UCHU



TAFUTA UKWELI 

II

Baada ya Musoke na Willy Gamba kuondoka nyumbani kwa Temu, kila mtu alitawanyika kuelekea kwenye hoteli yake.

Malisa aliyekuja kwenye mkutano huo akitokea Dar es Salaam, alikuwa amefikia Hoteli ya Sabasaba. Alijulikana sana katika kundi la wasomi na kiserikali alikuwa mmoja wa watu waliokuwa mstari wa mbele katika kupigania kuwepo Umoja wa Afrika. Hata maafisa wa ngazi za juu serikalini mara nyingi walitafuta ushauri kwake kila walipotaka kuzungumzia swala la Umoja wa Afrika.

Malisa alikuwa msomi na Mhadhili wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika kitivo cha Sayansi ya Jamii. Mara hii alipokuwa anakuja kwenye mkutano huu Arusha, Afisa mmoja wa ngazi za juu kabisa serikalini alimwomba amweleze mazungumzo na makubaliano ya mkutano wao, kwani serikali ilipenda kujuwa mambo gani PAM inafikiria kuhusu tatizo la Rwanda ili serikali nayo iweze kusaidia. Huyu Afisa wa serikali alimpa namba zake za simu za nyumbani na kumwomba ampigie baada tu ya mkutano.

Malisa alipofika Hotelini tu, ikawa yapata saa kumi na mbili na robo, alichukua ufunguo wa chumba chake mapokezi na kueleka chumbani. Alipofika chumbani alimwomba opereta wa simu pale hotelini ampatie simu ya Dar es Salaam na kumpa namba.

"Subiri kidogo nitakuita", opereta alimwambia.

"Haya asante, lakini nifanyie haraka maana nataka kutoka nina miadi", Malisa alimwomba opereta.

"Sasa hivi", aliambiwa.

Baada ya muda si mrefu simu iliita chumbani kwa Malisa.

"Hallo".

"Namba yako ya Dar es Salaam inaita", opereta alijibu.

"Haya asante", na akaunganishwa na namba hiyo ya Dar es Salaam ambayo iliendelea kuita.

"Hallo", mtu aliitikia baada ya muda kidogo.

"Hapa ni Arusha, mzee yupo?", Malisa aliuliza.

"Yupo, subiri".

Na baada ya muda kidogo akasikia, "Hallo, nani mwenzangu?".

"Malisa hapa, shikamoo".

"Marahaba, habari ya huko?".

"Salama".

"Vipi mkutano".

"Tumemaliza".

"Ehee, hebu nipe maazimio yenu kwani wazee huku wana shauku ya kusikia".

"Haya tega sikio nikueleze, mambo ni mazuri sana", Malisa alijibu na kumweleza mambo yote tokea mwanzo mpaka mwisho.

"Hizo ni habari njema", yule afisa alijibu na kuendelea. "Willy Gamba ni kijana wetu na ni mtu shupavu. Kwa hakika ataifanikisha hiyo kazi. Na mimi nitawaeleza wazee naamini wataridhika na hatua mliyochukuwa. Mnajua sisi kama serikali ni vigumu kuchukua hatua yoyote dhidi ya nchi nyingine, lakini nyinyi mkiwa umoja usio wa kiserikali mnaweza kutusaidia sana kwa mambo kama haya. Willy amefikia wapi?".

"Yuko hoteli ya Impala chumba namba 212. Huenda mzee si vizuri kumpigia simu sasa hivi tu atashituka", Malisa alijibu.

"Na kweli, ingawa ni kijana wetu basi tuache nyinyi muendelee nae. Asante sana kwa kazi nzuri, na mwanzo mzuri, watu wenye uchungu na Afrika kama nyinyi ndio mtakaoisogeza Afrika mbele katika kuleta maendeleo wakati tukielekea katika karne ya sayansi na teknolojia. Asante sana", yule afisa wa serikali alijibu na kukata simu.

Bila kujua alichokuwa amefanya, Malisa alifurahi sana kusikia sifa alizozitoa mtu huyu mashuhuri katika serikali ya Tanzania, kwa umoja wao. Minongono mingi jijini Dar es Salaam ilikuwa ni kwamba afisa huyu, ambaye watu wengi walipenda kumwita kwa kifupi tu kama 'JKS' alitegemewa kugombea Urais baada ya muda wa Rais wa sasa kumalizika.

Baada ya kukata simu ya Malisa tu, JKS alipiga simu nyingine. Mara hii ilikuwa simu ya masafa marefu, alipga Paris, Ufaransa. Na mara moja ikaitikiwa.

"Hallo, naomba kuzungumza na Jean Yves Francois".

"Subiri kidogo", alijibiwa.

"Hallo Francois, nani anaita?".

"Yaani huwezi kutambua sauti".

"Ah JKS. Ehe, nipe habari".

"Habari nzuri, sijui wewe huko?".

"Huku salama, tunasubiri tu kwa hamu kusikia Umoja wa Mataifa mahakama ya mauaji ya Rwanda ianze lini".

"Nasikia itaanza miezi minne ijayo huko Arusha".

"Aha, majina?", Jean aliuliza.

"Majina ni yaleyale mpaka sasa".

"Kwa hiyo upande wa watu wetu hakuna aliyeguswa?".

"Bado kabisa, ila kumetokea hali ambayo inaweza kutuletea madhara".

"Hali gani?", Jean alihoji kwa shauku.

"Unakumbuka niliwahi kukueleza juu ya chama kiitwacho kwa kifupi PAM?", alimwuliza.

"Nakikumbuka na nimekitafiti vilevile kujua msimamo wake. Wanachama wake wanapigania umoja wa waafrika ili kuleta haraka uhuru wa watu weusi dhidi ya ukoloni mambo leo, ili watu weusi waweze kujiamulia mambo yao wenyewe. Na vilevile walikuwa mojawapo ya makundi yaliyotoa shinikizo katika mkutano wa Arusha ili mgogoro wa Rwanda umalizike kwa njia ya amani. Hata mkutano wa Algers, walikuwepo wawakilishi wao, niliwaona maana nilikuwepo. Haya sema watu kama hawa wanaweza kuleta madhara gani?", Jean aliuliza.

"Wanaweza kuleta madhara makubwa sana", JKS alimjibu na kisha akaanza kueleza kwa kirefu jinsi Malisa alivyomweleza, na hatua ambazo tayari zilikuwa zimechukuliwa.

"Huyu Willy Gamba ni hatari, anaweza kuchambua kila kitu mpaka akafikia ukweli unaweza kukugusa hata wewe", JKS aliasa.

"Lililopo ni kuzuia asiende", Jean alijibu.

"Tutamzuia vipi na hayuko chini yetu?", JKS aliuliza.

"Mbona huelewi, kwani maiti inasafiri?".

"Aha, sasa nimekuelewa, lakini hiyo ni kazi kubwa", JKS alijibu.

"Hiyo ni kazi ndogo kabisa, si umeeleza kuwa mtu wako ameeleza kuwa leo huyo Willy Gamba analala Arusha. Hotel ya Impala na chumba amekupa namba zake, au sikukuelewa vizuri?", Jean aliuliza.

"Ni sawa kabisa, alinipa kila habari bila kuelewa maana yake, na mimi aliponieleza sikuelewa habari hiyo itakuwa muhimu", JKS alijibu.

"Hiyo ilikuwa muhimu sana. Unakumbuka kuwa tuna watu wetu kule Arusha, ambao walikuwa wasafiri na Rais aliyeuawa, lakini kwa ajili ya ujumbe wa Rais wa Burundi hawakwenda na wapo kule Arusha kama wageni wa serikali yako?", Jean aliuliza katika hali ya kukumbusha.

"Hao! hata juzi nilizungumza na kiongozi wao maana alikuwa ametokea Ngala kwenda makambi ya wakimbizi wa Rwanda kwa ajili ya kuwachukuwa vijana kumi muhimu ambao waliingia Tanzania baada ya kufunga kazi kule Rwanda. Alikuwa anataka msaada wangu kwa ajili ya makazi, nami nimewafanyia mpango katika nyumba za mashirika ya serikali pale Arusha na sasa wako salama salimini", JKS alijibu.

"Hiyo ni kazi nzuri sana. Kwa kazi hiyo na kwa habari ulizonipa leo, nitapeleka dola za kimarekani elfu ishirini kwenye akaunti yako kule Uswisi, kufika kesho jioni pesa zitakuwa zimeingia. Na kama kazi hii ya usiku ikifanikiwa dola zingine elfu ishirini zitapelekwa", Jean alimweleza JKS.

"Asante sana, nami nitafanya kazi kwa upande wangu. Nitampigia simu kiongozi wao hapo Arusha, Bwana Phillipe Habimana, atume vijana wawili waimalize hiyo kazi. Umeshatoa agizo, na agizo lako litatimizwa", JKS alijigamba.

"Oke, vizuri; unajuwa vijana wetu wana ujuzi wa hali ya juu, na swala la kuua kwako si swala tena la maana wameishaua sana kiasi kwamba kuua kwao sasa ni sawa na kunywa chai", Jean alijibu huku akiangua kicheko cha kejeli.

"Tena sana, juzi tu kwenye kambi huko Ngala wamemaliza kuua vikaragosi vinavyojipendekeza kwenye serikali mpya, kwa kuwashawishi wakimbizi waanze kurudi ili ionekane serikali ya sasa imeshaleta amani na usalama Rwanda ili iweze kuungwa mkono na jumuia za kimataifa. Ni baada tu ya kumaliza hiyo kazi ndipo Phillipe alipokwenda kuwachukuwa kwa msaada wangu. Hivyo, nikiwaagiza leo, hakika huyu Willy ajihesabu ni marehemu maana bado wana mori kabisa", JKS alijibu.

"Haya basi, nipigie simu kesho, baada ya kumaliza hiyo kazi. Na kama ukisikia habari zingine zozote, fanya kama kawaida na mimi nitafanya kama kawaida yangu", Jean alijibu na kukata simu.

Jean na JKS walikuwa wanafahamiana yapata miaka mitano sasa. Uhusiano wao ulianza wakati JKS alipokuwa na wadhifa wa kuamua juu ya ununuzi wa silaha mbalimbali zilizokuwa zinahitajiwa na serikali ya Tanzania. Jean Yvers Francois alikuwa kijana bado yapata miaka therathini na minane, na alikuwa tayari mfanyabiashara maarufu sana duniani. Alikuwa akifanya biashara ya kuuza silaha katika nchi zinazoendelea, na alimudu sana kupata biashara hiyo kwa urahisi kwa vile watu wengi walisema kuwa alikuwa mtoto wa kiongozi wa ngazi za juu kabisa katika serikali ya Ufaransa.

Kwa kutumia wadhifa wa baba yake na umaarufu aliokuwa nao baba yake katika nchi zinazoendelea, kijana huyu hakukosa biashara hii ya silaha na biashara nyinginezo zilizokuwa zikipita mbele yake. Lakini vilevile alinong'onwa kuwa, kijana huyu alijua kuwazawadia waliompa biashara, hasa viongozi wa ngazi za juu katika nchi za Kiafrika. Kutokana na sifa hii ya kutoa asilimia kumi na zawadi zingine, kijana huyu alikuwa akitafutwa na biashara badala ya yeye kuzitafuta hata ikasemekana kwamba viongozi fulanifulani wa nchi za Kiafrika iliwabidi wazungumze naye kwanza kabla hawajatoa maamuzi yoyote muhimu ya kibiashara.

Kwa hiyo, wakati JKS alipoagizwa na serikali ya Tanzania kutoa zabuni ya kisiri kwa makampuni yanayotengeneza silaha, mara moja alimtafuta Jean, maana viongozi wenzake walishawahi kumweleza kama angetaka kunufaika na wenzake pia wanufaike basi Jean ndiye  alikuwa mtu wa kuwasiliana naye. Ingawa wakati huo walikuwa hawafahamiani, lakini JKS alikuwa tayari ana anuani ya Jean kutoka kwa rafiki zake. Hivyo hakusita, akawasiliana naye. Ni baada ya kuwasiliana naye na kufanya biashara ya kwanza ndipo urafiki wa karibu sana ulipoanza kati yao.

Kwa vile Ufaransa ilikuwa na uhusiano wa karibu sana wa kiserikali na serikali ya Rwanda, Jean alijikuta ana uhusiano wa karibu sana na uongozi wa serikali ya nchi hiyo kuliko ilivyokuwa serikali za nchi nyingine za Kiafrika alizokuwa akifanya nazo biashara. Inasemekana kuwa, kwa njia moja ama nyingine, Jean ndiye aliyekuwa mshauri mkuu wa uongozi huo na hakuna uamuzi wowote uliofanyika bila yeye kuhusishwa. Kiuchumi, Jean alimiliki njia zote muhimu za uchumi wa Rwanda kwani uongozi wa serikali ya Rwanda ulimpa uwezo wa kufanya biashara yoyote aliyoitaka nchini humo, na uongozi huo ulinufaika kwa kujilimbikizia mali, na kumwachia anyonye jasho la wananchi wa Rwanda kwa kununua mazao yao yote kwa bei rahisi na kuwauzia bidhaa kwa bei ghali.

Kwa jinsi hii Rwanda ilimtajirisha Jean na viongozi wa serikali isivyo kifani. Na ndio sababu wakati wa mkutano wa kusuruhisha pande zote za mgogoro wa Rwanda mjini Arusha, Jean alikuwepo. Inasemekana alimtumia sana JKS kujaribu kuipotosha serikali ya Tanzania ili isione ukweli wa mambo ulivyokuwa Rwanda kutokana na urafiki wao wa karibu uliotokana na kupeana bakshishi.

Baada ya Jean kukata simu, JKS alitafuta kitabu chake cha simu na kutafuta simu ya Phillipe Habimana kule Arusha. Baada ya kuipata alimpigia simu.

"Hallo Habimana".

"Habari za leo", JKS alijibu na mara moja Phillipe akaitambua sauti.

"Nzuri mzee, shikamoo".

"Marahaba, sikiliza kwa makini, nina kazi nataka vijana wako wakaifanye usiku huu, tafadhali sitaki makosa ya namna yoyote yafanyike kwani yanaweza kuleta madhara kwa suala lenu zima. Nimeshazungumza na Jean.

JKS alitoa maagizo yake kwa kirefu na akamalizia.

"Narudia tena, mtu huyu ni hatari sana; vijana wako wasifanye mzaha wakafikiria ni mtu wa kawaida, si wa kawaida, hadhari yote ichukuliwe".

"Hamna matatizo mzee, hesabu kazi imekwisha, tuonane kwenye msiba wa Willy Gamba", Phillipe alijigamba.

ITAENDELEA… 0784296253   

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU