KASHESHE
VIII
Nkubana na
wale askari watatu walifika mpakani yapata saa tano na robo usiku. Walishangaa
kukuta moja ya magari yao halipo na wale madereva wa magari hayo pia
hawaonekani. Kwanza walifikiri huenda baada ya wao kuchelewa wale askari
waliona waondoke, lakini askari mmoja aliona damu mahali gari moja lilikuwa
limeegeshwa.
"Hebu
angalieni vizuri huenda Willy Gamba kafika hapa na kufanya uharibifu
tena", Nkubana alieleza huku mikono yake ikiwa imeshika nyonga.
Wakati
Nkubana na askari wake wakitafakari, ndipo mmoja wa wale askari alipoona maiti
za wale madareva wa magari zikiwa zimetupwa nyuma ya ua palepale kituoni.
"Shenzi
kabisa huyu ni WIlly Gamba alikuwa hapa, na kachukua hata gari pamoja na sare
zetu. Mtu huyu ni mshenzi sana, ole wake nikimuona sintangoja kumpeleka kwa
Jean, nitamuua mwenyewe keshanisumbua sana. Twende haraka Kibumba, lazima
atakuwa ameelekea huko", Nkubana aliwaamru askari wake.
Walitafuta
funguo za magari haya na kwa bahati nzuri. gari moja lilikuwa na funguo
zilizoachwa ndani. Hivyo wakaliwasha gari hilo na kwa kasi kubwa wakaondoka
kuelekea Kibumba, wakiamini kuwa watamkuta Willy huko.
...............................................................................................................
IX
Mapigano
makali kati ya kikosi cha Luteni Nyamboma na jeshi la Meja Kasubuga yaliendelea
kwa kila upande kutumia mbinu kuukabiri upande mwingine. Kwa muda wa saa moja
na nusu, Luteni Nyamboma hakurudi nyuma, lakini alikuwa amewapoteza askari wake
wapatao kumi na watano, lakini nao pia walikuwa wamefanikiwa kuwaua askari
zaidi ya arobaini wa jeshi la Meja Kasubuga. Luteni Nyamboma alipoona
anaelemewa na risasi zinamwishia aliwaamru askari wake waliobaki kurudi nyuma
ili wakimbilie mpakani ambako waliamini kuwa wangepata msaada zaidi.
Walirudi
nyuma kwa hadhari na walipoona sasa wanaweza kukimbia ili kuwatoroka wanajeshi
wa jeshi la Meja Kasubuga walifanya hivyo. Meja Kasubuga alimru jeshi lake
liwafukuze na kuwakamata. yeye mwenyewe alirudi ofisini kwake ili aweze
kupeleka habari Makao Makuu Kigali kueleza mambo yaliyokuwa yametokea. Col.
Rwivanga ndiye aliyepokea simu na alipoangalia saa yake ilikuwa saa tano usiku.
"Afande,
tumevamiwa hapa na jeshi la Intarahamwe na Wahutu wenye msimamo mkali,
tumepoteza askari kama arobaini hivi, lakini tumefanikiwa kumrudisha adui
nyuma, amekimbilia mpakani mwa zaire", Meja Kasubuga alimweleza Col.
Rwivanga na kisha kueleza kwa kirefu mapigano yalivyokuwa.
"Hivyo,
inaonekana hao ni askari wenye ujuzi mkubwa?", Col. Rwivanga aliuliza.
"Sana
afande, mpaka mimi nimeshangaa, nafikiri fununu tulizonazo kuwa kuna kambi
kubwa ya mafunzo yenye wakufunzi wenye utaalamu wa hali ya juu kuhusu mambo ya
kijeshi ni kweli kabisa".
"Willy
yuko wapi?".
"Katika
prukushani hii Willy na mwenzake wamechomoka, naamini wamekwishavuka mpaka.
Huyu mtu ataleta kasheshe kubwa, nadhani niruhusu sasa mimi na kikosi changu
tuvuke mpaka ili tuwasaidie, maana alitaka kwenda Kibumba na huko ndiko
kunasemekana kuna jeshi zima la Intarahamwe. Kwa vyovyote hawezi kurudi, kwani
taarifa za siri tulizonazo kama ni kweli kuna askari zaidi ya elfu kumi katika
kambi hiyo, na wakimbizi wote katika sehemu hiyo wamepewa mafunzo ya hali ya
juu ya kijeshi. Kwani wale wakimbizi wanaokataa kushiriki mafunzo ya kijeshi
wanauawa, elewa kuwa kuna wakimbizi zaidi ya laki moja wanaume, achilia mbali
wanawake na watoto. Hivyo, Willy yuko katika hatari kubwa, huenda hakujua
vizuri nguvu ya adui", Meja Kasubuga alimwambia Col. Rwivanga.
"Wewe
fanya kazi moja kwanza, wafukuze hao wavamizi mpaka mpakani, wakivuka mpaka
wewe na jeshi lako msivuke, mtusubiri hapo hapo mpakani. Mimi, Meja Tom
Kabalisa wa Banyamlenge na Bwana Mpinda wa vikosi vya vyama vinavyopinga
serikali ya Zaire tutakuja usiku huu kwa helkopita, naamini saa nane usiku
tutakuwa tumefika hapo mpakani, msivuke mpaka tufike", Col. Rwivanga
aliagiza.
"Sawa
afande, mimi naendelea na mapambano, jeshi langu sasa linaelekea mpakani hivi
sasa. Mkifika helkopita itue ile sehemu ya kawaida, tutakuwa tumeimalisha
ulinzi eneo hilo, nitawasubiri", Meja Kasubuga alisema.
"Asante
na kwaheri, msifanye chochote kwanza", Col. Rwivanga alisisitiza na
palepale akajiweka tayari kisha akatoka kwenda kuwafuata akina Mpinda na
Kabalisa kwa ajili ya kuelekea kwenye uwanja wa mapambano.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment