MBILINYI AWAAMBIA MAZIRI UPEPO WA KIMBUNGA UNAKUJA

Mbunge wa Mbeya Mjini kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Joseph Mbilinyi (pichani), amesema Mawaziri wa Serikali ya Awamu ya Nne ya Rais Jakaya Kikwete wanaotamba kuwa hawatang'oka kwenye wadhifa huo, watang'olewa kwa kimbunga kinachokuja.

Akizungunza Mbunge Mjini Dodoma saa 6:45 mchana leo, amemhakikishia Waziri Mkuu, Bw. Mizengo Pinda kuwa moto uliowashwa na wabunge bila kujali itikadi zao kisiasa, lazima mawaziri waliotajwa kuhusika katika kashifa ya ubadhirifu watangoka.

Amesema hata kama kimbunga hicho hakitang'oa nyumba nzima,lakini kitaondoka na paa la nyumba hiyo, akimwaanisha kuwa iwapo mawaziri hao wataendelea kung'ang'ania nyadhifa hizo, Waziri Mkuu Pinda atang'olewa kwa upepo huo.

"Sitanii, huu ni upepo wa kimbunga, kama hautang'oa nyumba, utaondoka na paa la nyumba, inasemekana kuna tetesi kuwa wameambia huu ni upepo tu utapita, nakuhakikishia Mheshimiwa Spika, upepo huu wa kimbunga lazima utawang'oa, watake wasitake", amesisitiza Mbilinyi.

Amewataka ni vyema mawaziri walioshindwa kazi ya kuwajibika waachie ngazi, kama walivyoombwa na Mbunge wa Vunjo, Bw. Agustine Mrema wa TLP. Mrema aliwaambia mawaziri hao kuwa iwapo kazi ya kuwajibika imewashinda, ni bora wakae kando ili wengine wafanye kazi hiyo.

Huku Waziri Mkuu Pinda akionesha kutabasamu, Bw. Mbilinyi amesema Tanzania ni moja ya nchi zenye vivutio vya kila aina, wanyama wanachukuliwa na kusafirishwa kinyemela bila kufuata taratibu za nchi, na kwamba baadhi ya wawekezaji huingia nchini na wageni kwa mgongo wa Luteni Kanali Mstaafu Abdulhaman Kinana.

Amesema kazi yao kama vyama vya upinzani Bungeni ni kupambana na Chama Tawala, ili kijisahihishe kwa wananchi, huku akiwataka wafanye maandalizi ya kushindana na CHADEMA watakapokuwa wapinzani.

"Mheshimiwa Spika, kazi ya kambi ya upinzania Bungeni ni kukosoa kila uozo unaofanywa na Chama Tawala, waache kufanya madudu, hii itawasaidia watakapokuwa wapinzani nao wajipange kutukosoa tutakapoingia madarakani kuwatumikia watanzania", anasema. 
Akishangiliwa na wabunge, huku wengine wakivunjika mbavu kwa vicheko, Bw. Mbilinyi (pichani tena), amesema upepo huo wa kimbunga, hautapita hivi hivi lazima utaharibu nyumba, kama itashindikana basi paa la nyumba hiyo litang'oka na waliomo watahama.

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU