KASHESHE
Ilikuwa
yapata saa tatu na nusu usiku wakati Willy na Bibiane walipokuwa wakijiandaa
kuelekea Kibumba, walivalia sare za Msalaba Mwekundu huku wakiwa wamebeba
silaha mbalimbali ndani ya mifuko ya nguo na mikoba waliyokuwa wamebeba yenye alama ya
Msalaba Mwekundu. Walibeba silaha zote za hatari yakiwemo mabomu ya
kisasa yaliyotolewa na Bibiane.
Willy alikuwa amevaa
saa iliyoendana na yale mabomu akiwa tayari kuyatumia wakati wowote wakati wa safari yao.
Walipofika kwenye gari na kufungua mlango ili waweke mikoba yao tayari kwa safari, mara moja Meja
Kasubuga alijitokeza akitoka gizani akiwa ameshika bastola yake mkononi akawauliza.
"Mnakwenda wapi Willy, hamkusikia maagizo ya Col. Rwivanga kwamba msifanye
chochote wala msiende Kibumba mpaka mtakapowasiliana nae kesho, haraka ya nini Willy?, mimi
sintaruhusu muondoke".
"Sisi
hatuendi Kibumba Meja, tuko hapa hapa sehemu ya mpakani ili kufanya utafiti wa hali ya
usalama katika maeneo hayo", Willy alijibu.
"Siamini,
huenda mnataka kuvunja amri ili mvuke mpaka, hilo sintaruhusu na nimeamru
kikosi changu hapa kiwazuie msiondoke hapa hotelini mpaka hiyo asubuhi, mimi
nina amri zangu. Willy naomba tafadhali rudini ndani tusije tukavunjiana
heshima kwa kuwakamata na kuwaweka chini ya ulinzi mpaka Col. Rwivanga
atakapofika hapa", Meja Kasubuga alionya.
Willy na
Bibiane waliangaliana, maana wao walikuwa wameamua kuendelea na kazi yao usiku
ule. Hawakuona sababu ya kusubiri kesho yake kwani wao walikuwa na mipango yao
tofauti ambayo haikuwahusu akina Col. Rwivanga. Nia yao ilikuwa kuwasaka Col.
Gatabazi, Nkubana na Jean. Wakati lengo la Col. Rwivanga na jeshi la RPF
ilikuwa kuliangamiza jeshi zima la Akazu.
"Naona
kama hutuamini Meja, hakuna tatizo tutarudi ndani tukalale", Willy alijibu
kwa sauti ya unyonge sana.
"Samahani
bwana Willy, mimi natii amri niliyopewa na wakubwa wangu wala msijaribu
kunitoroka maana hiyo haiwe.....", kabla hajamaliza kusema sentensi hiyo,
milio ya bunduki aina ya AK 47 ilisikika upande mwingine wa hoteli.
"Tumeingiliwa",
Meja Kasubuka alisema huku akikimbia kuelekea sehemu ulipotokea mlipuko huku
akitoa amri kwa wanajeshi wake kujitokeza tayari kwa mapambano dhidi ya wavamizi.
II
Wakati Jean
na wenzake wanatoka Goma kuelekea Kibumba saa moja na nusu ya jioni ile,
Nkubana akiwa na kikosi cha askari shupavu wenye mafunzo thabiti wapatao
thelathini hivi, walielekea mpakani kutafuta habari za Willy na Bibiane, kwani
walikuwa na hisia kuwa lazima wangewatafuta kwa vile Bibiane aliijua mipango
yao yote.
Nia ya Nkubana ilikuwa kupeleleza ili amuwahi Willy kabla Willy
hajawawahi, maana hii ndio sheria ya mchezo wao huu. Nkubana na kikosi chake
walipofika mpakani upande wa Zaire ilikuwa yapata saa mbili na nusu na ndipo
walipoelezwa na vikaragosi wao waliokuwa wamejipenyeza ndani ya vikosi vya
jeshi la RPF pale Gisenyi kuwa mtu mgeni aliyekuwa amefikia pale Meridien Hotel
alikuwa ofisa wa Msalaba Mwekundu na mkewe.
"Huyo
mkewe alifananaje?", Nkubana aliuliza kwa shauku.
"Afande,
ni mwanamke mrembo ajabu, utanisamehe afande lakini kusema kweli
nilipomwangalia yule mwanamke mara moja nilizini afande, ni mzuri sanasana chotara
yule?", askari alijibu huku mawazo yake yakiwa yamerudi kwa yule mwanamke
na kuanza kumfikiria huku mwili wake unasisimka.
Hata Nkubana
alipokuwa anakieleza kile kikosi chake. "Watu wetu wamefika yafaa tupange
mipango madhubuti tuwashambulie na kuwakamata hai kama bosi alivyoagiza",
yule askari hakusikia kabisa mpaka Nkubana alipomshitua tena. Wewe vipi, una
tatizo la kifafa", maana alianza kutetemeka.
"Hapana
afande, hapana, nafikiri ukame umetuathiri sana mawazo".
"Ukame
gani, wewe ni mwehu nini?, hetu tufahamishe huyu jamaa na mkewe wanakaa upande
upi pale hotelini?".
Yule askari
alieleza kila kitu kwa ufasaha jinsi hotelini ilivyo na akawaelekeza namna ya
kuingia mpaka kwenye chumba walichofikia akina Willy bila kushukiwa na askari
wa RPF waliokuwa wakilinda eneo hilo.
"Inapofika
saa tatu mara nyingi askari wengi wanaondoka kuelekea mpakani na wale wanaobaki
mara nyingi wanakuwa upande wa Ziwa. Hivyo itabidi tuvuke mpaka kabla ya saa
tatu na nitawaonyesha sehemu salama ya kupita, halafu tutajibanza sehemu mpaka
hapo askari wengi watakapotawanyika kuelekea kwenye malindo ya usiku halafu
ndipo tutavamia kwani askari watakaobaki tutaweza kuwamudu", yule
kikaragosi alielekeza.
"Maelezo
yako ni safi sana, unafikiri kutakuwa na askari kama wangapi, yaani watakaokuwa
wamebaki kwa ajili ya kulinda hoteli?", Nkubana alihoji.
"Hawawezi
kuzidi hamsini pamoja na mimi, maana leo ni zamu yangu kulinda hoteli",
yule askari alieleza.
"Ulikuwa
ulinde upande gani?", Nkubana aliuliza kwa shauku.
"Unande
ule niliokueleza kuwa tutapita halafu tujibanze maana askari anayelinda sehemu
hiyo ni mtu wetu, anajuwa kila kitu", yule askari alibainisha.
Nkubana
alimwangalia kwa makini yule askari na akaridhika kuwa alisema ukweli na
akamwamini.
"Kwanza
nenda na askari wangu mmoja mkavinjari, halafu mrudi. Kama kila kitu kiko
tayari na mambo shwari ndipo tutaanza kazi", Nkubana aliwatuma ili kuwa na
uhakika wa mambo na kuthibitisha maneno ya yule askari alivyoeleza. Baada ya
wale askari wawili kuondoka. Nkubana alibaki akiwaweka sawa askari wake tayari
kwa kuishambulia hoteli ya Meridien-Izuda ili waweze kuwakamata Willy na
Bibiane.
Wale askari
waliporudi na kumweleza Nkubana kuwa mambo yalikuwa shwari na vilevile kupata
habari kuwa yule mtu wa Msalaba Mwekundu na mke wake walikuwa wamelala baada ya
safari ndefu habari hizi zilimfurahisha sana Nkubana, akafikiri kuwa angeweza
kumteka Willy na Bibiane wakiwa wamelala na huenda wakiwa wanafanya mapenzi.
Alisikia hasira inampanda na palepale akakiamru kikosi chake. "Haya sasa
tunakwenda kazini".
ITANDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment