata taratibu utafikiri alikuwa amehisi
kitu. Willy alikuwa amebana kwenye kona kabisa ya upande wa pili wa nyumba.
Huyu mtu alipofika hapo tu, kama Simba anapomrukia Swala, Willy alimtia kabali
kwa nguvu zake zote. Yule mtu hakuweza hata kuguna maana kabali ile ilikuwa
kali, na huku akitumia utaalam kumuua kimyakimya kwa kumnyonga, Willy alimuua
yule mtu. Kisha, alimvuta mpaka kwenye ua wa nyumba na kumvua shati, akavua
lake na kuvaa la yule mtu kwani ukubwa wa mwili na urefu walikuwa wanalingana.
Akatwaa silaha yake ya AK 47 'Machinegun' ya Kirusi na kuelekea mbele.
Alipofika
kwenye kona ya mbele, Willy alimuona yule mtu mwingine akichungulia dirishani,
si mbali na aliposimama Willy. Willy alikohoa kidogo na yule mtu akageuka
kuangalia. Alionyesha ishala ya kumwita. Na yule, akijuwa fika kuwa alikuwa
mwenzake, alikuja haraka bila hadhari. Alipokaribia, na kwa ajili ya giza
aliamini ni yule mwenzake, alianza kusema, "Huko ndani naona mambo
yanaa...", kabla hajamalizia sentesi yake, Willy alimrukia na kumpiga
karate ya shingo na kumuua palepale. Alianguka chini kwa kishindo, na Willy
alipomrukia pale chini akammaliza. Baada ya Willy kumkagua alimkuta na Bastola
mbili, moja yenye kiwambo cha sauti na nyingine ya kawaida. Vilevile alimkuta
na kisu ambacho ukikibonyeza kinachomoka na kutoka urefu wa nchi tisa. Kile
kisu kilikuwa silaha hatari sana ikitokea watu wanapigana huku mmeshikana.
Willy alijihisi mtu mwenye bahati kwani silaha kama hii kama ingebidi kumenyana
bila kujuwa kuwa mtu anayo anakuondoa duniani haraka sana.
Sasa Willy
alikimbia mbele kuangalia kama kulikuwa na mtu mwingine, lakini hakukuwa na
kitu. Alipozunguka upande mwingine tena hakuna kitu. Kisha akachukua dakika
chache kuhakikisha kuwa hakuna hatari nyingine, na alipohakikisha ndipo
alipokwenda pale dirishani alipokuwa anachungulia yule mtu wa pili. Dirisha
lile lilikuwa sebuleni na lilikuwa wazi kidiogo. Pazia la dirisha lilikuwa
limerudishiwa kidogo kiasi kwamba ungeweza kuona ndani na kusikia maneno yote
yaliyokuwa yanazungumzwa.
Willy
alishangazwa kuwaona wanaume watatu na mwanamke mmoja ambaye mara moja
alimtambua kwani alikuwa Bibiane. Hawa wanaume wote walikuwa wametoa Bastola
zao wakizungumza na yule mwanamke. Wawili walikuwa wamesimama na mmoja ameketi
kwenye kiti kilichokuwa kinaangaliana uso kwa uso na alichoketi Bibiane.
"Nakwambia
hivi, sisi tumetumwa kuja kukuua na huyo huyo bwanako Jean. Faida yako kwake
imesisha sasa wewe ni mzigo na yeye hataki kubeba mzigo", yule aliyeketi
alimweleza yule mwanamke huku akionyesha kwenye sura yake maudhi na usongo wa
ajabu.
"Wewe
unatania. Jean! hawezi kusema hivyo. Kwa yote niliyomtendea na jinsi
tunavyopendana, Xavier sema jingine kama wewe na Col. Gatabazi mmeamua kuniua
basi niuweni, msimsingizie Jean, Jean ni wangu wa kufa na kuzikana",
Bibiane alijibu huku akionyesha sura ya hofu maana aliwajuwa hawa jamaa ni
wauaji.
"Wanawake
ni watu wa ajabu. Epa", yule mtu ambaye Bibiane alimwita Xavier alimwita
mmoja wa wale waliosimama.
"Eee",
yule mtu alijibu kwa woga vilevile.
"Siku
zote nakwambia wanawake ni wajinga, wewe huamini. Huyu anafikiri eti Jean
alikuwa anampenda, Jean alikuwa anamtumia tu kama chombo. Kwanza alikuwa
anakutumia kwa mambo yake ya kazi zake za kumwingizia pesa na pili, anapokuwa
huku Afrika alikuwa akijisaidia kutimiza haja zake za kimwili; hata siku moja
hajawahi kukupenda. Pale tu wewe na Col. Gatabazi mlipomweleza kuwa wewe
umemwona Willy Gamba na Willy Gamba kukuona mara moja alijuwa Willy Gamba
atakutafuta na akikupata utatoa siri, na ukitoa siri si ndiyo mambo yetu
yameisha! kwa hiyo, mara moja ametoa hukumu ya kifo kwako na sisi tumekuja
kutekeleza amri. Kwa kweli ni uhalibifu kwa kiumbe kizuri kama wewe kuuawa,
lakini wewe sasa ni mzigo kwetu nasi hatubebi mzigo," Xavier alieleza.
Kwa maelezo
haya Bibiane alijua kweli hukumu imetoka kwa Jean na huo ndio ulikuwa mwisho
wake. Pamoja na ujuzi wake wote wa kupigana hakuthubutu mbele ya Xavier na
wenzake kwani aliwajuwa vizuri, walikuwa wabaya mara kumi yake, na alijuwa kuwa
hao hawabembelezeki hivyo, alikata tamaa na hasira zikampanda dhidi na Jean na machozi
yakaanza kumtoka.
"Ukionana
naye mwambie atakufa kifo kibaya sana. Nami naamini kuwa huyo Willy Gamba
anayemuogopa kweli ndiye atakayenilipia kisasi", Bibiane alisema huku
akitetemeka kwa hasira.
Xavier
alisimama na kurudisha kiti chake nyuma. Bibiane naye akataka kusimama.
"Hapana, kaa hapohapo, usilete ujanja hapa. Huyo Willy baada ya muda si
mrefu mtaonana ahera, nasikia huko watu huonana tena. Hamtapishana zaidi ya
masaa mawili na yeye atakuwa marehemu kama wewe".
Willy,
ambaye alikuwa anasikia na kuona yote haya akiwa dirishani, alipoangalia usoni
mwa yule aliyeitwa Epa, akajuwa huyu ndiye akayemuua Bibiane. Aliangalia nafasi
aliyokuwa, akajuwa angeweza kumpiga risasi Epa na yule mwingine, lakini si
Xavier. Kwa vyovyote Xavier angemmaliza Bibiane, lakini hakukuwa na njia. Hawa
walikuwa ni wauaji wataalam, tena huenda wa kulipwa. Hivyo, ilikuwa ni afadhali
kwake kupambana na mmoja kuliko watatu na kwa maajabu ya Mungu angeweza
kumponyesha Bibiane ambaye akili yake ilimweleza kuwa angeweza kuwa mtu muhimu
kwake.
Xavier
alimkonyeza Epa. Yeye akavuta kiti na kuanza kugeuka. Bibiane akafumba macho,
lakini kabla Epa hajafyatua risasi, palepale Willy akiwa dirishani na mikono
yake yote ikiwa na Bastola, alimpiga risasi ya kichwa Epa na yule mwingine
kifuani, na Bibiane akajirusha nyuma ya kiti, Nkubana kama umeme akamimina
risasi dirishani. Lakini Willy alikuwa tayari amejitupa chini na kujiviringisha
na kisha kuchukua AK 47 akamimina risasi kama hamsini hivi kumtia kiwewe
Nkubana. Haya mambo yote yalitokea haraka sana kama kufumba na kufumbua.
Nkubana alipoangalia akajuwa Epa na Karekezi walikuwa wamekufa na hakujuwa
wamezungukwa na watu wangapi. Alijirusha kwenye dirisha upande wa pili ambalo
lilikuwa la kioo kitupu na kuangukia nje na kisha kujiviringisha tena. Bibiane
alichukua Bastola iliyodondoka kutoka kwa Epa na kujaribu kumpata Xavier lakini
naye alijitosa nje akaurukia ukuta wa mbele kwa nanma ya ajabu na kuangukia
uapnde wa barabarani. Willy alipokimbia upande ule wa pili ili kumuwahi Nkubana
alikuwa amechelewa, Xavier naye alikuwa ndio anaishia baada ya kuruka ule
ukuta.
Bibiane
alipoinuka pale alipokuwa amejitupa kumfuata Xaviar akajikuta anaangalia kwenye
mdomo wa AK 47.
"Tupa
silaha yako mama, uko chini ya ulinzi", Willy alimweleza Bibiane.
"Aheri
ya Musa kuliko ya Firauni, Bila shaka wewe ni Willy Gamba".
"Naamini
wewe ni Bibiane".
Willy
alimshika mkono Bibiane na bila hata kumwelezana wanaelekea wapi, wakakimbia
kwa tahadhari kuwa kutoka eneo hilo kabla askari na watu wengine hawajafika
kuangalia kilichotokea hapo kwani mlio wa risasi za Ak 47 ulikuwa umetikisa
eneo hilo na kusikika vibaya sana wakati huo wa usiku.
ITAENDELEA
COL. NI AFISA WA JESHI MWENYE CHEO CHA KANALI 0784296253
Comments
Post a Comment