UCHU



KASHESHE

VII

Ilipofika saa tano kamili za usiku, Willy Gamba na Bibiane walikuwa tayari wamewasili Kibumba. Bibiane alizijua vizuri njia za vichochoro za sehemu hii. Hivyo, walifika bila tatizo lolote. Bibiane alimuonyesha Willy sehemu yalipo maghala makubwa ya silaha ambayo baada ya Willy kuyaona, alitaka waanzishe mapambano dhidi ya watu wakiwa kwenye maghala hayo kwani aliamini hapo ndipo nguvu kubwa ya Akazu ilikuwa imewekwa.

"Sehemu hii inalindwa sana", Bibiane alimwambia Willy baada ya kutoka kwenye msitu na kuona kambi kubwa ya kijeshi ambayo ilimshangaza hata Willy.

"Walijenga lini kambi kubwa ya jeshi kama hii?", Willy aliuliza kwa mshangao.

"Hapa kulikuwa na kambi ya jeshi la Zaire, na Akazu walipewa kambi hii baada ya matukio makubwa ya Rwanda, na mara moja wakaleta vifaa vyao vya kivita na kuifanya kuwa kambi ya jeshi ya kisasa kabisa. Ina kila kitu kama unavyoona, taa, maji, mawasiliano, yaani kuna kila kitu cha kisasa nakwambia. Hata maafisa wa mashirika ya kimataifa yanayoshughulikia wakimbizi wanapotokea hapa kwa bahati mbaya wanaamini ni kambi ya jeshi la Zaire, maana kambi za wakimbizi ziko kilomita moja tu kutoka hapa upande ule wa kilima, hata wakiuliza basi huambiwa kuwa hii ni kambi ya jeshi la Zaire, na raia hawaruhusiwi kabisa kusogea karibu na kambi hii", Bibiane alimwambia Willy, ambaye wakati huo alikuwa ameshikwa na mshangao.

"Maghala ya silaha ni yapi?", Willy alihoji huku akichungulia kuangalia vizuri kambi hii akitumia kiona mbali. Bibiane alitumia nafasi hiyo kumwelekeza kila kitu. Kwa vile kambi ilikuwa ikiwaka taa utafikiri mchana waliweza kuona kila kitu vizuri kabisa.

"Kambi hii yote imezungukwa na seng'enge yenye umeme wenye nguvu kubwa unaoweza kumuua hata tembo haraka kama inzi, yaani ukigusa tu unakaushwa kwa umeme kama nyama", Bibiane alieleza.

Willy aliamua kwanza walifiche gari la jeshi walilokuwa wakitumia kwenye msitu ule, wakachukua mizigo yao ya kazi na kasha wakatafuta njia ya siri kwa ajili ya kuingia pale kambini.

"Hii kambi inaweza kuwa na askari kama wangapi kwa kukisia kwako?", Willy alimuuliza Bibiane.

"Eeeh… wanafika elfu tano na zaidi, wenye mafunzo ya juu sana, wale askari wa kikosi cha Rais wako hapa pia na askari wenye ujuzi mkubwa. Kuna makomandoo waliofuzu vizuri kama mia tano, halafu kuna askari wa kawaida wenye mafunzo mazuri vilevile zaidi ya elfu nne na mia tano. Hivyo, kuna askari kama elfu kumi hapa, na ndilo tegemeo kubwa la Akazu kurudi madarakani. Lakini kusema kweli wanaweza kushika tena madaraka, ukichukulia ari, uwezo na vifaa vya kijeshi walivyo navyo", Bibiane alimweleza Willy.

KKwa kweli kambi hii ilikuwa kubwa sana kiasi cha kumtia hofu Willy Gamba, kwani hakutegemea kabisa kukutana na kambi kubwa ya adui yenye idadi kubwa ya askari kama hii.

"Hebu nipe muda nifikiri kabla ya kujitumbukia huko", Willy alimwambia Bibiane.

"Hatuna muda Willy, hatuna muda kabisa kabisa, lazima ufahamu kuwa tunatafutwa na adui, na wakihisi tuko huku hakika tumekwisha", Bibiane alilalamika wakati Willy akimwangalia tu bila kusema kitu.

