Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama akizungumza na wadau wakati wa uzinduzi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi uliofanyika jijini Dar es Salaam
Na
Ismail Ngayonga wa MAELEZO, Dar
es Salaam
SERIKALI imewaagiza
Waajiri wote nchini kuwasilisha kwa wakati michango ya mafao ya fidia kwa
wafanyakazi ili kuwawezesha watumishi wao kupata huduma za matibabu pindi watakapoumia
au kuugua wakiwa katika maeneo yao ya kazi.
Agizo hilo limetolewa
leo Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera,
Bunge, Ajira, Kazi na Ulemavu) Jenister
Mhagama wakati alipokuwa akizindua huduma za utoaji wa mafao ya fidia na ubia
baina ya mfuko wa fidia kwa wafanyakazi (WCF) na watoa huduma za afya nchini.
Mhagama alisema suala
la uchangiaji wa mafao hayo sio la hiari ila lipo kisheria na hivyo ni wajibu
wa waajiri wote nchini kuhakikisha kuwa wafanyakazi wao wanaingizwa katika
mfumo huo ili kuwawezesha wafanyakazi kuwa na uhakika wa kulipwa fidia pindi
wanapokuwa kazini.
“Katika mwaka wa
fedha 2016/17 Serikali imelipa michango yote ya wafanyakazi wake, na huu ni
mfano unaopaswa kuigwa na waajiri wengine nchini, na natoa rai kwa Chama cha
Waajiri Nchini (ATE) na Shirikisho la Wafanyakazi nchini (TUCTA) linasimamia
suala hili” alisema Mhagama.
Aidha Mhagama alisema
lengo la kuanzishwa kwa mfuko huo wa wafanyakazi nchini ni kusaidia kutatua
kilio cha muda mrefu cha wafanyakazi wa sekta za umma na binafsi, ambao
wamekuwa wakilalamikia huduma hafifu zinazotolewa pindi wapatapo majanga
mbalimbali wakiwa kazini ikiwemo ajali na vifo.
Waziri Mhagama
alitaka Bodi ya mfuko huo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa sheria zilizopo
ili kuhakikisha kuwa waajiri wote hususani wa sekta binafsi wanawasilisha michango
kwa wakati.
Akifafanua zaidi
Waziri Mhagama aliuataka mfuko huo kujitangaza zaidi kwa sekta zisizo rasmi ili
kuwawezesha wananchi wengi zaidi hususani wa kipato cha chini kujiunga na mfuko
huo na kuwasaidia kufaidi huduma zinazotolewa.
“Natoa rai kwa mifuko
yote ya hifadhi ya jamii nchini ikiwemo wa WCF mjitangaze katika sekta zisizo
rasmi ikiwemo waendesha bodaboda, akina mama lishe, kwa kuwa idadi yao ni kubwa na hiyo itawezesha kupata wanachama wengi
zaidi” alisema Mhagama.
Kwa upande wake
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko huo, Masha Musomba alisema hadi kufikia sasa mfuko huo
umeweza kutoa usajili wa waajiri 5945
pamoja na kuendesha mafunzo mbalimbali ya kuwajengea uwezo watumishi wa mfuko
huo ikiwemo madaktari.
Aidha Musomba anasema
pia mfuko huo umeingia ubia na taasisi 7 za utoaji huduma za afya nchini,
ambazo ni Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Taasisi ya Mifupa Muhimbili
(MOI), na Taasisi ya Kansa ya Ocean Road.
Musomba anazitaja
taasisi nyingine kuwa ni Strategis, AAR, mfuko wa Jubilee, na Hospitali ya
Taifa Muhimbili, ambapo taasisi hizo zinazoendelea kushughulikia kesi 189
zilizolipotiwa katika mfuko huo.
Naye Mtendaji Mkuu wa
Chama cha Waajiri Nchini (ATE), Aggrey Mwinuka alisema mfumo huo wa fidia
umekuja katika wakati muafaka kwa kuwa sheria zilikuwepo katika vitabu na
hazikuwa na utekelezaji uliokusudiwa.
Mwinuka alisema ili
kuhakikisha kuwa malengo ya mfuko huo yanatekezeka ni wajibu wa Serikali
kuhakikisha kuwa inafanya majadiliano ya mara kwa mara na waajiri ili kuangalia
viwango vya makato ya michango ya wafanyakazi wa sekta ya umma na binafsi.
Mwenyekiti wa Bodi ya
mfuko huo, Emmanuel Homba alisema uwekaji wa mfumo wa mafao ya fidia utawezesha
wafanyakazi katika sekta za umma na
binafsi kuchangia kikamilifu katika Sera ya Serikali ya Awamu ya Tano ya ujenzi
wa uchumi wa viwanda nchini.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama akikata utepe kuzindua Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Kushoto ni Naibu Waziri . uzinduzi , Abdallah Posi.
Waziri Jenista Mhagama akisoma ujumbe baada ya kuzindua Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi jijini Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama akikabidhi Tuzo ya Ushiriki kwa mmoja wa wadau waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi uliofanyika jijin Dar es Salaam
Mkurugenzi Mtendaji Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi Masha Mshomba akiongea na wadau mbalimbali kabla ya uzinduzi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi uliofanyika jijini Dar es Salaam
Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi, Bw. Emanuel Humba akizungumza na wadau kabla ya uzinduzi wa Mfuko huo.
Baadhi ya Wajumbe wa Bodi ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi wakimsikiliza Waziri wa Kazi, Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Mfuko huo uliofanyika Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na walemavu, Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na Watendaji Wakuu wa Taasisi za Serikali na zisizo za Kiserikali baada ya uzinduzi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi uliofanyika Dar es Salaam
Baadhi ya Wajumbe wa Bodi wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi wakimsikiliza kwa makini Waziri Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Mfuko huo uliofanyika jijini Dar es Salaam (PICHA ZOTE NA BENJAMINI SAWE - MAELEZO
Comments
Post a Comment