UCHU



KAZI IMEANZA

IV

Ndege ya Chama Cha Msalaba Mwekundu ilitua kwenye uwanja wa ndege wa Kayibanda mjini Kigali yapata saa nne kamili. Willy Gamba alichukua mkoba wake na kutelemka.

"Asante", Willy alimshukuru rubani na kumpa dola mia za kimarekani.

"Asante sana mzee", yule rubani alishukuru na kufunga mlango tayari kwa kuruka tena.

Willy alikwenda moja kwa moja kwenye jengo la uwanja wa ndege na kuelekea Uhamiaji. Ulinzi uwanjani ulikuwa bado mkali lakini kwa sababu alikuja kwa ndege ya Chama Cha Msalaba Mwekundu na alikuwa amefanyiwa mpango na rafiki yake Dar es Salaam aje apokelewe na mmoja wa maafisa wa Msalaba Mwekundu walioko Kigali, yeye akiwa kama Afisa wa habari wa Msalaba Mwekundu kimataifa na ndivyo Chifu alivyomtayarishia pasipoti aliyoikuta nyumbani, taratibu zake pale uwanja wa ndege zilikwenda haraka bila kipingamizi chochote.

Katika pasipoti yake hii jina lake lilikuwa George Mambo.

Alipojitokeza tu nje, alimkuta mwenyeji wake aliyekuwa amevaa beji ya Msalaba Mwekundu na kwa vile na yeye toka alipotua tu aliweka beji aliyokuwa amepewa na Msalaba Mwekundu wakatambuana mara moja.

"Bwana George Mambo natumai", yule mwenyeji wake alisema huku akitoa mkono wa salamu.

"Ndio mimi. Habari zako", Willy alijibu na kusalimu.

"Nzuri, mimi naitwa Vicent Nyemazi, ni afisa wa habari hapa, na mimi ni Mhutu ila mimi siyo Mhutu mwenye siasa kali", Vicent alijibu huku akitabasamu.

"Vizuri sana na pole kwa yote yaliyotokea hapa nchini kwenu".

"Asante sana, ndio hali ya dunia. Gari nimeegesha hapo mbele", Vicent alieleza.

"Mkahawa wa hapa umefunguliwa?", Willy aliuliza.

"Ndio, uko wazi".

"Unajuwa nimeondoka asubuhi sana, sijanywa hata chai na ndege zetu kama unavyojuwa si kama ndege za abiria, hamna chochote hata kikombe cha chai", Willy alijibu huku akiangalia saa yake.

"Sawa, twende hapa kuna mkahawa mzuri, na hali imeanza kurudi kama zamani, hivyo vitu vingi vinaendelea kama kawaida.

Walipanda juu kwenye mkahawa na willy aliagiza kahawa na kipande cha mkate na Vicent akaagiza kahawa peke yake. Willy aliangalia saa yake kwa chati kabisa, akajuwa ile ndege ya Tanzanair ilikuwa karibu kutua, na alitaka tu kuona kama kungeweza kuwa na fununu za kuja kwake. Hii ilikuwa hadhari tu kwani aliamini hakuna mtu ambaye angeweza kujua kuwa anakuja kwa jinsi alivyokuwa ameondoka Dar es Salaam kisirisiri.

"Ah, vipi hali ya huko Ngara, nasikia hali ya wakimbizi ni mbaya sana, yaani chakula, maji na madawa ni taabu", Vicent aliuliza.

"Ni kweli hali ni mbaya, jumuiya ya kimataifa inajaribu kusaidia lakini wakimbizi ni wengi mno. Fikiria watu kama wa mji huu mnamo wiki moja watengeneze mji mwingine ambao haukuwepo kabisa, ambako ni porini tu hakuna huduma za kijamii za aina...". Kabla Willy hajamaliza kueleza mlio mkubwa ulitokea na mara ukatokea mlipuko. Willy na Vicent walikimbilia dirishani kuangalia kwenye uwanja wa ndege ambako ndiko mlipuko ulikotokea. Kwenye barabara zinakoondokea na kutua ndege wakaona vipande vya ndege vimesambaa na kuwaka moto.

"Kazi imeanza", Willy alisema na kumvuta Vicent mkono. Wakakimbilia chini kuangalia kwani vishindo vya kukimbia uwanjani vilisikika kutoka kila pahala.

Walipofika chini na kuelekea uwanjani walikuta magari ya jeshi aina ya Landrover yakiwa yamejaa askari yakielekea pale mabaki ya ndege yalipoangukia na wengine wakija huku kwenye jengo la uwanja ili kuzuia watu wasiende kule uwanjani.

Vicent na Willy walionyesha beji zao za Msalaba Mwekundu wakiomba wafike kwenye tukio lakini walikataliwa na askari ambao kwa sasa walikuwa wamechachamaa. Willy aligundua kuwa kumbe walishajua atafika na maskini yule rubani na afisa wa Msalaba Mwekundu waliuawa kwa kufikiri ni yeye. Willy alimshukuru Mungu kwa kumfanya afikiri na kufanya kama alivyofanya. 

Kweli kama Msoke alivyosema, kazi hii tayari ilionyesha kuwa ni ya hatari. Ila kilichomshangaza Willy ni jinsi yule mtu aliyeshambulia ndege ya Tanzanair alivyojuwa kuwa yeye angekuwemo mle ndani ya ile ndege. Hii ilionyesha kuwa kati ya wale maafisa wa PAM miongoni mwao kulikuwa na msaliti, lakini kwa sasa hakukuwa na haja ya kufikiria hicho ila kufanya kilichomleta Kigali. Huyu msaliti angetafutwa baadaye. Jinsi ile ndege ilivyokuwa imepigwa na kombora. Willy alijua kabisa kuwa hakuna mabaki ya binadamu ambayo yangeweza kutambuliwa, kwani kombora lililotumika lilikuwa kubwa wakati ndege yenyewe ilikuwa ndogo.

"Twende zetu, nipeleke hotelini, acha wanajeshi wafanye kazi yao", Willy alimvuta Vicent wakaondoka huku wakisesera kuelekea kwenye gari la Vicent.

"Kwanini wameipiga ile ndege?", Vicent aliuliza huku akifungua mlango wa gari.

"Huenda ilikuwa na hatari, bado unajuwa mambo hayajatengamaa hapa", Willy alijibu.

"Unafikia hoteli gani?".

"Nafikiri jaribu Meridian Hotel kama kuna nafasi", Willy alijibu na kuikacha Hotel Des Mille Collines aliyokuwa amepangiwa na rafiki za Musoke, kwani sasa hakukuwa tena na kumwamini mtu yeyote kwa vile hakujuwa nani alikuwa ametoa amri ya kupigwa kombora ndege aliyopaswa kuwemo na huyo mtu alikuwa anajuwa habari kiasi gani kumhusu yeye Willy.

"Sawa, pale hotelini wanatua na watu wetu kutoka mataifa ya nje wako pale. Na vilevile pana usalama maana ofisi zingine za jeshi ziko pale, na maafisa wengine wa jeshi wanakaa pale", Vicent alimweleza Willy. Wakati wakielekea Meridian Hotel walikutana na magari madogo ya jeshi, kama matatu, yakielekea uwanja wa ndege. Willy aliona wengi walikuwa maofisa wa vyeo vya juu na akahisi walikuwa wanakwenda kutathimini tukio lililotokea.

Walipofika Meridian walikuwa watu wako vikundi vikundi wakizungumza, bila saka walikuwa wamepata habari za tukio la uwanja wa ndege. Vicent likwenda mapokezi na kuzungumza na mmoja wa wafanyakazi wa pale ambaye alionekana kumfahamu sana, na baada ya muda kidogo Willy aliitwa kujaza fomu za kupatiwa chumba. Baada ya kupewa funguo alichukua mkoba wake na vicent akamweleza kuwa atamsubiri kwenye mkahawa wa hoteli.

"Si utataka twende ofisini?", Vicent aliuliza.

"Bila shaka", Willy alijibu.

"Basi utanikuta hapo kwenye mkahawa".

"Asante", Willy alijibu na kuelekea kwenye ngazi kwani alikuwa ameelezwa lifti zilikuwa hazifanyi kazi. Alikuwa amepewa chumba namba 412, ghorofa ya nne.

V
Baada ya Col. Gatabazi kuhakikisha kuwa hakuna kitu kilichobaki ndani ya ndege na ndege yenyewe, alielekea nyumbani kwake ili akampashe habari Jean. Alipompata Jean alimweleza. "Kazi tayari, mtu wako hata mfupa haukuonekana, kawa hewa".

"Safi sana, hakika mimi hupenda mtu wa vitendo na siyo maneno", Jean alijibu.

"Lililobaki ni la kujieleza kwanini tumeipiga hiyo ndege, lakini tayari mkuu nimemwandikia taarifa safi ambayo hawezi kuwa na mashaka nayo. Wasiwasi wangu Tanzania tu", Col. Gatabazi alieleza.

"Nilikwambia Tanzania niachie mimi. Tuongee jioni. Kama kawaida mzigo mwingine unatua leo, na ni shehena kubwa", Jean alijibu na kabla Col. Gatabazi hajajibu alikata simu.

Baada ya kukata simu ya Col. Gatabazi. Jean alimpigia simu JKS, Dar es Salaam. JKS, aliyekuwa na wasiwasi mkubwa aliipokea simu haraka ilipolia. "Nani".

"Jean hapa. Kigali Bingo!!, mambo safi".


ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU