TUTARUDI NA ROHO ZETU?



 SURA YA TATU

Alikuwa mtu wa umri wa kati. Sura yake ilionyesha dalili zote za kutocheka, macho yake yakionyesha dalili ya kuelemika. Kiasi alionekana kama pombe ilianza kumshinda nguvu, japo alitembea kwa uhakika.

Joram alimtazama kwa makini kabla ya kumjibu, "Una haki ya kukaa popote. Nchi huru hii".

"Asante", alijibu mtu huyo huku akijiweka kitini. Baada ya dakika mbili tatu za kunywa na kuvuta kwa utulivu alimgeukia Joram na kumwambia, "Samahani. Sina budi kulitoa dukuduku langu. Siku zote nimekuwa na hamu ya kuipata fursa hii ya kuketi nawe. Kama sikosei u Joram Kiango".

Joram alimtazama kwa makini mtu huyo. Alipochelewa kumjibu mgeni wake aliendelea.

"Tumekuwa tukikutana mara kwa mara katika majumba ya starehe. Kilichonifanya nikufahamu ni huyu msichana mzuri unayefuatana nae. Kwa kweli sina budi kukupa pongezi zako. Wazuri nimewaona na aina yake lakini huyu sijapata kuona. Ulimpataja yule dada Joram". Jambo moja lilikuwa limemvuta Joram katika kumsikiliza mtu huyu. Jambo la pili lilijitokeza. Sauti. Ilikuwa sauti ya kawaida, ikizungumza kiswahili cha kawaida katika masikio ya watu wa kawaida. Lakini katika masikio ya Joram Kiango, Joram ambaye alikuwa sasa amekaa chonjo, sauti hiyo ilificha uhalisia fulani.

"Unadhani una haki gani ya kunifahamu, na kumfahamu msichana wangu wakati mimi binafsi sikufahamu hata kidogo", Joram alimuuliza. Kama ambaye alilitegemea jibu lile yule mgeni alijibu mara moja japo kwa kusitasita.

"Mimi kwa jina naitwa ISmail Chonde. Ni mfanyabiashara wa siku nyingi. Nimezaliwa na kukulia hapahapa ingawa siku hizi naishi Nairobi".

"Na unawezaje kunifahamu kwa urahisi kiasi hicho?".

"Nasoma vitabu, nasoma magazeti. Hakuna asiyekufahamu Joram". Sauti iliendelea kuwa na walakini katika hisia za Joram.

"Inaelekea bado huna maswali ya kuniuliza bwana Chonde. Nataka kumuwahi huyo msichana unayemwita mzuri".

"Kweli. Inaonyesha aliondoka hapa akiwa amechukia", Joram alitabasamu.

"Naona umeona mengi zaidi ya hilo".

"Ndio, nimeona na kusikia mengi. Kwa kweli endapo utaniona mlevi, nilichokusudia kuongelea ni yule mzee aliyekuacha muda. Nafahamu yule ana madaraka makubwa serikalini. Kama sikosei alikuwa akikushawishi utoe mchango wako katika kupeleleza kuhusu matukio haya. Na niliona akiondoka bila furaha. Inaelekea umemkatalia. Hivi kweli umekataa katakata", Joram alimtazama kwa makini zaidi.

"Sielewi maswali yako yanaelekea wapi?", alihoji Joram.

"Inashangaza", Chonde aliongeza. "Joram ninayemfahamu mimi hawezi kuipoteza nafasi nzuri ya kuonyesha ushujaa wake. Afrika iko katika mashaka makubwa. Watu wanakufa hovyo. Majumba yanalipuka hovyo. Bara zima la Afrika liko mashakani. Joram ninayemfahamu mimi angetoa hata roho yake kupambana na hali hii", Joram alisikia na kupima sauti ile, akiilinganisha na uso wa msemaji. Ingawa aliongea kama mtu mwenye uchungu wnchi na hisia ya bara lake, bado hisia fulani zilimfanya Joram aone kitu kama kebehi katika macho yake. Kana kwamba alikuwa na hakika kuwa Joram na U Joram wake asingeweza kufanya lolote. Wazo hilo lilimuongezea Joram hamu ya kuendelea kumsikiliza.

"Bado sijaelewa unachotaka kusema", Joram alichochea.

"SIdhani kama wewe ni mzito wa kuelewa kiasi hicho", wakatazamana. Kila mmoja akimsoma mwenzake. Kisha Chonde aliangua kicheko kirefu kilichomwacha Joram akitabasamu. Baada ya kicheko hicho aliongeza, "Samahani endapo umeniona mhuni au mlevi. Sikuwa na nia mbaya zaidi ya kuzungumza nawe na kufahamiana. Kwa kheri". Aliinuka na kuondoka akielekea maliwatoni. Mwendo wake ulikuwa wa kilevi zaidi ya sauti yake.

Joram aliendelea kunywa taratibu. Alipomuona rafiki yake huyo mpya anayeitwa Chonde akitoka nje ya hoteli na kusikia mlio wa gari ukiondoka, Joram alielekea mapokezi ambapo alimsalimu tena msichana aliyekuwa hapo na kumuuliza kwa upole, "Samahani dada. Hivi huyu bwana aliyetoka sasa hivi anakaa katika hoteli hii?".

"Yule, hakai hapa. Huwa anatokeatokea tu. Kila mara huja na msichana wake. Leo ndio kwanza nimemuona akiwa peke yake. Sijui wamekosana nini na msichana huyo. Maana huyu bwana inaonekana pesa si moja ya matatizo katika maisha yake", msichana huyo alieleza.

"Pengine hawajakosana", Joram alimchokoza.

"Wamekosana. Bila hivyo asingenikonyeza mara mbili", Joram alicheka. Maongezi yao yalikatishwa kwa simu ambayo msichana huyo alikuwa akijibu. Alipotaka kuanza tena maongezi iliingia simu nyingine. Hii msichana huyo alionekana kuifurahia zaidi. Alizungumza kwa furaha huku akitabasamu. Baada ya kutoa chombo cha kuongelea alimgeukia Joram na kusema.

"Unaona, nimekwambia leo hana mtu. Ananiambia nikimaliza kazi nimkute hoteli ya New Afrika, chumba namba 104".

"Ndipo anapokaa?", Joram alihoji.

"Bila shaka".

Baada ya mazungumzo hayo Joram aliirudia meza yake na kuendelea kunywa. Mawazo yake yalikuwa yakimfikiria mtu huyo Chonde. Hakuelewa nini hasa ilikuwa dhamira ya maongezi yake yale. Alishuku kuwa pengine alikusudia kupata undani wa Joram na uamzi wake. Kwanini?, zaidi Joram alishuku kuwa mtu huyo hawakukutana kuzungumza kiajaliajali, bali alikuwa akimfuata yeye au Kombora kwa ajili hiyo. Juu ya yote hayo hisia za Joram kuhusu mtu huyo zilizidi kujiimarisha akilini. Aliona kama ulikuwemo walakini fulani katika sauti ya kiswahili chake ambayo iliutia dosari Utanzania wake. Hayo na kile alichoona katika macho ya mtu huyo zilimtia Joram hamu ya kumfahamu mtu huyo zaidi.

Hivyo dakika tano baadaye alijikuta mitaani akielekea New Afrika. Alipofika hapo alimwendea mfanyakazi wa mapokezi na kuzungumza naye hili na lile huku macho yake yakiwa kazini kutazama kama funguo namba 104 ulikuwepo. Aliuona akauliza juu ya mtu wa chumba fulani ambacho aliona ufunguo wake haupo.

"Yuko ndani, ameingia sasa hivi".

"Ngoja nikamuone", baada ya kwenda chumba hicho, Joram alipanda ghorofani hadi chumba namba 104 ambacho kilikuwa kimefungwa. Kuacha kwake tabia ya kutembea na bastola hakukuwa kumemfanya aache kutembea na vifaa vyake vidogo vidogo kama funguo malaya ambazo hazishindwi kulifungua kufuli la aina yoyote. Hivyo kitasa hicho cha mlango wa Chonde kilimpotezea nusu dakika tu.

Chumbani humo, Joram aliurudisha mlango na kuufunga kwa ndani. Kisha aliangaza huku na kule kwa makini. Kilikuwa chumba cha kawaida kama vilivyo vyumba vingine vya hoteli. Hivyo Joram hakuwa na kazi kubwa ya kupekuwa magodoro na viti. Hakuna chochote. Ndipo alipoliendea Kabati na kulifungua. Ndani ya kabati hilo kulikuwa na sanduku kubwa ambalo Joram alilifungua. Kulikuwa na pesa za kutosha pamoja na mavazi. Vitu hivyo havikumvutia Joram. Macho yake yalivutiwa na nyaraka mbalimbali ambazo alizipekua kwa umakini. Mengi yalikuwa makaratasi ya kawaida yaliyomuonyesha kuwa aliitwa Afith Chonde. Baada ya kupekuwa zaidi aliipata hati yake ya kusafiria. Aliifungua haraka haraka huku akianglia mihuri iliyogogwa katika nchi mbalimbali ambazo Chonde alikuwa amezitembelea. Alikuwa anatembea sana. Mihuri ya Nairobi, Lagos, Lusaka, Harare, London, New York, Hong Kong, Tripol na nyinginezo ilikuwa ikionekana waziwazi. Hilo lilimfanya Joram azidi kuvutiwa na mtu huyo. Hakuonekana kama mfanyabiashara mkubwa kiasi hicho. Zaidi ya vipindi alivyokuwa akitumia kutoka mji mmoja kwenda mwingine kwa muda mfupi, hivyo Joram alimshuku kuwa hakuwa mfanyabiashara wa kawaida. Hivyo akaongeza umakini katika upekuzi wake.

Kama alivyotegemea Joram aligudua mifuko ya siri katika begi hilo. Mifuko ambayo maafisa wa forodha wasingeweza kuiona bila ujuzi maalumu. Katika mifuko hiyo, Joram alikuta bastola moja aina ya Rivolver, maandishi mbalimbali ambayo alipojaribu kuyasoma hakuweza kwani yalikuwa yameandikwa kimafumbo mafumbo kwa hali ya kijasusi kamili, pamoja na kijaruba kimoja cha chuma kilichokuwa kimefungwa kwa ufunguo. Kijaruba hicho kilimvutia zaidi Joram. Alihisi kuwa kilikuwa kimeficha mengi zaidi ya yale aliyokuwa ameyaona. Hivyo alianza kujaribu funguo zake malaya. ilimchukua dakika kadhaa alipogundua kuwa asingeweza kukifungua kisanduku hicho. Kilitengenezwa maalumu kufunguliwa na mtu mwenyewe. Kiu ya Joram juu ya kumjua mtu huyu ikazidi. "Vipi awe na kisanduku kama hicho, kimeficha nini, na maandishi haya ya siri yanasema nini?, siyo bure. Liko jambo", Joram aliropoka.

"Ndio. Kuna jambo", sauti ilizungumza nyuma ya Joram. akageuka hima na kukutana na uso wa Chande akimtazama kwa kebehi. alikuwa kaketi juu ya kochi. alivyoingia chumbani kwa ukimya kama jini na kuketi kwa utulivu kipindi chote ni jambo ambalo lilimuongezea hofu Joram akaamini kuwa yule hakuwa binadamu wa kawaida. Akageuka kumtazama Chonde huku akiruhusu tabasamu zake kishujaa. Tabasamu ambayo ilifuatwa na sauti yake tulivu.

"Tumesema nimefumaniwa".

"Ndio umefumaniwa. Na bahati mbaya ni kwamba umefumaniwa na kifo. Binadamu hanichezei mimi na akaendelea kuishi", Chonde alisema huku akiinuka taratibu kutoka kitini. "ulijifanya umeacha mambo yako ya kuingilia mambo yasiyokuhusu. Kumbe ulikuwa ukijiburudisha kwa kujidanganya mwenyewe. Umekosea sana".

"Huwa nafurahia zaidi kuwaua watu wangu kwa mikono yangu", alisema Chonde akizidi kusogea.

Mzaha haukuwemo katika macho na sauti ya Chonde kisha alionekana ni mtu anayejua nini anachofanya. Jambo ambalo lilimfanya Joram asogeze mkono kuiendea ile bastola iliyokuwa imelala kando yake. kama alikuwa ameuhisi wepesi wa Chonde basi alikuwa hajauona. Mara tu mkono huo ulipoifikia bastola mguu wa Chonde ulitua juu ya mguu huo. Wakati huo huo Joram alipokea ngumi mbili nzito zilizomfanya Joram asahau bastola. Chonde hakuwa na roho mbaya kiasi hicho. Alimpa muda wa kujiandaa. Joram akavuta pumzi kwa nguvu na kuanza kumwendea Chonde. Alimshitua kwa mkono wa kulia, Chonde aliudaka na wakati huohuo akamkata Joram judo ya mgongo na kumfanya aanguke kifudifudi. Alipoinuka Chonde alikuwa akimsubiri huku akicheka.

"Wanasema Tanzania kuna mtu mmoja tu wa kujihadhari nae, ambaye anaitwa Joeam Kiango. Niko naye chumbani, sioni ujoram wake".

Maneno hayo yalimuuma Joram zaidi ya kipigo alichopokea. Akainuka ghafla na kumwendea Chonde akitumia mitindo na mbinu zake zote za kupigana. Vipigo kadhaa alimpata Chonde. Lakini kwa jinsi vipigo hivyo alivyompiga kwa hasira havikuwa na madhara kwa Chonde dakika chache baadae Joram alijikuta yuko chali sakafuni kasalimu amri. Chonde akaendelea kutabasamu.

Sasa Joram alimtazama Chonde kwa mshangao zaidi ya hasira. Ni mtu wa aina gani anaweza kumwadhibu kama mwanae, bila shaka si mtu wa kawaida. Amejifunza mengi kama anavyoonekana kujua mengi. Pamoja na kwamba kipindi kirefu kilikuwa kimepita bila Joram kufanya mazoezi ya viungo na akili, pamoja na kule kuzoea starehe za mahotelini na ulevi mwingi, bado hakuna kama binadamu yeyote angeweza kumfanya kama Chonde alivyokuwa amemfanya.

Ile hamu iliyokuwa imelala usingizini ikaibuka upya katika moyo wake. Hamu ya mapambano, vitisho, maafa, damu, na mikasa, hamu ya kuwatia adabu watu ambao wanependa kuwafanya vibaya binadamu wenzao. Chonde alionekana kama mmoja wao. Joram alimtazama tena na kutabasamu kwa uchungu huku akisema, "Haya umeshinda. Kinachofuata?".

"Ni kifo chako", Chonde alijibu kijeuri. "Siwapendi vijana watundu kama wewe. Kufa huna budi.

"Kosa langu".

"Unapenda kufa?".

Joram alifikiri kwa makini lipi angefanya kuahirisha hukumu hiyo ya kifo. Alihitaji muda ili ikiwezekana itokee njia moja ama nyingine ya kuyaokoa maisha yake. Akaanzisha maongezi kwa sauti ambayo aliifanya dhaifu kuliko alivyokuwa akimuuliza Chonde hili na lile. Chonde alikuwa mgumu wa kutoa habari kama jabali. Kati ya maneno ya kashfa na matusi kwa Joram, nchi na bara zima la Afrika hakutamka neno lolote litakalomfanya Joram ajue kuwa yuko katika ulimwengu wa ujasusi. Alichoambulia ni zile hisia tu kuwa Chonde hakuwa raia wa kawaida tu.

"Umeahirisha sana kifo chako", Chonde alisema baadae kama aliyekuwa akizisoma fikira za Joram. Sasa iliyobaki ni kazi ndogo ya kukutoa uhai. Nitakuua kwa mkono wangu wa kushoto. Maiti yako itaokotwa kesho ikiwa imevunjikavunjika kama mtu aliyeanguka kutoka ghorofani. Kwa jinsi ulivyobadilika kitabia hakuna atakayejuwa kuwa umeuawa", baada ya maneno hayo, Chonde aliinuka na kumwendea Joram kama alivyofanya awali, lakini macho yake yalitangaza kitu kimoja tu, kifo.

Joram alijiandaa. Akijua kuwa vita vilivyokuwa mbele yake vilikuwa vita vikubwa pengine kuliko alivyowahi kupambana navyo. Vita vya kuitetea roho yake. Akaikusanya akili yake yote na kumsubiri Chonde kishujaa.

Mara mlango ukagongwa.

Chonde aligutuka kwa mshangao na kuutazama mlango. Joram hakuipoteza nafasi hiyo. Aliruka na kuufanya mguu wake utue katika shingo ya Chonde. Lilikuwa pigo ambalo Chonde alilitegemea. Akalihepa na kuachia judo ambalo Joram aliikinga. Papo hapo mlango ukagongwa tena na kufunguka na kuruhusu msichana mzuri kuingia.

Alikuwa yule msichana wa mapokezi pale Embassy hoteli. Alitokwa na macho ya mshangao kuona miili yenye jasho, michubuko na damu, ya wanaume hawa, ilikuwa tayari kuvamiana. Wote walimtazama msichana huyo. Chonde akimlaani, Joram akishukru. Akiwa kama hajui lipi la kufanya msichana huyo aliduaa mlangoni, Midomo wazi.

"Karibu ndani. Tulikuwa tukifanya mazoezi ya viungo na huyu rafiki yangu", Chonde alimwambia yule msichana huku akivaa tabasam ambalo lilificha kabisa tabasam la mauaji. "Karibu ndani. Na wewe ndugu yangu nenda zako sasa. Tutakutana siku nyingine".

Joram hakuamini, aliyarekebisha mavazi yake na kutoka chumbani humo taratibu. Hakuwa amesahau kumwachia msichana huyo tabasam la shukrani.
*************************************************************

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU