KASHESHE
IX
Mapigano
makali kati ya kikosi cha Luteni Nyamboma na jeshi la Meja Kasubuga yaliendelea
kwa kila upande kutumia mbinu kuukabiri upande mwingine. Kwa muda wa saa moja
na nusu, Luteni Nyamboma hakurudi nyuma, lakini alikuwa amewapoteza askari wake
wapatao kumi na watano, lakini nao pia walikuwa wamefanikiwa kuwaua askari
zaidi ya arobaini wa jeshi la Meja Kasubuga. Luteni Nyamboma alipoona
anaelemewa na risasi zinamwishia aliwaamru askari wake waliobaki kurudi nyuma
ili wakimbilie mpakani ambako waliamini kuwa wangepata msaada zaidi.
Walirudi
nyuma kwa hadhari na walipoona sasa wanaweza kukimbia ili kuwatoroka wanajeshi
wa jeshi la Meja Kasubuga walifanya hivyo. Meja Kasubuga alimru jeshi lake
liwafukuze na kuwakamata. yeye mwenyewe alirudi ofisini kwake ili aweze
kupeleka habari Makao Makuu Kigali kueleza mambo yaliyokuwa yametokea. Col.
Rwivanga ndiye aliyepokea simu na alipoangalia saa yake ilikuwa saa tano usiku.
"Afande,
tumevamiwa hapa na jeshi la Intarahamwe na Wahutu wenye msimamo mkali,
tumepoteza askari kama arobaini hivi, lakini tumefanikiwa kumrudisha adui
nyuma, amekimbilia mpakani mwa zaire", Meja Kasubuga alimweleza Col. Rwivanga
na kisha kueleza kwa kirefu mapigano yalivyokuwa.
"Hivyo,
inaonekana hao ni askari wenye ujuzi mkubwa?", Col. Rwivanga aliuliza.
"Sana
afande, mpaka mimi nimeshangaa, nafikiri fununu tulizonazo kuwa kuna kambi
kubwa ya mafunzo yenye wakufunzi wenye utaalamu wa hali ya juu kuhusu mambo ya
kijeshi ni kweli kabisa".
"Willy
yuko wapi?".
"Katika
prukushani hii Willy na mwenzake wamechomoka, naamini wamekwishavuka mpaka.
Huyu mtu ataleta kasheshe kubwa, nadhani niruhusu sasa mimi na kikosi changu tuvuke
mpaka ili tuwasaidie, maana alitaka kwenda Kibumba na huko ndiko kunasemekana
kuna jeshi zima la Intarahamwe. Kwa vyovyote hawezi kurudi, kwani taarifa za
siri tulizonazo kama ni kweli kuna askari zaidi ya elfu kumi katika kambi hiyo,
na wakimbizi wote katika sehemu hiyo wamepewa mafunzo ya hali ya juu ya
kijeshi. Kwani wale wakimbizi wanaokataa kushiriki mafunzo ya kijeshi wanauawa,
elewa kuwa kuna wakimbizi zaidi ya laki moja wanaume, achilia mbali wanawake na
watoto. Hivyo, Willy yuko katika hatari kubwa, huenda hakujua vizuri nguvu ya
adui", Meja Kasubuga alimwambia Col. Rwivanga.
"Wewe
fanya kazi moja kwanza, wafukuze hao wavamizi mpaka mpakani, wakivuka mpaka
wewe na jeshi lako msivuke, mtusubiri hapo hapo mpakani. Mimi, Meja Tom
Kabalisa wa Banyamlenge na Bwana Mpinda wa vikosi vya vyama vinavyopinga
serikali ya Zaire tutakuja usiku huu kwa helkopita, naamini saa nane usiku
tutakuwa tumefika hapo mpakani, msivuke mpaka tufike", Col. Rwivanga
aliagiza.
"Sawa
afande, mimi naendelea na mapambano, jeshi langu sasa linaelekea mpakani hivi
sasa. Mkifika helkopita itue ile sehemu ya kawaida, tutakuwa tumeimalisha
ulinzi eneo hilo, nitawasubiri", Meja Kasubuga alisema.
"Asante
na kwaheri, msifanye chochote kwanza", Col. Rwivanga alisisitiza na
palepale akajiweka tayari kisha akatoka kwenda kuwafuata akina Mpinda na
Kabalisa kwa ajili ya kuelekea kwenye uwanja wa mapambano.
ITAENDELEA
0784296253
Comments
Post a Comment