SURA YA PILI
II
Joram
alikuwa ni mtu ambaye halewi kwa urahisi, tunaweza kusema kuwa alikuwa
amechangamka pindi Kombora alipokuwa amekaribia meza yake na kuketi.
"Karibu
sana Inspekta, karibu uketi", Joram alisema kwa uchangamfu huku akimwita
muhudumu wa hoteli hiyo. "Leo naweza kusema kuwa ni siku tukufu sana
kwangu kutembelewa na Inspekta Mkuu. Habari za siku nyingi mzee?".
"Polepole
kijana", Kombora alisema. "Wanasema siku hizi hata kuta zina
masikio".
"Kwani
kuna lolote la siri tunaloongea hapa mzee?, Siku hizi mambo yote ya siri
nimeachana nayo mzee. Nimeamua kuwa raia mwema na mtulivu kama ulivyokuwa
ukinitaka niwe", Lilikuwa jibu la Joram.
Kombora
hakutia neno. Akamgeukia Nuru na kumsalimu, "Bila shaka huyu ndiye yule
dada ambaye alikuwa na balaa la kulazimishwa kushirikiana na yule mwuaji ambaye
alikusudia kuangamiza viongozi wengi wasio na hatia?", Joram na Nuru
waliitika kwa vichwa. "Ni msichana shujaa sana. Msichana wa kawaida
angeweza kupoteza kichwa chake mara baada ya kukabiliwa na mkasa mkubwa kama
ule", alimaliza na kupokea kinywaji chake akaanza kunywa.
"Sivyo
mzee", Nuru alijibu. "Kila nikifikiria kile kitendo naona aibu kubwa
sana. Nisingestahili kukubali kulazimishwa kushiriki katika mauaji ambayo yangekuwa
ya kinyama kama yale. Ingawa yule jasusi Proper alikuwa kanilaghai kuwa
ungekuwa mzaha wa kawaida bado sikustahili kuafikiana naye. Uzalendo wangu
ulitiwa dosari na kitendo kile. Najaribu kutafuta nafasi ya kuudhihilishia moyo
wangu lakini sijafanikiwa...".
"Joram
ananinyima nafasi hiyo", Nuru aliongeza baada ya kusta kidogo.
"Ni
hilo tu ulilotaka kusema Nuru", Joram alidakia. "Nadhani hata
Inspekta amefuata kujadili hilo, au sivyo mzee.
"Inspekta
Kombora aliimeza bia iliyokuwa kinywani mwake. Kisha alijibu.
"Kiasi
ni kweli niko hapa kujadili hilo, kiasi siyo kweli". Alisita kidogo na
kuendelea. "Unajua hatujaonana kwa muda mrefu? Tangu ulipoondoka Arusha
kwa hasira baada ya kuitupa bastola yako hatujaonana tena. Nilifika katika
chumba cha dada huyu nusu saa baadaye na kuukuta ubongo ule na bastola.
Nilidhani umemuua wewe. Lakini bastola yako haikuwa imefyatuliwa walau hata
risasi moja. Mara kikatokea kile kitabu ambacho kilinifanya nielewe yote
yaliyotokea. Ndipo nikaelewa kwanini umekasirika na kuamua kuwa mnywaji".
"Niite
mlevi Inspekta, vyovyote sijali".
"Hapana.
Wewe si mlevi na wala huwezi kuwa mlevi. Ni mnywaji tu. Mnyaji ambaye hanywi
kwa ajili ya kupenda kunywa, isipokuwa kwa hasira baada ya kunyang'anywa fursa
ya kukitia risasi kwa mkono wako kichwa cha yule mshenzi. Sivyo Joram?"
Kombora alitulia akimtazama Joram. Mara Joram akakumbuka kuwa hajavuta sigara
kwa muda mrefu. Alitoa sigara moja na kuiwasha baada ya kuwataka radhi jirani
zake.
"Kuacha
hadhi yako ipotee kwa sababu ya kukosa kumuua mtu mmoja tu duniani!",
Kombora aliendelea, "Sioni kama ni haki. Ziko nafasi nyingi za kufumua
vichwa vya watu wenye haki kabisa ya kufumuliwa. Hati maalum inatayarishwa
ambayo itakuruhusu kufanya lolote kama afisa yeyote wa usalama mwenye jukumu maalumu.
