KASHESHE
III
Willy aliangaliana na Bibiane.
"Unasemaje tuwasaidie hawa ama vipi?", Bibiane aliuliza.
"Hapana tuendelee na mipango
yetu. Hii imekuwa bahati nzuri kwetu, naamini Meja Kasubuga ana uwezo wa
kuukabiri uvamizi huu, na nahisi walengwa wa uvamizi huu ni sisi tunatafutwa,
huenda kikosi cha Col. Gatabazi kimesikia ama kuhisi kuwa tuko hapa. Wakati wao
wanatusaka hii itatupa nafasi nzuri, kwanza kumtoroka Meja Kasubuga na pili
kuendelea na mipango yetu. Panda gari twende zetu Kibumba tukawasake hawa
majahiri", Willy alieleza huku wakipanda gari na kuondoka kwa kasi
kuelekea Kibumba.
IV
Wakati kikosi cha Nkubana kikisonga
mbele kuelekea hoteli Meridien-Izuda kilishitukiwa na askari mmoja wa doria
ambaye baada ya kusikia nyayo za watu zisizo za kawaida akapanda juu ya mti na
kuchungulia chini ya kjinjia kilichotelemka kutoka mlimani kuelekea hotelini.
Akisaidiwa na mbalamwezi askari hjuyu aliweza kukiona kikundi cha askari kadhaa
kikielekea hotelini hapo, baada ya kuthibitisha kuwa walikuwa askari wa adui na
jinsi walivyokuwa wakisonga mbele kwa tahadhari kubwa huku silaha zao zikiwa
zimewekwa tayari kwa mashambulizi.
Huyu askari wa doria alitelemka kwenye
mti haraka haraka na kimya ili asiwagutue wale wavamizi waliokuwa hatua kumi tu
karibu na ule mti na kwa kutumia uzoefu wa sehemu ile alikimbia kwa kutumia
njia za mkato na kwenda kutoa taarifa kwa kikosi kilichokuwa kwenye maandalizi
ya kuondoka kuelekea mpakani kisiondoke kwani kulikuwa na uvamizi.
"Kuna kikosi cha adui kinaweza
kutushambulia sasa hivi, kimetumia kichochoro namba tatu na kitafika hapa sasa
hivi, askari huyo alimweleza Mkuu wa kikosi hicho Sajenti Ibrahim.
"Oke, wewe kimbia kwa Afande
Kasubuga umweleze wakati sisi tunaelekea huko kuwasimamisha mpaka tupate
msaada", Sajenti Ibrahim aliamru na palepale akawaamru askari wake waweke
silaha zao tayari na kusonga mbele kuelekea kichochoro namba tatu. Njia zote
zilizokuwa zinaelekea kwenye hoteli hii zilipewa namba ili iwe rahisi
kuzitambua kwani zilikuwa nyingi. Yule askari wa doria alikimbia mpaka ofisini
kwa Meja Kasubuga lakini hakumkuta, kwani ndio wakati Meja Kasubuga alikuwa
amewasimamisha Willy na Bibiane wasiondoke, na kabla hajajuwa ampate wapi na
yeye alisikia milio ya bunduki akajuwa tayari mapambano yameanza.
Sajenti Ibrahim na kikosi chake
walifanikiwa kuwaona wale askari wavamizi wakisonga mbele kuelekea hotelini na
kwa vile hakujuwa walikuwa na nguvu kiasi gani aliamru askari wake waanze
kushambulia hata bila kulenga shabaha kwa uhakika ili kuwatia kiwewe. Na kweli
hii ilimshitua Nkubana kwani hakutegemea kukutana na upinzani haraka kiasi
hicho kutokana na maelezo ya yule askari muasi.
"Luteni Nyamboma", Nkubana
alimwita msaidizi wake, "Wewe endelea kukabiliana na hawa adui zetu ili
mimi na askari watano tuweze kupata mwanya wa kwenda kumkamata Willy. Fanya
mashambulizi makubwa ili askari wote wafikiri kuwa wanashambuliwa na kikosi
kikubwa ili wote waje upande huu na sisi tupate urahisi pale Willy alipo".
"Sawa, nimekusoma
Kamanda", Nyamboma alijibu.
Nkubana aliwachagua askari watano
wazuri pamoja na yule kikaragosi wao. "Wewe tupeleke chumba cha yule mtu,
tumia uzoefu wako wa hapa".
"Sawa afande, yule askari
alijibu huku akitetemeka maana alistaajabu namna walivyokuwa wamebainika na
kuonekana kwa adui mapema namna ile.
Mapigano makali yalianza na, kama
Nkubana alivyotaka, askari wengi wa kambi ile walielekea upande wa mapigano
kuongeza nguvu wakiongozwa na kiongozi wao Meja Kasubuga. Nkubana na askari
wake hawakupata kikwazo mpaka walipofika kwenye chumba alichopangiwa Willy.
Baada ya Nkubana kushuhudia umahiri
wa Willy Kigali, hakutaka kufanya makosa tena. Aliwapanga askari wake vizuri na
kwa hadhari kubwa, walipofika kwenye chumba cha Willy na kwa amri moja
wakaupiga mlango kwa nguvu zao zote na askari wawili wakaingia na mlango ndani
ya kile chumba. Chumbani hawakumkuta mtu isipokuwa mikoba miwili iliyokuwa na
nguo, Nkubana akautambua mkoba mmoja kuwa ulikuwa wa Bibiane, maana alipata
kuuona pale sebuleni kwa Bibiane mjini Kigali.
"Watakuwa wapi hawa?",
Nkubana alihoji, kisha akaendelea. "Wanaweza kuwa wamejiunga na askari wa
hapa wanaopigana na kikosi chetu au wamevuka mpaka".
Yule askari kikaragosi alikuwa
ametoka nje na akarudi na kusema. "Gari lao halipo, nafikiri wamekimbia
mapigano".
Nkubana aliposikia hivyo woga ulimwingia
kwani alijua mtu huyu amevuka mpaka. "Itatubini na sisi tuvuke mpaka sasa
hivi. Wao wameondoka na gari sisi itabidi twende kwa miguu sasa", Nkubana
aliamru huku ule upande wa mapigano makali yalikuwa yakiendelea.
"Itabidi turudi kuongeza
nguvu", askari mmoja alishauri.
"Hapana, Luteni Nyambona ana
ujuzi wa kutosha, akiona amezidiwa atarudi nyuma na kukimbilia mpakani. Huu ni
wakati mzuri kwetu kuondoka kuwafuata hawa washenzi", Nkubana alijibu huku
wakiondoka kuelekea mpakani.
V
Usiku ule Willy na Bibiane
walipokuwa wakielekea kwenye mpaka wa Rwanda na Zaire, mbalamwezi iling'aa sana
na kuyaonyesha mandhari safi ya milima ya Volkano ya Virunga.
Milima hii ilijulikana toka zama za
kale, ambapo hata Wagiliki wa zamani waliizungumzia sana milima hii wakiita
milima ya mwezi. "Sasa wewe mwenyewe unaweza kuona kwanini waliita
hivyo", Willy alimsimulia Bibiane.
"Inaonekana wewe umesoma sana
historia", Bibiane alieleza.
"Unajuwa kitu chochote hakiwezi
kuwa kitu bila historia. Ili uijue dunia hii lazima ujue historia. Hata
binadamu hawezi kuwa binadamu kama hana historia. Ndio maana mimi nikikwambia
naitwa Willy, lazima utaniuliza Willy nani, nitakujibu Willy Gamba. Halafu
utataka kujuwa baba yangu anatoka wapi halafu nitakwambia. Hii yote ni kutaka
kujua historia yangu ili uweze kujua namna utakavyoniweka. Hata nchi. Nchi
isiyokuwa na historia si nchi. Haiwezi kuwa na maendeleo. Sijui kama umenielewa
vizuri mpaka hapo?", Willy alijibu na kuhoji.
"Nimekuelewa vizuri sana Willy.
Kwa muda huu mfupi nitakaokuwa na wewe hakika nitajifunza mambo mengi",
Bibiane alimwambia Willy.
"Sasa walikuwa wanakaribia sana
mpakani, na Bibiane akasema.
"Tukivuka mpaka tu, lazima
tutakutana na kikosi cha jeshi la Zaire, Unasemaje?".
"Unazijuwa njia nyingine
tunazoweza kukwepa mambo ya mpakani?", Willy aliuliza.
"Ndiyo Willy, na ndio sababu
nimesema hivyo, hapo mbele utakata kulia nitakuonyesha njia ya siri wanayotumia
wapelelezi wa Akazu, lakini tuwe na tahadhari kubwa. Willy akakata kulia baada
ya mwendo wa dakika kadhaa mara njia iliisha. Kukawa na njia ya majani tu.
"Endelea tu. Ukikata tena kushoto. Tutakuwa tayari tuko Zaire. ni kilomita
kama moja tu kutoka hapa", Bibiane alimwambia Willy, baada ya kutembea
mwendo wa kilomita moja na baada ya kupita sehemu ya miti mingi walitokea
mahali pa wazi na upande wa kushoto wakaona taa zinawaka.
"Pale ndio mpakani upande wa
Zaire na ile ni kambi ya jeshi la Zaire", Bibiane alieleza.
"Tunaweza kupata magari ya
jeshi pale?", Willy alimuuliza Bibiabe.
"Lazima. Unataka tukaibe gari
moja la jeshi?", Bibiane alihoji.
"Unasoma sana mawazo yangu.
Tusiibe, tukachukue tu?", Willy alijibu na kuendelea. "Ili tusije
tukatia shirika la Msalaba Mwekundu dosari, yafaa tusiwe na gari lao kwenye
uwanja wa mapambano. Hapa tutapata mahali pazuri pa kulificha halafu tukachukue
gari la jeshi la Zaire. Itakuwa vilevile vigumu kusimamishwa na askari
hovyohovyo".
"Je kuhusu nguo
itakuwaje?", Bibiane alihoji tena kwa shauku.
"Kuhusu nguo tutawavua askari
walioko mpakani". Willy alisema huku Bibiane akicheka sana.
"Wewe una mambo. Mbona naanza
kusikia raha, usiku huu naona itakuwa kasheshe tupu", Bibiane alinena.
Walitafuta sehemu iliyokuwa na msitu
wakalificha gari la Msalaba Mwekundu na kuitoa mizigo yao. Gari lilifichika
vizuri sana kiasi kwamba ingekuwa vigumu mtu kuligundua mara moja.
"Tutalipitia kabla jua
halijachomoza", Willy alinena.
"Kama tukiwa hai", Bibiane
alijibu.
"Ili uweze kubaki hai fikiri
kuwa utakuwa hai. Na ukiwa hai ukifikiri utakufa. Utakufa tu", Willy
alifafanua.
"Sawa bosi. Tutarudi hapa
kwenye gari letu tukiwa hai", Bibiane alisema.
"Mawazo safi kabisa",
Willy aliongeza. Wakiwa wamebeba silaha zao na kila kitu walichohitaji kwa
mapambano usiku ule walianza kuinyemelea ile kambi ya jeshi mpakani Zaire.
Walipofika pale kituoni waliyaona magari matatu ya jeshi aina ya Landrover ya
wazi nyuma yakiwa yameegeshwa. Walipoangalia vizuri waliwaona askari watatu.
Kila mmoja akiwa ameegemea kwenye gari lake.
"Hao watakuwa madereva wa hayo
magari", Bibiane alibobota kwa sauti ya chini.
"Hata mimi nafikiri hivyo,
nahisi yalikuwa yamewachukua wale askari walioshambulia kule Meridiane hoteli,
maana inaonekana hawa askari wanaosubiri watu", Willy alijibu.
Kwa vile yale magari yalikuwa karibu
na ua wa michongoma na pale mahali. Willy alifikiri namna ya kuwashambulia bila
ya kuwagutusha watu wengine pale kikosini. Mara akawaona askari wote wanakuja
kuzungumza na yule askari aliyekuwa kwenye gari la mwisho karibu kabisa na ua.
"Bibiane kazi kwako, hapohapo
wewe mshambulie yule wa kushoto. Mimi nitamalizana na wale wawili. Wa kati na
kulia", Willy aliagiza huku hawa askari wakiwa sasa wameegemea kwenye
magari yao huku wameipa visogo sehemu ile waliyokuwa wamejibanza akina Willy.
"Wale tutumie bastola zenye
kizibo tusipoteze muda", Bibiane alishauri.
"Hapata, tunahitaji kila risasi
tuliyonayo isipotee bure, pale ambapo tunaweza kulinda risasi nashauri tutumie
njia nyingine, au unaogopa hutaweza kumkaba sawasawa?", Willy alimuuliza
Bibiane.
"La, hasha! naweza sana Willy
na wewe mwenyewe utanishuhudia leo; haya twende", Bibiane aliamru.
Huku wakitambaa chini kama nyoka,
waliwanyemelea wale askari. walipofika usawa wa gari la kwanza Willy alisema.
"Sasa", wote wawaili walirukia na bila kuwapa nafasi hata ya
kushituka, Willy aliwapiga wawili karate kwenye vichwa akitumia mikono yake
miwili na kupasua vichwa vyao palepale. Bibiane alimrukia yule wa kushoto na
kumbana shingo na kisha kuikata kwa mikono yake. Hawa askari waliuawa kama
kondoo. Hawakutoa upinzani wa aina yoyote, huenda kwa vile hawakutegemea
kushambuliwa kama lile mahali pale. Kisha walizivuta maiti zao mpaka nyuma ya
ua, wakawavua zile sare za jeshi na kuzivaa haraka haraka. Bibiane alichekelea
sana maana zilikuwa kubwa. Hata hivyo akazifungafunga zikamwenea hivyohivyo.
"Utaweza kukimbia ama kupigana
na adui ukiwa na magwanda haya?", Willy alimuuliza Bibiane huku akicheka.
"Tena ndio mazuri zaidi hasa
kwa judo na karate", Bibiane alijibu.
Willy na Bibiane walibeba mizigo yao
na kisha wakachungulia ndani ya magari na kukuta la gari la katikati likiwa na
funguo. Waliweka mizigo yao ndani na kuliwasha na kisha kuondoka. Walipoangalia
saa ilikuwa yapata saa nne na nusu usiku. Waliondoka bila mtu yeyote pale
kuhisi kitu. "Moja kwa moja Kibumba", Bibiane alisema.
Comments
Post a Comment