UCHU



KASHESHE

XVI

Anatoile Kabuga alimwangalia Willy kwa jicho baya sana, alimuona kuwa ndiye kikwazo na adui wao namba moja kwa kuwachelewesha Inyenzi na washirika wao kushika madaraka ya nchi ya Rwanda. Hata hivyo aliamini kuwa hakuna mtu mwingine zaidi ya Willy atakayeweza kupena na kuingia katika ngome yao.

"Nitakupa historia kidogo", Anatoile Kabuga alianza kumweleza Willy Gamba. "Willy Gamba, lazima ufahamu kuwa sehemu hii ya Maziwa Makuu katika Afrika watu wa kwanza wa asili ni wabantu. Wabantu ndio walioishi eneo hili la Maziwa Makuu kwa karne nyingi sana tena wakiishi kwa raha mstarehe bila migogoro wala matatizo mpaka walipokuja watu wenye asili ya Kihemetiki ambao baada ya kufika eneo hili walianza kuleta chokocoko, vita wakitokea Kaskazini na Mashariki mwa Afrika. Kwa ufupi, Watutsi wamo kwenye kundi hilo. Tangu wafike katika sehemu hii amani imekosekana kabisa. Karne mbili zilizopita walianza kuweka Ufalme wao katika eneo hili baada ya vita vikali na wabantu wa sehemu hii na kuwashinda. Waliweka wafalme wao waliowaita wafalme wa Kihima ambao walitawala kutoka Bahari ya Hindi mpaka Atlantiki, sehemu ambayo sasa ni Zaire, Rwanda, Burundi, Tanzania, Uganda na Kenya", alinyamaza kidogo kisha akaendelea.

"Willy Gamba. Nitakueleza kwa kifupi sana maana hatuna muda wa kupoteza. Lakini kwa sababu wao walikuwa wachache na wakawa wanaendeleza utawala wa mabavu na unyanyasaji kwa wabantu ambao ndio waliokuwa wengi, hali inayoendelea mpaka sasa, mapigano ya kuukataa utawala huo yaliendelea sehemu zote, hatmaye ufalme huo ukaangushwa katika sehemu zingine na kubaki sehemu ambayo sasa ni Rwanda na Buurundi. Na hali hii iliendelea mpaka wakati wa Ukoloni ambapo katika Rwanda utawala wa ukandamizazi wa Watutsi dhidi ya Wahutu na wabantu ambao ndio wengi katika Rwanda, uliendelea. Miaka yote hii mpaka vita vya pili vya dunia Watutsi wachache waliendelea kutawala na kuwanyanyasa Wahutu wakihakikisha kuwa hawapati elimu, madaraka na hata mali. Ni mpaka juzi tu, mwaka 1957, Wahutu walipojikomboa na kushika madaraka, na hawa Inyenzi wakakimbilia nchi jirani ikiwemo Tanzania. Wakati wa utawala wetu tulijaribu sana kuwaweka karibu lakini siyo wote waliotaka kutawaliwa na walio wengi sababu wao walijiona wana hadhi ya juu kuliko sisi. Vilevile, waliapa kuwa lazima watatafuta njia mbadala warudi kututawala maana sisi ni watumwa wao. Na kwa taarifa yako kila Mtutsi anamuona kila Mbatu kama mtumwa wake. Ndivyo wanavyokuona wewe hata kama unawasaidia kwa sababu wewe ni Mbantu na ndivyo wanavyoniona hata mimi. Sasa basi tatizo kubwa lilikuja wakati nchi jirani ilipopata kiongozi mwenye asili hiyohiyo ya Kitutsi, na akawa na nguvu na akaahidi kuwasaidia Wahutu ili wautoe utawala wa wabantu katika Rwanda, Yaani watu wenye asili ya Kitutsi tu ndio watawale sehemu hii ya maziwa makuu ikiwemo Zaire, Rwanda, Burundi, Tanzania, Uganda na Kenya. Sisi tulipopata habari hizi tukajua eneo lote hili la maziwa makuu halitapata amani ikiwa hawa Watutsi wanazidi kuzaliana na kuwa wengi eneo hili. Njia pekee ya kuleta amani ni kuhakikisha mmewaua waume, wake kwa watoto, ili kuua kabisa nguvu yao. Leo hawa tusipowaangamiza nakueleza wewe Willy Gamba, Tanzania haitakuwa na amani na wala Zaire, Uganda na Kenya hawana amani maana hawa wana asili ya kujipanua. Ni watu hatari ajabu, na kama mngejuwa kuwa hawa ni watu wa kuteketezwa kabisa hata mmoja asionekane katika sehemu hii".

"Ngoja nikukata kauli, umesema watu wengi katika eneo hili la maziwa makuu ni wabantu, hawa Watutsi wachache watatawala vipi", Willy aliuliza huku akisogeza vidole vya mkono wake wa kulia kujaribu kama vingeweza kuifikia saa yake aliyovaa mkono wa kushoto.

"Unasema nini, tunavyozungumza nani anatawala Rwanda, Burundi na Uganda, watu wengi katika nchi hizi ni watu gani, sisi wabantu, sasa nini kitawashinda kutawala Zaire, Tanzania na Kenya kama wameweza katika nchi hizo, njia pekee ni kuwateketeza ili waishe, wasiendelee kutunyanyasa na kuleta vita vya mara kwa mara katika eneo letu. Hawa na Wayahudi hawana tofauti. Ngoja nikwambie Willy Gamba, hawa Watutsi hata kama ukiona Mtutsi amezaa na wewe lazima atatembea na Mtutsi mwenzie ili azae Mtutsi, kazi yako wewe itakuwa ni kukuza damu isiyokuwa yako. Na wamehakikisha wanawake wao wamesambaa dunia nzima, lakini kila mwanamke wa Kitutsi ahakikishe mahali alipo anapewa mimba na Mtutsi mwenzie tu. Huku wanawake wao kusambaa ni njia mojawapo ya kujipanua ili waweze kufanya kampeni yao kwa kuhurumiwa na mataifa mengine. Hivyo, mauaji haya tuliyofanya ni kwa niaba ya wabantu wote na sasa hivi tuko tayari kuurudisha utawala wetu Rwanda na Burundi ili heshima ya mbantu katika eneo hili ipatikane. Baada ya kuichukua tena Rwanda mara hii tutataka viongozi wote katika eneo hili waelewe ukweli huo na watuunge mkono kuwatokomeza Watutsi hawa. Vinginevyo nakwambia Willy Gamba watatawala tena sehemu yote hii, la sivyo hakuna amani katika eneo hili. Vita vitaendelea kwa miaka mingi. Sisi Akazu ndio tumaini pekee la sehemu hii, bila sisi kesho tawala zote za sehemu hii zinazotawaliwa na wabantu zitatikiswa na kumalizwa. Hivyo, wewe Willy ni msaliti, unawasalti wabantu kwa kuwasaidia Inyenzi ili waweze kutawala ardhi halali ya wabantu. ndio sababu tumekuhukumu kifo. Na, wote wawe wabantu au taifa lingine, wakibainika wanasaidia Inyenzi lazima wauawe. Na sasa wewe utauawa ili Akazu ifanye kazi yake ya kuwakomboa wabantu", Kabuga alisema kwa sauti nzito iliyoashiria hasira ya ajabu ambayo kila mtu pale ndani alihisi kapagawa.

"Yote hayo uliyoyasema yanaweza kuwa na ukweli mwingi tu, lakini ukweli huwa hautoi uhalali wa kuangamiza kabila zima. Hii ni kinyume na haki za binadamu. Njia nyingine itafutwe kuwadhiti na si kuwaangamiza", Willy alijibu huku kidole chake cha karibu na gumba kwenye mkono wa kulia kikiwa kimefika kwenye ufunguo wa saa yake na kukandamiza ufunguo wa saa na kusubiri kuona kifo chake ama kifo cha jeshi la Akazu.

"Unasema haki za binadamu, sisi wabantu hatuna haki mbona............", Kabuga hakumaliza sentensi yake teknolojia ilianza kufanya kazi yake.

ITAENDELA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU