KASHESHE
XI
Nkubana
aliamua kuwasiliana na Col. Gatabazi kwa simu ya upepo. Alipompata alikuwa tayari
amewasili Goma na walikuwa wameanza mkutano. Nkubana alieleza kwa kirefu yote
yaliyotokea na kisha akashauri. "Huyu Willy Gamba hajui nguvu zetu. Hivyo,
ameamua kwenda kujinyonga huko Kibumba, mimi naelekea huko kwenda kuongeza nguvu na kuwashitua
makamanda wetu ili tumkamate kabla hajaleta kasheshe zake".
"Sawa,
fanya hivyo, Jean anahitaji kumuona akiwa hai", Col. Gatabazi alikubaliana na Nkubana na kumweleza shabaha ya bosi wao Jean.
"Vilevile
nitazungumza na makamanda hapa ili waniruhusu tupeleke jeshi mpakani kumsaidia
Luteni Nyamboma kudhibiti mpaka wa Zaire, mpaka hapo amri ya kuishambulia
Rwanda itakapotoka. Sisi tuko tayari, naamini uamzi utatoka haraka ili kazi
ianze alfajiri ya leo. Hebu ngoja kidogo usizime radio yako", Col.
Gatabazi aliwaeleza wenzake mambo yalivyokuwa Gisenyi na jinsi ambavyo Nkubana
alikuwa akihisi kuwa Willy ameelekea Kibumba. Mara moja Jean alisimama baada ya
kusikia habari hii ya Willy kuelekea Kibumba. Haraka alichukua radio na kutoa
maagizo kwa Nkubana.
"Sikia,
sisi tunakuja huko sasa hivi, tutakuja kwa ndege yangu na mimi nitaondoka. Sasa
hivi bado tunawasiliana na Kamanda Bazimaziki awahi uwanja wa ndege. Waeleze
wakiwakamata Willy na Bibiane wasiwaue kwanza mpaka tufike, hao ni halali
yangu", Jean alitoa amri.
"Unafikiri
ni busara sisi viongozi wa juu kwenda huko?", Anatoile kabuga alihoji.
"Bila
shaka, huko ndiko yaliko majeshi yetu na ndiko tutakapotoa amri", Jean
alieleza msimamo wake.
"Mimi
pia nafikiri tuwe pale wakati wanajeshi wanaelezwa kukaa tayari kwa ajili ya
kuanza vita alfajiri, hii itawaongezea mori", Jenerali Kasongo alijibu.
"Na
mimi nimefurahi sana kwa uamzi huo, kuanzia sasa ofisi yetu kubwa ya kuratibu
shughuli za vita itakuwa hukohuko Kibumba, maana ndiko kwenye vifaa vyote,
sioni sisi tutafanya nini hapa wakati kila kitu chetu kiko kule", Col.
Gatabazi alieleza kwa sauti ya juu.
"Sawa,
wengi wape", Kabuga alijibu.
Kisha
wakawasiliana na Col. Marcel Bizimaki, ambaye ni Kamanda wa jeshi la Akazu
wakitumia njia ya simu ya satellite, wakamweleza kuwa wote walikuwa wanarudi
hapo tena, kwa ajili ya kutoa mwongozo na ruksa ya kuanza mapambano dhidi ya
adui alfajiri ile. Vilevile, alielezwa aweke vikosi vyake vyote kwenye
tahadhari ili waweze kumsaka na kumkamata Willy Gamba akiwa hai.
"Karibuni,
nitawapokea na nitawaweka kwenye nyumba ya mkufunzi wetu mkuu. Kamanda Moris
ambayo ina ulinzi mkali pia inalindwa na mitambo ya kisasa ya usalama. Na
mtakapokuwa pale kwake itakuwa rahisi kwenu kuona kwa macho jinsi majeshi yetu
yanavyosonga mbele kupitia mitambo ya kisasa kabisa", Col. Bizimaziki
alitamba.
Kundi zima
liliondoka kuelekea uwanja wa ndege, likiwa tayari kuelekea Kibumba, ambako
kuna umbali usiozidi dakika kumi kwa ndege, Jean alifikiria kuwa ni vizuri kuwa
na ndege yake karibu, ikiwa kwa bahati mbaya kikatokea kitu na kutakiwa
kuondoka ghafla na kujisalimisha aweze kufanya hivyo kwa ndege yake. Wakati
wanaelekea uwanja wa ndege. Co. Gatabazi aliwasiliana tena na Nkubana.
"Uko
wapi sasa?".
"Nimekwisha
kuwasili Kibumba na sasa naelekea kwenye lango kuu la kuingilia ndani,
nimewasiliana nao kwa radio wananisubiri", Nkubana alimweleza Col
Gatabazi.
"Sawa,
kazi yako kubwa ni kumkamata huyo Willy na kikaragosi chake huyo Bibiane na
uwalete kule mlimani ilipo nyumba ya Kamanda Moris, sisi tutakuwa huku muda si
mrefu", Col. Gatabazi aliagiza.
"Nitafanya
hivyo afande. Mara hii kaingia mkenge yeye mwenyewe", Nkubana alijibu.
"Lakini
mtu huyu ni hatari sana, naomba umwambie Kamanda Bizimaziki mchukue tahadhari
kubwa sana. Hata tulipofika sitaki makosa yatokee", Col. Gatabazi
alisisitiza.
"Sawa
afande, tutafanya hivyo, lakini mtu mmoja na mwanamke mmoja wanaweza kufanya
nini mahali kwenye kambi kubwa ya jeshi kama Kibumba?", Nkubana alihoji.
"Wewe chukua
hadhari ya hali ya juu huyu mtu si wa kawaida", Col. Gatabazi alisisitiza
na kuzima radio.
Nkubana
alifahamu kuwa viongozi wake walikuwa na mashaka na Willy, lakini Nkubana yeye
hakuna na wasiwasi. Aliamini kuwa huu ndio ulikuwa mwisho wa Willy Gamba.
Ulinzi na uwezo wa kambi ya Kibumba ulikuwa mkali mno, kiasi kwamba ilikuwa
vigumu sana kwa mtu mmoja kuingia na kutoka salama. Gari lilisimama na
kumwondoa Nkubana katika mawazo yake. Walikuwa wamefika kwenye lango kuu na
kusimama kama ilivyo sheria ya kusimama na kukaguliwa kabla ya kuingia ndani ya
ngome hii.
Nkubana
alipoangalia saa yake ilikuwa yapata saa sita na nusu usiku.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment