KAZI IMEANZA
III
Ilikuwa saa
tatu na dakika kama tano hivi, Mulamba alipompigia simu JKS. JKS alikuwa tayari
amefika ofisini.
Simu ya moja
kwa moja kwa JKS ililia na haraka akainua. "Nani", aliuliza kwa
shauku.
"Mulamba,
mzee".
"Haya
vipi mmempata?".
"Mzee
huyu mtu tumeweza kupata nyendo zake zote, ila hatukuweza kumpata yeye kabisa
maana alikuwa hatua moja mbele kila tulipokuwa karibu kumpata".
"Una
maana gani, hebu sema mambo ya kueleweka", JKS aliuliza kwa ukali.
"Ndio
nilitaka nikupe ripoti kamili mzee. Kutokana na taarifa za uchunguzi wetu,
aliondoka Arusha jana kwa ndege ya kukodi ya Tanzanair, hivyo hakulala Arusha
ila alilala hapa Dar es Salaam. Leo asubuhi ameondoka Dar es Salaam kwa ndege
hiyo hiyo ya kukodi ya Tanzaniair na anaelekea Kigali. Habari za watu wangu
nilizozipata hivi punde ni kwamba ameondoka Mwanza mnamo saa tatu kamili
kuelekea Kigali. Hali ndivyo ilivyo mzee. Sijui tukusaidie nini tena?",
Mulamba aliuliza.
"Ndege
hiyo ya Tanzaniar ni namba ngapi?", JKS aliuliza.
"Namba
zake ni MHZT 12".
"Sawa
basi asante, nikikuhitaji nitakutafuta".
"Haya,
asante mzee", Mulamba alijibu huku akipumua kwani alikuwa amejawa na
wasiwasi angetakiwa kufanya nini tena kwani hakutaka kazi yoyote ya kuhusiana
na Willy Gamba, maana mtu huyu alikuwa ni moto wa kuotea mbali. Alibaki
anashangaa tu hasa ni nini kilikuwa kinatokea kati ya serikali na Willy Gamba.
JKS
alijishika kichwa na kujua kazi imekuwa ngumu na yeye peke yake asingeiweza.
Huyu Willy Gamba alikuwa kweli kabisa mtu wa hatari na hakika kuwapo kwake
Rwanda kungezua balaa, lazima kila njia ifanyike kabla hajaleta madhara.
Hakukuwa na njia nyingine ila kurudi kwa Jean maana yeye alikuwa na uwezo
mkubwa kufanya mambo Rwanda kuliko yeye. Uwezo wa JKS uliishia ndani ya mipaka
ya Tanzania, isipokuwa tu propagada ya kisiasa ndio angeweza kusaidia kokote ulimwenguni
kwani alikubalika sana duniani kote kisiasa. Ingawaje Jean alikuwa amemwamru
ampigie simu ikiwa Willy ameshauawa, lakini JKS alionelea afadhali atukanwe
kuliko kunyamaza. Aliinua simu akampigia Jean kwenye simu yake ya kutembea nayo
(Mobile).
"Hallo",
Jean alijibu baada ya kupokea.
"JKS
hapa".
"Ehe,
mambo mazuri?", Jean aliuliza kwa shauku.
"Hapana,
mambo yanazidi kuwa magumu", JKS alijibu na akamweleza jinsi sasa Willy
Gamba alivyokuwa anaelekea Kigali.
"Mbona
mtu huyu nitampenda", Jean alijibu kwa kejeli.
JKS
alinyamaza. Hakuwa na la kusema.
"Hapa
kweli tunashughulika na mtu mjuzi, huyo anatakiwa apambane na watu wenye ujuzi
kama yeye. Basi niachie huyo mtu kwa sasa. Nitarudi kwako baadae, nipe hiyo
namba ya ndege na maelezo mengine yote kuhusu hiyo ndege na huyo mtu
wako", Jean alimalizia.
JKS alimpa
maelezo yote huku akifurahi kuwa Jean ameelewa na hakuweza kumkasirikia. Baada
ya kumpa maelezo JKS alikata simu na kuinuka kitini na kwenda kusimama
dirishani mwa ofisi yake na kuwaangalia ndege aina ya tausi waliokuwa wakicheza
nje tu ya dirisha lake.
Mara mawazo
yake yakarudi kwa Willy Gamba. Kuuawa kwa Willy ndio kupata kwake Urais, maana
huyu mtu asipouawa anaweza kuchokonoa ukweli wa mambo na kuleta kashifa ambayo
ingeweza kumgusa hata yeye kwani JKS alikuwa mmoja wa watu waliokuwa wanahusika
na swala zima la Rwanda, tokea maswala ya kisiasa mpaka kufikia mauaji. Na
serikali ya Tanzania ilikuwa imeweka mambo yote yahusuyo Rwanda chini yake na
ofisi yake kwa vile aliaminika kuwa ni kiongozi mwadilifu.
Baada ya
kukata simu ya JKS, Jean alipiga simu Rwanda kwa rafiki yake alikuwa ndani ya
Jeshi la RPF. Baada ya RPF kushika madaraka Rwanda, Col. Gatabazi alikuwa wa
kwanza kupata simu iliyofanya kazi. Hii yote ilikuwa kwa hisani ya Jean ambaye
alikuwa na uhusiano wa karibu na mkuu wa jeshi la Ufaransa lililokuwa Rwanda
pamoja na mkuu wa Idara ya Usalama wa Nje wa Ufaransa (DGSE). Inasemekana kuwa
Jean ndiye aliyewasaidia hata kupata vyeo hivi kutokana na kuwa kwake karibu na
uongozi wa juu wa serikali ya Ufaransa.
Jean alikuwa
kama ndiye mshauri mkuu wa serikali ya Ufaransa kuhusu maswala ya Rwanda.
Kutokana na kuwa kwake karibu na Rais pamoja na watu wote muhimu ndani na nje
ya serikali ya Rwanda. Kwa hiyo baada ya Kigali kuangukia mikononi mwa RPF tu
na maofisa wa jeshi hilo kujinyakulia nyumba za kukaa zilizokimbiwa na maofisa
wa serikali ya MNRD. Col. Gatabazi ambaye siku zote alijulikana kama mkereketwa
mkubwa wa RPF, hakuwa mkereketwa ila msaliti na ndiye aliyekuwa akitoa siri
zote za RPF kwa Jean, na Jean akazitoa kwa rafiki zake wa serikali ya MNRD. Kwa
hiyo, baada ya kupata nyumba tu Jean alihakikisha kuwa Col. Gatabazi anapata
simu ili kila kilichokuwa kinaendelea ndani ya RPF kimfikie.
Kutokana na
huo uhaini wake Col. Gatabazi alijipenyeza na kujiweka karibu kabisa na
kiongozi wa RPF na akaaminika sana. Inasemekana alikuwa Mhutu, lakini mama yake
alikuwa Mtutsi. Baba yake alifariki akiwa na umri wa miaka miwili na akakulia
kwa mjomba wake na kwa vile alikuwa amechukuwa umbo la mama yake alitambuliwa
kama Mtutsi tu. Ila yeye alijuwa ni Mhutu na inasemekana aliwahi kuambiwa kuwa
baba yake aliuawa na wajomba zake kwa vile hawakutaka dada yao aolewe na Mhutu.
Hivi kinyongo alikuwa nacho moyoni na ndio sababu alipopata nafasi ya kuwasaliti
Watutsi alifanya hivyo kwa moyo mmoja.
Baada ya
serikali ya MNRD kuanguka na RPF kuingia, Jean alimhakikishia Col. Gatabazi
kuwa serikali hiyo isingeweza kukaa madarakani kwa muda mrefu kwani
ingepinduliwa na yeye angeiongoza serikali inayofuata. Jean alimhakikishia kuwa
serikali ya Ufaransa isingeiruhusu serikali ya RPF ikae madarakani kwani
viongozi wake walikuwa na mwelekeo wa Kiingereza kwa kukaa kwao Uganda na hivyo
wangeathiri nguvu (influence) ya Ufaransa ndani ya Rwanda kitu ambacho Ufaransa
isingekiruhusu kabisa. Kwa hiyo kwa kushirikiana na viongozi wa serikali ya
MNRD waliokimbia na watu wengine walio ndani kama Col. Gatabazi kwa msaada wa
serikali ya Ufaransa. Jean alikuwa anatayarisha jeshi la kuivamia tena Rwanda
na kuchukua madaraka toka kwa RPF. Kwa hiyo, Col. Gatabazi alikuwa
anajitayarisha kuwaggeuka wenzake mara wakati wa kufanya hivyo utakapofika.
Col.
Gatabazi alikuwa anataka kutoka nyumbani kwenda ofisini kwake, Merridian Hotel,
ambako ndiko ofisi zake zilikuwa kwani ndiye aliyekuwa anashughulikia uratibu
wa shughuli zote za vikosi mbalimbali vya jeshi la RPF na kuripoti kwa mkuu wa
majeshi.
Simu ililia.
Hallo Col. Gatabazi?".
"Jean".
"Mbona
leo unanipigia simu saa hizi? Saa zetu unazijuwa", Col. Gatabazi aliuliza.
"Kuna
dharura", Jean alijibu na kumweleza juu ya Willy Gamba na athari za kuwa
kwake Kigali.
"Hivyo
ni vizuri hiyo ndege yake ingetunguliwa ikiwa hewani iwe mwisho wa tatizo la
huyu mtu maana toka jana anatusumbua, nafikiri hiyo ndio njia rahisi",
Jean alimalizia.
"Si
Tanzania italalamika sana na kwa sasa hivi serikali ya RPF inataka sana
kueleweka vizuri, hasa kwa serikali kama ya Tanzania", Col. Gatabazi
alijibu kwa njia ya kuuliza swali.
"Usijali,
Tanzania inaunga mkono kwa kusema hiyo ndege iliruka anga zetu bila ruhusa hata
haikutoa habari huko Tanzania kama ilikuwa inakuja Kigali. Hilo niachie mimi na wewe
utasikia itakavyokuwa maana utacheka", Jean alijibu.
"Basi
ngoja niwahi kwani watatua kwenye dakika thelathini zijazo kutokana na maelezo
yako ya saa walizoondoka mjini Mwanza".
"Asante,
kwa heri, ila nipigie simu baada ya tukio".
"Sawa",
Col. Gatabazi alijibu.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment