UCHU

SURA YA KUMI NA MOJA

KAMPALA

JKS aliamka mapema asubuhi huku roho yake ikiwa na furaha nyingi sana. Sasa hivi alikuwa akielekea benki kwa ajili ya kuchukua pesa zake. Hisia za urais wa Tanzania zilimjia katika mawazo yake, akatamani kuwa kiongozi wa Tanzania ili atimize ndoto yake ya kuwa mheshimiwa rais wa Tanzania.

Baada ya kustafutahi kwa chai nzito, alipiga simu kwenye benki yake hapo Geneva na kuuliza mahali ilipo. Baada ya kupata maelekezo sehemu na mtaa ambao benki ipo, alipiga simu mapokezi na kumuomba mhudumu amletee teksi saa tatu kamili ili impeleke benki.

Baada ya kujiweka sawa, alitelemka chini taratibu ilikuwa majira ya saa tatu kamili, akiwa amebeba mkoba wake wa ngozi ya mamba mkononi aliokuwa amepewa kama zawadi na rafiki yake Jean.

Alipofika chini alikuta teksi inamsubiri mbele ya hoteli. Alifungua mlango wa nyuma kama VIP akaingia, akampa dereva anuani ya benki, baada ya kuthibitisha ni eneo gari dereva aliondoa gari huku mawazo ya JKS yakiwa juu ya baraza lake la mawaziri baada ya kuukwaa  urais.

Jean alikuwa amempa jina la meneja wa benki na kumweleza kuwa akifika benki amwone meneja huyo. Alipofika benki alitelemka na kumwambia mwenye teksi amsubiri akaingia ndani ya benki na kuelekea mapokezi. alimwonyesha yule msichana wa mapokezi jina la meneja. Asubuhi ile meneja alikuwa bado hana watu wengi, hivyo akamkaribisha vizuri sana.

"Karibu Mheshimiwa, nikusaidie nini?", meneja wa benki aliuliza JKS baada ya kuingia ofisini kwake.

"Asante", JKS alijibu na kutoa bahasha yenye maelezo yake yote. Meneja aliipokea kwa tabasmu na kuifungua bahasha na kuanza kusoma. Alivuta Kompyuta yake na kuanza kushughulika. Meneja, akiwa anatabasamu tena alimgeukia JKS na kumweleza, "Samahani, hii akaunti imefungwa jana na aliyeifunga ametoa pesa zote na kusema mtu yeyote akifika hapa kuuliza juu ya akaunti mwenye kitambulisho namba hii, aelezwe kuwa akaunti hiyo imefungwa maana mkataba umeisha. Samahani sana mheshimiwa, nina wateja wengine wananisubiri".

JKS alichanganyikiwa. Aliinuka, mara akamuona yule meneja wa benki anakuwa mkubwa zaidi na yeye JKS anakuwa mdogo na chumba kinazidi kuwa kidogo, akasikia anakosa pumzi halafu giza nene likamuingia mara akaanguka chini na kupoteza fahamu. 


ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU