KASHESHE
XVIII
Wakati huo
Jean alikuwa ameanza kumvua nguo Bibiane ili atimize ahadi yake kama
alivyoahidi kuwa atafanya nae mapenzi kabla ya kumuua, wakati akikaribia
kutimiza ahadi yake, ghafla mlipuko mkubwa ulitokea eneo hilo na kuleta hofu,
palepale nyumba ile ikasambaratika vipande. Bahati nzuri nyumba hii ilikuwa
imetengenezwa kwa mbao tupu ili likitokea tatizo kama hili Kamanda Morris
asihatarishe maisha yake.
Kwa vile
Bibiane alikuwa akiutegemea mlipuko kama huo, ulipotokea tu hakuzirai kama
wengine. Alizitupa mbao zilizomwangukia mwilini mwake, akainuka na kuanza
kumsaka Willy ambaye wakati huo alikuwa amefungwa kwenye kiti pale ukumbini.
Kumbe mlipuko ulipotokea kile kiti kilirushwa pamoja na Willy Gamba mpaka nje
kwenye bustani. Bibiane aliangalia huku na huko kwa tahadhari kubwa, maana watu
wote walikuwa wamelala chini kwa hofu. Vilio vilisikika eneo lote la kambi hii
mara akamuona Willy Gamba na kiti chake akiwa nusu amezirai.
Milipuko ile
iliendelea kuleta hofu na kusababisha mwanga mkubwa katika eneo lote. Milio na
mwanga ilionekana na kusikika mpaka Goma, Gisenyi na sehemu nyingine kwani sasa
mizinga na makombora nayo nayo yalianza kulipuka bila mpangilio na kusababisha
Jean na wenzake kupatwa na taharuki. Bibiane alitoa kisu chake kidogo alichokuwa
amekifika kwenye nywele zake, akiwa tayari kabisa kummaliza Jean. Na kwa
kutumia hiki kisu alifanikiwa kuzikata kamba alizokuwa amefungwa Willy Gamba
kisha akamtingisha hadi Willy akapata fahamu. Baada ya Willy kuzinduka Bibiane
akamshika mkono. Willy alisimama wakakimbia kuelekea sehemu ile ya Magharibi ya
kambi mahali ambapo kulikuwa na mstu mkubwa.
Walipokimbia
kama mita hamsini hivi Bibiane alitoa bomu la kurusha kwa mkono akalitupa
kwenye ile nyuma kisha wakajitupa chini. Bomu hilo liliporipuka likasambaratisha
eneo hilo halikubakiza mtu wala kitu kilichokuwa ndani ya nyumba hii au mita
thelathini kuzunguka nyumba hii. Wakati wanaelekea kwenye ule mstu mabomu,
mizinga na makombora yaliyokuwa ndani ya maghala makubwa ya kuhifadhia silaha
yaliendelea kuripuka yenyewe.
"Kazi
ipo Willy, wamelikoroga acha walinywe sasa", Bibiane alisema kwa kebehi.
"Kazi
yenyewe si kidogo, wamelala matajiri wataamka masikini", Willy alijibu
wakiwa wemeingia kwenye msitu.
"Naona sasa
tumechoka, kazi hii inatosha kabisa kwa siku moja ya leo", Willy alieleza
wakiwa wametokeza kwenye sehemu ya majani mazuri chini ya mbaramwezi.
"Hapa panafaa kupuzika, au
vipi", Willy aliuliza.
"Hapa
tumetafutiwa na Mwenyezi Mungu ili tupumzike baada ya hii kasheshe. Nilikuwa
natamani ufike muda nipate mahali ambapo dunia itakuwa mimi na wewe tu. Na
mahali hapo ni hapa, yaani mimi, wewe, mbaramwezi, nyota, malaika na
Mungu", Bibiane alieleza.
Willy alivua
gwanda lake la juu akatandika chini kwenye majani, Bibiane akavua pia na
kusema. "Hili tutajifunika".
Willy
akamwinua na kumbeba mikononi kisha akambusu na kumlaza juu ya gwanda lake.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment