HOFU

SEHEMU YA KUMI NA MBILI

NI FUNDISHO

"Hebu jamani, tusikilize taarifa ya habari", msichana mmoja aliwanyamazisha wenzake, Akina Bon na Mike walikuwa wamekaa kwenye bustani ya New Arusha Hoteli. Kipaza sauti kilikuwa kimetundikwa kwenye mti katikati ya bustani.

"Hivi kuna habari gani kwenye taarifa ya habari mpaka watu wote wanasogea kusikiliza. Utafikiri kumezuka vita", Mike aliuliza kwa mshangao.

"Wewe unakaa Yerusalemu ya wapi?. Hata usijue matukio yaliyotokea jana usiku hapa mjini?", msichana mwingine alimuuliza Mike kwa kebehi.

"Mimi sujui", Mike alijibu.

"Sasa tulia usikilize", alisema.

"Haya mtoto", Mike alijibu na taarifa ya habari ikaanza.

"Sasa ni saa moja kamili".

"Ifuatayo ni taarifa ya habari kutoka Radio Tanzania. Dar es Salaam... Arusha. Habari za kuaminika kutoka Arusha zinasema kuwa vijana shupavu wa Afrika wamevunja ngome ya makaburu. Ngome hiyo iliyokuwa chini ya majahili wa jeshi la "KULFUT" ama Gongo la chuma iliyoundwa na makaburu kwa lengo la kuongeza hofu kwa nchi huru za Afrika. Kikiongozwa na tajiri wa mjini humo aitwae Ferozali Kassam ama F.K. Kimeteketezwa kabisa. Vyombo na vifaa vingi vya kisasa kwa ajili ya uimarisha ujasusi vimekamatwa. Nia ya kikundi hicho kuweka ngome mjini Arusha ilikuwa kuhujumu mkutano wa wapigania uhuru ambao hata hivyo umeanza leo mjini humo. Habari za kuteketeza ngome hiyo zimepokelewa kwa shangwe kuu na wakuu wa nchi huru za Arika.

"Hata hivyo kiongozi mmoja wa wapigania amezionya nchi huru za Afrika. Amesema ni lazima kuwa macho kwani aduni sasa ameanza kutangatanga. Kwa sababu maji yamewafika shingoni. Vile vile ameiomba jumuia ya Kimataifa kuzidi kuwabana makaburu kiuchumi ili kuleta mabadiliko ya haraka nchini Afrika Kusini. Kwa lengo la kuutokomeza ubaguzi wa rangi na kuleta utawala wa walio wengi. Amewaonya makaburu kuwa mapambano ya silaha yatazidi ndani ya Afrika Kusini. Hakuna kurudi nyuma.

"Habari zingine kutoka Pretoria. Afrika Kusini zinasema: Baada ya makaburu kupata habari ya kuteketezwa kwa ngome ya 'KULFUT', mapambano mapya na makali yamezuka. Mpaka tunakwenda hewani mapambano makali yalikuwa yanaendelea. Wazalendo katika kitongoji cha Soweto wanapambana vikali na polisi wa makaburu....".

"Mmesikia sasa", yule msichana wa pili aliwauliza.

"Tumesikia mtoto. Lililobaki sasa ni sisi kucheza na kula vyetu huku tukishangilia ushindi. Tutumie vyetu mpaka liamba", Mike alijibu.

"Mwenyezi Mungu akupe nini", yule msichana wa kwanza alisema.

"Napendekeza tuondoke hapa, twende kutumia sehemu nyingine. Maana leo ni leo, asemaye kesho ni muongo", Bon alisema huku akiinuka. Alimshika mkono msichana aliyekuwa karibu naye. Aliondoka taratibu. Mike naye alifuatia huku macho ya watu yakiwafuatlia pia.

II

"Hebu nikuulize Nyaso. Kwanini uliamua kumuua F.K", Willy alimwuliza Nyaso. Wakati huo alikuwa anajigeuza kifuani. Baadaye alimkumbatia.

"Nisingependa wewe kunikumbusha jambio hilo. Huo ni mzigo wangu. Ni heri niubebe mimi mwenyewe", Nyaso alijibu taratibu.

"Oke, mtoto", Willy aliitika taratibu halafu alimbusu.

"Willy".

"Ehe".

"Kazi yako tumeimaliza. Lakini sasa ni mwanzo wa kazi nyingine mpya. Kazi hiyo ni yangu. Unakumbuka wewe mwenyewe uliniahidi", Nyaso alisema kwa sauti nyororo.

Willy alimwangalia Nyaso. Alimgeuza humo ndani ya shuka walilokuwa wamejifunika. Alimbusu tena. Alimwangalia machini kwa mahababa. Mara akamwambia.

"Nikumbushe kesho. Kwa sasa hivi ni kazi tofauuti. KILA KAZI NA WAKATI WAKE".

MWISHO WA HOFU


WAPENDWA WASOMAJI WA HADITHI ZA KUSISIMUA ZA UPELELEZI, TUMEFIKIA TAMATI AMA MWISHO WA KITABU CHA HOFU, KILICHOANDIKWA NA HAYATI A.E MUSIBA. MWISHO WA KITABU HIKI NI MWANZO WA VITABU VINGINE VYA KUSISIMUA KAMA UCHU, KIKOMO, KUFA NA KUPONA NA KIKOSI CHA KISASI.





Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU