GISENYI
VIII
Willy Gamba
na Bibiane walisafiri salama kutoka Kigali mpaka Gisenyi bila kukutana na
kituko cha aina yoyote Barabarani. Lile gari lenye alama ya Msalaba Mwekundu liliwafanya wasafiri bila
kupata usumbufu na habari zilikuwa zimetumwa mapema na wale askari watatu
waliotumwa kutangulia mbeke ili lile gari la maofisa wa Msalaba Mwekundu lisibugudhiwe.
Walipofika Ruhengeri walipumzika huku kila mmoja wao akili yake ikifanya kazi
jinsi ya kukabiliana na jambo lililokuwa mbele yao.
Baada ya mapumziko ya saa
moja hivi, Willy na Bibiane waliendelea na safari yao na kuwasili Gisenyi saa
nane za mchana. Moja kwa moja walikwenda Hoteli Meridien-Izuba, ambako
walipanga kuonana na maofisa ambao Col. Rwivanga alikuwa amewapasha habari
waonane nao na wawape habari kamili kuhusu uhalifu unaofanywa huko Gisenyi na Kibumba,
ili kama walikuwa wamebahatisha kupata habari zozote wazipate hapo.
Meridien
Hoteli Izuza ilikuwa moja ya hoteli nzuri sana ingawa vita vya wenyewe kwa
wenyewe nchini Rwanda vilikuwa vimeiathiri kidogo hoteli hii, lakini ilibaki kuwa safi pamoja na
misukosuko ilivyokuwa sehemu hii. Ikiwa kwenye ufukwe wa Ziwa Kivu, mpakani mwa
Zaire, huku kwa mbali ukiangalia milima ya volkano ya Virunga, kweli
Meridien-Izuda palikuwa mahali pazuri sana pa kupumzika.
"Umepapenda
hapa?", Bibiane alimuuliza Willy Gamba.
"Mbona
wewe unapenda kusoma mawazo yangu?", Willy aliuliza.
"Ubaya
uko wapi Willy, fikiri kama tungekuwa tunakuja hapa kwa ajili ya mapumziko na
si hii kazi ya hatari, huoni kuwa ingekuwa raha sana, mimi naona tungestarehe
sana", Bibiane alijibu.
Huku
akitabasamu Bibiane alitoa mkoba wake ndani ya gari huku Willy akijibu. "Sawa mama
umeshinda".
Baada ya
gari la Msalaba Mwekundu lililokuwa likitumiwa na Willy na Bibiane kusimama,
askari wanne walielekea kwenye gari hilo, walipofika karibu mmoja wao moja kwa
moja akauliza. "Natumaini nyinyi ni Bwana na Bibi George Mambo wa Msalaba
Mwekundu kutoka Makao Makuu Nairobi?".
"Bila
shaka", Willy alijibu bila kusita huku Bibiane amejikausha utafikiri kweli
alikuwa mke wake, baada ya kutambulishwa vile, Willy alitambua kuwa huyu
mwanamke alikuwa kweli amefundishwa vizuri mambo ya upelelezi maana Willy
hakumweleza mapema jinsi ambavyo wale askari wangetambulishwa hapa. Kazi yote
hii ilikuwa imefanywa na Col. Rwivanga.
"Kamanda
Kasubuga anawasubiri pale ofisini kwake", yule askari alimweleza Willy
Gamba.
"Twende",
Willy alimweleza Bibiane.
"Hapana,
wewe nenda tu, mimi nitakusubiri hapa", Bibiane alijibu na Willy akaelewa
maana na sababu ya Bibiane kubaki pale, akafurahi moyoni kuwa kweli alikuwa
amepata mshirika katika kazi.
Kamanda
Kasubuga alikuwa mtu mwenye rika la Willy na baada ya Willy kuingia ofisini
kwake aliinuka kwenye kiti alichokuwa amekaa akisoma faili moja hivi, huku
akitabasamu akamlaki Willy.
"Karibu
sana", Kamanda Kasubuga alimkaribisha Willy.
"Asante",
Willy alijibu huku wakishikana mikono na Kamanda Kasubuga alimwonyesha ishara
yule askari aliyemleta Willy awape faragha kidogo, yaani aondoke awaache peke
yao.
Baada ya
yule askari kutoka Kasubuga alisema, Lo! Bwana Willy Gamba ni wewe huyu, Sifa
zako na wewe mwenyewe hufanani. Col. Rwivanga amenieleza yote na mimi
nikamweleza kuwa nimekusikia sana nilipokuwa Tanzania. Mimi nimefanya kazi na
Jeshi la Tanzania na vyeo vyangu vyote mpaka hiki cha umeja nimevipata nikiwa
Tanzania".
"Alaa!
nashukuru sana", Willy alijibu na kuketi kwenye kiti.
"Oke,
bila kupoteza wakati, habari kutoka kwa kijana wetu ambaye juzi tu tumeweza
kumnunua kutoka katika jeshi la Zaire linalolinda mpaka na sisi zinaeleza kuwa
leo hii yapata saa kumi na mbili na nusu asubuhi waliwasili watu wawili upande
ule wa Zaire na kupokelewa kwa heshima zote za kijeshi na kisha wakaondoka
kuelekea kwenye makambi ya wakimbizi kule Kibumba. Baada ya maelezo ya jinsi
wale watu walivyofanana tulielewa mara moja kuwa mmoja wao alikuwa Col. Gatabazi.
Hivyo, Col. Gatabazi kafika na yuko Kibumba", Meja Kasubuga alieleza.
"Hizo
ni bahari njema sana, sasa ngoja na sisi tupumzike halafu giza likiingia na
sisi tutakwenda Kibumba", Willy alijibu huku Meja Kasubuga akimwemwesa.
"Sawa
mzee, ila tumewawekea chumba kimoja maana ni mimi tu ninajua wewe ni nani, hawa
askari wengine wote wanajua kweli wewe ni afisa wa Msalaba Mwekundu na kwamba
kwa vile unajua utakaa Rwanda kwa muda mrefu umekuja na mke wako", Meja
Kasubuga alimweleza Willy.
"Hapa
taabu", Willy alijibu kwa mkato.
"Safari
ya Kibumba, tumeagizwa na Mkuu wetu kuwa tufuatane, maana siku zote nimetaka
kuvuka na kikosi changu cha hapa lakini nimekuwa nakatazwa, lakini leo
nimeamriwa tufuatane wote, sijui safari itakuwa saa ngapi?".
"Sijui,
tutaangalia wakati huo si na wewe unakaa hapa hapa hotelini?".
"Ndiyo
mzee, niko chumba namba 110, nyie mtakuwa nambari 220 kwenye vyumba
vinavyofuata".
"Sawa",
Willy alijibu na kuaga. Aliporudi pale kwenye gari alimkuta Bibiane anapiga
soga na wale askari.
"Tupelekeni
chumba namba 220", Willy aliwaeleza wale askari.
Askari mmoja
aliingia ndani ya gari baada ya kushusha mizigo yao, akawapeleka kwenye banda
lililokuwa na chumba nambari 220. Yule askari alipoondoka Bibiane akasema,
"Kwa vile kuna kitanda kimoja tu wewe utalala ng'ambo ile na mimi ng'ambo
hii".
"Lo,
kumbe ulikuwa unajidai bure, sasa umeanza masharti".
"Si
tulisema kazi kwanza?", Bibiane alijibu huku akifunga mlango kwa funguo na
kuanza kuvua nguo huku akiendelea kusema, "mimi nitaoga kwanza.
"Sawa
mama", Willy alijibu huku mawazo yake yakiwa tayari yameanza kupanga
mipango ya usiku ule. "Tukimaliza wote kuoga tuitishe chakula kidogo
halafu tupumzike angalau kwa masaa mawili ndipo safari ya Kibumba ianze",
Willy alimwambia Bibiane.
"Amri
itatoka kwako baba, mimi kazi yangu ni kutii amri tu", Bibiane alijibu
huku sasa akiwa amevua nguo zote pale kitandani.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment