SURA YA TATU III
Wakati huo
huo Joram Kiango alikuwa akipokea simu iliyopigwa ofisini mwake.
"Sauti
yako i tamu mno masikioni sister, yaelekea nawe u kiumbe mzuri sana. Siwezi
kuukataa kamwe mwaliko wa mtu mwenye sauti nzuri kama hiyo, Baada ya saa moja
nadhani nitafika... Haya... Ahsante... Umesema wapi vile... Heh... Light
Lodge?... Hapo siyo?. Nitafika baada ya saa moja...", akaweka simu chini
na kuukunja uso wake akimtazama Neema Iddy, katibu wake ambaye pia alikuwa
akumtazama.
"Nani?",
Neema alihoji kwa shauku.
"Anajiita
waridi".
"Waridi?
Anataka nini?" Joram alipochelewa kujibu. Neema aliongeza. "Sikujua
Joram kama nawe u mroho wa wanawake kiasi hicho. Sauti tu unaridhika na kuahidi
kumfuata? Angalia Joram. Utaingia katika mtego. Una maadui wengi katika nchi
hii".
"Nalijua
hilo", Joram alisema. "Siendi kwa sababu ya sura wala sauti yake kama
nilivyosema. Kilichonivutia ni maelezo yake. Anasema yeye ni yule msichana
ambaye alipigwa pale baa ya Forest of Flowers. Anadai kuwa nia yake ni
kunishukru pamoja na kunipa habari fulani ambayo inasisimua".
"Malaya
kama yule! Hana habari yoyote. Anachotaka ni kukupata wewe tu".
"Hapana",
Joram alimkatisha. Sauti yake ndiyo iliyonifanya nivutiwe hata kumwahidi kuwa
nitakwenda. Inavyoonyesha kuna kitu zaidi ya anachosema. Nahitaji kujua ni
nini. Zaidi ya sauti, nadhani utakumbuka kuwa jana binti huyo alilia sana
akilitaja jina langu. Sijui alivyonijua".
"Ni
mimi niliyekutaja kwanza".
"Ni
kweli, lakini hiyo siyo sababu ya kumfanya aniite jina langu mara nyigi tena
kwa ufasaha kiasi kile. Ni kama mtu aliyekuwa akinifahamu kitambo".
"Wewe
si mtu unayefafamika Joram?".
"Pamoja
na hilo", Joram aliongeza. "Ni wapi alikopata namba yangu ya simu?
Tuseme kwenye vitabu vya simu. Kwa nini ahangaike kiasi hicho? Na kwa nini iwe
mapema hivyo? Neema, huoni ni mwujiza huu? Jana tu alikuwa hoi. Leo anazungumza
kwa uchangamfu kabisa na yuko logi badala ya hospitali! Huoni kama kuna jambo
hapo? Yaonyesha kuwa ananitafuta. Yawezekana hata jana alikuwa akinihitaji mimi
tu hakuwa majeruhi wala mgonjwa!" Akasita kidogo kabla hajaongeza kwa
sauti ya chini akisema: Na atanipata. Kwa muda mrefu nimekuwa sina kazi ya
kufanya".
Wakati huo
Joram alikuwa wima akivuta droo hii na ile, akiweka hiki mifukoni na hiki
kiunoni. Mara akaanza hatua za haraka kuelekea mlangoni.
"Yaani
unakwenda Joram, mara hii!", Neema aliuliza kwa mshangao.
"Naam".
"Mapema
namna hiyo? Si umemwambia baada ya saa moja?".
"Niliamua
kumdanganya. Siamini kama yeye ananieleza ukweli mtupu, hivyo nami sioni ubaya
wa kumweleza uongo kidogo. Nataka kufika mapema kidogo nione anachofanya".
"Lakini
ujihadhari", Neema alimwambia wakati akivuka kizingiti cha mlango.
"Usijali
Neema", Joram akamjibu bila kugeuka nyuma.
ITAENDELEA 0784296253
Comments
Post a Comment