Baada ya Willy kutafakari kwa dakika kadhaa alilazimika kumwambia Bibiane. "Nikisema nahitaji muda wa kufikiri nina maana dakika tano tu, lakini niwe peke yangu, naamini sasa umenielewa?", Willy alimwambia Bibiane huku akielekea kwenye kichaka kilichokuwa hatua chache kutoka walipokuwa wamesimama.

"Kumbe unaamini uchawi, wewe unakwenda kuloga, mimi nifanyeje sasa?", Bibiane alimkebehi Willy.

"Jifanyie lolote kwa imani yako", Willy alijibu huku akipotelea kwenye kichaka. Inasemekana katika hali kama hii ya hatari Willy husali sana akimuomba Mungu. Baada ya dakika kadhaa Willy alirudi alimkuta Bibiane akiwa amebeba silaha za kiasi chake akiwa tayari kwa kusonga mbele kwa ajili ya mapambano dhidi ya jeshi la Akazu.

"Ehe, sema sasa tunasonga mbele ama tunarudi nyuma kumsubiri Col. Rwivanga?", Bibiane aliuliza.

"Tunaendelea", Willy alijibu kwa mkato huku akitoa vifaa vyake vya kazi kwenye mkoba wake.

Willy alibeba silaha na vifaa vilivyokuwa vimebaki, na kwa hadhari kabisa wakaanza kuelekea kwenye ile seng'enge yenye umeme.

"Mara nyingi ulinzi si mkali sana upande wa ua kwa kuwa wanaamini hakuna kitu kinachoweza kuzipenya hizi seng'enge bila kufa kwa umeme, maana kila siku wanyama wanakutwa wamejikaanga wenyewe. Vilevile, kitu chochote kinachokaribia mita moja ishara inaonekana kwenye chumba maalum kinachodhibiti usalama wa kambi hii kama kuna kitu kinasogelea seng'enge mara moja hatua za haraka za usalama wa kambi zinachukuliwa.

"Yote haya yamefanywa lini?", Willy alitaka kujua.

"Sababu ya pesa Willy, pesa, askari wa kukodishwa kutoka Afrika Kusini ndio wameleta vifaa na teknolojia hii iliyopo hapa kambini. Tukifanikiwa utajionea mwenyewe", Bibiane alidokeza.

Walipokuwa mita kumi kutoka usawa wa seng'enge walisimama na Willy alitoa kifaa maalum kwenye mkoba wake. "Tutapita chini ya seng'enge, baada ya kuchimba handaki".

"Itatakiwa liwe mita mbili kwenda chini, vinginevyo tutakaushwa kama mikaa", Bibiane alisema huku akionyesha wasiwasi.

"Hili bomu", Willy alisema akiwa ameshika bomu dogo lenye ukubwa wa yai la kuku. "Lina uwezo wa kuchimba handaki la urefu wa mita kumi na upana wa mita tatu, na kina cha mita tatu unasemaje?".

"Sikupingi, kwa teknolojia ya sasa hata mimi nimeona maajabu mengi katika vifaa vya vita, teknolojia imeendelea sana. Haya chimba tuone".

Willy alishika kisu na kuanza kuchimba shimo la mita moja kwenda chini, kisha akawasha lile bomu na kulitumbukiza pale shimoni na kulifukia.

"Litalipuka baada ya nusu dakika turudi nyuma haraka tulale chini".

"Halitasikika baada ya kulipuka?".

"Hapana, bomu hili limetengenezwa mahususi kwa ajili ya matumizi kama haya, ili kuziba mlio ndio sababu tunalizika chini ya ardhi", Willy alimwambia Bibiane na kumtoa hofu.

Baada ya nusu dakika bomu lile lililipuka na kutoma sauti kidogo, hii yote ilitokana na kazi ya Willy na kukatokea handaki zuri kwa ajili ya wao kupita bila kikwazo.

"Bwana, hakika kazi yako nimeipenda, sasa tuingie ndani tukafanye kazi iliyotuleta, kikwazo hiki ndicho kilikuwa kinanipa wasiwasi mkubwa", Bibiane alisema wakati wakiingia ndani ya handaki ili wapite kwa ajili ya kuwakabiri wanajeshi zaidi ya elfu kumi ndani ya kambi yao.

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU