KASHESHE
XIV
Wakiwa ndani
ya kambi hii, Willy na Bibiane walijificha kwenye vichaka vilivyokuwa kando ya
njia ambayo magari ya jeshi yalikuwa yanapita kuelekea kwenye jumba analoishi
Kamanda Morris.
Walikuwa
wamefanikiwa kuvuka kizuizi cha kwanza kutoka kambini bila kushitukiwa, na moja
kwa moja walitumia vichaka kujificha huku wakiua askari waliokuwa wakilinda
maeneo hayo, mpaka wakafika sehemu hii wakitafuta nafasi nzuri ya kuishambulia
nyumba ya Kamanda Morris ili waweze kuukabiri uongozi wa juu wa Akazu.
"Ikitokea
gari lisilo na askari wengi nyuma au hata likiwa na askari wawili ama watatu
tulivamie na kulifanya letu ili tulitumie litupeleke kule juu bila kuwashtua
walinzi. Kwa vile tumevaa sare zao tunaweza kujaribu kuingia mpaka ndani bila
shida ndipo tuanze mapambano, kama tutakuwa bado hatujashitukiwa", Willy
alimwambia Bibiane.
"Kama
nilivyowahi kukwambia nyumba hii inalindwa kwa mitambo maalumu ya kisasa. Nje
kuna kamera nne zinazopeleka picha kwenye televisheni ndani ya chumba cha
udhibiti wa mitambo, ambamo kuna askari wanaangalia mitambo hii kwa zamu, kwa
saa ishirini na nne kila kinachotokea nje kinaonekana kwenye televisheni hizi,
kamera hizi ninafanya kazi katika mzunguko wa kilomita moja kutoka eneo la
kambi. Vilevile ndani ya chumba hicho kuna vifaa vya kisasa kwa ajili ya
kunanasa sauti na mazungumzo yoyote ya radio kwa radio kwa umbali wa zaidi ya
kilomita mia moja. Pia wanaweza kunasa picha zinazoletwa kwa rada kama kuna
kitu kinaruka sehemu hii. Hivyo, tukijaribu kufanya chochote lazima tutaonekana
moja kwa moja", Bibiane alimuasa Willy.
Baada ya
kutafakari kwa sekunde kadhaa, Willy alitoa kile kitochi chake chenye miali ya
leza akampatia Bibiane.
"Sikia,
mimi ninacho kingine, kama tutafanikiwa kuikaribia ile nyumba tutagawana njia,
wewe utaelekea mashariki mimi nitapita magharibi, kitu cha kwanza kabisa ni
kuua zile kamera za upande wako kwa kutumia miali ya chombo hiki. Ukiwasha tu
na kuelekeza miali hii kwenye hizo kamera basi zinakufa papohapo, hazifanyi
kazi tena. Harafu unaweza kukitumia haraka kukata ukuta kama tulivyofanya
wakati tunaingia kwenye maghala ya silaha, Pia unaweza kukitumia chombo hiki
kupofua mtu yeyeto macho. Tukifanikiwa kuifikia ile nyumba basi tuivamie na kuanza
mapambano, hapo ndipo kuna kufa ama kupona. Jean na wenzake ama sisi.
Tukifanikiwa tutaonana ndani, nataka umuonyeshe Jean mafunzo yote aliyokupeleka
ulihitimu vizuri na unao iwezo mkubwa wa kutumia nafasi kama
ulivyofundishwa".
Wakati Willy
bado anaeleza waliona gari aina ya Landrover la jeshi linakuja, nyuma ya gari
hilo kulikuwa na askari wawili waliokuwa wamesimama wakiwa wamevalia mavazi ya
kijeshi kama wao.
"Gari
hilo, kazi kwako Bibiane", Willy alitoa amri, na gari lilipokaribia wote
walilirukia kwa nyuma na kuingia ndani bila kutoa kishindo. Wale askari wawili
walikuwa wakizungumza huku wakiangalia mbele. Willy alimuonyesha ishara
Bibiane, na kwa kutumia vipaji vyao vya karate, waliwavamia wale askari na
kuwaua palepale na kisha kuwainamisha chini ndani ya lile gari bila kutoa
kishindo cha kuwashitua wale waliokuwa mbele ya gari. Wakawalaza vizuri na
kuwafunika kwa turubai lililokuwa ndani ya lile gari.
