SURA YA PILI
Kati ya watu
ambao wameisumbukia sana nchi hii, wakiziweka roho zao katika minada ya maafa
na kwato za mauti wakiilinda nchi isimezwe na jangwa la misukosuko
inayosababishwa na majasusi hatari wa Afrika, ni Mzee huyu Mkwaju Kombora.
Tangu utoto
wake baada ya kumaliza kidato cha sita, alijikuta akitoka chuo hadi chuo, huku
akifundishwa mbinu mbalimbali za kupambana na adui. Baada ya kuhitimu vizuri
alijikuta akivaa magwanda ambayo mabega yake hayakukoma kubadilikabadilika hadi
alipojikuta Inspekta wa kikosi hiki maalumu. Kupanda kwake ngazi mara kwa mara
kulitokana na moyo wake wa kishujaa na juhudi zisizo kifani katika kuwakabili
adui wa nchi. Mara kwa mara alikuwa akiwashinda adui zake isipokuwa safari
chache ambazo alielekea kukata tamaa. Hata hivyo asingekosa kumshukuru Mungu
kwani nyakati hizo alitokea kijana yule ambaye alisaidia kuwanasa adui kwa hila
zake za kutatanisha. Kijana ambae jina lake lisingeweza kumtoka akilini, huyo
ni Joram Kiango.
Kombora
asingesahau mchango wa kijana huyu katika mikasa ile ambayo Mswahili mmoja
ameamua kuandika vitabu ili apate chochote kile na kuviita Dimbwi la Damu,
Mikononi mwa Nunda, Nasikia kuua tena na Salamu kutoka Kuzimu. Hata hivyo, kama
polisi wengine, Kombora asingeweza kutamka hadharani kuwa Joram alifanya lolote
la haja isipokuwa alibahatisha na kuhatarisha maisha yake. Lakini leo Kombora
alitamani kumbembeleza Joram, hata kwa kumuangukia miguuni, endapo ingebidi,
amsaidie katika kuutatua mkasa huu ambao ulikuwa ukimtoa jasho yeye na polisi
wenzake wote wa nchi zilizo mstari wa mbele kwenye ukombozi Kusini mwa Afrika.
Yalikuwa
yakitokea mambo mengi. Mambo mazito na ya kutisha zaidi ya walivyoyafahamu
wananchi wa kawaida ambao wanategemea gazeti, radio na televisheni ziwape
habari. Kila mmoja alikuwa ameshika mikasa ya kuteketea kwa mamia ya maisha ya
watu wasiokuwa na hatia ambao walipata ajali ya kutatanisha katika uwanja wa
mpira huko Nigeria. Pia ni wengi waliosikia juu ya kuungua kwa maghala ya
chakula bila sababu mahususi inayoeleweka huko Harare. Zaidi, hakuna mtanzania
ambaye hakupata kusikia kuungua tena kwa jengo la Benki kuu ambalo lilikuwa
likijengwa upya.
Hayo ni
maovu ambayo yalisikika katika vyombo vya habari na mitaani. Hayakumtisha sana
Kombora. Lakini kulikuwa na haya ambayo yalikuwa bado siri mioyoni mwa wakubwa
wa idara ya usalama wa taifa. Haya ambayo hayasemeki wala kutangazwa.
Viongozi
wanane wa vyama kadhaa vya wapigania uhuru wa Afrika Kusini na mwakilishi wa
PLO hapa nchini ambao walikuwa wakikutana kwa faragha katika jengo moja jijini
Dar es Salaam walikuwa wamefariki ghafla katika moja ya ajali zisizoeleweka.
Hakuna anayefahamu kikamilifu chanzo cha vifo hivyo, isipokuwa kwamba walikufa
kwa kuungua moto uliolipuka ghafla katika chumba chao cha mkutano. Juhudi zote
za kutafuta chanzo cha moto huo hazikufanikiwa.
Zaidi ya
hao, kuna wale mawaziri wa nchi zisizofungamana na upande wowote ambao
walinusurika kufa katika ajali ambayo haikutofautiana na hii ya Dar es Salaam.
Mkutano wao ulikuwa umeandaliwa kufanyika katika chumba fulani katikati ya jiji
la Lusaka. wakati wakijiandaa kwenda huko lilitokea suala jipya ambalo
lilichelewesha msafala wao zaidi ya nusu saa hivi. Kuchelewa huko kuliyaokoa
maisha yao. Kwani chumba hicho kililipuka kwa moto na kupoteza maisha ya
wafanyakazi wawili wa chumba hicho na kuharibu vifaa vyote. Kama awali, chanzo
cha moto huo hakikupata kufahamika mpaka leo.
Hayo ni
baadhi tu ya mambo yaliyotokea. Kulikuwa na hisia kuwa mkono wa makaburu wa
Afrika Kusini ulikuwamo katika vitendo hivyo. Lakini hisia hizo hazikuwa na uhakika
kamili sasa baada ya ushahidi mdogo ambao ulikuwa ukielekea kutoweka kwa njia
nyingine ya kusikitisha.
Ushahidi huo
ulikuwa ukielekea kuchipuka baada ya ule moto ambao uliteketeza benki kuu. Yuko
askari mmoja ambaye alisema aliamini moto huo ulisababishwa na mtu mmoja ambaye
alifika katika jengo hilo usiku na kujiita kuwa ni mmoja kati ya mafundi ambao
walikuwa wakishughulikia jengo hilo. Jengo lilikuwa chini ya ulinzi mkali wa
askari huyo ambaye alimwamru mtu huyo kusimama na mikono yake iwe juu. Mtu huyo
alitii amri na kumsihi askari kwa maneno mengi kuwa amesahau kitu cha muhumu
sana kwake katika jengo hilo, jambo ambalo lilimfanya askari amruhusu kuingia
ndani baada ya kumpekua kwa umakini mkubwa. Mtu huyo aliingia harakahara na
baada ya dakika kadhaa alirudi huku akiwa ameshikiria hirizi mkononi na kusema
kwa furaha. "Nilikuwa nimesahau hii, ndugu yangu. Bila kuwa na hii mfukoni
siwezi kuishi zaidi ya masaa ishirini na nne", mtu huyo alisema
akimuonyesha yule askari ile hirizi.
Askari huyo
hakuwa amemwamini sana mtu huyo, kutokana na jinsi alivyomuona mkakamavu maana
hata alipoelekezwa mtutu wa bunduki hakuonekana kubabaika. Hivyo jengo hilo
lilipolipuka moto masaa kadhaa baadaye, askari huyo alilieleza tukio hilo kwa
wakubwa zake ambao walimweka kati ya watu ambao walilazimika kuongea na Kombora
ana kwa ana. Baada ya kumsaili kwa mapana na marefu, Kombora alielekea kuamini
kuwa mtu huyo aliyeingia katika jengo hilo usiku alihusika kwa njia moja au
nyingine katika janga hilo. Lakini pindi walipobuni mbinu za kuanzisha msako wa
kumtafuta mtu huyo, askari huyo ambaye ni mtu pekee aliyewahi kumuona mtu huyo,
alikutwa akielea baharini pwani ya Magogoni akiwa maiti. Hakuna aliyeweza
kueleza kilichomtoa kwake Magomeni Mikumi na kuja kuogelea kwa mara ya mwisho
Magogoni.
Ilikuwa
dhahili kuwa askari huyo aliuawa.
Jambo ambalo
lilimfanya Inspekta Kombora na wenzake wazidi kuamini kwamba kulikuwa na namna
katika ajali hizo zilizotokea katika miji mbalimbali ya Afrika huru. Juhudi zao
za kutafuta chanzo na watendaji wa maafa hayo hazikuelekea kuzaa matunda yoyote
zaidi ya hisia tu, kwamba Afrika Kusini ilihusika. Hisia ambazo ziliongezewa
uzito na vitisho ambavyo vililetwa kwa njia mbalimbali zikitishia uhai wa
maisha ya watu na nchi ambazo eti zingeendelea na msimamo wao wa kuibana Afrika
Kusini. Vitendo ambavyo, licha ya kusababisha hofu na mashaka, vingeweza
kupunguza hamasa za moyo wa kimapinduzi katika fikra za mashujaa endapo
zingeachiwa kuendelea. Ni hapo ndipo Inspekta Kombora alipozikumbuka silaha zote
na kutamani zielekezwe Afrika Kusini. Ni hapo pia alipowakumbuka mashujaa wote
na kutamani waelekee Afrika Kusini. Na kati ya mashujaa hao jina la Joram
Kiango lilitangulia kumjia rohoni.
Hiyo ilikuwa
baada ya kuwasiliana na wakuu wa vikosi vyote maalumu vya upelelezi katika nchi
zote zilizokwisha husishwa na maafa hayo ya kutatanisha. Walishauriana kuwa
kila nchi ifanye juu chini kuhakikisha kisa cha maafa hayo kinafahamika na
ikiwezekana maafa hayo yakomeshwe. Ndipo Inspekta Kombora alipoanza kufanya
kila juhudi. Tumaini pekee ambalo lilielekea kumpatia walau fununu, yaani yule
askari mlinzi wa benki kuu alikuwa sasa ameuawa kwa hila. Harakati za
kupeleleza nani alihusika katika kumuua askari huyo hazikuwa zimezaa matunda
yoyote. Hivyo Inspekta Kombra alijikuta hajapiga hatua yoyote katika jukumu
hilo. Badala yake alijiona kama kiwete ama mtu aliyepooza ambaye anasubiri
maafa ya moto unaomjia kasi.
"Joram
lazima ashirikishwe", Kombora alifoka kimoyomoyo.
Alikuwa na
habari zote za Joram, kuwa tangu baada ya mkasa wa salamu toka kuzimu alikuwa
ameiacha ofisi yake na kuanza maisha ya kiupuuzi ya kustarehe katika mahoteli
na mabaa akijistarehesha na yule msichana mzuri wa Arusha aitwaye Nuru.
"Yeye
si mtu wa kuupoteza muda wake katika mabaa. Kipaji chake kinahitajika sana
katika vita hii. lazima apatikane", Inspekta Kombora alisema huku akiinuka
kutoka kitini.
Alimtuma mtu
ambaye alizunguka katika mahoteli makubwa na kumpata Joram. Lakini, kama
Inspekta Kombora alivyotegemea, majibu ya Joram yalikuwa ya kijeuri kiasi
kwamba mtu huyo alijiona mjinga na kurudi kwa Inspekta Kombora akiwa amechukia. Jambo ambalo lilimfanya jioni hii Inspekta Kombora mwenyewe ayavue magwanda
yake na kuvaa mavazi ya kawaida, kisha akajitosa katika ukumbi wa Embassy ambao
aliambiwa kuwa Joram alikuwemo akistarehe.
*************************************************************
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment