KASHESHE
X
Willy na
Bibiane walitambaa chini kwa chini kama nyoka na hatmaye wakayafikia majengo
yaliyokuwa upande wa pili kutoka sehemu waliyotokea.
"Haya
ni maghala ya kuhifadhia silaha, ni makubwa sana yana silaha nyingi za
kisasa na vifaa vya kila aina vya kijeshi, zikiwemo silaha mpya za kisasa
kabisa kwa ajili ya vita", Bibiane alieleza.
"Itabidi
tuingie ndani kwanza ndio tutajua cha kufanya", Willy alieleza.
"Mlango
uko upande ule kabisa, yaani unatazamana na majengo ya upande ule kabisa,
ambako ndiko kuna ofisi na nyumba za kulala askari. Ulinzi upande ule ni mkali
sana na lango la upande ule linafunguliwa kwa chombo maalumu ambacho
kinahifadhiwa kwa mmoja wa makamanda wa juu wa jeshi lao", Bibiane
alieleza.
"Kuta
za maghala haya zimejengwa kwa teknolojia gani, au wametumia nini kujenga, tofali za simenti ama mabati?", Willy
aliuliza.
"Kampuni
moja ya Afrika Kusini iitwayo Super Frame ndiyo iliyojenga maghala haya pamoja
na mabanda yote unayoyaona tena kwa muda wa mwezi mmoja tu. Kila kitu kililetwa
hapa kwa helkopita kubwa zilizokodishwa kutoka Urusi na hapa waliunganisha tu
hizi kuta na kuezeka. Wakati wa joto kuta zake zinaleta ubaridi na wakati wa
ubaridi kuta hizi zinaleta joto, hivyo sijui zimetengenezwa kwa teknolojia
gani?", Bibiane alijibu.
"Nimeelewa,
baada ya hayo maelezo yako, teknolojia hii imetoka Marekani na inatumika kwa kujenga
nyumba za gharama nafuu, lakini zenye kudumu kwa muda mrefu hata zaidi ya
matofali ya saruji", Willy alijibu.
"Wewe
kuna kitu usichokijua katika Ulimwengu huu", Bibiane alitania kisha
akaendelea. "Sasa tunafanyaje Bwana kujua?".
"Utaona,
sasa hivi tutaingia ndani", Willy alijibu kisha akafungua na kupekua kwenye mkoba
wake, akatoa kifaa kimoja kilichofanana na kalamu lakini hiki ni kinene kidogo. alikifungua
akatoa mfuniko wa mbele na kukifungua tena nyuma, baada ya kukifungua zilitoka
betri mbili ndogo sana, Willy akazikagua kuona kama ziko sawa, kisha akazirudisha.
"Haya,
rudi nyuma hiki chombo kinatoa miale aina ya leza bimu na hii miale ina nguvu za ajabu na
miale hii inakata huu ukuta utadhani kisu ndani ya siagi, rudi nyuma yangu
kabisa", Willy alisema Bibiane akarudi nyuma kwa hofu.
"Nasubiri kuona", Bibiane alitania.
"Subiri utaona japokuwa umeingiwa na hofu, lakini usiogope maana hapa hakuna ujanja zaidi ya kumuomba Mungu".
Willy
alisukuma nyuma ya kile chombo kama mtu anavyosukuma kalamu wakati anataka
kuandika, na mara moja miale myekundu ilijitokeza Willy akaielekeza kwenye
ukuta na taratibu alikata saizi ya mlango sehemu ile walipokuwa, alipomaliza
akakizima kile kifaa chake.
"Mbona
hujakata chochote?", Bibiane aliuliza.
"Subiri
kidogo, hii ni sawa na sayansi inayotumiwa na madaktari siku hizi kupasua mwili
wa binadamu, wewe uko wapi mama, wenzio twaelekea karne ya ishirini na moja,
karne ya sayansi na teknolojia wewe bado upoupo tu. Siku hizi mtu anafanyiwa opresheni, anapasuliwa
tumbo, halafu baada ya saa moja anarudi nyumbani mwenyewe na haoni sehemu iliyopasuliwa",
Willy alimkoga Bibiane aliyekuwa anashangaa.
Willy
aliiangalia saa yake kisha akaufungua mkoba wake akatoa kitu kama bawaba kisha
akaipachika kwenye ukuta kikanasa.
"Hiyo
ni sumaku?", Bibiane alihoji.
"Ndiyo,
inashika kitu chochote hata kama ni mbao".
"Ama
kweli wewe mkali Willy, sikutegemea kabisa".
"Au
vipi", Willy alijibu. Huku akiitumia ile bawaba alivuta taratibu na ile
sehemu ikachomoka na kuacha uwazi wenye ukubwa wa mlango.
Willy na
Bibiane walijikuta wanaangalia ndani ya ghala kubwa sana lililojaa silaha.
"Ingia
sasa, mbona kama umepigwa na radi!" Willy alimweleza Bibiane.
"Bado
nashangaa, hakika mambo uliyonionyesha ama kweli ujuzi huzidiana", Bibiane
alijibu huku akiingia ndani ya ghala la silaha.
Willy
akitumia chombo kingine kwa kukishikanisha na ile bawaba, ile bawaba ilitoka
akaiweka upande mwingine wa kipande cha ukuta alichokuwa amekata, kisha na yeye
alipoingia ndani ghala alivuta kile kipande cha ukuta kwa nguvu zake zote na
kukipachika mahali pale tena. Mtu yeyote angepita pale kwa macho tu bila
darubini asingejua kuwa pale pamekatwa. Bibiane hakuna na neno la kusema
isipokuwa kuangalia ile sehemu tu.
"Wewe
ni mkali kwelikweli", Bibiane alirudia kusema.
"Kwa
mambo mengi si hili tu", Willy alisema kwa kumwemwesa.
wakiwa ndani
Willy alishangaa kuona ghala kubwa sana la silaha. Kwa vile taa zilikuwa
zikiwaka kwa ndani hawakuamini macho yao. Hata Bibiane hakujuwa kuwa Akazu
walikuwa wamejiimarisha kiasi hiki. Mara ya mwisho Bibiane kufika hapa ilikuwa
kama miezi mitatu iliyopita na katika hii miezi mitatu silaha nyingi, yakiwemo
makombora ya masafa marefu na mafupi, vifaru, ndege aina ya MIG 21 na 23.
mizinga, magari ya kivita, helkopita za kivita zilikwishaletwa eneo hili!
Hakika ilikuwa ajabu na kweli.
"Hawa
watu wanajipanga kupigana na Rwanda tu ama nchi nyingine jirani?", Willy
aliuliza kwa mshangao.
"Nia
yao ni kupigana na serikali ya Rwanda basi, hakuna kingine", Bibiane
alijibu na kuongeza. "ila wanataka kuyapiga majeshi ya RPF kipigo
kitakatifu, wasijejaribu tena mara baada ya kufukuzwa Rwanda".
"Fedha
za kununulia vifaa hivi vyote watakuwa wamepata wapi?", Willy aliuliza.
"Miaka
yote hii unafikiri walikuwa wakifanya nini?, wamewaibia wananchi mali zao zote.
Akazu na Jean ni matajiri ajabu. Wana uhusiano na Rais wa Zaire na kiongozi wa
waasi wa UNITA kule Angola. Almasi za Angola na Zaire dalali wake ni Jean. Sasa
wewe fikiria wana utajiri wa kiasi gani?", Bibiane alijibu.
"He,
sasa nimekuelewa mama".
"Kila
kitu kilipangwa kwa ustadi wa hali ya juu. Hii ingewezekana kuchukua silaha zao
kwa kutumia muda mfupi sana kwama wangeshambuliwa. Willy aliamini kuwa hii
kweli ilikuwa kazi ya askari wa kukodishwa kwani hakika hili lilikuwa ghala la
silaha lililotayarishwa na kupangwa na watu wenye ujuzi wa juu sana.
Willy na
Bibiane walitembea kwa hadhari lakini kwa haraka wakijificha ndani ya vivuli
vya zile silaha. Waliziangalia silaha hisi kiasi kwamba walianza kusahau
kilichowaleta hapa.
"Unayaona
makombora haya Willy", Bibiane alimwonyesha Willy makombora
yaliyotengenezwa Urusi. Kisha akaendelea. "Haya makombora ni aina ya SAM
16 yalitekwa na majeshi ya Ufaransa wakati wa vita vya Ghuba, Februari 1991 na
kupelekwa kwenye maghala ya silaha huko Ufaransa lakini kutokana na mahusiano
wa karibu kati ya Jean na viongozi w ngazi za juu wa Ufaransa waliamua kumuuzia
Jean makombora hayo. Katika makombora haya yamo yaliyotumika kuipiga ndege
iliyokuwa imewabeba marais wa Rwanda na Burudi Aprili 6, 1994. Ni Jean na Akazu
ndio waliamru rais auawe kwa sababu alikuwa ameanza kwenda kinyume na maagizo
yao wakati wa mkutano wa Arusha, nakumbuka niliwahi kukueleza".
"Kama ndivyo,
basi hawa Akazu na Jean ni wabaya kwelikweli, sasa naamini", Willy alisema
huku hasira zikimpanda dhidi ya watu hawa.
"Lililobaki
sasa ni kuziteketeza silaha hizi zote, naamini kuwa jeuri na nguvu ya Jean na
Akazu tutakuwa tumeimaliza", Bibiane alieleza.
"Mkuki
wa nguruwe, kwa binadamu mchungu, itabidi sasa tutumie yale mabomu yako
aliyokuletea Jean, maana kazi kama hii ndio saizi yake", Willy alishauri.
"Unafikiri
kwanini nilisema tuyachukue, nilijua. Kwanza ni madogo, na pili yana nguvu
kubwa ya ajabu. Ghala kubwa kama hili, matano au sita yanaliteketeza kabisa na
hakibaki kitu. Hili senduku linatosha kuiteketeza Kigali nzima. Nia ya Akazu
ilikuwa wakishindwa mpango huu basi waiteketeze Kigali nzima na vyote vilivyomo
bila kujali maisha ya watu", Bibiane alieleza.
Willy
alimwangalia Bibiane kwa jicho kali, baada ya kutafakari akaelewa kwanini Willy
alibadilika vile, ikamlazimu Bibiane kubadili maneno. "Haya tuyatege,
nafikiri ulikuwa unasoma maelezo sasa unajua nini cha kufanya".
"Bila
shaka", Willy alijibu sasa akiwa makini tayari kwa kazi. Kwa hesabu zake
alitega mabomu ambayo alihakikisha angeteketeza kila kitu ndani ya lile ghala.
Bila kushitukiwa walitoka kwa kupitia sehemu ileile na kisha wakairudishia ile
sehemu ya ukuta kiasi kuwa hakuna ambaye angefikiria kuwa kuna mtu aliyewahi
kupitia pale.
"Umesema
kama ukitumia hii saa ya kulipua haya mabomu unatakiwa kuwa umbali gani, nina
maana haya mabomu tuliyotega", Bibiane aliuliza huku wakiambaa na ukuta
kuelekea kwenye mabweni ya kulala askari.
"Umbali
usizidi kilomiota moja", Willy alijibu.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment