HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

II

Ilikuwa yapata muda wa saa tatu na nusu usiku, Willy na Nyaso walibisha hodi kwenye chumba cha Willy baada ya kujua kwamba wenzake walikuwa wanamsubiri ndani. Willy na Nyaso walikuwa wamefika pale chumbani kwa kupitia njia tofauti kama walikuwa hawafahamiani. Willy alikuwa amepanda kwa kutumia ngazi, wakati Nyaso alitumia lifti.

"Nani", Bon aliita kwa sauti.

"Willy".

Bon alifungua mlango huku akiwa na bastola mkononi. Alipomuona msichana Bon alirudisha mlango haraka haraka.

"Na wewe woga umezidi, karibu ndani Nyaso", Willy alimkaribisha huku akirudisha mlango baada ya Nyaso kuingia ndani.

"Maama", Mike alisema kwa mshangao.

"Nini?", Willy aliuliza kwa kebehi.

"Wewe huwa unawatoa wapi hawa?".

"Malaika huyu ama mwanadamu?", Mike aliendelea kushangaa.

"Wewe unafikiri vipi?", Willy alimuuliza.

"Malaika", Mike alijibu huku wote chumbani wakimwemwesa.

"Subiri sasa niwafahamishe kwa huyu 'malaika'. Mtoto huyu anaitwa Nyaso. Ni Nyaso tu. Msiulize zaidi. Nyaso hawa ndiyo rafiki zangu niliokuwa nikikueleza. Yule maneno mengi ni 'Kikuyu' toka Kenya. Huyu ni Bon toka Afrika Kusini na yule pale anayejifanya mkimya ni Rocky kutoka Zimbabwe", Willy alisema.

"Nashukuru kuwafahamu", Nyaso alijibu.

"Sisi ndiyo tunapaswa kushukuru kwani kumfahamu mtoto mzuri kama wewe ni fahari ati", Mike alisema.

"Willy kweli watanzania mnatoa watoto, mimi sina hata maneno. Hivi vijana wa hapa mtaweza kujenga?, Mtoto kama huyu akisema umpe mshahara wako wote wa mwezi unaweza kukataa? La hasha rocky alisema.

"Ahsante kwa sifa ulizonipa", Nyaso aliitika.

"Sikia sauti yake nyororo", Bon aliongeza.

"Wacha sauti na sura, Nyaso anayo mengi zaidi", Willy aliasa.

"Haya Willy, umemleta huyu mrembo ili tukusifu ama unayo mengine zaidi?". Mike aliuliza.

"Wacha maneno mengi, nyinyi wakenya mkijua kiswahili kadiri, sisi watanzania huwa watufui dafu", Willy alisema.

"Hayo ndio maendeleo", Mike aliongeza.

"Hebu jamani, nisikilize kwa makini. Sikuja na msichana huyu ili kuwakoga. Kusema kweli mambo yamepamba moto tayari na ni lazima na sisi tuwemo kazini", Willy alisema halafu aliwaeleza juu ya mazungumzo yake na Nyaso, juu ya F.K na mwisho jinsi walivyokwenda kwa Chris na kukuta ameuawa.

"Tunao uhakika kuwa F.K ndiye aliyefanya mauaji hayo. Mimi ninahisi amekuwa na wasiwasi baada ya kusikia kwamba mimi nimemhoji sana Chris. Kwa hiyo aliamua kutumia mbinu zile zile za siku zote: Yaani maiti hawana maneno. Hii ina maana kwamba fumbo limefumbuliwa tayari. Majasusi tunaowatafuta wamejificha kwa F,K. Kutokana na maelezo ya Nyaso kuhusu jumba la F.K. lilivyo ni dhahili kwamba majasusi hao wako mle ndani, hivyo kazi imebaki kwetu", Willy alisema.

"Sasa mipango iko vipi bosi?", Bon alimwuliza Willy.

"Kwanza kabisa mimi na Nyaso tutakwenda kufanya uchunguzi kwenye jumba la F.K. kama nilivyowaeleza, jumba hilo linazo njia za chini kwa chini. Na kama hivyo ndivyo, basi mle kuna sehemu nyingi ambazi ni za siri. Kwa sababu hiyo mimi naona ni bora niende na Nyaso ambaye atanionyesha mahali jumba hilo lilipo. Baada ya kufanya utafiti, nitarudi hapa ili tujadili jinsi gani ya kuwakabiri hao majasusi usiku huu, ama mnasemaje?", Willy aliuliza.

"Hisia zetu ni sahihi. Sasa kwa nini sisi sote tusivamie jumba hilo mara moja na kufunga kazi", Mike alipendekeza.

"Hapana Mike, huenda kazi yenyewe isiwe rahisi kama unavyofikiri. Haitakuwa vizuri sisi sote kujitumbukiza bila kufanya uchunguzi. Uwezekano wa kuangamia sisi sote upo, na hilo litakuwa pigo kubwa kwa Afrika huru na kwa wapigania uhuru wa Afrika Kusini. Hivyo utakuwa ushindi kwa makaburu. Amini usiamini, mapambano yanayoendelea huko Afrika Kusini, kwa kiwango kikubwa, yanategemea ushindi wetu", Willy alijibu.

"Mimi nakubaliana na wewe kabisa", Bon alisema halafu akaendelea, "Kusema kweli, vita kamili vimeanza ndani ya Afrika Kusini. Ushindi wetu hapa utawatia hamasa vijana wa kizalendo ambao wanapambana na askari wa makaburu. Nia ya makaburi ni kutuvuruga sisi huku na kufanya wana-ukombozi walio ndani na nje ya Afrika Kusini kuchanganyikiwa. Vita vya Ukombozi tayari vimevuka hatua ya kutumia mawe na marungu. Awamu hii ni ya kutumia silaha za moto. Hivyo, na sisi tuwe tayari kujitoa muhanga ili matunda ya uhuru yapatikane kwa watu wetu", Bon alisema.

Willy alikuwa karibu kuzungumza jambo fulani, mara simu ililia. Wote waliangaliana halafu Willy aliamua kusikiliza simu.

"Hallo", Willy aliitikia.

"Mimi ni mzee Hamisi, naomba kuzungumza na Willy", sauti ya mzee Hamisi ilisikika.

"Mwenyewe nazungumza, habari za saa hizi mzee", Willy alijibu.

"Habari ni nzuri, Willy nakuhitaji uje hapa nyumbani kwangu haraka kwani nina habari muhimu sana", Hamisi alisema, Willy alisita kidogo halafu akamjibu.

"Sawa, nakuja", halafu alikata simu bila kusema maneno zaidi.

"Huyo ni nani?", Mike aliuliza.

"Ni mzee Hamisi, anasema ni lazima niende nyumbani kwake kwani ana habari muhimu", Willy alibu.

"Hivi sasa itabidi mimi, Rocky na Nyaso tuandamane mpaka kwenye jumba la F.K. Sisi tutafanya utafiti halafu turudi hapa", Bon alishauri.

"Hiyo ni sawa, wewe Mike huna budi kubaki hapa. Kama kuna habari zozote, tutawasiliana. Bon na Rocky ni lazima kuchukua tahadhari kubwa kwani katika mazingira ya jumba kama lile, kunaweza kukatokea jambo lolote", Willy aliasa.

"Huyu Hamisi anakaa wapi?", Nyaso aliuliza.

"Anakaa kwenye nyumba za maafia huko Kijenge, karibu na barabara iendayo Themi Hill. Kwa hiyo tutaondoka wote halafu nyinyi mtaniacha barabarani. Baada ya kuzungumza na mzee Hamisi, mimi nitatafuta njia yangu mwenyewe ya kurudi ili tukutane hapa tena. Sasa Nyaso, wewe telemka chini na kutusubiri kwenye gari", Willy alielekeza.

Wote watatu walichukua silaha ambazo walifikiri wangezihitaji. Willy pia, ingawa alikuwa anakwenda kwa mzee Hamisi, alichukua silaha akiwa tayari kwa lolote. Wanaume walishajuwa kwamba walikuwa wanawinda na huku wakiwindwa. Mike ambaye alikuwa na jukumu la kubaki pale hotelini, naye alikaa tayari na silaha zake. Walipokuwa tayari, walielekea kwenye gari huku kila mmoja akitumia njia tofauti na wenzake.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU