Waswahili
wanasema, hujafa hujaumbika, msemo huu una maana kubwa sana kwa binadamu
hususan wale waliopatwa misukosuko ama majanga makubwa kama Ndugu Fidelis Duwe (pichani), mkazi
wa Mbamba-Bay, Wilaya ya Nyasa, mkoani Ruvuma.
Duwe kijana shupavu
mwenye mwili wa wastani uliojengeka alikumbwa na dhoruba kubwa iliyosababisha baadhi ya
viungo vyake vya mwili kubaki majini wakati akikabiliana na Mamba hatari aliyemkamata
ili awe kitoweo chake.
Uhodari wa
Duwe umesababisha awepo kwenye historia ngumu ya watu waliobahatika kuponea
kwenye tundu la sindano, unaweza kusema chupuchupu kuliwa na Mamba mwenye njaa kali. Alikamatwa na Mamba wakati
akiogelea ndani ya Ziwa Nyasa, katika eneo liitwalo Zambia (siyo nchini Zambia).
Duwe anasema
ilikuwa jioni, wakati alipokwenda Ziwani kwa ajili ya kuoga kama ilivyo kawaida
ya wananchi wa Mbamba-Bay, wakati anapaka sabuni mwilini ghafla alinaswa na
Mamba mwenye njaa kali na akaanza kumkata viungo vya mwili wake kwa meno makali.
“Baada ya
kupaka sabuni, nilitaka nirudi ili niondoe sabuni mwilini, ghafla
nilikamatwa na Mamba, tukaanza kushindani, wakati yeye analazimisha kunipeleka
chini mimi nilikuwa najaribu kumvuta ili nisiende chini”, anasema na kuongeza
kuwa alipambana na Mamba huyo kwa dakika 15.
Anasema
wakati anaendelea kupambana na Mamba huyo ndani ya maji alisikia sauti za
wavuvi wakipita huku wakiimba ndani ya Mtumbwi wao, bahati nzuri alizifahamu
sauti zao hivyo akapiga kelele kuomba msaada.
“Waliniuliza
wewe unafanya nini hapo, kuna Mamba wakali sana hapo, mimi niliwaambia kuwa hao
Mamba unaosema mmoja kanikamata ndio niko naye hapa, kwanza walidhani nafanya
dhihaka, lakini baada ya kutafakari walikuja na kuniokoa, Mamba akaniacha na kukimbia”, anasema Duwe.
Anasema
pamoja na kuokolewa kutoka midomoni mwa Mamba, alikuwa amejeruhiwa vibaya,
mikono yake yote ikiwa imekatwa mara tatu na damu nyingi zikimvuja. Hakuna alieamini
kuwa atapona kutokana na hali mbaya aliyokuwa nayo wakati huo.
Duwe
anasimulia kuwa baada ya kuokolewa kutoka majini na wavuvi aliowataja kwa
majina ya Benard Mpay na Sikuzani ambaye sasa ni marehemu, alipelekwa haraka
hospitali ndogo ya Mbamba-Bay, ambako alipata huduma ya kwanza na baadaye
akapelekwa Liuli ambako alipata huduma ya uhakika.
Mungu
alinisaidia sana, baada ya kuokolewa kutoka midomoni mwa Mamba, nilipelekwa
hospitali, walinifanyia huduma ya kwanza, lakini hawakuwa na vifaa vya uhakika,
bahati nzuri siku hiyo kulikuwa na Meli, ikanipeleka Liuli ambako nilipata
huduma ya haraka, nikashonwa na kuungwa mifupa ya mikono yangu, leo niko hai”,
anaesema na kuonyesha majeraha makubwa aliyopata mwilini.
Kuhsu
mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa, Duwe anasema, Malawi inajaribu kufurahisha
umma, kwa kuwa hakuna asiyejuwa kuwa mpaka halisi wa nchi hizi yaani Tanzania
na Malawi ni katikati ya Ziwa Nyasa. Hivyo amewataka viongozi wa nchi hizi
kukaa katika meza ya mazungumzo.
Anasema ni
kweli kabla ya Nyasa kuwa WIlaya, walikuwa wakipata baadhi ya huduma za jamii
kwa karibu kutoka Malawi, lakini wamalawi pia walipata huduma zingine kutoka
Tanzania kama ilivyo sehemu zingine zilizopakana na Tanzania.
Duwe
ameiomba serikali kuongeza kasi ya miundombinu, kwani hivi sasa wananchi
walioko sehemu hiyo wanapata mawasiliano ya karibu kutoka Malawi, tofauti na
Tanzania hivyo likitokea jambo lolote Tanzania hawawezi kujua kama ilivyo kwa
Malawi.
IMEANDIKWA
NA NYAKASAGANI MASENZA 0784296253
MWANNDISHI MWANDAMIZI WA ZBC, MSANGU SAID AKIONGEA NA NDUGU FIDELIS DUWE, KANDO YA ZIWA NYAMA, MAHALI AMBAPO ALINUSURIKA KULIWA NA MAMBA..
SEHEMU YA ZIWA NYASA, MAHALI AMBAPO NDGU FIDELIS DUWE ALIKUWA AKIOGA KABLA YA KUKAMATWA NA MAMBA NA HATIMAYE KUOKOLEWA NA WAVUVI.
HAPA NI ZIWA NYASA, SEHEMU YA MBAMBA-BAY KARIBU NA MPAKA WA MALAWI.
Comments
Post a Comment