Kisha wakajifanya ndio
wale askari kwani walivaa kofia za chuma za wale askari waliowaua. Gari
lilipopunguza mwendo na kusimama, Willy alitoa ishara wote wakaruka na kuelekea
pande mbili tofauti. Bibiane akaelekea kulia, Willy kushoto. Kwa vile wote
walikuwa wamevaa nguo za kijeshi kama wale askari wengine, hakuna
aliyewashitukia. Willy aliongoza kwenye ile nyumba bila wasiwasi huku
akipigiana saluti na askari wengine wa pale. Alipofika karibu kabisa na nyumba
ile aliona ile kamera. Wakati Willy anaiona ile kamera ya upande huu wa
kushoto, Bibiane naye alikuwa akijipenyeza upande wa kulia, akaiona ile kamera
wa upande wake.
Kama vile
walivyoambizana, wote walitoa zile tochi zao zenye miali ya leza na kuzielekeza
kwenye kamera hizo. Macho ndani ya zile kamera yalikufa palepale na kukatisha
mawasiliano ya kutuma picha za pande zote mbili kwenye televisheni. Na baada ya
kufanya hivyo tu Willy alijipenyeza na kwenda kuitafuta ile kamera ya upande wa
kusini.
Mle ndani ya
chumba maalumu kilichokuwa na mitambo walishituka baada ya televisheni
zinazopokea picha kutoka kulia na kushoto kushindwa kutuma picha.
"Tumeingiliwa,
hii si bure", Kiongozi wa wale askari waliokuwa wakiendesha mitambo ndani
ya chumba alisema na kwenda kumweleza Kamanda Morris. Kamanda Morris na wenzake
walikuwa katikati ya mkutano wakati yule askari alipofungua mlango na kuingia ndani.
"Kuna
nini?". Kamanda Morris alimuuliza kwa shauku huku kundi zima likisimama
kumwangalia yule askari kwa taharuki.
"Televisheni
zote za kulia na kushoto hazileti picha, inawezekana zimeharibiwa", yule
askari alisema.
"Tayari
yuko hapa", Col. Gatabazi alijibu na kuinuka kutoka kwenye kiti. Kabla mtu
mwingine hajasema lolote, mlango ulifunguliwa na askari mwingine kutoka chumba
cha kingine mitambo nae akaingia na kueleza. "Sasa kamera zote hazileti
picha".
Kundi zima
la Akazu na mamluki wao wakaingiwa na hofu.
"Huyu
mtu ameweza kufika mpaka kutuingilia hivi kwa namna gani, Nyinyi hamna ulinzi
wa kutosha hapa", Jean alifoka kwa hasira huku akionyesha hofu.
"Usitahayali
Jean, lazima ufurahi kuwa mtu wetu kajileta mwenyewe na hataweza kuondoka hapa
akiwa hai", Col. Gatabazi alijibu huku akielekea mlangoni na kwenda nje
akifuatiwa na Kamanda Morris.
"Twende
zetu tukamsake, mambo yameiva sasa", Col. Gatabazi alimwambia Kamanda
Morris.
Nkubana
ambaye naye alikuwa amefika kwenye eneo la nyumba hii akiwa anahisi Willy na
Bibiane wangekuwa wamefika, alizunguka eneo hili kwa hadhari kubwa huku
akiwachunguza kwa makini kila askari waliokuwa karibu yake, aliwaangalia
machoni mwake. Kutokana na kitendo cha pale mpakani alijuwa kuwa Willy na
Bibiane walikuwa wamevaa sare za jeshi sawa na wao. Wakati Bibiane anapiga
miali ya leza kuua ile kamera ya kusini Nkubana alikuwa karibu nae kabisa
lakini alikuwa bado hajamtambua. Ile miale ilipotoka kwenye tochi ya Bibiane na
kuunguza jicho la kamera likatoa mwanga wa kati baada ya sekunde kadhaa jicho lake likaungua.
Nkubana
alisitushwa na mwanga uliotokea na kuua kamera. Akamwangalia Bibiane na macho yao yalipokutana
mara moja wakatambuana. Kama umeme Nkubana alitoa bastola yake kiunoni ili awahi kummalize
Bibiane. Bila hata kufikiri kuwa Bibiane alikuwa fundi zaidi, alimuelekezea ile mionzi ya leza machoni na palepale akajitupa
chini kukwepa risasi, Nkubana alipiga risasi hovyo kwani alikuwa amekwisha pofuka macho na
kupiga makelele, "Bibiane huyu hapa kanipofua macho".
Risasi zote
alizorusha Nkubana hazikumpata Bibiane ambaye alijiviringisha na kuinuka mahali
penye mlango ambao Col. Gatabazi na Kamanda Morris walikuwa wanaufungua ili
kutoka nje, baada ya kumsikia Nkubana akipiga kelele. Hivyo, mlango
ulipofunguliwa tu, Bibiane alijitupa pale mlangoni na kuwakumba Col. Gatabazi
na Kamanda Morris, kitu ambacho hawakukitegemea na wote wakaangukia ndani huku
wakifuatiwa na risasi zilizoelekezwa kwa Bibiane.
"Acheni
acheni kupiga risasi, mtaleta madhara makubwa", Ofisa mmoja wa jeshi la
Akazu aliamru baada ya kuona kilichotokea. Bibiane ndiye aliyekuwa wa kwanza
kuinuka na alipoinuka huku katoa Bastola yake, askari mmoja aliyekuwa analinda
mle ndani alimpiga kichwani kwa kitako cha bunduki; Bibiane alianguka chini na
kuzirai.
Jean,
aliyekuwa anaangalia yaliyokuwa yanatokea huku akiwa amezugukwa na kundi la
viongozi wa Akazu na marafiki zake wa jeshi la Zaire, aliagiza, "Msimuue.
Nasema mpelekeni bafuni mmwagieni maji. Kwanza mfungeni kamba, sikujua mtoto
huyu ni hatari kiasi hiki. Kumbe sikupoteza fedha zangu bure nilipompeleka
kwenye mafunzo ya kijeshi. Nilikuwa nasikia sifa zake tu leo nimemuona mwenyewe
akiwa kazini, nimefarijika sana".
Col.
Gatabazi na Kamanda Morris sasa walikuwa wamesimama huku wakiwa na hasira ya
kutaka kummaliza Bibiane.
"Wewe
huna akili nzuri kweli, huyu mwanamke ni mtu hatari halafu unasema umefarijika,
huyu ni mtu wa kuuawa sasa hivi si mtu wa kusubiri". Col. Gatabazi
alihamaki.
"Poa,
Col. tulikubaliana kuwa kabla sijamuua ni lazima nifanye naye mapenzi mara ya
mwisho. Hakuna mwanamke aliyewahi kuniridhisha kimwili kama huyu. Ngoja
azinduke halafu nitimize ahadi yangu ndipo nitakuachia umuue", Jean
alieleza.
Willy
aliposikia purukushani na milio ya risasi upande ule wa kusini na kelele
alizopiga Nkubana alijua kuwa kwa Bibiane mambo tayari yameharibika. Alitumia
hii vurugu na yeye akakimbilia ule upande wa kusini. Alipofika akamuona mtu
anataka kubebwa ili aingizwe ndani, alikuwa haoni na hakujua yule ndiye alikuwa
mtu aliyepambana na Bibiane na kupofuliwa macho. Kwa vile nia ya Willy ilikuwa
kuingia ndani na kuwaangamiza viongozi wa Akazu, aliona amepata upenyo wa
kuweza kufanya hivyo. Huku akijifanya kama mmoja wa askari wa pale, aliwahi na
kumuondoa askari aliyekuwa anataka kumbeba Nkubana kumpeleka ndani na
kumuonyesha ishara ambayo yule askari hakuelewa lakini akafikiri huenda yule ni
askari mwenzake ndiye aliyeamriwa kufanya vile.
Willy
alimshika Nkubana kiunoni na kumweleza. "Afande ngoja nikuongoze ndani
ukapumzike, huyu mshenzi Willy atatutambua leo".
"Nia
aibu kwangu, mimi Nkubana kufanywa hivi na mwanamke, mimi nia yangu ilikuwa
kumuangamiza kabisa Willy kwa mikono yangu, nasikia uchungu sana", ndipo
Willy alipotambua kuwa huyu aliyekuwa amemshika alikuwa Nkubana. Alifurahishwa
sana na kazi ya Bibiane.
"Usihofu
Afande, tutakulipizia, hapa huyo Willy kafika, atawezaje kutoka hapa, huyu mtu
ni mwendawazimu. wakati Willy akieleza hayo walikuwa wamefika mlangoni na
kuingia ndani ya sebule kubwa ya nyumba hiyo.
Bila kuhisi
kuwa huyu aliyekuwa akimuongoza Nkubana alikuwa ni Willy Gamba, Col. Gatabazi
alimweleza.
"Mkarishe
pale kwenye kiti, halafu askari toka haraka mkamsake huyo Willy Gamba".
"Ndio
Afande", Willy alijibu huku akielekea kwenye pembe nyingine ya ile sebule
kulipokuwa na makochi. Wakati huo Willy alimsikia Kamanda Morris akitoa amri
kwenye kipaza sauti kuwa askari wote walioko pale wapange mstari mara moja
kuizunguka nyumba na kila mmoja amnong'oneze afisa wake lile neno la siri
wanalotumia wakati wa usiku. Wakati huo huo Willy aliliona kundi la Akazu na
Jean likizunguka meza na mmoja wao kutamka, "Nafikiri tuyaamrishe majeshi
yetu yaanze kusogea, tunapoteza muda kwa huyu Willy, mtu mmoja asitupotezee
muda hata kama ni hodari atakua wangapi, sanasana hawazidi mia, ndio atakuwa
amefanya nini?", Kabuga alieleza.
"Namuunga
mkono bwana Kabuga. Askari wachache wabaki wamshughulikie huyo Willy, wengine
waanze kuelekea mpakani, huku kusubirisubiri kunaweza kutuletea madhara.
Tumeshaona tuko tayari kabisa, hakuna wakati tumekuwa tayari kama wakati
huu", Col. Gatabazi alieleza.
"Oke,
nami nakubali, kwanza huyu Bibiane kesha fufuka?", Jean aliuliza.
Willy
alikuwa amekwisha mkalisha Nkubana huku akili yake ikipiga hesabu za haraka
namna ya kuwateka hawa Akazu na vibaraka wao.
"Wewe
askari njoo hapa, na wewe uninong'oneze neno la siri tunalitumia usiku", Kamanda
Morris alimwita Willy wakati alipotaka kutoka nje. Willy alikuwa hajui hilo
neno la siri, hivyo mtego huo ulikuwa umemnasa. Karibu na Kamanda Morris
alikuwepo Jean akaagiza chumba cha mitambo askari wamlete Bibiane aweze
kuulizwa alipo Bibiane.
"Willy
alimsogelea Kamanda Morris na ghafla alimrukia Jean na kumkaba na kuvuta kwenye
ukuta, bastola kichwani kwa Jean na kusema, Jean huna haja ya kumtafuta Willy,
niko hapa. Kundi zina lilisimama huku askari wote wakiwa wamepigwa na butwaa.
Kamanda Morris, Jenerali Kasongo, Meja Masamba, wale askari wa kukodiwa na hata
Nkubana, japo alikuwa kipofu walitoa bastola zao.
"Msifanye
mchezo wowote, wekeni silaha zenu zote hapo kwenye meza, mkifanya mzaha huyu
bwana yenu Jean atakuwa historia nitamwangamiza", Willy Gamba alieleza kwa
ukali. Wote walijua hatari. "Na mtu asisogee hapa wala asiondoke humu
ndani. Ila wamlete Bibiabe", Willy aliendelea kuamru.
"Fanyeni
anavyosema", Jean alieleza huku akitetemeka huku mkojo ukimtoka
chapachapa.
Kamanda
Morris alitaka kutoka ili kwenda kumleta Bibiane, lakini Willy alikataa,
"Mtu hatoki huku ndani, nimesema kwa lugha inayoeleweka, umenipata wewe
Kaburu".
"Kampuni
yenu ya mamluki naijua safari hii mmeingia hasara, mmetengeneza faida kubwa
katika biashara hii, lakini leo nasema tena, safari hii mmeingia hasara".
Kamanda
Morris alimwagiza askari mmoja amlete Bibiane, ambaye alikuwa tayari amepata
fahamu. Na Kamanda Morris akawa amesema na neno moja ambalo Willy hakulielewa.
"Umesema nini wewe kibaraka?", Willy alihoji huku macho yake
yakionekana mekundu.
"Nimeita
mwisho jina la yule askari", Kamanda Morris alijibu. Lakini Willy machale
yalimcheza. Wakati bado anafikiria lile neno aliwahi kulisikia wapi, ghafla
ukuta aliokuwa ameuegemea ukapitishwa umeme na yeye akamsukuma Jean upande
mwingine na kuruka nyuma ya makochi.
Nguvu ya ule
umeme ilikuwa kubwa kiasi cha kumfanya Willy kupoteza fahamu baada ya kuanguka
chini. Kamanda Morris alikuwa amejiwekea usalama wa kila aina na alikuwa
amemzidi Willy maarifa, mara moja kila mmoja alichukua silaha yake, na Bibiane
kabla hajafanya lolote alikuwa ameshikiliwa vizuri na askari watatu.
"Mfungeni
kwenye hicho kiti, sasa tutamla nyama vizuri", Col. Gatabazi aliagiza.
Bwana Kabuga akiwa bado anatetemeka kwa kuwa mambo kama haya yalitokea kama
miujiza alidai arudi kwenye ndege ili waondoke eneo hilo.
"Hapana,
kaa uone maana ya utawala", Jean alijibu baada ya kuinuka kutoka mahali
alipokuwa amedondoka na macho ya chuku akiwa ameyaelekeza kwa Bibiane aliyekuwa
anafungwa kwenye kiti. Kisha, akamwendea Bibiane na kumnasa kibao, akisema
"Mbio za sakafuni huishia ukiongoni, janja yako kwisha. Lakini kabla
mwisho wako haujafika niliahidi nitafanya mapenzi na wewe kwa mara ya
mwisho".
"Utawahi,
kwani na wewe unadinda", Bibiane alijibu.
Jean
alimnasa tena kibao na kusema, "Umesahau nilivyokuwa nakunyanyasa
kitandani".
"Wewe
ni mgonjwa na huu ndio mwisho wako", Bibiane alijibu kwa dharau.
"Unachekesha,
huu ndio mwanzo wangu na mwisho wako", Jean alijibu na kugeuka nyuma,
kwani wakati mawazo yake yakiwa kwa Bibiane, Kamanda Moris alileta kifaa cha
umeme na kumfunga Willy kwenye kiti na kumtingishatingisha ili azinduke.
"Willy
alipozinduka tu, Jean alikuwa wa kwanza kumfikia na kuanza kumpiga vibaya sana
mpaka Willy akaanza kutoa damu puani.
"Wewe
mwanaume gani, mpaka mwanaume mwenzako afungwe ndio umpige, si umfungue tuone
nani mwanaume hapa, kati yako Jean na Willy", Bibiane alisema kwa dharau.
"Ngoja
amalize hasira zake, huyu mshenzi hatufanyia mambo mabaya sana", Col. Gabatazi
alidakia huku akisogea na kumchakaza Willy kwa makofi yaliyomfanya azirai tena.
"Basi
inatosha, kabla hajala umeme nataka nimpe maneno yake. Nikimaliza kusema
Kamanda Morris fanya kazi yako. Huyu tayari tumemhukumu kifo, na atakufa si kwa
risasi bali kwa umeme, kama wahalifu waliohukumiwa kunyongwa kule Marekani.
"Kufa
si tatizo, kila mtu atakufa", Willy alisema baada ya kuzinduka na
kuongeza, "Ila hata mkitumaliza leo, lakini hamfiki popote".
"Wewe
ni mwehu, sisi tuna jeshi la kuikamata Rwanda chini ya wiki moja, unasema nini
mwehu wewe, utapata habari utakapokuwa ahera", Col. Gatabazi alitamba.
"Wewe
ndiye nani", Willy aliuliza.
"Mimi
ndiye Col. Gatabazi".
"Nijulishe
basi kwa wengine maana kata anayehukumiwa kifo hujui majaji waliomhukumu",
Willy alihoji akiwa na maana ya kuvuta muda kama kuna njia nyingine ya kujiokoa
aweze kufanya hivyo.
"Huyu
hapa ni Anatoire Kabuga, ndiye kiongozi wa Akazu. Najua unafahamu Akazu ni
nini. Wale rafiki zetu toka jeshi la Zaire. Anayeingiza ni Col. Marcel
Bizimaziki, ambaye ni kamanda wa Akazu anayesaidiwa na huyu mzungu. Kamanda
Morris kutoka kampuni ya kijeshi ya Afrika Kusini. Na waheshimiwa huyu ndiye
adui yetu namba moja Willy Gamba, kutoka Tanzania lakini na yeye tuna habari
kuwa kazi hii anaifanya kwa kukodishwa. Hivyo, hawakilishi msimamo wa Tanzania
hata kidogo katika suala hili; yeye na Kamanda Morris hawana tofauti na huyu
Bibiane ni msalti kama mnavyomjua. Niliwahi kumshawishi Jean kuwa karibu sana
na mwanamke akajua siri zake ni balaa kwani wao fikira zao zinatoka chini na si
juu kichwani. Si watu hawa, lakini hakunisikia, sasa ona madhara
aliyotufanyia", Col. Gatabazi alilalamika.
"Kazi
na dawa, bila kuwa karibu na mwanamke mzuri anayekupa mapenzi vizuri huwezi
kufikiri sawasawa, usisahau Col. Gatabazi hata sisi tumenufaika sana na huyu
kiupmbe, mimi binafsi nilikuwa na bahati ya kufaidi mwili wake hivyo usinionee
wivu, ngoja nikafaidi mara ya mwisho", Jean alijibu. Akimuonyesha ishara
askari aliyekuwa karibu amfungue kamba ili ampeleke chumbani. Willy sasa fahamu
zake zilikuwa zimerudi na akili yake ilikuwa ikifanya kazi ya ziada namna ya
kuponyoka toka ndani ya balaa hii.
Aliona azidi
kununua muda kidogo wa kuomba.
"Huenda
nimefanya yote haya bila kujua undani wa suala zima hili, kwa sababu kwa akili
ya mtu yeyote haya mauaji mliyofanya na kuyatekeleza yanafanya akili isikubali
maana yalikuwa ya kikatili na kunyama. Kabla sijanyongwa naweza angalau
kuelezwa sababu zilizowafanya mkatekeleza mauaji mabaya ya aina hii ambayo ni
ya kipekee baada ya Dikteta Hitler?".
Wakati Willy
anamuuliza Col. Gatabazi, Jean na Kamanda Morris walikuwana wananong'onezana na
Kamanda Bizimaziki ili askari waondoke kuelekea mpakani. Willy, huku macho
yakifunguka kwa shida kutokana na kipigo aliweza kuwaona jinsi
wanavyonong'onezana na vilevile akaweza kuona jinsi Bibiane anavyofunguliwa
kamba kutoka kwenye kiti na kupelekwa kwenye mlango uliokuwa ukielekea
chumbani. Aida, alihisi Jean alikuwa anataka kufanya nini. Yote haya
yalifanyika wakati Willy akiongeza kasi ya kuwaza jinsi ya kujinasua ili aweze
kukamilisha kazi yake iliyomfikisha haba badala ya kukata tamaa.
Acha mimi
nimjibu, wewe endelea na shughuli inayotusubiri, ambayo ni muhimu zaidi.
Nimefurahi kuona kuwa huyu Willy anataka kujua sababu na sababu nitazitoa
mimi", Anatoile Kabuga, Kiongozi wa Akazi, alijibu huku akiangalia saa
yake iliyoonyesha kuwa ilikuwa saa nane na nusu usiku.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment