Tangu aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba (pichani) akabidhi Rasimu ya Pili ya
Katiba, kumekuwa na chokochoko, visa, matusi na kejeli kwa wajumbe
wenzake hasa kwa sababu rasimu hiyo imependekeza muundo wa muungano wa
Serikali tatu.
Rais Jakaya Kikwete alianza kukosoa muundo huo
alipokuwa akifungua Bunge Maalumu la Katiba akisema kuwa utazaa
serikali legelege ya Muungano na itashindwa hata kulipa mishahara ya
jeshi hivyo laweza kupindua nchi.
Baada ya hapo, basi ndiyo wajumbe wa CCM wamejawa mori na kuanza kuvurumisha kejeli kwa Warioba na tume yake. Wengine kama Waziri William Lukuvi wamekwenda hadi
kanisani na kuanza kuwatisha wananchi kuwa jeshi litapindua nchi kama
Serikali zitakuja.Kituko zaidi ni maelezo ya mbunge wa Mbinga
Magharibi, Kapteni John Komba aliyesema kuwa ataingia msituni endapo
serikali tatu zitakuja.
Ni kauli za aibu ambazo huwezi kutegemea kuwa
zinaweza kutolewa na waheshimiwa wetu. Kama kauli hizo zingetolewa na
wabunge wa upinzani basi ndiyo usiseme. Hivi haya malumbano yote ni ya nini ikiwa lengo ni
kuboresha tu Muungano? Ingekuwa kweli kwamba Jaji Warioba ametangaza
kuvunja muungano kweli, wote tungemlaumu. Lakini kama lengo ni
kuboresha, tatizo liko wapi?
Hivi karibuni, Jaji Warioba amehoji maswali saba
ambayo kama yatapatiwa majibu na wanaopinga muundo wa Serikali tatu basi
tuendelee na muundo uliopo. Nifafanua tu hapa machache. Kwanza, kwa nini wanapinga muundo wa Muungano wakati walioupendekeza ni wananchi. Wiki iliyopita katika safu hii niliuliza, kama
Rais Kikwete na wanaCCM hawakutaka muundo huu, kwa nini waliunda Tume ya
Mabadiliko ya Katiba ilihali wakijua kabisa tume kama hizo zilishatoa
mapendekeo kama hayo?
Kama wananchi ndiyo wanataka serikali tatu, kwa nini wapingwe? Kama wananchi wanapingwa basi tukubaliane kuwa muungano huu siyo wananchi bali ni viongozi na masilahi yao.
Jaji Warioba na baadhi ya wajumbe wa Tume ya mabadiliko ya Katiba wakiteja jambo kabla ya kuwasilisha rasmu ya Katiba Mpya Bungeni Dodoma iliijadiliwe na wabunge
Comments
Post a Comment