TUTARUDI NA ROHO ZETU



SURA YA KUMI

III

Wakiwa angani ndani ya Helikopta, Nuru aliweza kuona vizuri baadhi ya maiti za makachero wa makaburu waliouawa huku wakiwa wamevalia sare pamoja na silaha zao mikononi. Walikuwa wamelazwa sakafuni mbele ya lango kubwa la kuingia katika mojawapo ya vyumba ndani ya jingo hilo lililozungukwa na ua wa seng'enge. Halikopta ililizunguka jumba hilo mara tatu. Von alikuwa akitumia darubuni kuona huku na huko. Aliporidhika na hali ya usalama, alimwamru rubani wa Helikopta hiyo kutua kando ya ua huo karibu na kichaka mahali ambapo mtambo huo ulikuwa kando ya mji.

Ilikuwa safari ya dakika mbili tatu tu, kutoka mjini hadi kufika kwenye mtambo huo. kabla ya kuanza safari hiyo Von alikuwa ametupiana maneno yasiyofaa na msaidizi wake ambaye alikuwa ameshangazwa na maamzi ya Von kuambatana na Nuru ndani ya Helikopta.

"Sikubaliani kabisa na uamzi huo. Nadhani ni wewe ndiye uliyetunga sheria hizi, kumpiga risasi mtu yeyote atakayeonekana akiusogelea mtambo ule, awe raia wa nchi hii ama mgeni. Vipi leo aende huyu mhalifu ambaye bado tunawatuhumu yeye pamoja na mwenzake ambaye yawezekana kuwa yuko huko akifanya mauaji ya siri kwa makachero wetu".

"Huyu ni mateka wangu", Von alimjibu. "Bado nina mengi ya kumsaili. Zaidi ya hayo kama kweli Joram yuko huko tutamtumia huyu kumfanya Joram asithubutu kuendelea na chochote anachowaza kichwani mwake", Von alitetea msimamo wake.

"Bado sikubali", Msaidizi huyo alisimamia hoja yake. "Nimeandaa kikosi cha askari wanne ambao ulipaswa kufuatana nao huko. Kadhalika nilikuwa nikisubiri amri yako ili nitume askari wengine zaidi ya hamsini kwa njia ya magari. Inaonekana yote ninayofanya ni kazi bure".

"Ni bure kabisa", Von alimjibu. "Unajua kabisa kuwa mtambo ule unalindwa katika hali isiyo na shaka kabisa. Hata kama mtu atafanikiwa kuingia ndani hawezi kabisa kufanya uhalibifu wa aina yoyote. Pamoja na juhudi zake zote bado ataambulia kufa tu. Hivyo nakushauri urudi na hao askari wako uliowaandaa. Nitakwenda mimi, huyu mateka na rubani tu. Sawa", Von alieleza kwa msisitizo.

Msaidizi huyo alimtazama Von kwa hasira na mshangao. Von hakuwa na kawaida hiyo. Alikuwa amezithamini sana hekima zake hususan katika masuala yote ya kiusalama katika nchi hii kwa kipindi chote, miaka yote walipokuwa wakifanya kazi ya kuilinda nchi yao. Lakini vitendo vyake masaa machache yaliyopita vilimchanganya kabisa. Vilikuwa vitendo ambavyo havikubaliki. Yeye kama mtu wa pili katika suala zima la usalama wa utawala huo hakuona kama kuna sababu ya kumtii Von hata kwa hilo. Hivyo alimtupia jicho la hasira na kumwambia, "Kwa mara ya kwanza nitafanya kinyume cha matakwa yako".

"Na kwa mara ya kwanza nakwambia kuwa... kuwa... Hufai kufanya kazi chini yangu. Baada ya suala hili nitaangalia suala lako", Von alisema huku akimsukumiza Nuru ndani ya Helikopta akamwamru rubani kuondoka haraka.

Hata hivyo moyoni Von alikuwa na mashaka kuhusu maamzi yake hayo. Alijua kabisa kuwa alikuwa akifanya kosa kubwa sana kufuatana na Nuru huko aendako. Lakini pia aliamini kuwa hiyo ilikuwa nafasi yake ya pekee kufanya mapenzi na msichana huyo na kisha amuue. Ndani ya jumba hilo la mitambo kulikuwa na vyumba kadhaa kikiwepo chumba maalumu kwa ajili ya faragha za wakubwa tu. Chumba hicho kilikuwa na mtambo wa televisheni inayotumia nguvu ya setilaiti iliyoko angani inayotumika kuitazama miji mbalimbali ya Afrika kwa umakini mkubwa. Vilevile kulikuwa na chombo maalumu ambacho kiliwawezesha makaburu kutazama shughuli zote zinazofanyika katika kila chumba ndani ya jumba hilo.

Ilikuwa kawaida kwa Von kujifungia ndani ya chumba hicho mara kwa mara kwa ajili ya kutazama utendaji kazi wa mitambo hiyo na jinsi wahandisi wanavyofanya kazi bila wao kujua. Mhandisi mmoja katika jumba hilo aliwahi kupoteza kazi na uhai wake baada ya kushukiwa na Von kuwa alikuwa na dhamila mbaya ya kuhujumu mtambo huo. Hata hivyo kifo cha mhandisi huyo machoni mwa watu ilionekana kama ajali iliyosababishwa na dereva aliyelewa na kumgonga mtu aliyekuwa akitembea kando ya barabara katikati ya mitaa ya Johannesburg. Leo Von alikusudia kukitumia chumba hicho kujistarehesha na mwili wa Nuru kabla ya kutulia na kuanza kuangalia kwa furaha watu wanavyoteketea kwa moto katika miji ya Dar es Salaam, Lagos, Lusaka, Harare na kwingineko.

Furaha iliyokuwa ikichemka katika fikra za Von iliingia nyongo baada ya Helikopta yake kupita juu ya jengo hilo na kushuhudia jinsi walinzi wa eneo hilo walivyolala hovyo wakiwa maiti baada ya kuuawa. Kutokana na hali hiyo, Von aliingiwa na hofu, akamtupia Nuru jicho la chuki. Tamaa aliyokuwanayo dhidi ya Nuru ikaanza kuyeyuka taratibu na nafasi yake kuchukuliwa na hasira kali. Von alitamani ammalize Nuru papo hapo ili kusahau yote aliyokuwa akihitaji kwake. Wazo jingine likamjia akilini kuwa. Kwa vile Nuru anaonekana katili sana asiyeogopa kifo kama walivyo wanawake wengine anaowafahamu. Hata hivyo Von akajipa moyo kuwa Nuru anaweza kufa baada ya kutaabika sana. Akaamini kuwa hakuna mateso yatakayomtaabisha zaidi ya kushuhudia kifo cha mpenzi wake Joram Kiango.  Von akiwa na uhakika asilimia mia kuwa Joram alikuwa mahali fulani katika jengo hilo akilia na kusubiri kifo, Von alitoa bastola yake na kuigongagonga kwenye kisogo cha Nuru. Baada ya Helikopta kutua, Von alimwamru Nuru.

"Twende", Von alisema kwa hasira mara baada ya kushuka kutoka ndani ya Helikopta huku akimwamru rubani awe makini wakati akimsubiri.

Nuru alitelemka na kufuata maelekezo ya Von. Kila walikopita kulikuwa na miili kadhaa ya marehemu waliouawa hovyo, baadhi wakitokwa na damu baada ya kujeruhiwa kwa risasi zilizoingia miilini mwao.

Kiasi fulani ilimshangaza Von kuona jinsi mtu mmoja Joram Kiango peke yake alivyofanikiwa kuwaangamiza askari wengi kiasi kile bila wao kujitetea. Lakini hali hiyo haikumshangaza Nuru hata kidogo. Wala hakuhitaji kusimuliwa. Nuru akiwa mtu anayemfahamu vizuri Joram na hila zake nyingi alijua kuwa Komando huyo alitumia njia moja ama nyingine kuwafikia askari hao wa makaburu na kuwashikisha adabu pamoja na kujiamnini kwa kuwa na silaha za kisasa na bunduki aina ya sub machine gun. 

Baada ya kufanya kazi yake ipasavyo Joram, akitoka kona moja kwenda kona nyingine katika ngome ya adui, Joram alifanikiwa kutoa hati zake za bandia na kuwaonyesha askari wa makaburu. Hati ambazo zilifungwa kwa namna fulani kiasi cha kuhifadhi hewa ya sumu ambayo bila shaka iliwafanya askari wa makaburu kulewa ghafla. Hivyo akawa na nafasi nzuri ya kuwaua mmoja baada ya mwingine bila kutumia silaha nzito.

Kilichomshangaza Nuru ni kutokufahamu Joram alikuwa wapi na akifanya nini muda wote huo tana katika eneo la hatari kama hilo. Nuru alikuwa amekadilia kuwa dakika tano zingetosha kabisa kuuteketeza mtambo huo na kutoweka. Na kwa mjibu wa ramani yao ndani ya jumba hilo hakukuwa na ulinzi wowote zaidi. Nuru akajiuliza vipi Joram asitokee na kummalizia Von. Mtu mnene, ambaye hakuwa na uwezo wowote wa kupambana na Joram.  Nuru akaamini kuwa ndoto yao unakaribia kuwa kweli, akamuomba Mungu moyoni mwake ili wamalize kazi na kuondoka kurudi Tanzania.

Von hakumpa Nuru nafasi ya kuwaza zaidi. Alikuwa akimsukumasukuma kwa mtutu wa bastola yake haraka haraka. Nuru hakuwa mzito, mara moja alielewa kuwa Von alimtanguliza ili amfanye kuwa ngao yake endapo lolote lingewatokea tofauti na mategemeo yake. Baada ya Von kukagua baadhi ya vyumba vya jengo hilo, akiwa amemtanguliza Nuru kama kawaida, walifika katika chumba maalumu ambacho Von na viongozi wengine hukitumia kwa ajili ya mapumziko.

Ukiondoa makochi na kabati lililojengwa ukutani, chumba hicho hakikutofautiana na maabara au studio ya aina yake katika macho ya Nuru. Mashine na mitambo kadhaa ilikuwa imepangwa kwa tafasiri fulani, kutani kukiwa na screen zilizopangwa katika hali ya kupokea habari mbalimbali. Von aliiendea mashine moja ambayo machoni mwa Nuru ilionekana kama komputa, akaanza kubonyeza swich aina kwa aina mara kioo katika ukuta mmoja kilipata uhai na kuanza kuonyesha mambo ya ajabu. Baada ya hali kutulia Nuru aliweza kuona teknolojia hiyo inavyofanya kazi, waliweza kuona chumba baada ya kingine katika jengo hilo. Kupitia screen hiyo kilionekana chumba kilichokuwa na mitambo ya aina mbalimbali ya kutisha. 

Nuru aliweza kuwaona wahandisi watatu waliokuwa makini wakifanyakazi ya kuongoza mitambo hiyo huku wakiwa hawana dalili zozote kuwa mambo yalikuwa yakienda mrama. Kitendo cha wahandisi hao kuwa makini na kazi yao kilimfurahisha sana Von, akaangua kicheko cha furaha. Ni yeye aliyependekeza kuwa ishara ya hatari kwa usalama wa mitambo hiyo zisiwafikie wahandisi hao wasije wakapatwa na hofu na kusababisha setilaiti iliyoko angani kukosa mawasiliano kutoka ardhini, jambo ambalo lingeweza kusababisha maafa na hasara isiyokadiliwa. 

Kwa jinsi jengo hilo lilivyoandaliwa Von alikuwa na hakika kabisa kuwa ingemhitaji binadamu mwenye moyo wa malaika kuwafikia wahandisi hao na kufanikiwa kuuharibu mtambo huo. Aliamini kuwa Joram hakuwa na moyo huo. Ni hilo tu lililokuwa likimtia nguvu Von. Sasa akaamini kuwa hakuwa amekosea. Kwa muda aliwatazama tena wahandisi hao wanavyowajibika. Wakiamini kuwa leo ilikuwa siku maalumu ya kazi kubwa hivyo walifanyakazi zao kwa umakini na juhudi ya hali ya juu. Kisha Von alibonyeza kuona sehemu nyingine. Chumba hicho kikahama na vyumba vingine vikaanza kuonekana katika kioo.

"Nataka umuone mpenzi wako atakavyokufa ama mahali alikofia", Von alimwambia Nuru huku akimwelekezea tabasamu la kifedhuli lililoyasindikiza maneno yake, "Keti tafadhali. Keti hapa ili uweze kuona kwa starehe jinsi Afrika inavyoteketezwa kwa mioto ya ajabu".

ITAENDELEA 0784296253

Comments

HABARI ZILIZOPITA

HEKAYA ZA ABUNUWASI

HISTORIA YA VITA VYA KAGERA 1978 - 79

PATA HADITHI ZA UPELELEZI ZA KUSISIMUA

TUTARUDI NA ROHO ZETU?

Vifaa vya Kijeshi vilivyotia fora maonesho ya miaka 50 ya Uhuru

HOFU