Zaidi kimetengwa kifungu maalumu cha fedha ambacho kitaingizwa katika akaunti
yako ili pesa zisiwe kipingamizi..."
"Taratibu
Inspekta", Joram alimkatiza. "Vipi, mbona mema mengi hivyo, kama
sikosei unachotaka kusema ni kwamba unaniomba nishiriki katika kutafuta kiini
cha maafa haya yanayotendeka katika nchi za mstari wa mbele. Na kama sikosei
nadhani mtu uliyemtuma kwangu amekupa majibu yangu rasmi. Msimamo wangu ni
uleule. Na utaendelea kuwa uleule. Kama mngefahamu Joram ambaye alikuwa mpenzi wa
Tanzania na Afrika kwa ujumla, lazima muelewe kuwa Joram huyo amekufa. Aliyeko
hai mbele yako, ni Joram mpya. Joram ambaye hana na wala kiu ya kushiriki kwa
njia moja ama nyingine katika masuala yoyote ya nchi. Aliyeko mbele yako ni
Joram wa mastarehe, Joram wa kutumia. Hata dada yangu Nuru hapa nadhani
anaelewa".
Ndipo
Kombora alipoona ugumu wa kazi iliyoko mbele yake. Kumshauri Joram ilikuwa sawa
na kulilazimisha jabali lielee juu ya maji. Akiwa mtu ambaye hakuzoea
kuwabembeleza binadamu wengine, hasa wanaume, Kombora alisema kwa sauti ambayo
ilificha hasira na unyonge.
"Pengine
unajua unachokifanya. Lakini nadhani hujui ni kiwango gani cha madhara
yanayolikabiri taifa hili endapo tutashindwa kuukomesha uovu huu
unaotunyemelea. Niruhusu nikusimulie mambo ya kutisha ambayo hayajavifikia
vyombo vya habari".
"Haitasaidia",
Joram alimjibu Inspekta Kombora, "Utaupoteza bure muda wako. Ninachohitaji
kusikia ni habari za burudani tu. Kama kuna burudani mpya ambayo sijaiona,
kinywaji kipya ambacho sijakinywa au muziki mpya ambao sijausikia, nitafurahi
endapo utanisimulia. Juu ya vifo vya marais na raia wasio na hatia na wenye
hatia, si kazi yangu tena".
"Hata
hivyo sauti yako haifanani kabisa na madai yako Joram. Kuna watu ambao silika
yao ni kukesha katika mabaa na kwenye madansi, wewe si mmoja wao. Kuna
wanaostarehe kusubiri maafa ya kusikitisha, wewe si mmoja wao Joram. Kuna
wanaofurahia radha ya pombe na utamu wa muziki zaidi ya kazi na ushujaa, wewe
si mmoja wao vilevile".
"Zamani,
Inspekta. Sasa hivi mimi ni mmoja wao. Na kama huna maongezi mengine zaidi ya
hayo mzee, nitashindwa kuendelea kukusikiliza", Joram alimaliza na kutoa
sigara yake na kuiwasha.
Kombora
hakuona kama angeweza kufanya lipi la kumshawishi Joram. Alimtazama Nuru kama
aliyehitaji msaada wake. Akayaona macho yake mazuri yaliyojaa uzuri katika hali
yake ya kukata tamaa. Hilo kiasi lilimfariji Kombora. Alifahamu kuwa anaye
msaidizi ambaye angesaidia katika juhudi zake za kumrejesha Joram Kiango katika
dunia ya Joram Kiango. Kombora hakuwa mgeni katika dunia hii alijua kuwa
mwanamke mzuri ni silaha. Hivyo akamtupia Nuru jicho la kumtaka aelewe kuwa
anautegemea msaada wake. Kisha aliinuka na kuaga bila ya kumaliza kinywaji
chake.
"Hukufanya
vizuri, Joram", Nuru alimwambia.
"Mfuate
mkazungumze vizuri".
"Hivyo
tu, sikia...".
Nuru
akavunjika moyo. Uchungu ukamwingia rohoni. Alijilazimisha kuendelea kunywa
pombe, lakini haikumuingia. Baada ya jitihada nyingine alimtaka Joram radhi,
akaondoka kutangulia chumbani.
"Samahani,
naweza kuketi hapa", alisema mtu mmoja akimsogelea Joram baada ya Nuru
kuondoka.
********************************************
ITAENDELEA 0784296253
Comments
Post a Comment