HOFU

KABLA YA USIKU WA MANANE

III

"Ahsante". F.K. alimwambia mzee Hamisi baada ya kuzungumza na Willy.

"Hebu ondoa huo mtutu wa bunduki kwenye kichwa changu. Unajua mimi ni mzee sana na kuniweka katika hali hii kunaweza kunisababisha nipate ugonjwa wa moyo. Kazi uliyotaka nimekufanyia, zaidi unataka nini", mzee Hamisi aliuliza.

"Ha ha", F.K. aliangua kicheko kwa jeuri halafu akaendelea, "Mzee Hamisi sina budi nikushukuru kwa yote uliyonifanyia, maana bila kupata habari ulizonipa mipango yangu isingefikia hatua hii. Wewe ni mtu mwenye ujuzi na uzoefu katika shughuli za usalama. Sina shaka umeshahisi kitu gani kinatendeka baada ya kuona unavamiwa na kundi la Wazungu. Hawa ni askari kutoka Afrika Kusini. Ufahamu fika kwamba wewe ni msaliti wa nchi yako. Hii imetokana na nyinyi watu wenye vyeo Serikalini kupenda pesa. Pesa nilizokupa zilikufanya uisaliti nchi yako. Ha ha! Uchu wa pesa utaimaliza Afrika. Je, unajua adhabu ya usaliti ni nini", F.K. aliuliza kwa kebehi.

"Usiniue F.K. kwani hata ukiniua, Willy atakumaliza...", Hamisi alisema huku akipapatika.

"Stumke, fanya kazi yako", F.K. aliamrisha, mzee Hamisi aliinuka na kabla hajachukua bastola yake kutoka kwenye koti, alipigwa risisa ya paja na kichwani na kufa papo hapo.

"Sasa msubiri Willy. Nina imani kazi yenu itakuwa rahisi", F.K. alisema huku akimpa Stumke swichi ya gari lake. Stumke alikuwa kiongozi wa yale majasusi yaliyomvamia mzee Hamisi, na ambayo sasa yalikuwa yakimsubiri Willy. Baadaye F.K. alichukua funguo za marehemu Hamisi kutoka mezani kwake na kuaga.

"Stumke, tuonane nyumbani. Lakini nawashauri mkae macho sana. Ingawaje Willy atakuja bila tahadhari, ni mtu hodari kupindukia. Msimpe mwanya bali mtumie mbinu zote mnazozifahamu", F.K. alionya.

"Usiwe na wasiwas, F.K. mimi nilikwisha ongoza kundi hili hili na kuteketeza kikosi kizima huko Namibia. Itakuwaje tushindwe mtu mmoja?, Huyo mfute kutoka kwenye orodha ya adui walio hai. Labda asitokee!", Stumke alijigamba.

ITAENDELEA

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU