UCHU


KASHESHE

XIII

Huyu Willy Gamba lazima atakuwa kaingia hapa, hatujui kapita njia ipi na yuko sehemu gani?", Nkubana alimwambia Col. Gatabazi kwa njia ya radio.

"Haiwezekani, hakikisha kwanza", Col. Gatabazi alijibu kwa hofu.

"Hakika ni yeye Willy Gamba, tumekuta sehemu imechimbwa chini ya ua mita kama tatu hivi kwenda chini, hata hatujui imetumika nini kuchimba ardhi. Kwa maana hiyo, tumeanzisha operesheni kali ya kumsaka ndani na nje ya kambi, japokuwa hatuna uhakika kama bado yuko ndani ama ametoka. Hakika mtu huyu ni hatari sana, itabidi kuongeza ulinzi katika eneo hilo hususan mahali mlipo, nitatuma askari zaidi kuimarisha ulinzi hapo", Nkubana aliahidi.

"Kuna madhara yoyote kafanya huyo Willy", Col. Gatabazi alihoji kwa wasiwasi.

"Mpaka sasa hakuna, tumekagua sehemu zote ni salama isipokuwa hapa kwenye ua palipochimbwa ardhi, ni sehemu hii tu".

"Nani kagundua eneo hilo limechimbwa na muda gani umepita toka hali hiyo itokee", Col. Gatabazi aliuliza tena kwa shauku.

"Niko hapa katika eneo husika afande", Nkubana alijibu. Baada ya ukimya wa sekunde kadhaa akaendelea. "Askari wetu mmoja wa doria aliyepangwa kulinda eneo hili la ua anasema haiwezi kuwa zaidi ya dakika kumi na tano hivi zilizopita. Nafikiri bado hajaingia ndani, anasubiri ama ameona ndege wakati mnaingia, anaweza kuwa anajipanga kujaribu kuanzisha mashambulizi. Ujue yuko pamoja na Bibiane ambaye anaijua sehemu hii vizuri sana".

"Bibiane anataka kulipa kisasi, kwa hiyo lazima watakuwa wanaelekea hapa baada ya kuona tumetua kwa ndege, ongeza ulinzi, nafikiri umebashiri sawasawa", Col. Gatabazi alijibu.

Baada ya kuzungumza na Nkubana kwa radio, Col. Gatabazi aliwafahamisha wenzake kuhusu maelezo ya Nkubana. "Huyu mtu ni hatari sana, lazima atakuwa anaelekea hapa, nimeagiza ulinzi uongezwe zaidi. Nia yake ni kutuangamiza sisi kwani Bibiane atakuwa amemweleza yote kuhusu uongozi wetu. Naomba wote tuwe katika hadhari, huyu mtu ananitia wasiwasi maana anaonekana amepania ni mjuzi na haogopi kitu. Watu wa aina hii ni hatari sana", Col. Gatabazi alieleza.

"Hapa hawezi kuingia, ajaribu aone moto, hii itasaidia kumkamata kirahisi maana nyumba hii inalindwa na mitambo maalumu ya kisasa, kuna kamera zimetegwa eneo hili. Na tunaweza kuona sehemu zote zinazoizunguka nyumba hii kwa mara moja, kwenye chumba chetu kuna vifaa vya kuangalia usalama wa nyumba hii, kuna televisheni nne ambazo zinaangalia mzunguko wa eneo hili kwa umbali wa kilomita moja. Hii ina maana hata sehemu ya upande huu wa kambi tunaona. Halafu pale kambini kuna mitambo kama hii, sijui imekuwaje hawakuweza kumuona!", Kamanda Morris alieleza kwa mshangao.

"Hebu twende kwenye hicho chumba chako", Jean ambaye pia alianza kuingiwa na hofu, alieleza. Wakaelekea kwenye chumba cha mawasiliano na usalama wa kambi hiyo.

Walipoingia ndani ya chumba hiki waliwakuta askari kama sita hivi waliokuwa wakisimamia kuendesha ile mitambo ya ulinzi mle ndani. Wakiwa ndani waliweza kuona picha za maeneo yote yaliyozunguka ile nyumba, waliwaona pia askari waliokuwa wakilinda eneo hilo. Kwa kweli, kulikuwa na askari wengi kila mahali wakiwa tayari kupambana na adui kwa njia yoyote. Kupitia mitambo hiyo waliweza kuwaona askari wengine zaidi wakiongezeka na kujipanga kwa ulinzi zaidi.

Kwa vile kambi hii inao komandoo zaidi ya mia tano waliofuzu vizuri mafunzo yao, hii ilimpa jeuri Jean na Col. Gatabazi kuwa na imani kuwa hakuna adui anayeweza kuleta rabsha mbele ya vijana hao ambao pia walikuwa sehemu ya ulinzi wakati huo.

"Kukitokea kitu chochote cha hatari, sisi tutakuwa wa kwanza kukiona hata kabla ya askari wa hapo nje hawajakiona. Tumeweka taa kali za ulinzi ili eneo hili lionekane kama mchana na kamera zetu zichukue picha kwa ufasaha zaidi", Kamanda Morris aliwaeleza na kufanya wageni wake waridhike na maelezo hayo na kuamini kuwa hakuna madhara.

"Lakini ikitokea bahati njema Willy Gamba akamatwe, huyu atakuwa mfungwa mikononi mwangu, msimuue tafadhari, nileteeni hapa nimle nyama taratibu. Nasisikia kuonja nyama yake", Jean aliagiza.

"Na Bibiane?", Col. Gatabazi aliuliza huku akimwangalia Jean.

"Huyu nitapenda kufanya naye mapenzi kwa mara ya mwisho kabla hajaenda ahera", Jean alijibu huku uso wake ukionyesha uovu wa ajabu na mate yakimjaa mdomoni.

"Huyu mtu ni mgonjwa", Col. Gatabazi alijisemea moyoni.

"Tunaweza kuendelea na mkutano", Jean aliagiza baada ya kujiridhisha na hali ya usalama wa kambi, wakarudi kwenye chumba cha mkutano walikokuwa Kamanda Morris, Bizimaziki na wataalamu wengine wa kijeshi waliokodishwa, waliendelea kuwaeleza jinsi mipango ya mashambulizi ilivyokuwa imepangwa.

Meza moja ilikuwa na ramani ya nchi za Zaire, Rwanda na Burundi na baadhi ya nchi zote za maziwa makuu zikitumiwa kuonyesha jinsi ambavyo jeshi la Akazu lilivyojiandaa kusonga mbele katika kuivamia Rwanda, wakitumia askari wa miguu, magari ya kisasa ya kivita, vifaru, makombora ya masafa mafupi na marefu pamoja na ndege za kivita, yote ni kuivamia nchi hiyo kijeshi.

 
ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU