UCHU



WAPENDWA WASOMAJI WA BLOG YA MPIGANAJI, TUNAWAOMBA RADHI KWA KUKOSA HADITHI HII, KULITOKANA NA SEHEMU HII KUWA NDEFU NA HIVYO KUHITAJI MAANDALIZI YA MUDA MREFU. SASA ENDELENA KUPATA UHONDO JINSI WILLY ALIVYOINGIA KIGALI.

CENTRE CHRISTUS

Ilikuwa yapata saa moja ya usiku wakati Willy alipofika kwenye kituo cha kidini cha Centre Christus. Alikuwa bado anasikia maumivu ya ubavuni yaliyotokana na mapambano ya juzi yake. Hata hivyo, aliamua kuendelea na kazi kwa vile muda ulikuwa hamruhusu kungoja apone kabisa.

Langoni mwa kituo hiku alimkuta mtawa mmoja aliyemwuliza jina, na baada ya kujitambulisha mtawa huyu alimchukuwa Willy na kumpeleka kwenye nyumba ya Padri Marcel Karangwa ambaye alimkuta akimsubiri.

"Karibu sana Willy Gamba, karibu Kigali. Kigali inanuka mauti; hata nyumba ya Mungu inanuka mauti", Padri Karangwa alimkaribisha sebuleni mwa nyumba yake.

"Nashukuru sana Padri hasa kwa kukubali mimi nije nikuone mara tu baada ya maafa yaliyotokea kwenye kituo chako hiki, nashukuru sana", Willy alijibu.

"Unakaribishwa sana, Bwana Musoke amenieleza kila kitu, nasi tunafarijika sana kukutana na watu kama nyinyi ambao mnaweza kuleta matumaini ya amani ya nchi kama hii. Kweli, tuko tayari kukupa maelezo yoyote unayohitaji kwa shughuli yako", Padri Karangwa alimweleza Willy.

"Asante Padri, mimi nisingependa nichukuwe muda wako mwingi kwa vile una majukumu makubwa ya kukijenga upya kituo hiki na kurudisha imani ya watu katika nyumba ya Mungu", Willy alijibu wakati mmoja wa watawa akileta chai na kahawa.

"Utakunywa chai au kahawa", Padri Karangwa alimuuliza Willy.

"Chai ya rangi", Willy alijibu na kupewa chai ya rangi na kipande cha mkate na Padri Karangwa akapewa kahawa.

"Bwana Musoke alisema ungependa kujuwa kwa kifupi hasa ni nini kiini cha chuki iliyokithiri kati ya makabila haya ya Kitutsi na Kihutu".

"Sawa kabisa", Willy alijibu.

"Kwanza kabisa mimi ni Mtutsi...". Alipoanza kuongea akaingia Padri mwingine. Padri Karangwa alimkaribisha na kumjulisha kwa Willy Gamba. "Huyu Padri Boniface Sibomana na ni mmoja wa watu waliopona mauaji". Kisha akamjulisha Willy Gamba. "Na huyu ni Willy Gamba, mwandishi wa habari kutoka Tanzania, ambaye pia amekuja kama wengine wengi waliomtangulia kutupa pole na kutaka kuelewa vipi watu wa nchi moja wanaweza kugeukiana na kuuana kikatili namna hii.

Willy na Padri Sibomana walipeana mikono na wakaketi chini kuendelea na mazungumzo.

"Kama nilivyokueleza mimi ni Mtutsi, lakini Padri Sibomana ni Mhutu, sasa sema tofauti yetu sisi kimaumbile ni nini?", Padri Karangwa alimwuliza Willy. Willy aliwaangalia wote wawili. kweli kimaumbile kati ya hawa wawili hasa hakukuwa na tofauti.

"Hakuna", Willy alijibu huku mapadri hawa wawili wakitabasamu.

"Kama hakuna jibu la swala zima la mauaji ya Watutsi na Wahutu wenye msimamo wa wastani, basi mauaji haya yalishinikizwa kisiasa na kikundi cha watu wachache wenye madaraka makubwa katika Serikali ya Rwanda. Mara nyingi vita ya wenyewe kwa wenyewe katika Rwanda ikisingiziwa kuwa ni vita ya kikabila. Hii si kweli na inapotosha ukweli, ila yanapotokea mauaji kama haya ndipo ujenzi wa chuki wa kikabila unajengwa. Wahutu na Watutsi wameishi pamoja kwa karne nyingi na tofauti zao si hizi tunazoziona leo, kwani hakukuwa na chuki kati ya makabila haya. Ni utawala wa kikoloni wa kugawa nitawale na baadaye. Serikali zetu zilizoongozwa na ubinafsi na uchu wa madaraka uliohubiri kuwepo tofauti kati ya wahutu na Watutsi, tofauti ambazo awali hazikuwepo. Kwa kifupi ni kwamba ili mbinu za kisasa za kuyatumia makabila haya mawili ili watawala wabaki kwenye madaraka ambayo yamesababisha mauaji haya ya kikatili ambayo tumeyashuhudia", Padri Karangwa alinyamaza kidogo ili anywe kahawa yake wakati Willy na Padri Sibomana wakimsikiliza kwa makini. 

Kisha Padri Karangwa aliendelea. "Kama nilivyosema mwanzo, mauaji ya kikatili Rwanda hayakutokea ghafla tu kiwendawazimu eti kwa sababu kabila moja lilikuwa likilichukia kabila lingine. Mauaji ya Rwanda yalikuwa yamepangwa siku nyingi na kwa ufasaha kabisa na watawala wa nchi yetu. Ili kulielewa hili na ili mtu asisingizie kuwa mauaji haya yametokana na ukabila inabidi kwa kifupi tuangalie historia ya Rwanda kwa maana ya makabila haya mawili ya Watutsi na wahutu", Padri Karangwa alieleza.

"Nafikiri kweli ni vizuri tupate historia fupi ya jinsi chuki ilivyojengeka maana mauaji haya ya Watutsi na Wahutu wenye siasa kali ni ya kinyama yaani binadamu ameweza kuwa mharibifu na mkatili kiasi hiki", Willy alisema kwa kusikitika.

"Historia ya Rwanda inaonyesha kwamba watu wa kwanza kuishi Rwanda walikuwa wawindaji ambao ni kizazi cha kabila dogo la Watwa. Inasemekana kuwa wakulima, ambao ni Wahutu, ndio waliofuatia na kisha wafugaji ambao ni Watutsi, ndio walikuwa wa mwisho kufika, na wote waliishi pamoja kila ukoo ukiwa na utawala wake wa kichifu. Kusema kuwa Watutsi walikuja kama wavamizi na kutaka kutawala kwa nguvu makabila mengine si kweli, kwani wana historia wengi wameupinga usemi huo, ila kitu ambacho kilitokea ni kwamba karibu vizazi ishirini vilivyopita ukoo mmoja wa Kitutsi ulioitwa Nyinginya ulipata sifa katikati ya Rwanda na kuanzisha utawala wa kifalme ambao ulitawanyika kwenda kusini mwa Rwanda ya sasa.

Lakini historia inaonyesha kwa bunge lao la wakati huo lilikuwa linaitwa 'abini', nalo liliwashirikisha Wahutu na Watutsi pamoja. Na kwa vile utawala wa Wanyinginya ulikuwa na nguvu, machifu wa Kihutu katikati ya kusini mwa Rwanda walimezwa na kukubalika kama Wanyinginya. Hapa ndipo swala la ukabila wa Kihutu na Kitutsi ulipotambuliwa, si kutokana na ukoo wa Kihutu au Kitutsi bali kwa kutokana na hadhi mtu aliyokuwa nayo. Ukiwa mtawala, hata ukiwa Mhutu uliitwa Mtutsi. Kama huna mali uliitwa Mhutu, na hivyo hii hali iliashiria kuoana kwingi kati ya Wahutu na Watutsi. Ndiyo sababu hata wewe umeshindwa kututoa tofauti," Padri Karangwa alinena.

"Kama si vitambulisho hivi mara nyingi kweli huwezi kujua Mhutu ni yupi na Mtutsi ni yupi maana vile vile tunazungumza lugha moja, tofauti na nyinyi," Padri Sibomana alidakia.

"Huko ndiko ninakokwenda," Padri Karangwa alisema na kisha kuendelea, "Kusema kweli tofauti halisi ambayo ilibaki ilikuwa kwa wahutu wa kaskazini ambao waliendelea na utawala wao mpaka hapo wakoloni walipofika. Pamoja na kwamba utawala wa Wahutu wa kaskazini haukumezwa na utawala wa ukoo wa Nyiginya, bado wahutu hawa na watutsi waliishi bila matatizo."

"Matatizo yalianza lini? Willy aliuliza.

"Usiwe na haraka, mimi taaluma yangu ni ualimu nakupeleka taratibu uelewe na huko tutafika," Padri Karangwa alimjibu na kisha kuendelea, "Tatizo hasa lilianza wakati wakoloni walipofika Rwanda mwishoni mwa karne ya kumi na tisa. Wamisionari wa Kijerumani na kisha askari wa Kijerumani walipofika Rwanda walikuta utawala uliojengeka wa ukoo wa Nyinginya ambao kama nilivyosema ulikuwa ukoo wa Kitutsi. Kama walivyokuwa wakoloni wote walitumia tawala walizozikuta kuwasaidia kutawala. Hivyo, Wajerumani na kisha Wabelgiji baada ya kukuta utawala wenye nguvu ulikuwa wa kitutsi wakaamua kuutumia huu utawala na kuubadilisha uwe wa kinyanyasaji ili ile sera yao ya gawa utawale iweze kufanikiwa. Kwa kusaidiwa na wakoloni sasa watutsi walifuta nafasi yoyote waliyokuwa nayo wahutu kabla ya wakoloni na kuwanyang'anya mali na madaraka, na hii yote ilichochewa na wakoloni ili kuwagawa watu wa nchi hii. Na, kwa vile ilikuwa vigumu kuwatofautisha wahutu na watutsi kwa urahisi mnamo mwaka wa 1933-34 vitambulisho vilianzishwa na wakoloni kwa wananchi wote wa Rwanda vikiwatambulisha kikabila yaani Wahutu, Watutsi au Watwa na vitambulisho hivi hivi ndivyo vilivyotumika katika mauaji haya na mengine mengi yaliyokwisha tokea.

"Kwa kutumia vitambulisho hivi basi maendeleo ya Wahutu na Watwa yalizimwa kabisa?", Willy aliuliza.

"Ndiyo, yalizimwa na hata shule nafasi zote zilitolewa kwa Watutsi, kanisani nako baada ya Omwami kubatizwa kuwa mkatoliki hata kanisa liliwabagua Wahutu. Kanisa Katoliki wakati huo ndilo lilikuwa linamiliki karibu shule zote katika Rwanda. Hivyo liliwasomesha Watutsi na kuhakikisha Wahutu hawapati nafasi ya kusoma ila walibaki na haki ya kuhubiriwa tu", Padri Karangwa alijibu.

"Kwa hiyo vitambulisho vilikuwa moja ya mambo yaliyojenga ukabila ndani ya Rwanda?", Willy aliuliza tena.

"Ndiyo, kabla ya vitambulisho ilikuwa vigumu kujuwa huyu ni kabila gani na vitambulisho kama nilivyosema hapo mwanzo, vilianzishwa na wakoloni wa Kibelgiji ili kujenga ukabila ili wautumie huu ukabila kuwagawa Wanyarwanda kwa faida yao ili iwe rahisi kuwatawala. Baada ya kupewa vitambulisho watu wote waliotambuliwa kama Wahutu walinyanyaswa na kunyimwa hazi zozote na elimu na vilevile mali na hata Wahutu wa Kaskazini ambao walikuwa wakijitawala wenyewe, wakoloni mnamo mwaka 1912 walimshinikiza na kumsaidia Omwami atwae madaraka katika sehemu hizi. Kutwaa madaraka Kaskazini mwa Rwanda kwa Watutsi kulikataliwa na Wahutu wa sehemu hii na mapigano makali yalitokea yakiongozwa na Mhutu aitwae Ndugutse. Kwa vile Watutsi walikuwa wakisaidiana na wakoloni, Wahutu walishindwa na wakatawaliwa na Watutsi. Wahutu wengi waliuawa na huo ndio ukawa mwanza wa uhasama na chuki kati ya Wahutu wa Kaskazini na Watutsi. Sasa, ukiangalia mwanzo mwa hii vita ulikuwa umechochewa na wakoloni maana, kama nilivyosema hapo mwanzo, wakoloni walipofika walikuta makabila haya yakiishi kwa amani", Padri Karangwa alijibu.

"Ilikuwaje sasa baadaye Wahutu kuja kutawala Rwanda", Willy aliuliza.

"Baada ya vita kuu vya pili Watutsi walianza kuomba uhuru kama ilivyokuwa katika nchi zingine za kiafrika. Wakoloni wa Kibelgiji kuona hivi, na jinsi Watutsi walivyokuwa na nguvu na walivyokuwa wamesoma, wakaingiwa na wasiwasi, wakajuwa Watutsi wasingewahitaji iwapo watapata uhuru. Hivyo Wakoloni wa Kibalgiji wakaamua kuwageuka na kuwasaidia Wahutu kuwaunga mkono. Viongozi wa Kihutu walikuwa wachache na wote walikuwa na kisomo kidogo walichopata kwa Wamisionari. Hivyo, kwa vile hawakuwa na nguvu zozote za kiutawala, walipoanza siasa, siasa yao ikawa ya kikabila. Hivyo mwaka 1957 chama cha kupigania haki za Wahutu, kikiongozwa na Gregoire Kayibanda, kilianzishwa kikiitwa Permehutu. Na Wakoloni wa Kibelgiji, wakiwa sasa wamewageuka Watutsi, walianza kukisaidia chama cha Permehutu, huku wakikitafutia nafasi ya kuuangusha utawala wa Watutsi. Nia yao ikiwa kuwaingia kwenye madaraka Wahutu ambao hawakuwa na nguvu ili waendelee kuwategemea kama wangepata uhuru. Hii ingewasaidia wakoloni kuendeleza maslahi yao kwani Wahutu wangewategemea sana kuwalinda dhidi ya Watutsi waliokuwa na nguvu za kijeshi na utawala. Kwa hiyo wakoloni ndio wangeendelea kutawala kiaina kwani watawala wa Kihutu wangekuwepo kama mfano tu.

"Je, viongozi wa Kitutsi hawakushituka?", Willy aliuliza.

"Walianza kushituka lakini mambo yalitokea kwa ghafla sana wakati Omwami Rudahigwa alipofariki kiajabu mjini Bujumbwe mwaka 1959. Jeshi la Ubelgiji lilisimamia kuangushwa kwa utawala wa Kitutsi ambao ulikuwa na umwagaji wa damu vibaya sana. Jeshi la Ubelgiji lililowasaidia Watutsi kuanzia mwaka 1912 sasa liliwasaidia Wahutu na ile chuki ya mwaka 1912 ya Wahutu wa kaskazini ilijitokeza na inasadikiwa kuwa Watutsi wapatao elfu kumi waliuawa na wengi wao wakakimbilia nchi jirani. Hivyo, Wahutu ndio wakawa watawala chini ya Kayibanda baada ya kusaidiwa na wakoloni wa Kibalgiji kuwaweka madarakani", Padri Karangwa alieleza.

"Kwa nini baada ya hapo vitambulisho viliendelea, si Wahutu wangeachana navyo sasa maana vilikuwa vinawabagua?", Willy alitaka kujua.

"Hapana, mambo sasa yaligeuka; Wahutu sasa ndio walikuwa watawala. Hivyo, wakaanza kuwanyanyasa Watutsi. Na vitambulisho hivyo hivyo vilivyowasaidia Wahutu kuwatambua Watutsi na kuwabagua, hata Watutsi wengine wakabadili vitambulisho vyao na kujiita Wahutu maana sasa kibao kilikuwa kimewageukia. Ingawaje Watutsi ndio waliokuwa wamesoma lakini sasa walibaguliwa na Wahutu waliokuwa hawana kisomo maana ndio waliochukua madaraka serikalini. Elimju yote sasa ilitolewa kwa wahutu na Watutsi wakabaki kuangaika na kunyanyaswa. Wengi wao wakaanza kukimbia. Kwa vile jeshi asilimia kubwa lilibaki la Kibelgiji hivyo hakuna kitu ambacho Watutsi wangefanya. Ingawaje Watutsi waliokimbia walijaribu kuishambulia Rwanda kwa kuunda jeshi la msituni lakini hawakufua dafu. Jeshi zaidi la kuongeza nguvu liliitwa mara moja toka Ubelgiji kuja kutokomeza maasi mara uvamizi wa kitutsi ulipoanza. Kwa hiyo, katika miaka yote ya sitini hali iliendelea kuwa ya wasiwasi nchini Rwanda huku watutsi wakiendelea kuuwawa na kunyanyaswa",

"Ilikuwaje Habyarimana akafanya mapinduzi, maana yeye ni Mhutu na utawala ulikuwa Wakihutu? " Willy aliuliza.

"Swali zuri," Padri Karangwa alijibu na kisha akaendelea, "Serikali ya Kayibanda ilianza kuishiwa mbinu na Wabelgiji wakaanza kuichoka maana sasa ilikuwa inakuwepo kwa sababu ya ukabila tu. Mnamo mwaka 1973 Kayibanda akafanya makosa. Kwa vile Watutsi walikuwa wamenyimwa nafasi yoyote katika serikali, kibiashara na sehemu zingine zozote, sehemu waloyokimbilia ilikuwa ni ndani ya kanisa. Hivyo, Seminari nyingi zilijaa Watutsi pamoja na vyuo vikuu ambavyo viliitwa vyuo vya Watutsi. Kwa hiyo, mwaka 1973 ili kuwaondoa Watutsi katika vyombo vyote vya elimu, serikali ilianza kushambulia seminari, shule na vyuo vikuu. Kwa vile vyombo vyote vya elimu vilikuwa mikononi mwa kanisa katoliki Askofun wa kanisa katoliki akaanza kupiga makelele na kulaani serikali. Hata hivyo, huyu Kayibanda kabla ya kushika madaraka alikuwa katibu wa  Askofu huyu na alikuwa akiwaunga mkono wahutu. Hapo ndipo Wabelgiji tena wakapata nafasi na kumtumia Meja Generali Habyarimana kufanya mapinduzi na kumtoa rais Kayibanda.Haybarimana alikuwa Mhutu wa kaskazini na Kayibanda wa kusini. Utawala wake ulipokelewa kwa shangwa na Watutsi na Wahutu ukifikiriwa utakuwa utawala wa haki na usawa lakini hali haikuwa hivyo, badala ya kuwa na mgawanyiko wa Watutsi na Wahutu mambo yalizidi. Sasa kukawa na upendeleo kwa Wahutu wa kaskazini na kuwabagua Watutsi na Wahutu wa kati na kusini. Ndiyo sababu Wahutu wenye siasa ya wastani waliuawa katika mauaji ya aprili wakiwamo wanasiasa, wafanyakazi wa serikali na wafanyabiashara, wote walikuwa wa kusini. hivyo, kufika wakati wa sasa sera ya gawa nitawale iliendelea katika Rwanda."

"Maelezo yako toka mwanzo yameonyesha kuwa Wahutu na Watutsi kama watu hawakuwa na tatizo kati yao. Wamekuwa wakitumiwa na watawala wa kikoloni na watawala wa kizalendo ambao wamekuwa wakiwachonganisha ili wakosane na kwa kukosana kwao wao wafaidike," Willy alieleza.

"Haswa, ndiyo sababu nimeeleza yote haya uweze kulielewa tatizo la Rwanda. Tatizo letu si ukabila, tatizo letu ni uongozi."

"Sasa nini kilifanya hali ifikie mauaji, kama ni tatizo la uongozi nchi nyingi za Kiafrika zina tatizo hilo. Na kama ni kutumiwa na mataifa ya nje nchi nyingi zinatumiwa hivyohivyo, mauaji kama haya ni ya pekee katika dunia, hayana mfano," Willy alimuuliza Padri Sibomana ambaye alikuwa akisikiliza kwa muda mrefu bila kusema kitu.

"Nafikiri hilo swali lako ndilo kila mtu anajiuliza, maana mauaji haya tuliyo yashuudia hayana mfano, hata ya Hitler yalichukua muda mrefu maana vita vilipiganwa kwa miaka, lakini mauaji haya yanashinda fikra kwani yalianza dakika chache tu baada ya kufa Rais na kusambaa nchi nzima utafikiri moto wa petroli," Padri Sibomana alisema.

"Wakati wa Habyarimana kulijitokeza kikundi kidogo cha watu kilichomzunguka ambacho ndicho kilichokuwa kinafaidika na utawala wake. Kikundi hiki kilikuwa cha watu wa kaskazini kutoka sehemu za Gisenyi na Ruhengeri nacho kilijulikana kwa jina la Akazu. Kikundi hiki kilijilimbikizia mali na madaraka, kilijenga ngome ya kukizunguka na hakuna kikundi kingine kilichoweza kupenya ngome hiyo. Hivyo, ili Rais na kikundi hiki waweze kuendelea kujilimbikizia mali na madaraka kilihakikisha kuwa hakuna biashara wala nafasi ya uongozi inayoweza kupatikana mahali popote bila kikundi hicho kutoa ruksa. Kikundi hiki kilikuwa cha Wahutu. Hivyo, uhalali wa serikali ulipoanza kushitukiwa, kwa vile kikundi hiki cha Akazu kilikuwa kimejilimbikizia mali nyingi, kilianza kuitumia mali hii na ya serikali kujenga jeshi lake, redio yake, magazeti na kutumia vyombo hivi kuwachochea Wahutu, ambao ndio wengi, wawachukie Watutsi ambao sasa walikuwa wanausaili uhalali wa serikali hii wakiwemo Wahutu wapendao amani na usawa ambao waliitwa Wahutu wenye msimamo wa wastani. Kufikia mwaka 1990 kulikuwa hakuna Mtutsi mwenye madaraka katika serikali, kwa mfano kati ya wakuu wa mikoa kumi na moja hakukuwa na Mtutsi hata mmoja; kati ya vyeo 143 vya juu serikalini hakukuwa na Mtutsi hata mmoja; kati ya mabalozi wote walioteuliwa kwenda nje Mtutsi alikuwa mmoja tu. Na kati ya wabunge sabini, ni watutsi wawili tu waliokuwa wabunge. Katika jeshi walihakikisha hakuna Mtutsi na hasa jeshi la kumlinda Rais lote lilikuwa na Wahutu na Wahutu hao vilevile walikuwa ni ama ndugu za Rais au wa mkewe", Padri Karangwa alieleza.

"Sijaelewa vizuri jinsi hali hii ilivyoashiria kufikia mauaiji yaliyotokea", Willy alisema huku akionyesha sasa kuwa makini zaidi.

"Huku ndiko ninakokwenda. Hawa Akazu pamoja na familia ya Rais walifikia kujiita miungu wadogo. Walifanya kila walichotaka. Kuna habari za kuaminika kuwa kuna Mzungu mmoja rafiki yake sana na Rais ambaye alikuwa anawatengenezea fedha kwa maana ya kuchapisha na wao wanamlipa mazao kama kahawa kwa bei yake, na mazao mengine yoyote aliyohitaji; na pia kuna tetesi kuwa hata bangi ililimwa na watu hawa na kusambazwa na huyu Mzungu. Kusema kweli, hawa watu walitajirika kuzidi kiasi na wakajisahau kabisa. Ili kubaki katika hali hii kama nilivyosema mwanzo, ilibidi sasa wachochee ukabila. Walikuwa wameshafilisika kisiasa, uhali wa utawala ulikuwa hauna msimamo tena. Hivyo, kimbilio lilikuwa ni ukabila na kuhakikisha Wahutu wananufaika na utawala, na ilikuwa ni rahisi sana kuwachochea na kufanya lolote ambalo viongozi wao wa Kihutu walitaka wafanye. Uchochezi wa Wahutu ulizidi kuanzia mwaka 1988 baada ya kongamano la Watutsi lililofanyika Washington D.C Marekani na kuamua kuiondoa serikali tawala madarakani. Mkutano huo pia ulihuhudhuliwa na Wahutu ambao walikuwa wakipinga mwenendo wa serikali tawala. Haja ya wakimbizi wa Kitutsi kurudi nyumbani kwa njia yoyote ile ndiyo ilikuwa msukumo wa kongamano hili huku Marekani, kwani Rais alikuwa akieleza kuwa wakimbizi hawana haki tena ya kurudi Rwanda kwa kuwa nchi ilikuwa ndogo mno na isingeweza kuwapokea tena". Padri Karangwa alinyamaza kidogo na kuchukua glasi ya maji.

Padri Sibomana akatumia wakati huu kumkata kauli kidogo. akasema, "Padri alilisahau swala la wakimbizi wa Kibanyarwanda Uganda, maana hili lina uhusiano mkubwa mno na hali hii yote anayoieleza".

"Bila shaka Padri Sibomana, nilikuwa bado niendelee huko ila kwanza nilitaka kuonyesha mshikamano wa Wahutu ulikuwaje", Padri Karangwa alijibu.

"Sawa Padri, endelea", Padri Sibomana aliafiki.

"Kama alivyo kumbusha Padri Sibomana, wakimbizi wengi walijiunga na jeshi la NRA la Uganda katika miaka ya themanini. Hao walimsaidia Rais wa sasa wa Uganda kuchukua madaraka. Kwa kawaida, wakimbizi mara kwa mara hujiingiza kiurahisi jeshini kuliko kukaa bure na hii vile vile huwapa tamaa ya kutafuta njia za kijeshi kurudi kwao. Na hivi ndivyo ilivyokuwa kwa wakimbizi wa Kibanyarwanda waliokuwa Uganda, wengi wao wakiwa Watutsi na Wahutu wachache. Makamanda wengi wan NRA walikuwa wakimbizi wa Kibanyarwanda. Baada ya kushika madaraka Uganda ubaguzi ulianza wa wakimbizi wa Kinyarwanda Uganda. Waliwapinga hasa waliokuwa wapinzani wa serikali na raia wa kawaida wa Kiganda waliona  hawa wakimbizi kama wanaokuja kuwanyang`anya haki zao kwa vile walikuwa wakishika vyeo vya juu katika jeshi la NRA ambali sasa ndilo lililokuwa likitawala Uganda. Ilikuwa ni hali hii na nia ya kurudi kwao kwa hali yoyote sasa, iliyo ashiria kuzaliwa kwa RPF. Hivyo makamanda wa Kinyarwanda walikuwa NRA sasa waliamia RPF.

"Inasemekana Rais wa Uganda, ili asiwe na matatizo nyumbani kwake kwa sababu nilizozisema hapo juu, alikuwa msukumo mkubwa wa kuisaidia RPF ili wakimbizi hawa walazimishe kurudi kwao kwa kutumia nguvu za kijeshi. Kutokana na hali hii mnamo tarehe 1 oktoba 1990 watoto wa wakimbizi wa Kinyarwanda, ambao walikuwa wapiganaji wa NRA, walikusanyika kusini- magharibi mwa Uganda na siku hiyo ya tarehe moja wakaivamia Rwanda. Ingawa hawakufanikiwa, lakini nguvu yao ilifahamika na kusababisha kiwewe kwa utawala wa Rwanda, na hapa ndipo mipigano ya kuwaangamiza Watutsi wote na Wahutu waliokuwa wanaunga mkono jitihada za Watutsi ilipoanza kupangwa na Akazu. Kama nilivyosema hapo mwanzo ili uchochezi kwa Wahutu dhidi ya Watutsi upate kufanikiwa, kundi lililokuwa linafaidika na utawala huu liliunda jeshi lake lililoitwa Interahamwe. Interahamwe maana yake ni "wale wanaovamia na kupigana pamoja". Jeshi hili liliundwa toka sehemu mbali mbali nchi nzima na kufundishwa na kikosi maalumu cha Rais kataka kambi za Gabiro na Bigongwe, na wote waliochaguliwa walikuwa Wahutu isipokuwa kamanda wao alikuwa Mtutsi ambaye baba yake alikuwa amechukua kitambulisho cha Kihutu. Wengi wa Interahamwe walikuwa ni vijana ambao walikuwa hawana kazi, Wakipewa vinywaji na pesa wakifundishwa kuwachukia Watutsi na kufanya maasi ya aina yoyote ile tokea kubaka, kunyang`anya mpaka kuua. Wizara ya ulinzi ndiyo iliyotoa silaha na kutoa sehemu za kufanyia mafunzo ingawa Interahamwe ilibaki mali ya Akazu na cha tawala. Vilevile wakimbizi wa Kirundi nao walichukuliwa na kuingizwa katika jeshi hili Iterahamwe. Inasemekana kuwa hawa wakimbizi wa Kirundi, ambao ni Wahutu, walikuwa wakatili zaidi kuliko hata wenzao wa Rwanda. Wakuu wa Interahamwe hawakuishia hapo tu bali walienda mpaka Goma, Zaire, ambako nako walichukua askari wa kujiunga na Interahamwe. Wazaire waliochukuliwa ni wale wenye asili ya Kihutu lakini Wazaire wanye asili ya kitutsi kwa jina la Wabanyamulenge, wao walikataa kwani wao walikuwa wanaunga mkono harakati za RPF.

"Hawa Interahamwe walikuwa wengi kiasi gani?" Willy aliuliza.

"Hata kufikia tarehe 6 aprili na baada ya kifo cha Rais na mauaji kuanza inasemekana kwamba kila Mhutu sasa alikuwa Interahamwe, lakini Interahamwe waliochukua mafunzo haswa walikuwa wamefikia kiasi cha elfu kumi."

"Inasemekana yalifanyika mauaji mengi kwa silaha hafifu kama rungu, panga na kadhalika.Hii ni kwasababu haya marungu yaliweza kutengenezwa kienyeji na kwa urahisi au vipi?" Willy aliuliza.

"Hapana, marungu na mapanga haya yaliagizwa na kundi la Akazu kutoka China. marungu haya yalipendekezwa na Akazu kwani kila yalipotumiwa yalitoa maumivu ya ajabu kwa adui. Na inasemekana kuwa watu wengi walitoa pesa kununua kuuawa na risasi kuliko kustaimili kifo cha rungu. Marungu haya, kwa mfano yalianza kuingia Rwanda tokea januari 1993 yakipakuliwa toka Mombasa kupitia Nairobi na kuhifadhiwa kwenye maghala Kigali na Kibungo. Lakini, pamoja na marungu haya serikali ya Rwanda, kati ya mwaka 1992 na 1994, iliagiza silaha kubwa kubwa toka Ufaransa. Vile vile silaha zingine zilitoka Ulaya ya mashariki kupitia Zaire. Ufaransa, hata hivyo, ndiyo iliyokuwa mfadhili mkubwa wa siliha kwa serikali ya Rwanda. Inasemekana yule mzungu rafiki wa Rais na Akazu ndiye alipanga mipango yote ya uuzaji wa silaha kati ya Ufaransa na Rwanda. Inasemekanaq kuwa Mfaransa huyu ambaye pia alikuwa na uhusiano wa karibu na Ikulu ya Ufaransa alifikia kuwa mshauri mkuu wa Rais na ndiye aliyekuwa anamshauri Rais afanye nini, aseme nini na hata mauaji mengi inasemekana yalitokana na ushauri wake. Na kwa vile Rais na watu wake walitaka kutawala maisha, huyu mtu ambaye alikuwa akiwapa silaha za hali ya juu ili RPF isiweze kufurukuta, walimwonja kama Mungu, hata ndege ya Rais inasemekana ilitolewa kama zawadi nja mtu maarufu wa huko Ufaransa kwa mipango ya huyu mtu," Padri Karangwa alieleza.

"Kwa hiyo mauaji haya ya Rwanda yalipangwa, na siyo kwamba yalitokea tu kwa bahati mbaya, kwa kuchukizwa na kifo cha Rais?" Willy aliendelea kumdadisi Padri.

"Bila shaka. Hili kundi la Akazu lilikuwa na vyombo vya propaganda vingi ambavyo vilisaidia kuingiza chuki kati ya Wahutu na Watutsi ili iwe rahisi kuwatumia Wahutu katika mpango wao wa kuwamaliza Watutsi ili waweze kutawala milele. Magazeti kama Kangura na Stesheni ya Redio ya RTLM vilikuwa vinamilikiwa na kundi hili. Gazeti hili lilianzishwa katikati ya mwaka 1990 na liliungwa mkono na chama tawala pamoja na Rais na familia yake huku likiongozwa na rafiki wa Rais. Vilevile lilikuwa likifadhiliwa na huyo Mfaransa. Kazi kubwa, kama nilivyo sema hapo awali , ilikuwa ni kuchochea chuki kati ya Wahutu na Watutsi, huku radio hiyo na gazeti hilo vikiwahamasisha Wahutu wajiweke tayari kuwashambulia na kuwavamia Watutsi ambao kila wakati liliwasema kuwa wanataka kurudisha utawala wao wa kifalme, kila Mhutu amwue Mtutsi aliye karibu nae. Maneno makali kama haya ambayo yaliyotokea kila siku katika vyombo hivi yalikuwa ni chanzo kikubwa kwa mambo yaliyotokea kwanzia tarehe 6 Aprili alipouawa Rais," Padri Karangwa alieleza.

"Naona saa zimeenda, tumezungumza sana maana sasa yapata saa tatu na nusu usiku. Lakini kabla hatujamaliza Padri hasa nani alimuua Rais?" Willy aliuliza.

Sura ya Padri alibadilika na kisha akauliza, "Unataka maoni yangu binafsi?"

"Ndiyo kwani kwa maoni yako kutokana na ulivyonieleza unaweza kuhisi, na hisia zako zinaweza kuwa sahihi,willy alijibu.


"Maoni yangu binafsi ni kwamba Rais aliuawa na Akazu. Ilipoonekana kuwa Rais alikuwa ameamua kutia sahihi ya makubaliano ya Arusha, hiki kikundi chake cha Akazu kikajua huu ndio utakuwa mwisho wao kufaidika. Hivyo wakaamua kumuua Rais ili katika machafuko hayo, waweze kupanga serikali mpya na kusimika utawala wao mpya ambao ungewahakikishia kuendelea kufaidi. Ukweli kuwa watu wake ndio waliomuua kwa kuogopa utawala wa kidemokrasia ambao ungefuata baada kutia saini makubaliano ya Arusha, ulijitokeza katika gazeti lao la Kangura, katika gazeti hilo ilitabiriwa kuwa Rais angeuawa na askari wa jeshi la Rwanda mnamo mwezi wa machi 1994 kufuatia kukubali kwake kusaini makubaliano ya Arusha. Gazeti hilo ambalo lilichapishwa mnamo mwezi wa Januari 1994 liliendelea kusema kuwa atakayemwua Rais atakuwa ni Mhutu. Na likasema kuwa waandishi wa gazeti hilo na rafiki zake na Rais huyo walimuasa asiweke saini makubaliano ya Arusha lakini ilionekana kuwa Rais alikuwa amebanwa sana na serikali zilizokuwa zikisuluisha mgogoro kiasi kuwa alikuwa hana msimamo. Hivyo, gazeti hilo katika toleo hilo, lilisema kuwa Rais atauawa na hapo ndipo vitatokea vita na damu nyingi itamwagika na jeshi la UNAMIR lisingeweza kufanya kitu. Lilizidi kumshauri Rais akatae kutia saini makubaliano hayo vinginevyo kifo chake hakitaepukika. Na yote yaliyoandikwa kwenye toleo hilo ndiyo yaliyotokea. Rais alipokubali tu kutia sahihi makubaliano ya Arusha basi hawa watu wake wakatimizi ahadi yao kwani wao ndio walioshika hatamu zote za serikali kuanzia utawala mpaka jeshini. Kwa hiyo, baada ya kusikia amekubali makubaliano ya Arusha basi walikiamurisha kikosi cha mizinga cha Kanombe, na ndege ya Rais ilipokuwa inakaribia kutua makombora matatu yalipigwa, mawili yakaipiga ndege; Rais na watu wote waliokuwemo, ikiwa pamoja na Rais wa Burundi, wakauawa. Akazu walipanga kuwa baada tu ya Rais kuuawa basi jeshi lao la Interahamwa lingeanza mauaji mara moja ya kuakikisha kuwa Watutsi wote pamoja na yeyote aliyekuwa anawaunga mkono anauawa. Mbinu hii ilikuwan ni kutaka RPF kukosa watu wa kuwaunga mkono ndani ya nchi hiyo na hivyo kushindwa vita. Lakina ya mungu mengi, mambo hayakwenda moja kwa moja kama walivyotarajia," Padri Karangwa alieleza na kuchukua glasi ya maji na kunywa.

"Lo maelezo yako yameniingia vizuri na nafkiri kutokana na ulivyoeleza kweli Rais aliuawa na mfumo wake mwenyewe wa kung`ang`ania madaraka kwani hata wakati alipokuwa amefikia kubadili mawazo yake, mfumo wake  aliokuwa ameuweka haukumpa nafasi. Hivyo, ilibidi ummalize ili ubinafsi wa watu wake waliomzunguka uendelee,"m Willy alisema huku akiwa kama anajisemea mwenyewe.

"Watu ka nyinyi basi ndio mnaotakiwa mueneze habari hizi ili viongozi wengine wajue kuwa utawala wa mabavu, na wakung`ang`ania madaraka ili wewe tu ndio ufaidike una mwisho wake, na mwisho wake ni mbaya ata ufanyeje,"Padri Sibomana alidakia.

"Tutajitahidi kueleza ukweli huu," Willy alijibu.

"Nafikiri itakuwa vizuri kesho kama ukipata nafasi uje nikuonyeshe mauaji yalivyo fanyika, uone ukatili usio kifani,"Padri karangwa alimweleza Willy.

"Nitajitahidi, lakini kwa vile nina shughuli nyingi inabidi nirudi haraka Arusha. Kama sitaweza kufika maelezo yako yanatosha. Na kabla basi sijaondoka nikuulize swali."

"Uliza usiwe na wasiwasi, sisi tumefurahi kuwa nawe hapa wala hatuoni kama muda unaenda" Padri Karangwa alijibu.

"Unafikiri baada ya RPF kuchukua madaraka kutakuwa na maana na uelewano Rwanda? au niulize tena vingine baada ya haya mauaji ya kikatili dhidi ya Watutsi yalivyofanywa na Wahutu, unafikiri kutakuwa na uelewano kati ya makabila haya hata kama RPF itaweka utawala wa demokrasia?"

"Hilo swali gumu lakini nafikiri ndilo swali lenye maana kubwa sana. Uelewano kwa sasa utakuwa mgumu. Vidonda vya mauaji ya ndugu zao Kitutsi bado vibichi na kama binadamu lazima kutakuwa na kisasi, kwa hili tusijidanganye. Pili,  baada ya RPF kuchukua madaraka maelfu ya Wahutu wamekimbia ni wakimbizi huko Tanzania, Zaire, na nchi zinginezo. Kati ya hawa waliokimbia na hasa waliokimbilia Zaire, ni wale Interahamwe na wanajeshi wa serikali ya zamani. Kwa vyovyote, hawa nao wataanza kujikusanya na kuunda tena jeshi la kuja kuvamia tena Rwanda, na Serikali ya sasa haita kubali. Hivyo, vita vitaendelea na itaendelea kwa muda mrefu kama jumuiya ya kimataifa itaendelea kulipa kisogo swala hili la Rwanda. Tatu, miongoni mwa wakimbizi wanaoumia ni wanawake na watoto, na watoto hawa taabu watakazozipata huko watakuwa wanaelezwa kuwa ni sababu ya Watutsi ambao wamewafukuza nchini mwao na hivyo kujenga chuki tena. Watoto wa Kitutsi vilevile watakuwa wanaelezwa ndugu yako fulani aliuawa na Wahutu; na kwa vile kila familia iliathirika chuki hii itazidi kujengeka maradufu. Mimi maoni yangu ni kwa serikali ya RPF isilipize kisasi. Wakimbizi wote warudishwe nyumbani. Wale ambao wanajulikana kabisa ndio waliusika na kuongoza mauaji haya ya kikatili, wakamatwe kokote duniani waliko na wafikishwe maakamani. Kama dunia hii isivyokuwa na usawa, wale wote walioongoza mauaji haya kwa vile wana pesa tayari wapo nchi za nje wanakula starehe. Wanaohangaika sasa ni wanawake na watoto; hii si sawa. Lazima hawa watu wakamatwe hasa kundi la Akazu, wote wakamatwe wafikishwe maakamani,"Padri Karangwa alimalizia huku sasa machozi yakimlengalenga.

"Kwa kweli, hali ya nchi yetu hii itayumba kwa muda mrefu. Wote wanachotegemea sasa ni serikali ya RPF iweze kuwahamasisha wananchi waweze kusameheana ili tujenge taifa jipya. Nakubaliana na Padri Karangwa kuwa ili tukio kama hili lisitokee tena, wote waliohusika na kitendo hiki wafikishwe mbele ya maakama wahukumiwe na adhabu kali itolewe ili kitu kama hiki kisitokee tena popote duniani, maana ni kitu cha kutisha ambacho kinafanya akili isikubali kuwa binadamu anaweza kuwa katili na mharibifu namna hii kama ilivyotutokea sisi hapa. Hapa Willy, dunia isinyamaze mpaka hapo wote waliohusika wameadhibiwa," Padri Sibomana alitoa maoni yake.

Huku akiinuka, Willy alishukuru na kusema, "kusema kweli sina maneno ya kuweza kueleza jinsi ninavyo shukuru kwani naweza kurudi Arusha kesho maana yote nimepata niliyotaka kujua kwenu na nimejifunza mengi, asante sana. Nipatapo nafasi nitawatembelea tena. Nikishindwa kuja kesho mara nyingine nitakuja kwa mapumziko. Asanteni sana, tena sana."

"Nasi tunashukuru sana kwani kuja kwako kumetufariji kumbe kuwa huko duniani kuna watu wanaoyajali matatizo yetu yaliyotupata. Asante sana," Padri Karangwa alimalizia, kisha wakamsindikiza Willy mpaka kwenye gari lake; akaondoka.

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU